Sunday, November 29, 2009

HE, ETI WAZEE HAWAPENDI KUVAA CONDOM!

Naomba muniwie radhi kwa kile nitakasimulia hapa leo, maana inawezekana nisiwafurahishe baadhi ya wasomaji wa blog hii au wanablog wenzangu. Ni jambo ambalo nililitafakari sana kabla hata sijaamua kuliweka humu nikaona ni bora niliweke ili niwashirikishe wadau wa blog hii.

Jana majira ya jioni nilitoka na shoga yangu kwende kupata mtori katika mgahawa ulioko jirani na nyumbani. Nakumbuka ilikuwa ni majira ya saa kumi mbili za jioni hivi. Wakati tunaendelea kula mtori wetu mara wakaja akina dada wawili ambapo walikaa katika meza iliyoko jirani na meza tuliyokaa.
Walikuwa wakicheka kwa furaha kuonesha kuwa ni marafiki ambao aidha walipoteana siku nyingi au walikuwa wanapeana habari kama ilivyo kawaida ya kina dada kila wakutanapo.

Hatukuwajali na tuliendelea na stori zetu, lakini nilijikuta nikivutiwa na mazungumzo yao. mmoja wa wale kina dada alikuwa akimasimulia mwenzake jambo fulani ambalo lilinivutia kulisikiliza. Hebu ngoja niwamegee kile nilichosikia kama kilivyo, sitapunguza wala kuongeza ili nisipunguze utamu maana kwangu mimi simulizi ile ilikuwa ngeni kwangu.

Yule dada alikuwa akimsimulia mwenzie juu mambo yaliyomkuta juma lililopita, na simulizi yake inaanza kama ifuatavyo:

Basi, mwenzangu huku kula kwangu vichwa, jana si yakanikuta ya kunikuta......
Hee! bibi wewe ni yapi hayo yaliyokukuta tena? Aliuliza mwenzake waliofuatana naye.
Yule dada akaendelea kusimulia mkasa wenyewe, Si unajua mishe mishe zangu za kutafuta mishiko {Nadhani Fedha} basi juzi mida ya usiku majira ya saa tatu nikazama zangu Club, na kwa kuwa nilipigika ile mbaya nilikuwa nimepania kuwa ni lazima nisitoke kapa, ile natia maguu tu maeneo ya viwanja mara ikasimama Toyota Hurrier moja nyeupe jirani na niliposimama kwenye kiosk kimoja ili kununua zana si uanjua huwezi kwenda vitani bila silaha...... mara kioo kikafunguliwa, na mzee mmoja hivi wa makamu ambaye ndiye aliyekuwa akiendesha lile gari aliniita, nilisita kidogo, unajua mie siwahusudu sana mablakii wa kibongo kwa kuwa hawakati mshiko wa maana, nilijivuta hadi pale aliposimama yule mzee, aliniomba nipande kwenye gari ili tuzungumze, nilimuuliza tunaenda wapi, aliniambia kuwa tunakwenda kupata chakula cha usiku mahali kama kampani tu. "Sikiliza mzee mie niko kazini kama ni biashara sema una kiasi gani, sio mambo ya misosi, kwani mie nilikwambia nina njaa?" nilimwambia kisha nikaanza kuondoka kwa madaha, akaniomba nirudi tumalizane, na niliporudi akaniuliza nitahitaji kiasi gani, nikamtajia kiasi kikubwa cha hela nikidhani atashindwa, akaniambia powa twen zetu......basi tukaondoka zetu

Yule mzee alinimbia kuwa anayo nyumba yake maeneo ya mbezi beach na ndipo tunapokwenda kupumzika, alionekana ni mtu wa heshima na aliyekuwa akiongea kwa upole, aliendesha kwa kasi na alikuwa haongei alikuwa amefungulia muziki wa kizungu wa taratibu kwa sauti ya juu kidogo. tulipofika alipiga honi geti likafunguliwa na mlinzi, tukaingia ndani na kupaki gari kisha tukashuka na kuingia ndani, lilikuwa ni jumba la kifahari hasa. Tulipoingia pale sebuleni nilikuta kuna sofa nzuri za maana na kulikuwa na Bar, yule mzee aliingia pale Bar na kuchukua whisky na barafu na kujimiminia kisha akanimiminia na mimi, nilikataa na kumwambia kuw napendelea Ram badala yake, aliingia kwenye ile Bar na kunichukulia Bacard na Coke na glass ya barafu na kuniletea.

