Saturday, February 21, 2009

SIHITAJI KUKAMILISHWA NA YEYOTE.

Kamradi kangu

Hebu chukulia kama umeambiwa uandike wasifu wako kwa mtu usiyemfahamu ambaye unaamini akiusoma wasifu huo atakujua kwa asilimia mia moja kuwa wewe ni mtu wa namna gani.
Jiulize ni kitu gani hasa utaandika katika kuueleza wasifu wako ili huyu mtu msiyefahamiana kabisa akufahamu kupitia maandishi yako?

Kwa mfano labda utaanza kwa kusema, “mimi ni mwanamke au mwanaume, ni mwanafunzi; mfanyakazi au nimejiajiri nakadhalika nakadhalika.
Labda utaeleza juu ya vitu unavyovipenda na vile usivyovipenda, pamoja na tabia yako kama vile ni mwenye aibu, chakaramu, mtu wa kujirusha, mkimya, mpole, na tabia nyingine ambazo zinaweza kumfanya mtu atakayesoma wasifu wako akufahamu vizuri.

Jaribu kuchunguza tabia za marafiki zako wote pamoja na ndugu na jamaa waliokuzunguka, Je unadhani yupo japo mmoja ambaye mmetokea kufanana kwa kila kitu?
Sidhani, na kama yuko labda itakuwa ni baadhi ya vijitabia fulani mnafanana lakini haiwezi kutokea mkafanana kwa kila kitu.

Vipi kuhusu ndugu mliozaliwa tumbo moja, yawezekana kweli mkafanana kwa kila kitu? Jamani si tumezaliwa na baba mmoja na mama mmoja, Kwa nini sasa tusifanane kwa kila kitu?
Hii nadhani haiwezekani, na haitatokea iwezekane hata siku moja.

Kwa mtazamo huo basi, naamini kwamba kuna Koero mmoja tu hapa duniani, naye ni mimi, kama kuna mtu anatumia jina la Koero, basi hiyo ni coincidence, lakini hawezi kufanana na mimi hata kidogo, tembea dunia yote hii, Koero ni mimi tu. Kwa hiyo mimi ni mtu maalum kama ulivyo wewe na mwingine.
Binafsi najivunia kwa jinsi nilivyo na najikubali kwa kila kitu, kama ninayo kasoro, basi wewe ndio umeiona kwa mtazamo wako lakini mimi sijaiona.

Hivi karibuni nimetofautiana na mama yangu juu ya mustakabali wa maisha yangu.
Eti anataka nirejee chuoni ili kuendelea na Masomo, wakati nimeshadata na Biashara zangu. Baada ya lile zengwe la kurejeshwa nyumbani na chuo kufungwa nimejikuta nikipata uamuzi mwingine wa kuendesha maisha yangu, na nimeona niwe mfanyabiashara.
Elimu niliyoipata ya Kidato cha sita inatosha sana kwani nimeshajijua kuwa mimi ni nani na hata nikiendelea na masomo ya chuo kikuu sidhani kama itanisaidia sana katika kufikia malengo na matarajio yangu. Na hata kama nikisoma na kupata shahada kumi sidhani kuwa hayo ndio malengo yangu, sana sana naona ni kupoteza muda bure.

Nimeona nijikite kwenye biashara, kwa sababu naona kuwa ni kipaji changu na nina matarajio makubwa sana hapo baadae ya kuwa mmiliki wa kampuni kubwa yenye matawi karibu nchi nzima, hivyo ndivyo ninavyoiona biashara ya yangu.
Nadhani utaniuliza kama utaalamu wa kuendesha hiyo biashara nitauapa wapi? Jibu ni rahisi sana, nitaawajiri hao wasomi wenye shahada zao na kwa hakika bishara yangu itakuwa ikiendeshwa kwa ufanisi, kwani naamini naweza kuajiri hata Profesa, si ilimradi nimlipe mshahara mzuri na marupurupu?
Kwani hamjui kuwa nchi hii watu wanasoma ili wajiriwe badala ya kujiajiri?

Kwa nini mama yangu anakazania nisome? Anatafuta kuridhisha nafsi yake. Mama yangu anao ndugu zake ambao wamesomesha watoto wao mpaka vyuo vikuu na wanazo nafasi kubwa wengine wakiwa serikalini na wengine wakiwa wameajiriwa na mashirka ya kimataifa wakiwa wanashikilia nafasi za juu, sasa wakikutana kwenye vikao vyao vya ndugu, kila mmoja huanza kujisifu kuwa wanae wamesoma au wanaendela na masomo ya elimu ya juu, ilimradi kutaka kujionyesha kwa wengine kuwa watoto wao ni wasomi.
Kwa upande wa familia yetu dada zangu na kaka zangu wote ni Graduate, mimi tu ndiye nimechomoa kuendelea na elimu ya juu.

Kwa kweli baba yangu hana tatizo na uchaguzi wangu, lakini mama, Duh! Ameng’ang’ania kweli nirejee kusoma, na mimi nimekataa kabisa.

Mimi naamini kila mtu anao wasifu wake na malengo yake haihitaji mtu aje akukamilishe kwa kukupangia kuwa ufanye nini juu ya maisha yako.
Mtu kukubali kupangiwa nini cha kufanya juu ya maisha yako ni kupotea njia, ni sawa na kupanda basi la kwenda Mtwara wakati nia yako ni kuelekea Arusha!
Ukweli ni kwamba wako vijana wengi wanakabiliwa na changamoto inayonikabili sasa. Binafsi nimeweza kukabiliana nayo na ninaamini nitashinda kwani baba yuko upande wangu, lakini ningependa kuwashauri vijana wenzangu kwamba tusikubali kuburuzwa na matakwa ya wazazi, sisi ni watu kamili hatuhitaji wazazi watukamilishe.



Naomba nisitafsiriwe kama nawakatisha tamaa wale wanaotaka shahada, hapa nimeeleza malengo yangu, naamini pia ninyi mnayo malengo yenu, kama malengo yako ni kusoma, basi soma mpaka upate shahada yako ya uzamili ikiwezekana uwe hata Profesa,


Samahani nimeandika makala hii nikiwa na mchanganyiko wa hasira na msongo wa mawazo, hata hivyo naamini watambuzi watanielewa.

