Friday, April 24, 2009

JE HUYU NI NANI?

Alikwenda kijijini kumtembelea bibi yake, na hapa alikuwa akielekea Kanisani.



Thursday, April 23, 2009

SHAMBA LA BIBI KOERO


Hili ni shamba la Bibi Koero. Picha hii niliipiga mwaka jana mwanzoni kabla sijaanza kublog, nilipoenda kumtembelea bibi yangu Koero huko Upareni. Nakumbuka nilipofika bibi yangu alifurahi sana, kwani nilikuwa sijaenda kumtembelea kwa takribani miaka mitatu hivi. Kutokana na furaha aliyokuwa nayo, alinichinjia Jogoo mkubwa nikamfaidi peke yangu.
Nimemkumbuka sana bibi yangu, laiti ningekuwa na mabawa ningeruka kama ndege na kwenda kumtembelea bibi yangu Koero.

Wednesday, April 15, 2009

ONGEZEKO LA WATU NA UHARIBIFU WA MAZINGIRA- SEHEMU YA PILI

Eti tunaambiwa tusizaane!
Wiki mbili zilizopita nilizungumzia ongezeko la umasikini duniani, na niliahidi kuwa nikipata muda nitajadili kuhusu ongezeko la watu na uharibifu wa mazingira duniani.

Makala hii ni muendelezo wa makala ya kwanza, bofya hapa kuisoma.
Kwa mujibu wa chapisho hilo, inaonesha kuwa kwa wastani, kila sekunde moja wanazaliwa watoto watano hapa duniani, na wakati huo huo watu wawili wanafariki dunia, achilia mbali zile mimba zinazoharibika.

Maana ya tofauti hiyo kati ya vizazi na vifo ni kwamba watu watatu wanaongezeka duniani kila sekunde moja. Ukizidisha idadi hiyo utagundua kwamba kuna ongezeko la watu 11,000 kwa saa na watu 265,000 kwa siku na hii inafanya dunia kuwa ongezeko la watu milioni 100 kwa mwaka.

Hivi sasa dunia ina watu wapatao bilioni 6.7. Mwaka 1750 kulikuwa na watu milioni 800 tu duniani. Kufikia mwaka 1850 idadi iliongeka na kufikia watu bilioni 1.8.
Mwaka 1950 idadi ya watu ikawa bilioni 2.5. Ilichukuwa miaka 50 idadi ya watu kufikia bilioni 6 yaani mwaka 2000. Inakisiwa kwamba mpaka kufikia mwaka 2010 idadi ya watu hapa duniani itafikia watu bilioni 7, ikiwa ni ongezeko la watu bilioni 1 kwa muda wa miaka 10.
Ukiangalia mtiririko wa takwimu hizo utagundua kwamba idadi ya watu imekuwa ikiongezeka kwa kasi hapa duniani kuanzia karne ya 19.

Kwa mfano nchi yetu ya Tanzania iko chini ya kiwango cha ongezeko la watu hapa duniani ukilinganisha na nchi nyingine zilizoko dunia ya tatu.
Tanzania ina ukubwa wa eneo la mraba mita la 342,100, karibu sawa na Misri ambayo ina ukubwa wa mita za mraba 384,300.

Pamoja na kwamba tofauti ya ukubwa kati ya nchi hizi mbili ni ndogo sana lakini Tanzania imezidiwa kwa idadi ya watu karibu mara mbili na Misri. Kwani wakati Tanzania ikiwa na idadi ya watu wapatao milioni 38, Misri ina idadi ya watu wapatao milioni 71.

Ikiwa utaiunganisha Tanzania na nchi ya Benin iliyoko Afrika Magharibi ukubwa wake utalingana na nchi ya Misri, kukiwa na tofauti ndogo sana. Ukijumlisha idadi ya watu wa nchi ya Benin wanaokadiriwa kufikia milioni 7 na idadi ya watu wa Tanzania unapata idadi ya watu wapatao milioni 45, ikiwa bado ni chini ya idadi ya watu wa nchi ya Misri.