Yule mzee alikuwa akiifakamia ile Whisky kwa kasi ya ajabu kama vile alikuwa akiwahi mahali, anishika mkono na kuniingiza chumbani kwake, nilimuuliza kuwa mkewe yuko wapi, aliniambia kuwa hainihusu na nisitake kujua juu ya mkewe, alikuwa akiongea kwa hasira kama vile tumegombana vile, alinitupa kitandani na alinivamia kama nyati aliyejeruhiwa pale kitandani,.....nilianza kuogopa, nikamuomba atulie nivue mwenyewe...Shoga yangu wee kwani alinisikia, nilibaki kimya kusubiri kitakachotokea, lakini nilishtuka nikamuuliza kama anazo Condom, maana sikuwahi kujinunulia pale kwenye kiosk, akaniambia kuwa hana Condom na hayuko tayari kuvaa condom kwa kuwa sio utamaduni wake,

"Hee mwenzangu ulikuwa hujui...Wazee huwa hawapendi kuvaa condom, kwani hata mie yaliwahi kunikuta pia, tena mara tatu,mie sivitaki kabisa vizee," alidakia mwenzie.

Basi mwenzangu niliogoppa ile mbaya,ikabidi nimuombe anipa pesa yangu kabisa tuliyopatana, yule mzee akanyanyuka na kwenda kabatini, nikajua amefuata pesa, mara akarudi akiwa na Bastola mkononi, niliogopa nusura nizimie, kisha akaniambia kwa ukali. "Sikia wewe malaya, ukileta ubishi nitakuua na hakuna atakayeuona mzoga wako, usiniletee masihara kabisa, unasikia?" aliongea kwa ukali na alionesha kabisa alidhamiria kunifanyia unyama, nilitulia kama maji mtungini, kwanza sikujua nipo wapi na hata sijui akinitoa hapo nje nitaelekea wapi. Alinifanyia alivyotaka tena pekupeku, nakwambia, dada hakunibakisha si mbele wala nyuma, nilikuwa namuomba mungu amalize hamu yake anirudishe aliponitoa.

Alimaliza nakuniruhusu nikaoge kisha anirudishe aliponitoa, niliingia bafuni na kuoga harakaharaka ili niwahi kuondoka maana niliogopa asije akanirudia tena. Basi shosti nilipomaliza nilivaa haraka haraka bila hata kujipodoa na nilipotoka pale sebuleni nilimkuta ametulia akiangalia TV huku akiendelea kunywa whisky yake taratibu.

Tuliondoka pale na kunirudisha pale kijiweni kwangu, ambapo pia alinipa mshiko wangu kama tulivyopatana, yaani nakwambia hata sikuona kama ile hela ina maana kwangu, nilijuta na kujiona kama mjinga kumkubalia yule mzee, kwani sina uhakika kama hajaniachia miwaya, maana alikuwa hana wasiwasi wakati anajua wazi juu ya shughuli yangu ya kujiuza.

"Shoga sasa si ukapime ujue afya yako?" Alishauri mwenzie...
" Nyoo akapime nani? Mie? Thubutuu, haki ya nani sithubutu! ya nini nipime nijiuwe bure kwa presha".

Waliendelea kusimuliana uchafu wao na sie tukaondoka mahali pale, lakini moyoni nilikuwa na maswali kadhaa niliyokuwa nikijiuliza, juu ya ile shughuli waliyokuwa wakiifanya wale mabinti ambao kwa mtazamo wangu wangeweza kujiajiri na kujipatia kipato cha kuwawezesha kujikimu. Kingine ni kile walichodai kuwa wazee hawapendagi kuvaa condom, swali la kujiuliza, hivi wake wa wazee wenye tabia hizi ziko salama kweli? Na je ni wazee au hata vijana wangapi wenye tabia hizi ambao wamepoteza maisha na kusababisha mayatima na wajane kuongezeka na kuwa mzigo kwa jamii na serikali?

Kusema kweli nilivutiwa sana na simulizi ile ambayo kiukweli ilikuwa hainihusu, ila kutokana na umbeya wangu nimeona niwamegee wanablog na wasomaji wenzangu ili tutafakari kwa pamoja.

Thursday, November 26, 2009

NAJARIBU UPANDE WA PILI-VUKANI NDANI YA KWANZA JAMIII........

Wengi watanisoma humo

Rafiki yangu Markus Mpangala aliwahi kunishauri kuwa niwe muandishi wa habari, nikakataa wazo lake, lakini siku za hivi karibuni nimevutiwa sana na Gazeti la Kwanza Jamii na nimeona nitume Vijimakala vyangu humo, ili sauti yangu ya nyikani iwafikie wengi..........

Monday, November 23, 2009

TUMEMUENZI VIPI HAYATI HUKWE NZAWOSE?

Hayati Hukwe Nzawose

Ahsante kaka Mubelwa kwa kunipa Link ambayo imeeleza kwa muhtasari maisha hadi kifo cha msanii huyu Hukwe Nzawose.