Tuesday, February 17, 2009

HIVI WAMETUZAA ILI TUWE WAO?

Tukiwezeshwa kukuza vipaji vyetu tunaweza.

Wazazi wanatakiwa kujua kwamba, mtoto ni binadamu aliye kamili kabisa. Ni binadamu ambaye anatakiwa kuwa na haiba yake na ubainisho wake kama yeye. Mzazi anapofikiria na kuamini kwamba, mtoto nilazima awe mfano wake anakosea. Kama mzazi ni dakitari kama mzazi anapenda sana mziki, kama mzazi anachukia sana mpira basi anataka mtoto naye awe hivyo, huo sio ukomavu.

Mimi naamini kwamba bila mzazi kujua kanuni au misingi kadhaa inaweza kuwa vigumu kwake kumlea mtoto bila kumwingizia athari mbaya ambazo yeye mzazi aliwekewa na wazazi wake. Hebu fikiri, ni wazazi wangapi ambao wanamlea mtoto kana kwamba mtoto huyo siyo binadamu kamili? Ni wengi sana wanaomlea mtoto huyo awe kama wao au kama wao wanavyotaka.

Kumbuka kila mzazi anapewa dhamana ya kumfanya mtoto kukuwa na kufikia kiwango cha juu kabisa cha ufahamu na binadamu mwenye faida kwa wengine. Ni dhamana ya kuhakikisha kwamba mtoto anapokuwa mkubwa anafanya kila kilicho chini ya uwezo wake.

Mzazi kwa hali hiyo, anapaswa kukagua na kuelewa upendeleo wa mtoto vipaji na hofu zake. Kwa kujua hivyo anakuwa kwenye nafasi ya kumudu kukuza vipaji vyake, lakini pia kumuhakikishia kuhusu usalama na uwezo wake.

Mtoto anatarajia kupendwa na wazazi wake muda wote bila mashariti. Kumpenda mtoto wakati tu anapofanya kile atakacho mzazi na kutompenda anapokosea kwa vipimo vya mzazi huo ni udhaifu mbaya kabisa. Kupenda kwa mashariti huharibu badala ya kutengeneza tabia ya mtoto.

Mtoto anahitaji kuwekewa mipaka ya yale anayoweza kusema kufanya na kujihusisha nayo. Lakini mipaka hii ni lazima iwe ni yenye kuaminika. Mipaka yenye kutegemea mazingira au hali ya mzazi na hivyo kuwa inabadilika sana kumharibu mtoto. Leo mzazi anasema hiki hakifai kesho anasema kinafaa. Leo anasema, watoto hawaruhusiwi kufanya hiki kesho anabadilika na kusema wanaruhusiwa.

Kuna wazazi ambao hawajawahi kuwasifu watoto wao hata mara moja hata wanapofanya mambo mazuri na makubwa sana.wanachosubiri wao ni watoto hao kukosea tu. Inashauriwa wazazi waone mazuri zaidi kuliko kuona mabaya zaidi ya mtoto. Bila kukosea hakuna kukua na mzazi anayemwonesha mwanae kuwa kukosea ni dhambi anajaribu tu kumuharibu mtoto huyo.

Mzazi anatakiwa kumsaidia mtoto kujenga ndoto kubwa za baadaye na sio kumvunja nguvu katika ujenzi wa ndoto hizo. Mtoto anaposema kwamba anataka kuwa raisi wa nchi, mzazi amwambie kwamba inawezekana na kumfundisha angalau kwa kiwango chake cha ufahamu kwamba anaweza kuwa.

Mzazi ana wajibu wa kumfanya mtoto wake kujenga tabia ambazo zitamsaidia ukubwani. Kama mwanaye hataki kuwa wa visasi akikosewa na wenzake mzazi asioneshe kwamba hao wenzake wanastahili adhabu bali zaidi msamaha. Kusisitiza msamaha kwanza kabla ya adhabu humsaidia mtoto kujua umuhimu wa kuvumilia wengine.

Kuna kanuni nyingi ambazo mzazi anatakiwa kuzifuata katika kujaribu kuwa mzazi bora zaidi ambaye halei mtoto kwa kufuata athari ambazo alipewa na mzazi wake bali kwa kuzingatia hali halisi ya saikolojia ya binadamu. Hizo nilizokutajia ni baadhi tu.

Friday, February 13, 2009

A COFFEE FARMER OF MBINGA

Jana nilikuwa nasoma kitabu kimoja ambacho hakikuwa na jalada kwa hiyo imeniwia vigumu kujua kama kilikuwa ni cha darasa la ngapi, kitabu chenyewe kina mkusanyiko wa hadithi tofauti tofauti, na mojawapo ni hii inayozungumzia kilimo cha Kahawa Mbinga ( Nashangaa kwa nini haikuwa ni Kilimanjaro).
naomba anayefahamu hadithi hii atujuze kama inapatikana katika kitabu gani na ni cha darasa la ngapi?

Mzee Ngwatura in his Farmer

In the south-west of Tanzania, between Songea town and Lake Nyasa, stands the little town of Mbinga. It is the head of the Mbinga Area, an area which is now famous for its good coffee. Only a few years ago this was one of the least known parts of the country, and the people were among the poorest in Tanzania, but in the last few years there have been many great improvements there. The Roads have improved and are improving still further. Traders commonly go to the market there to sell or exchange their goods. Every year, mud houses are being pilled down, and more modern ones made of bricks with iron roofs are being built in their place. The Mbinga people are becoming famous. And it is all because of coffee.

Coffee comes from the round red fruits of a small tree. Inside each fruits there is a pair of seeds called beans, and these beans are used to make a pleasant hot dink rather like tea, but with special taste of its own. The Arabs have been drinking coffee for many hundreds of years and in more modern times it has also become the favourite hot drink in Europe and America, where ground coffee and tins of coffee powder are on sale in all the shops. The Mbinga people didn’t know anything about coffee until a few years ago. Now many Mbinga farmers have rows and rows of coffee beans and ear n a good deal of money.