Hii inaonesha bado nchi hii ina kiwango kidogo sana cha idadi ya watu ukilinganisha na nchi nyingine zilizo katika dunia ya tatu.
Kwa hiyo sioni sababu ya serikali yetu kupiga kelele sana kuzuia watu wasizaane, Je tunataka hayo mapori yaliyoenea hapa nchini wakae kina nani?

Kwa mujibu wa takwimu za Umoja wa Mataifa, imekadiriwa kwamba watoto milioni 1.6 huzaliwa kila mwaka hapa nchini. Na kwa mujibu wa takwimu zilizotolewa hivi karibuni na wizara ya afya zinaonesha kwamba watoto wanaosajiliwa ni 140,000 kila mwaka ikiwa ni asilimia 10 tu ya watoto wanaozaliwa, hii inaonesha kwamba kuna idadi kubwa ya watoto wanaofia tumboni, na wale wanaofariki baada ya kuzaliwa inakuwa haijachukuliwa na kuingizwa kwenye takwimu za serikali.
Hata hivyo inakadiriwa kwamba watoto wapatao 51,000 hufariki baada ya kuzaliwa hapa nchini, na wakati huo huo 43,000 hufia tumboni kila mwaka.

Kwa mujibu wa takwimu hizo inaonesha kwamba bado tunayo safari ndefu ya kupunguza idadi ya vifo vya watoto wanaozaliwa hapa nchini, kabla hatujaanza kupiga kelele ya watu kuzaa kwa mpango.

Ni hivi karibuni tumesikia Nchi ya Australia ikipiga la mgambo kuwaalika wahamiaji ili kujaza mapori yaliyo matupu.

Unajua sababu ni nini?

Wenzetu wamepambazukiwa na kung’amua kwamba watu ni rasilimali kama nguvu kazi ikitumika vizuri.
Wakati sisi tunapiga kelele watu wasizaane, wenzetu wanapiga kelele wahamiaji waende wakaijaze nchi, hapa napata kizunguzungu.

Hata hivyo chapisho hilo linabainisha kwamba mataifa makubwa yameanza kuonesha wasiwasi juu ya ongezeko la watu hapa duniani.
Mataifa hayo yanadai kuwa ongezeko la watu linasababisha uharibifu mkubwa wa mazingira, na hivyo kutishia dunia isiwe salama.

Kwani kumekuwa hakuna udhibiti wa kutosha kiasi kwamba watu wamekuwa wakitawanyika kwa ajili ya kutafuta makazi na hivyo kuvamia maeneo ya misitu ya asili na vyanzo vya maji na kufanya uharibifu mkubwa mkubwa wa mazingira.

Imebainika kwamba iwapo watu hao watasogezewa miundo mbinu kama vile Barabara, shule, hospitali, na huduma mbali mbali za kijamii, ina maana ya kuhalalisha uharibifu wa mazingira.

Pia wataalamu hao wanadai kwamba ongezeko la watu haliendi sambamba na ujenzi wa miundo mbinu ambayo itasaidia kulinda uharibifu wa mazingira.

Labda niwaulize ndugu wasomaji, hivi nchi masikini na zile nchi tajiri zenye viwanda ni zipi hasa zinazoifanya dunia hii isiwe salama? Wao wana viwanda wanazalisha sumu kila uchao huku wakitulisha vyakula na madawa yenye sumu ili kujikusanyia utajiri, halafu leo wanasema kuwa nchi masikini ndizo zinazochangia uharibifu wa mazingira na kuifanya dunia isiwe salama, huu ni uonevu wa hali ya juu.

Hebu tuangalie upande mwingine wa shilingi wa kadhia hii.
Kuzungumzia ongezeko la watu, unazungumzia ongezeko la soko, kwa maana ukuaji wa biashara, nguvu kazi, na ongezeko la viwanda, na hivyo ukuaji wa uchumi kuongezeka. Kwani kwa jinsi idadi ya watu inavyozidi kuongezeka na ndivyo uchumi unavyozidi kukua, hebu angalia nchi kama ya China, India, Marekani na iliyokuwa Urusi kabla haijasambaratika, ukuaji wa uchumi katika nchi hizo ulitokana na kuwa na idadi kubwa ya watu.
Ila naomba nitahadharishe kidogo hapa, ninapozungumzia ongezeko la watu na ukuaji wa uchumi nazungumzia nchi kutumia nguvu kazi katika kuzalisha na kuwa na serikali makini inayowawezesha wananchi wake kufikia malengo yao na sio watu kuwa wavivu wakisubiri kila kitu kifanywe na serikali.