One person who can tell you all about it is Mzee Francis Ndunguru Ngwatura. He is a coffee grower at a little village called Mandita, about ten miles from Mkinga. The whole area is mountainous, and at certain times of the year the weather is quite cold and misty. Because of the mists there is a saying ‘Ukungu kama Mandita’ which means ‘as misty as mandita village’. Mzee Ngwatura has been growing coffee since 1943, when he planted 274 trees.
At that time he knew nothing of the present importance of the crop to the Mbinga people and to himself. He and his friend Mzee Setman got the idea of planting coffee from Mzee setman’s relations at Mhagawa Asili, and the Mhagawa people got it from the people living near Moshi in the north. It was not till later that Mzee Ngwatura came to like the taste of coffee himself , although at first he sweetened it with honey instead of with sugar. He now has at least three thousand coffee trees, and his farm is still growing.

Mzee Ngwatura works hard all the year round, but the busiest time of the year is harvest time. The harvest is usually gatherd between September and January when the fruits are red and ripe, and as it needs more than one pair of hands to pick them, Mzee Ngwatura has to pay a larger number of people to help him. The picking goes on all day, and in the evening the ripe fruits are put into special machines which get the beans out the skin. This work used to be done by hand but of course when it is done by machine it is much quicker and easier. After that, the beans are washed and put in large pots, where they remain covered with sacks for about a week. Then they are washed again and spread out on special wire nets to dry. The drying, which takes two or three weeks, is usually the job of Ngwatura’s wife, Mama Katarina. She sees that the beans do not receive too much hot sun and she can tell whether they are properly dry just by looking at them. Then they are put into sisal sacks ready for sale.
On the special day of the sale, Mzee Ngwatura and his helpers carry their sacks to the market-place, Gulio, a short distance from his home. There the coffee is examined and divided into three different sorts, called A, B, and C. The best sort is A. Then the whole crop is weighed, and Mzee receives his payment, Makopesho. After the sale the cpffee is taken by lorry to the nearest Co-operative at mbinga, and then to Moshi in the north, where the beans are put into machines to rub the skin off and then sold again and sent to other countries.

The coffee commonly bought in shops is a sort of brown powder with a very pleasant smell. It is made from beans which have been roasted and ground. You just put a spoonful of coffee powder in a cup and pour boiling water on it. Some people like their coffee black and strong, while others like it white, with milk in it. Most people like to add a spoonful of sugar, which makes it taste pleasantly sweet.

There is plenty of work on Mzee Ngwatura’s coffee farm all through the year, not just at harvest time. As the trees get older, they no longer produce good fruits, so new trees have to be planted to take their place. Every November and December, Mzee sows some of his beans four to six inches apart in straight rows .When they are about a foot tall he digs them up with their roots and plants them in specially prepared holes spaced nine feet apart.
These holes are dug about September and left open till planting time, when they are filled up with rich black soil. That is where the young plants slowly grow into small trees. But it is three or four years before they start producing fruit, and in that time the spaces between them must be kept free of weeds and each plant must be protected from cold winds. Then when the trees are old enough, they must be sprayed several times a year with a sort of medicine that kills harmfully insects, and at least ones a year the branches must be carefully cut back so that the trees will be low and strong and will produce plenty of good fruit.

But Mzee Ngwatura does not spend all his time producing coffee. He has fruit trees too, and he keeps cows, goats, sheep, Pigs and hens. He used to keep a shop and he has now opened it again. He has built a pair of modern brick houses with iron roofs, one for himself and the other for his sons. All his sons and daughters have been to school to be educated for he believes that it is the job of all modern Tanzanian to improve their minds through education. And to grow more and better crops both for food and for trade.

Wednesday, February 11, 2009

NDOA NYINGI NA TALAKA NYINGI!

Siku hizi hazidumu!

Hivi karibuni nilibahatika kusoma mahojiano ya Mwanamuziki wa kundi la zamani la muziki, maarufu kama Spice Girls la nchini Uingereza Geri Halliwell. Nilisoma mahojiano yake mtandaoni aliyoyafanya na Gazeti la Woman’s Day la nchini humo.
Labda niwakumbushe wale wasiolifahamu kundi hili la Spice Girls.Kundi Hili liliwahi kuvuma sana miaka ya 90 nchini uingereza likijumuisha wanamuziki wanne, Victoria, aliyeolewa na Mchezaji maarufu wa soka nchini Uingereza David Beckgham, Emma, Melanie na Geri Halliwell.

Katika Mahojiano hayo, mojawapo ya maswali aliyoulizwa na mwandishi, ni hili la yeye kutoolewa pamoja na kwamba ana mtoto. Majibu yake kwa swali hilo ndio yaliyonisukuma nikae kitako kwenye Kompyuta yangu na kuandika makala hii.
Akijibu swali hilo, Geri alisema kwamba hana imani kabisa na maisha ya ndoa, na ndoa kwake sio mojawapo ya agenda zake katika maisha.

Alisema katika kizazi hiki familia nyingi zimeshuhudia kuvunjika kwingi kwa ndoa kama ilivyotokea kwa wazazi wake. “Katika makuzi yangu nimeshuhudia ndoa nyingi zikivunjika mpaka nimefikia kuona kwamba ndoa hazina maana kabisa” alisema Geri.
Aliendelea kusema kwamba haoni ndoa hata moja ya mfano ambayo anaweza kuitumia kama Dira yake inayoweza kumshawishi kuolewa, ingawa anapenda sana kuwa na watoto wengi.

Siku hizi hapa nchini vijana wengi wamekuwa wakifunga ndoa kila uchao, lakini hata hivyo Talaka nazo zimekuwa zikiongzeka vile vile. Ndoa zimekuwa nyingi sana kwa sababu watu huoana kiholela. Kuoana kumekuwa rahisi na kusiko kujiuliza mara mbili, ukilinganisha na zamani. Kwa sababu hiyo ndoa zinavunjika sana. Kwa kuangalia ukweli huo utagundua kwamba talaka siyo nyingi sana bali ndoa za hovyo ndiyo nyingi, kwani huanza ndoa na talaka hufuata.

Wanaume na wanawake na hata wavulana na wasichana huoana bila ya kujua sababu ya kuoana kwao. huona kwa sababu wameambiwa kuna kuoana, huoana kwa sababu umri unaenda au kwa sababu watu wameona watu fulani wakiwa na furaha wakidhani ni kwa sababu ya ndoa.

Wazazi nao wanawalazimisha au kuwashinikiza vijana wao kuoa au kuolewa wanataka kuona tu kwamba nao wana wajukuu, wanataka kujua vijana wao wakiwa na wenzi wao ili wajisikie vizuri. Wanaogopa kuambiwa, ‘binti wa fulani hajaolewa mpaka sasa hivi’ au ‘vijana wa fulani wahuni tu hawataki kuoa’. Wazazi nao hawana sababu ya kwa nini vijana wao waoe au kuolewa.

Kuna haja ya wazazi kuwafanya au kuwasaidia vijana wao kujijua vizuri wenyewe, kabla hawajaingia kwenye uhusiano wa dhati wa kindoa. Inabidi kijana ajiuluze kama yu tayari kwa ndoa na je hana jambo ambalo litamzuia au kumfanya ashindwe kutimiza wajibu wake wa ndoa, kwa mfano masomo, kazi na mengine?
Je kijana anaamini nini kuhusu ndoa yaani ndoa kwake ni nini? Kama kwake ndoa ni kupata furaha, kukimbia matatizo ya nyumbani, kuzaa, kuwa huru kuamua mambo yake na sababu nyingine kama hizo inabidi ajiulize tena na tena kama sababu hizo ni sababu za msingi.

Wanaoingia kwenye ndoa siku hizi wengi hawajiulizi kama wako tayari kupata watoto. Unakuta mwanamke akizaa wanaanza kuhisi kwamba walikosea kuoana na hapo kutoka nje huanza na hata kutekelezana wakati mwingine. Hata kama wanataka watoto huwa hawajapanga namna ambvyo watawalea na kama wangependa kuwa na watoto wangapi na maswali mengine kama hayo.

Lakini, kunakushindwa kwingi katika kujiuliza ni kwa kiasi gani mtu anawaza kuwakubali wengine na kuyachukua matatizo yao. Ni vema kijana akajiuliza kama anaweza kuvumilia kasoro au udhaifu wa wenzake kama anaweza kukabili mabadiliko ambayo yanaweza kutokea kwenye uhusiano.

Siyo mtu kujijua peke yake lakini hata kumjua mwingine ni tatizo pia. Mtu anaingia kwenye uhusiano wakati hamjui vema anayeoana naye. Anamjua kwa sura na mwili ndiyo lakini zaidi ya hapo hajui kingine chochote kuhusu huyo mwingine, hajui kwamba ni Malaya, hajui kuwa ni mchoyo, hajui ni mkata tamaa, hajui kama ni “mtoto wa mama” hajui chochote kumhusu.

Unakuta watu wamekubaliana kufunga ndoa, lakini mmoja au wote hawajuani mwingine anatokea wapi hasa. Anasena tu “wazazi wake sijui ni wenyeji wa wapi, sijui Tanga vile, sijui Iringa!”

Ukweli ni kwamba bila kumjua mtu vizuri ni hatari kuoana naye. Wakati mwingine wenzetu ni watu wanaozalisha nguvu hasi nyingi duniani, wakorofi wenye kijicho, walipa visasi, wenye zarau, wapenda shari na mengine. Lakini kwa sababu wanatutendea vema katika wakati fulani tunaamini hawana tatizo.

Wasichana wengi wanakubali kuoana na wanaume ati kwa sababu siku hizi hakuna wanaume. Ni nani amesema hakuna wanaume? Msichana ameona kabisa kijana ni mgonvi na pengine ameshawahi hata kumpiga lakini anajiambia “nikimkosa huyu ndiyo basi sitoolewa tena” kisha anaolewa na wanaishi kwa mwaka mmoja tu.

Wanalazimika kuingia kwenye uhusiano ambao wanaona kabisa hautadumu. Hufanya hivyo kwa hofu ya kuwa wapweke. Wanaogopa sana kubaki bila kuolewa kwa sababu eti wamesikia mtaani kwamba wanaume hawapatikani kirahisi. Aibu tupu!
Mara nyingi vijana wanaongozwa na kuhemkwa badala ya tafakari katika kuingia kwenye ndoa. Wanapokuwa kwenye uhusiano kuhemkwa kunaisha na wanarudi kwenye hali halisi ambayo wanashindwa kuibeba.

Kuhemkwa huku ndiko wenyewe wanakokuita kupenda. Wanasema kabisa “nimependa sana siwezi kumwacha pamoja na kunipiga na umalaya wake” Ebo! Mtu ni Malaya na kama hiyo haitoshi bado huwa anakupiga halafu unasema huwezi kumwacha? Kama huo si uwendawazimu ni nini?

Mara nyingi nyingi kuhemkwa kunaisha wakiwa tayari na watoto wawili na maisha wakati huo yanakuwa yameharibika. Wengine kuhemkwa kunaishi wakiwa tayari na ukimwi, wengine wakiwa na chongo, na wengine wakiwa na BP na kisukari juu, kwa sababu ya maumivu makubwa ya kihisia.

Kuna watu wazima ninaowajua ambao nao wameshabadili wake na wanaume mara kadhaa. Kila ndoa wanayoingia inabomoka. Kisa ni kufuata mihemko badala ya kufuata hekima. Hawajifunzi ndoa ya kwanza wala ya pili, wanatembea na kosa lilelile, yote hiyo ni kuhemkwa badala ya kujua na kupenda.

Nakubaliana na Geri Halliwell kwamba, kuna talaka nyingi. Lakini kama nilivyosema, nadhani kuna ndoa za kuhemkwa nyingi, na ndizo zenye kusababisha talaka nyingi.

Monday, February 9, 2009

KUSENGENYA: TABIA ISIYO NA MWISHO MZURI

Mwisho wake ni maumivu

Hebu chukulia umechelewa kufika kazini , unapofika ofisini unasikia sauti za wafanyakazi wenzako wakizungumza kwa ndani, unapofungua mlango na kuingia, ghafla wananyamaza na kukuangalia kwa mshangao!
Jiulize walikuwa wanazungumzia nini?