Naomba nikiri kwamba aina ya maisha tunayoishi hapa nchini hatuwezi kupiga hatua kimaendeleo hata kama kukiwa na ongezeko la watu. Watanzania tu-wavivu mno kiasi kwama tunashindwa kutumia fursa zilizopo na matokeo yake wageni ndio wanaozichangamkia, huku sisi tukibaki kuwa watazamaji.

Wengi tunapenda njia za mkato katika kujiletea maendeleo na ndio maana vitendo vya rushwa na ufisadi vinaiyumbisha nchi.
Kama tunataka maendeleo ya kweli yatupasa kubadili namna yetu ya kufikiri, la sivyo tutazaana na kujikuta tukibaki kuwa ombaomba ndani ya nchi yetu.

Katika kipindi hiki ambacho dunia imetikiswa kutokana na kuyumba kwa uchumi duniani, inabidi kila mtu ajiulize afanye nini ili kujiletea maendeleo na sio kukaa na kulalamika na majungu, haitatusaidia zaidi ya kupoteza muda huku dunia ikiendelea kusonga mbele kwa kasi ikikuacha ukiwa umesimama.

Thursday, April 9, 2009

AMADOU NA MARIAM: WAO WAMEWEZAJE?

Pamoja na kwamba ni walemavu wa kuona lakini wameweza.

Ni katika viunga vya Bamako nchini Mali ndipo historia ya wanamuziki hawa wawili vipofu, mtu na mkewe ilipoanzia na kusambaa, kuanzia kule nchini Burkina fasso, Ivory Coast, Asia, Ulaya na America.
Wanamuziki hawa ni Amadou na Mariam ambao ambao wanazidi kuishangaza dunia kutokana na umahiri wao kimuziki.
Historia inaonesha kwamba wanamuziki hawa, Amadou Bagayoko ambaye ni mpiga gita na mwimbaji, aliyezaliwa mwaka 1954, katika jiji la Bamako nchini Mali na
Mariam Doumbia ambaye ni mwimbaji mahiri aliyezaliwa mwaka 1958, walikutana katika chuo cha vijana wasioona, wakiwa wanafundishwa stadi mbalimbali za maisha ambapo walijikuta wote wakiwa na kipaji cha muziki.

Mnamo mwaka 1974, Amadou alianza kupiga muziki na bendi ya Les Ambassedous Du Hotel.

Kufikia mwaka 1980, Amadou alioana na Mariam na wakati huo huo walianzisha bendi yao wenyewe pamoja na chuo cha kufundishia muziki kwa wale wasioona.

Hadi kufikia mwaka 1985 wanandoa hawa walikuwa wamejijengea umaarufu mkubwa kwa muziki wao wa Blues wenye vionjo vya gitaa Rock, mirindimo ya Violin yenye asili ya Syria na vyombo mbali mbali vya muziki vyenye asili ya Cuba, Misri, Columbia na India. Vyombo vyote hivyo kwa ujumla wake vilileta ladha ya muziki wa Afro Blues.

Ziara yao ya kwanza, nje ya Mali ilikuwa ni ile ya kitembelea Burkina Fasso mwaka 1986, na baadae Ivory Coast ambapo walikaa kwa miaka 7 na kufanikiwa kurekodi kaseti zipatazo 5.

Kaseti hizo ziliuzwa sana na kuwajengea umaarufu Afrika Magharibi na hivyo kupata wafadhili ambao waliwapeleka nchini Ufaransa kurekodi santuri ambayo iliwatangaza dunia nzima na kuwafanya kupata mialiko ya kwenda kutumbuiza kwenye matamasha mbali mbali ya muziki duniani.

Mnamo mwaka 2003 wanamuziki hawa walikutana na mwanamuziki maarufu wa Kilatini Manu Chao ambaye aliwasaidia kutengeneza santuri yao maarufu ya Dinanche a Bamako ikiwa na maana ya Jumapili ndani ya Bamako ambayo nayo iliuzwa sana.