Kwa kuangalia mfano huo kwa haraka utagundua kwamba walikuwa wanazungumzia jambo linalokuhusu au walikuwa wanakusengenya. Kwa mujibu wa watafiti mbalimbali, imethibitishwa kuwa wanawake na wanaume wote wanasengenya, labda kinachowatofautisha ni uwiano kwamba wanawake ndio wasengenyaji wazuri zaidi ya wanaume.

Hebu jaribu kutembelea kwenye saluni za kike, utakuta hakuna kinachozungumzwa huko zaidi ya kusengenya, tena kibaya zaidi ni usengenyaji wa kubomoa na kuharibu umaarufu wa watu wengine. Kama wamemtembelea mwenzao au kuhudhuria mazishi ya msiba unaomhusu mwenzao, shuhudia mazungumzo yatakayotawala wakati wanarudi.

Njia nzima mjadala utakuwa unahusu maisha ya mwenzao, kwamba hana hiki , hana kile, au mazishi hayakuwa mazuri kama ya fulani, pia hata kulinganisha thamani ya jeneza la maiti na umaarufu wa mhusika. Utawasikia wakisema “kuringa kote kule kumbe si lolote wala si chochote, ndani kwake kubaya, hana hata kitu cha thamani ukilinganisha na mavazi yake na umaarufu wake”.

Litazungumzwa hili na lile ilimradi tu kumbomoa mhusika. Hivi karibuni niliamua kufanya kautafiti kadogo pale ilipo biashara yangu kwa kuwauliza baadhi ya wateja wangu na wapita njia wengine. Nilizungumza na baadhi ya wanawake pamoja na wanaume kadhaa kuhusu hili suala la kusengenya. Dada mmoja aliyejitambulisha kwa jina la Sharifa, alithibitisha kuwa ni kweli sisi wanawake tunaongoza kwa kusengenya, lakini alitetea kuwa kuna tofauti ya kusengenya na kumzungumzia mtu au watu kwa mazuri na mafanikio yao.

Sharifa alibainisha kuwa sio vibaya kumzungumzia mtu kutokana na mafanikio yake, kwani hiyo kuwapa fursa ya kujifunza kulingana na mafanikio ya mwenzao, pia hata wanapozungumzia mapungufu ya mtu, hiyo ni kwa ajili ya kujifunza kutokana na mapungufu ya mwenzao. Dada mwingine aitwae Bupe, alisema kuwa hata wanaume nao husengenya, yeye alishawahi kumfuma mvulana ambaye punde tu alitoka kufanya naye mapenzi akiwasimulia wenzake jinsi yeye (Bupe) alivyo awapo kitandani, kuanzia mwili wake hadi namna anavyofanya mapenzi.

Ukweli ni kwamba hakuamini tukio lile kwa sababu mvulana aliyemwamwini na kuamini kumkubali kuwa mpenzi wake baada ya kumtongoza kwa muda mrefu, angeweza kusimulia yale yote aliyoyasikia. Kibaya zaidi hata wale waliokuwa wakisikiliza ule utumbo walionekana kwa nje, kuwa ni watu wenye busara. “Usiwaone wamekaa kwenye makundi wakizungumza ni wasengenyaji wazuri sana, tena usidhani wanajadili jambo la maana, sanasana wanazungumzia wanawake wale waliotembea nao alisisitiza Bupe”.

Kijana mmoja aitwae Dikupila ambaye anamiliki saluni ya kunyoa nywele jirani na ofisi yangu, kwa upande wake aliyewatetea wanaume kuwa siyo wasengenyaji, kwani hayo ni mambo ya wanawake. “Sisi wanaume kusengenya! Haiwezekani, hayo ni mambo ya wanawake, sana sana ukikuta mwanaume anajadili udhaifu wa mpenzi wake hadharani basi ujue huyo jamaa anamatatizo makubwa ya kiakili” alisema Dikupila.

Watu wengi wa jinsia tofauti niliobahatika kuzungumza nao walikuwa wanakiri kusengenya lakini walikuwa wanajaribu kutengeneza fasili ya neno kusengenya kwa namna ya kukidhi haja zao. Kwao kusengenya walisema ni mtu kutafuta namna ya kujifunza kuwa bora kupitia makosa ya wengine. Je tabia hii inaweza kuachwa? Wengi walikiri kwamba siyo rahisi tabia hiyo kuachwa kwani imekuwa ndiyo sehemu ya maisha, kwamba haiwezekani watu kukaa pamoja na kuacha kuzungumza matukio na yanapozungumzwa matukio, ni lazima yatawahusu watu hivyo kujikuta watu wanasengenya.

Na tabia hii imejikita kila mahali kuanzia nyumbani, mitaani, hadi maofisini, mashuleni na vyuoni. Binafsi naamini kwamba tabia inaweza kuachwa kwa watu wakijikita zaidi katika kufanya kazi na kuwa wabunifu, hasa maofisini. Kama ni suala la mazungumzo iwe ni ya kuleta ufanisi na tija katika kazi kwani waajiri hulipa mishahara kutokana na ufanyaji wetu wa kazi na uzalishaji.

Utakuta mtu anafika kazini amechelewa na akifika anaanza kusengenya, atazungumzia hili na lile wakati muda unaenda na muda wa kazi ukiisha anafunga kazi na kuondoka. Ukichunguza utakuta tangu asubuhi hakuna chochote alichofanya zaidi ya umbea. Watu wa aina hii wanakuwa wa kwanza kulalamika mishahara ikichelewa. Yapasa watu kubadilika na kutia shime katika ubunifu.

Majumbani na mitaani vilevile nako hapafai. Kwa mfano utakuta mtu ana saluni yake na ana wateja wengi wanasubiri kuhudumiwa lakini wahusika utawakuta wanatumia muda mwingi kusengenya na hivyo kupoteza muda bure. Wale wateja wenye haraka kwa kawaida huwa wanaondoka na kutafuta mahali pengine. Hivyo ikiwa watu watajirekebisha kwa kufanya kazi kwa bidii na kuacha tabia ya kusengenya naamini nchi hii uchumi wake utakua kwa kiwango kizuri na kila mtu atafaidi matunda ya jasho lake.

Ni vema kama mtu hawezi kusema jambo lolote zuri kuhusu mwenzake akakaa kimya, kwani ni njia bora ya kusitiri heshima yake.

Friday, February 6, 2009

WAPO AMBAO HAWAJAWAHI KUONESHWA UPENDO

Hawajawahi kuoneshwa upendo
Kuna mamia kama sio maelfu ya watoto hapa nchini ambao hawajawahi kuhisi upendo hata kidogo kutoka kwa wazazi kama ambavyo wangestahili kuupata. Kuna idadi kubwa ya watoto wanoenda vitandani wakiwa wapweke, wakiwa na njaa, bila ya uhakika wa usalama wa leo na hata kesho.
Sio kwamba watoto hawa wanaishi na watu wengine, hapana, huishi na wazazi wao waliowazaa, lakini wanajua kidogo sana au hawajui kabisa kuhusu upendo.

Kuna wale watoto ambao huenda kukosa upendo huko kunatokana na ugumu wa maisha ambapo wazazi wamelazimika kukimbia nyumba zao katika kuhangaika au hata kujikuta wakiwa jela na kuwaacha watoto hao mikononi mwa dunia, katika mazingira yoyote yawayo ni kwamba kuna idadi kubwa ya watoto wa aina hiyo hapa nchini.

Kama sehemu ndogo tu ya wale miongoni mwetu ambao tumebahatika kuwa na uwezo kidogo tungeamua kutumia sehemu ndogo ya ziada katika mapato yetu na sehemu kidogo ya muda wetu kuwasaidia watoto hawa, tungekuwa tumewaokoa wengi kati yao ambao kwa kawaida huishia mahali pabaya bila hiyari zao.

Hata kama msaada au vitendo vyetu kwa watoto hawa vitakuwa vinaonekana vidogo sana kwetu au kwa wengine kama ilivyo kwa matendo mengine yoyote ya upendo, juhudi hizo zingekuwa hazijapotea bure.

Kwa kadiri ambavyo misaada yetu hiyo ingeonekana midogo, bado ingekuwa ni mikubwa sana kwa kuchanganya na ya wengine.
Hebu jaribu na jitahidi sana kutoa msaada hata mdogo sana pale ambapo unaona wazi kabisa kwamba kuna mtoto mwenye mateso, ambaye una uhakika atafikia umri kama wako akiwa hajui maana ya upendo.

Jaribu kujiweka kwenye nafasi yake uone ni kwa vipi ingekuwa kama ni wewe uliyekosa upendo huo, kumbuka kwamba kizazi kilichopita kiliwezesha kizazi hiki kilichomo kuwepo kwa sababu ya upendo kwa kila binadamu mwingine bila kuangalia nasaba zao.
Hebu jitahudi kwa upande wako kuhakikisha kwamba unasaidia kufanya kizazi kijacho kije kuwepo.

Thursday, February 5, 2009

PAPA HUYU ALIKUWA NI KIBOKO!

Hawa hawakushuhudia vibweka vya Papa Leo wa tano

Papa Leo wa tano. Umeshawahi kumsikia huyu? Basi,alikuwa ni Papa wa aina yake, ambaye alifikia wakati fulani alisema kuwa hakuna Mungu. Alikuwa anapenda anasa usisikie. Kila siku alikuwa akialika marafiki zake kwa ajili ya kula, kunywa na kucheza. Alikuwa akifanya harambee ya kuchangisha fedha kwa ajili ya kufanya anasa, kama vile hakuwa na akili nzuri. Alikuwa akiuza vyeti maalumu ambavyo ati vilikuwa vinamfutia mnunuzi dhambi zake na ambavyo vingemwingiza Peponi. Hiyo yote ikiwa ni kumpatia fedha za kuponda mali. Ndugu yetu, jiulize kuhusu hizo sadaka zako unazotoa, ni mungu au ibilisi? Kwenye hizi imani ni lazima mtu awe makini, kwani dini maana yake sio mtu kuwa kipofu. Kama unataka kujua zaidi kuhusu papa huyu, soma kitabu kiitwacho, “The book of Heroic Failures”.

Tuesday, February 3, 2009

NILISHINDWA KUMSAIDIA ZINDUNA: SEHEMU YA PILI

Hawawezi kupiga kelele kama hivi

Hivi karibuni niliandika habari iliyohusu kifo cha rafiki yangu Zinduna ambacho kilitokana na kujiua kwa kunywa idadi kubwa ya vidonge vya Klorokwini.
Mnamo Januari 24, 2009 ndio alikuwa ametimiza miaka mitatu kamili tangu kufariki kwake.
Niliandika habari ile kama kumuenzi, lakini pia nilikuwa na dhamira ya kutaka kujadili kuhusu tatizo la Depression ambalo kaka Mubelwa Bandio kanisaidia kulitafsiri kwa Kiswahili kuwa linajulikana kama tatizo la Msongo wa mawazo.
Ahsante kaka Mubelwa kwa kunielimisha.

Sababu zinazotajwa kupelekea msongo wa mawazo ni nyingi, lakini kubwa kabisa zinazompelekea mtu kupatwa na msongeko ni hizi zifuatazo;

· Kupoteza ajira au kuwa na wasiwasi wa kupoteza ajira,
· Kuwa na umasikini wa kupindukia kiasi cha kukosa matumaini ya kujikwamua,
· Kutoridhika na hali ya kiuchumi na kushindwa kukabiliana nayo kutokana na shinikizo la watu wanaokuzunguka,
· Migogoro isiyokwisha ya ndoa au ya kifamilia,
· Matukio kama yale ya vifo vya wazazi, kutekelezwa utotoni, udhalilishwaji wa kijinsia na maradhi sugu.