Wakati wa Kombe la Dunia mwaka 2006 nchini Ujerumani, wanamuziki hawa kwa kushirikiana na mwanmuziki wa Ujerumani Herbert Gronermeyer walirikodi wimbo maalum wa kombe la dunia ambao ulishika namba moja katika vituo vya Redio vya

Ujerumani na hivyo kuzidi kujijengea umaarufu mkubwa katika maisha yao ya muziki. Wanamuziki hawa wamefanikiwa kutoa santuri 7 ambazo zote zimewaletea mafanikio makubwa.

Ukweli nikwamba wamepitia katika mazingira magumu kwa kiasi fulani hadi kufikia katika kilele cha mafanikio waliyo nayo sasa. Kuna wakati iliwalazimu kuhamia Ivory Coast ili kutafuta soko la muziki wao.

Katika mahojiano waliofanyiwa hivi karibuni walikiri kwamba, chuo cha vijana wasioona walichosomea ndio chanzo cha wao kufahamiana na kuibua vipaji walivyonavyo katika muziki.

Walisema kwamba hiyo ndio iliyosababisha wao kuanzisha chuo chao cha kuwafundisha vijana wasioona muziki.

Hii inadhihirisha kwamba ni kwa kiasi gani wenzetu waliona umuhimu wa kuwawezesha watu wenye ulemavu, hasa wenye ulemavu wa kuona.

Sasa hivi kuna vijana wengi walemavu wanaozurura hovyo mitaani nchini kwetu na hata wengine kufikia kuwa ombaomba kwa sababu hawakufundishwa staidi za maisha na wala hawakuandaliwa mazingira mazuri ya kujiajiri.

Ukweli ni kwamba tunavyo vyuo vichache sana vinavyofundisha staidi za maisha kwa watu wenye ulemavu ambavyo vingi vinamilikiwa na taasisi za kidini, Idadi ya vyuo hivi hailingani na idadi ya walemavu walioko hapa nchini.

Katika karne hii ya sayansi na teknolojia ilitakiwa ile dhana ya kuona kwamba ni mkosi kuzaliwa mtoto mlemavu katika familia iwe imefutika, kwa sababu siku hizi kuna nyenzo nyingi zilizogunduliwa ambazo ni rahisi kutumiwa na walemavu katika kuzalisha mali na kuchangia pato la taifa, badala ya kuiacha nguvu kazi hii kupotea bure.

Amadou na Mariam licha ya kuwa ni walemavu wasioona wametoa ajira nyingi kwa vijana wa nchini Mali kupitia muziki wao.

Hata hapa nchini kwetu, iwapo serikali itafungua vyuo vingi kwa ajili ya walemavu ili wafundishwe staidi za maisha na kuandaliwa mazingira mazuri ya kujiajiri, kuna uwezekano mkubwa wa kuibua vipaji na kupunguza ukali wa maisha kwa ndugu zetu hawa wenye ulemavu.

Si vyema watu hawa wakipuuzwa kwani kila mtu ni mlemavu mtarajiwa, hujafa hujaumbika.

Wednesday, April 8, 2009

NIKIKOSEA MNIVUMILIE

Hata hizi ziliwahi kukosewa

Wakati mwingine ukikuta kuna makosa ya herufi kwenye Blog hii, naomba uyavumilie, kwani hilo ni kosa la kiuchapaji tu. (Typing error)


Kama hutaki kukubali kama hilo ni kosa la kiuchapaji, basi ngoja nikwambie ni kwa nini.


Mwaka 1985 , Yugoslavia ilitoa noti mpya. Katika noti hizo kulikuwa na picha ya Rais wa zamani wa nchi hiyo, Hayati Josip Broz Tito (7 May 1892 - 4 May 1980). Lakini tarehe ya kifo chake kwenye noti hizo ilikuwa imekosewa.


Hebu niambie, noti ina maandishi gani mengi hadi ikosewe tarehe? Lakini hebu niambie inabidi watu wangapi waipitie noti hiyo kabla haijaidhinishwa kuchapwa?