Dalili za msongeko zinatofautiana kati ya mtu na mtu, lakini nitajaribu kutaja chache;
· Kukosa usingizi au kua na usingizi mzito usio wa kawaida. Kukosa raha,
· kujiona ni mwenye hatia,
· Kuwa na wasiwasi, Kuishiwa na nguvu kusiko kwa kawaida, Kukosa hamu ya kula au kuwa na hamu ya kula sana na hivyo kupelekea kupungukiwa na uzito au kuongezeka uzito,
· Kukosa matumaini na kuyaona maisha kama hayana maana,
· Kuwa na mawazo ya kuuwa au kujiuwa ya mara kwa mara na mara nyingi dalili hii inaweza kudumu akilini kwa miaka mingi bila mtu kujua.
· Na hata kama mwathirika anatamka haja ya kufanya hivyo inakuwa ni kama kufanya masihara, kwa mtu asiye elewa, lakini lazima ifahamike kwamba wanaotamka hivyo wamedhamiria.

Mara nyingi watu wanaotamka kutaka kujiuwa au wale wanaofanya jaribio la kutaka kujiuwa ni kwamba wanapiga kelele za kuomba msaada ili wasikilizwe, na kama wakipuuzwa matokeo yake ni kutekeleza kile walichodhamiria.

Wapo watanzania wanaosumbuliwa na tatizo hili la msongeko, lakini labda kwa sababu hatuna takwimu sahihi ndio sababu tatizo hili limekuwa halifahamiki. Wapo watu wengi sana wameuwa au kujiua kutokana na tatizo hili la msongeko, lakini kwa bahati mbaya sana watanzania wengi hulihusisha tatizo hili la msongeko na imani za kishirikina. Kuhusisha hali hii na ushirikina hakuna ukweli wowote na matokeo yake wengi wamejiua na kuuwa kutokana na kutopata tiba muafaka.

Yatupasa sasa kuyaangalia matatizo ya aina hii katika mkabala tofauti badala ya kukimbilia ushirikina, hiyo haiwezi kutusaidia na badala yake itatuletea maumivu zaidi.

Ukweli ni kwamba, kuna wakati dalili za msongeko hujitokeza kwa njia ambayo ni vigumu kwa mtu kujua kwamba mwenzio anakabiliwa na tatizo hili. Hata hospitalini inahitaji wataalamu wazuri sana kubaini baadhi ya dalili na hata wanapobaini bado kuna suala la ugumu wa kutibu msongeko. Huweza kutibu msongeko kwa dawa za hospitalini peke yake bila msaada wa ushauri.

Tukumbuke kwamba wengi wetu tunaishi kwenye maisha ya ushindani na mabadiliko ni ya haraka sana, kuna migogoro mingi ya kindoa na kuvunjika moyo kwingi kimaisha. Hivyo kila mmoja anaweza kuingia kwenye kusongeka.

Kwa upande wa matibabu hakuna matibabu ya moja kwa moja yanayotajwa kutibu msongeko, bali wataalamu wa magonjwa ya akili wanaweza kutoa dawa kulingana na tatizo la magonjwa yanayoonekana. Hata hivyo inapendekezwa mgonjwa kufanyishwa mazoezi ya viungo pamoja na ushauri nasaha au ushauri wa kisaikolojia(psychotherapy)

Kama ukiona mtu wa karibu yako ana msongeko unashauriwa hatua ya kwanza ni kumpunguzia hali ya kutokua na matumaini na kumpa moyo wa subira kwa kuyaona matatizo aliyonayo kama changamoto za maisha.

Pia inashauriwa sana kuwa naye karibu, isitokee hata mara moja akaachwa peke yake. Hata kama inaonekana kukerwa na kile kitendo cha kumchunga na kuwa mkali, hiyo isikutishe na wala usikasirike kwani hizo zote ni dalili za msongeko.

Narudia tena kusema kwamba, watanzania wengi wana msongeko ingawa hawajui. Kujiua kwingi kunatokea sana hivi kunatokana na msongeko. Hata ukisoma ujumbe unaoachwa na wale wanaojiua kama ule ulioachwa na Zinduna unaweza kuligundua jambo hili.

Ujumbe kama vile “nimeona maisha hayana maana”, “ugumu wa maisha umenishinda”, au “hawanitaki hivyo nimeona sina maana” ama “amenikataa na hivyo naondoka nimpe nafasi”.

Lakini kama nilivyosema, yanapotokea haya, maelezo yatakayotolewa ni kwamba, amelogwa. Mara nyingi watu wanaojiua wanakuwa wameshafanya majaribio ya kujiua hata mara mbili huko nyuma, kama tulivyoona kwa Zinduna.

Lakini cha ajabu hakuna anayejali kuchukua hatua za matibabu mtu anapofanya majaribio ya kujiua, kwani huonekana kuwa baada ya kuokoka kwenye jaribio la kujiua hatarudia tena. Hivyo sio kweli.

Monday, February 2, 2009

HAWA NDIO WATUMISHI DUNI ZAIDI-SEHEMU YA PILI

Hakuna wa kuwatetea!

Hivi karibuni shirika la Umoja wa kimataifa linaloshughulika na kuangalia ukiukwaji wa haki za binadamu (Human Right Watch) lilifanya uchunguzi kuhusiana na unyanyaswaji wa wafanyakazi wa kazi za nyumbani katika nchi za El-Salvado, Guantamala, Indonesia, Malasia, Morocco, na Togo.

Katika taarifa ya shirika hilo la Human Right Watch inaelezwa kwamba uchunguzi uliofanywa katika nchi nilizozitaja hapo juu umeonyesha kwamba unyanyasaji wa kimapenzi au kubakwa ndio tatizo kubwa linalowakabili wasichana wanaofanya kazi za ndani katika nchi hizo. Kwa bahati mbaya,wasichana hawa huogopa kutoa taarifa kwa kuhofia usalama wao,kwani wengi ni wahamiaji haramu kutoka nchi nyingine ambao husafiri kwa siri katika nchi hizo kwenda kufanya kazi za ndani kwa ajili ya kusaidia familia zao ambazo nyingi ni masikini.

Kwa mfano katika nchi ya El-Salvador asilimia 15.5 ya wasichana wanaofanya kazi za ndani waliobadili waajiri walikimbia unyanyasaji huu wa kijinsia au kubakwa.