Naamini ni watu wengi tu waliipitia lakini bado ilikosewa!


Naomba mnivumilie kwa mcharazo….

Sunday, April 5, 2009

JE HILI NALO LISEMWE NA NANI?

Tunavumilia mengi

Ni siku ya Ijumaa niko ofisini kwangu nimekaa nikiendelea na kazi zangu kama kawaida mara napata mgeni. Mgeni huyu ni rafiki yangu Farida mwenyeji wa kule Arusha niliyesoma nae kidato cha tano kule Morogoro, ingawa baadae mimi nilihamia shule ya binafsi hapa jijini Dar es salaam na kumuacha rafiki yangu kule Morogoro akiendelea na kidato cha sita.

Ni takribani miaka mitatu imepita bila kuonana na rafiki yangu huyu kwani kwa mara ya mwisho tulikutana pale baraza la mitihani mwenge wakati tulipofuatilia result slip zetu.

Ilikuwa ni furaha isiyo kifani kukutana na rafiki yangu huyu ambaye wanafunzi wenzetu walikuwa wakituita pacha wakidai eti tunafanana. Tangu wakati huo tulipoachana pale baraza la mitihani hatukuwahi kuonana wala kuwasiliana.

Nilimuuliza Farida kwamba yuko wapi na anafanya nini? Simulizi zake ndio zilizo nifanya nipate mada ya kuweka humu bloguni leo. Ukweli ni kwamba jambo ninalotaka kuzungumzia si geni sana kwa wasomaji wa blog hii, kwani ni jambo ambalo lipo sana, labda tu niseme kuwa siku za hivi karibuni limezidi kukua tena kwa kasi ya ajabu. Nimeona kama tusipolisemea sisi wanawake, hali inaweza kuwa mbaya sana hapo baadae.

Baada ya kumaliza kidato cha sita Farida hakupata alama nzuri za kumuwezesha kujiunga na chuo kikuu, lakini hata hivyo aliamua kujiunga na chuo cha Kimoja maarufu hapa jijini (Naomba nisikitaje) ili kusoma masomo ya biashara na masoko.
Chuoni hapo Farida alikutana na unyanyasaji mkubwa wa kijinsia, ambao ni vigumu mtu kuamini ukisimuliwa. Vinara wakubwa wa unyanyasaji huo wa kijinsia ni walimu, kwani wakimtaka mwanafunzi hawatarajii kukataliwa na kama mwanafunzi akimkataa mwalimu atarajie kufeli katika somo la mwalimu huyo.

Farida anabainisha kuwa kuna ushirikiano mkubwa miongoni mwa walimu katika kuwafelisha wanafunzi jeuri wasiokubali kutoa penzi kwa walimu hawa wakware, na cha kushangaza hata walimu wa kike ambao ndio wangekuwa msaada kwao lakini hali haiko hivyo nao wanashirikiana na walimu wa kiume kuwakandamiza wanafunzi wa kike.

Ingawa amefanikiwa kumaliza na kufaulu lakini haikuwa rahisi sana kwani ilimlazimu kurudia masomo mawili zaidi ya mara mbili ili kuweza kufaulu. Naamini wote mtakubaliana na mimi kuwa unyanyasaji wa kijinsia upo sana, na sio tu kwenye Elimu bali pia kwenye ajira kuanzia serikalini hadi kwenye sekta binafsi kote huko hapafai kumechafuka ile mbaya.

Swala hili limekuwa ni gumu kushughulikiwa kisheria kutokana na matukio mengi ya namna hii kutoripotiwa katika vyombo vya dola kutokana na kwanza Polisi wetu kutoyapa uzito unaostahili matukio ya namna hiyo na pia waaathirika kuona aibu kuripoti juu ya udhalilishwaji wanaofanyiwa kwa kuhofia swala hilo kuripotiwa kwenye vyombo vya habari na hivyo kuogopa kuchekwa na jamii. Tatizo lingine ni mazingira ya kupatikana kwa ushahidi wa kutosha wa kuwatia hatiani wahusika kutokana na vitendo hivyo kufanywa kwa usiri mkubwa.