Tatizo lingine linalo wakabili wasichana hawa ni kufanyishwa kazi nyingi kuliko kawaida bila kupata muda wala siku ya kupumzika. Binti mmoja aitwaye SARIHATI mwenye umri wa miaka 17 ambaye ni mhamiaji kutoka Indonesia aliyekwenda kufanya kazi Malaysia aliliambia shirika la Human Right Watch kwamba, alikua anaamshwa saa kumi alfajiri na kuanza kufanya kazi hadi saa moja jioni bila kupumzika. Aliendelea kusema, tangu alipoajiriwa na huyo mwajiri wake hakubahatika kutoka nje pale nyumbani na mwajiri wake huyo alikua na kawaida ya kumpiga mara kwa mara.

“Yule mama mwajiri wangu alikua na kawaida ya kunifokea na kunitukana bila sababu ya msingi na wakatia mwingine hunipiga sana. Nilikua natamani kutoka, lakini ameficha hati yangu ya kusafiria na nilikua naogopa serikali ya Malaysia kwamba angenikamata na kuniweka ndani kama mhamiaji haramu” alisema SIRHATI.

Taarifa hiyo ya Human Right Watch ilibainisha pia kwamba nchi ya Togo ndiyo inayoongoza kwa wasichana wengi kutoka nchini humo kusafiri katika nchi za Benin, Ghana, Nigeria na Niger kwenda kufanya kazi za ndani,wengiwao wakiwa wametoka kwenye familia za kimaskini.

Tatizo hilo la kusafirisha wasichana kutoka vijijini kwenda mjini kufanyishwa kazi za ndani halipo Togo peke yake, hata hapa nchini kwetu limekuwepo kwa mda mrefu. Lakini siku za hivi karibuni limekua kubwa kwani kumeibuka mawakala wanaosambaza vipeperushi maofisini hadi kwenye magazeti wanatafuta wafanya kazi wa ndani.

Mawakala hawa ndio wanao safiri mikoani na kwenda kuwahadaa wazazi wa wasichana hawa na kisha kuwaleta mjini na kuwauza na wengine kufanyishwa shughuli za ukahaba kwenye madanguro.

Tunapoelekea, mawakala hawa hawataishia kuwauza hawa wasichana nchini peke yake kwani kuna uwezekano mkubwa biashara hii kuvuka mipaka na kufanyika nje ya nchi za kiarabu ambapo kuna uhaba wa watumishi wa ndani.

Ninasema huenda itakua hivyo kwa maana ya taarifa rasmi. Lakini ukweli ni kwamba, kwa taarifa zisizo rasmi ni kwamba kuna wasichana wa Tanzania Uarabuni na hata kwenye baadhi ya nchi za Ulaya, ambao ni mayaya na watumishi wa ndani, ambao ni kama watumwa.

Ikumbukwe kwamba familia nyingi vijijini zinaishi katika lindi la umaskini na ndio sababu imekua rahisi kwao kuhadaiwa kirahisi na kuwaachisha mabinti zao shule na kuwakabidhi kwa mawakali hawa matapeli kwa ujira mdogo.

Shirika la kazi duniani (ILO) limeshatoa mwongozo kuhusiana na ajira hii ya watumishi wa ndani.

Kwanza limeagiza kwamba watumishi wote wa ndani wasiwe chini ya miaka 15 na wasiwe wameachishwa shule au wasiwe wamenyimwa furusa ya kwenda shule, na pia ihakikishe kwamba gharama za elimu, yaani ada haziwi kikwazo kwa watoto wa maskini kutopata elimu.

Pili zitungwe sheria mahususi za kuwalinda wafanya kazi hawa wa ndani kwa kuhakikisha wanalipwa mishahara mizuri, wanalipwa saa za ziada ya kazi yaani (over times) mapumziko ya siku moja kwa wiki, na mafao mengine stahili pindi wanapoachishwa kazi.

Tatu kuanzishwe namba ya simu ya bure (Tollfree) kama ilivyo kwa polisi kwa ajili ya kuwawezesha wasichana hawa wakifanyiwa vitendo vya unyanyasaji kutoa taarifa kwenye vyombo vya usalama. Namba hizo zitangazwe kwenye vyombo vya habari mbalimbali kama vile magazetini, redioni, na kwenye runinga.

Nne kuwachukulia hatua kali za kisheria wale wote watakao kamatwa na kukutwa na hatia ya kuwatesa na kuwanyanyasa kijinsia na kuwabaka watumishi wa ndani.

Tano kuwaokoa na kawatoa wasichana hawa mikononi mwa waajiri watesaji na kawapa hifadhi kabla ya kurejeshwa makwao, na kama watakua wameumizwa wameathirika kisaikolojia wapate tiba, kabla ya kurejeshwa makwao.

Iwapo serikali yetu itazingatia mwongozo huu, naamini unyanyasaji kwa watumishi wa ndani utapungua kama sio kuisha kabisa.

Hata hivyo ni vyema pia mawakala wanaotafutia watu, watumishi wa ndani wadhibitiwe wasiwe wanawaachisha watoto shule, na umri wa watumishi wa ndani pia uzingatiwe kulingana na mwongozo wa shirika la kazi duniani(ILO).

Hivi karibuni serikali imetoa muongozo juu ya mishahara ya watumishi hawa, Je mpaka sasa utekelezaji umefanyika kwa kiasi gani?
Je watumishi hawa wanafahamu mahali pa kufikisha kilio chao kama utekelezaji huo haufanyiki?
Je wameelimishwa kwa kiasi gani juu ya haki zao za msingi?

Tunaogopa na kusubiri kitu gani katika kutetea masilahi ya watumishi hawa au ni kwa sababu kila nyumba watumishi hawa wapo, na nyumba za wakubwa zinawatumishi zaidi ya watano. Hivyo kuchokoza ili walipwe vizuri kwa mujibu wa sheria ni kuharibu ‘dili’ zao?


Inabidi tukubali kwamba watumishi wa majumbani ndio watumishi duni na wanaonyanyaswa kuliko wengine hapa nchini. Bahati mbaya hakuna anayewatetea!!!!!!!