Inapotokea mwalimu anamfanyia mwanfunzi wake vitendo vya unyanyasaji kijinsia au kumbaka, inakuwa ni vigumu kwa mwanafunzi kutoa taarifa kwa sababu anamuona mwalimu kama ndiye ameshikilia mustakabali wake wa maisha kielimu.

Kusema ukweli athari ni kubwa sana kuliko tunavyofikiria kwa sababu wanafunzi wengi wa kike wanaathirika kwa kupata ukimwi, au maradhi mengine ya zinaa au kupata ujauzito na kuachishwa shule, na matokeo yake wanafunzi hawa huumia ndani kwa ndani na kupata matatizo mengi ya kiakili.

Hata wakuu wa shule au vyuo vyenye unyanyasaji huu wa kijinsia wakiulizwa mara nyingi hukanusha vikali kuwepo kwa tatizo hilo katika shule zao au vyuo vyao, zote hizo zikiwa ni juhudi za makusudi kulinda umaarufu wa shule au chuo husika.

Hebu muulize mwanamke yeyote wakiwemo wale ambao wanashikilia nafasi za juu serikalini kuhusu jambo hili, kama hutashangazwa na kile utakachosikia kutoka kwao, utakuta kama hawakukutana na udhalilishwaji wa kijinsia walipokuwa shule ya msingi, sekondari au chuoni basi itakuwa ni katika ajira, kote huko hapafai, hali ni mbaya kweli kweli. Sasa sijui na hili gonjwa la ukimwi, tutapona kweli?

Nilipoamua kujiajiri niliangalia mambo mengi na hili likiwemo, ingawa mimi haikunitokea kwa kiwango cha Farida lakini pia nilijikuta nikiwa na wakati mgumu wakati fulani, nikitakiwa rushwa ya ngono ili nipate ajira ( rejea makala yangu ya
JAMANI HIVI HALI HII MPAKA LINI?)
Ukweli ni kwamba kuna aina nyingi za unyanyasaji wa kijinsia lakini nitaelezea aina tatu za unyanyasaji wa kijinsia ambao ndio ulioshika kasi hapa nchini.

Aina ya kwanza ni unyanyasaji wa mwanamke kuombwa rushwa ya ngono. Hapa mwanamke analazimika kumkubali mwanaume ili apate haki yake. Kwa maana kwamba mwanaume ananufaika kwa kumpata mwanamke ili amsaidie kupata huduma fulani ambayo ni haki yake.
Aina ya pili ni ile ya kumnyima raha mwanamke kwa kumnyanyasa mara kwa mara au hata kumpa adhabu isiyostahili kwa kosa dogo , kwa sababu tu alimkataa mhusika kimapenzi.
Aina hii hutokea sana mashuleni na vyuoni, na hii inawaathiri sana wanafunzi wa kike kisaikolojia, kwa sababu uwezo wao kimasomo unashuka na wakati mwingine kushindwa kuendelea na masomo.
Aina ya tatu ni ile ya kumtomasatomasa, kumbusu, kushika sehemu za siri au hata kumfanyia mwanamke vitendo vya kimapenzi bila ridhaa yake. Vitendo vya namna hii mara nyingi vinafanyika kama utani, hasa huko maofisini.
Mara nyingi mwanamke anayefanyiwa vitendo vya namna hii asipoonesha kukerwa ndivyo mhusika atakavyoendelea kumfanyia vitendo vya udhalilishaji zaidi, ambapo kuna uwezekano mkubwa wa kumfedhehesha ndani ya jamii .
Unaweza kushangaa kuona kwamba miongoni mwa waathirika wa unyanyasaji wa aina hii ni wake za watu ambao wameshindwa kujistahi kwa kutoweka mipaka ya utani. Unyanyasaji wa aina hii unaweza kuepukwa kabisa kama sio kukomeshwa kabisa iwapo tutaweka mipaka ya utani.
Kujistahi ni jambo la heshima sana na mwanamke yeyote anayeweka msimamo wake wazi kwa kumkemea mwanaume yeyote anayejaribu kumfanyia vitendo vya udhalilishaji wa aina hii, bila kujali kuwa ni mwalimu wake au mkubwa wake kikazi, anakuwa anajijengea heshima kubwa.