Kusema ukweli sikufahamun kama Hukwe Nzawose amekwisha fariki siku nyingi kiasi hicho, sijui ni kutofuatilia kwangu habari, au msiba wake haukupewa uzito unaostahili kwenye vyombo vyetu vya habari.

Lakini nina maswali kadhaa ambayo ningependa kupata majibu:

Je Serikali yetu iliwahi kumtunukia nishani yoyote ya heshima Dr. Hukwe Nzawose, kabla na baada ya kifo chake?

Je kazi zake zinatumika vipi katika kutangaza utamaduni wetu hapa nchini na hata nje ya nchi?

Je kuna mnara wowote wa kumbukumbu ambao umejengwa kule Bagamoyo kuonyesha kuthamini mchango wake pale chuo cha sanaa Bagamoyo?

Mwisho naomba nitoe changamoto kwa wasomi wetu, kwamba kuna haja ya wao kukaa chini na kuandika historia ya mtu huyu ili iwe ni kumbukumbu kwa vizazi vijavyo.

Saturday, November 21, 2009

ETI HUYU NI NANI?

Huyu ni nani?

Ndugu wasomaji, leo nilikuwa nachungulia mtandaoni nikajikuta nikivutiwa na hii picha ya huyu jamaa, naambiwa kuwa eti ni Mtanzania na anaishi ughaibuni. Mnaomfahahamu, naombeni mnijuze.....Huyu ni nani?

Wednesday, November 18, 2009

NIKAPIGIWA “EMCHEKU”

Usiku ndio muda muafaka

Ni usiku wa saa tatu hivi, niko kijijini kwa bibi Koero, na tuko jikoni tunaota moto, huku akinisimulia simulizi mbalimbali juu ya maisha. Bibi Koero ni hodari wa kutoa simulizi zenye kufundisha na za kusisimua.

Tukiwa katikati ya mzungumzo, mara tukasikia michakato ya miguu huko nje kuashiria kuwa kuna mtu huko, “Emcheku aha” ilikuwa ni sauti ya kiume kutoka nje, bibi aliniambia nitoke ili kuangalia kuwa ni nani.

Nilipotoka, kwa kuwa kulikuwa na giza, niliona kivuli cha mtu, lakini alikuwa na kurunzi yenye mwanga hafifu, na alikuwa akiiwasha na kuizima, nilirudi ndani kwa hofu na kumweleza bibi Koero mauzauza niliyokutana nayo huko nje.

Bibi Koero alicheka sana, na kuniambia kuwa, huyo ni mgeni wangu, kaja pale kuposa, na mlengwa ni mimi kwa kuwa hakuna binti mwingine pale nyumbani bali ni mimi.
Nililishangazwa na aina ule ya posa, kwangu mimi ile ilikuwa ni habari, na ili kujua mengi zaidi, nilimdadisi bibi Koero ili anisimulie juu ya utaratibu huo.

Bibi Koero anasimulia kuwa enzi zao, binti akivunja ungo, vijana huanza kufika pale mida ya usiku kupiga hiyo “Emcheku” inawezekana wakafika zaidi ya wavulana kumi kwa usiku mmoja kulingana na uzuri na tabia ya binti huyo.
Emcheku ni salaam ya heshima anayotoa mvulana anapokwenda kuchumbia.

Kwa kawaida wavulana hao wakifika kila mmoja kwa muda wake na kupiga hiyo Emcheku, Binti husika huambiawa atoke nje kuonana na mvulana huyo na kama hajampenda basi humweleza na huyo kijana huondoka zake, na akitokea mvulana anayempenda, basi hupewa ruhusa na binti huyo ili alete Posa na hapo ndio milango hufunguliwa kwa mvulana huyo kumtembela mchumba wake.

Mara nyingi matembezi hayo hufanywa usiku na mvulana akifika binti huruhusiwa na wazazi kutoka nje ili kuzungumza na mchumba wake, lakini walikuwa hawaruhusiwi kukutana kimwili au kuonjana mpaka utakapofika muda muafaka watakapofunga ndoa takatifu.

Tofauti na zamani, bibi Koero, anasimulia kuwa, siku hizi vijana wamebadilika sana na wengi wameuharibu utaratibu huo na kuugeuza kuwa kichaka cha kufanyia ngono. Wavulana siku hizi kama anamtaka binti, hupiga hiyo Emcheku na binti akiridhia, humhadaa, mpaka amuonje na akifanikiwa kuingia mitini na posa inaota mbawa.

Unaweza kukuta mvulana anawahadaa wasichana zaidi ya kumi lakini aisoe hata mmoja baada ya kuwaonja.

Wasichan nao wamekosa subira, kila wakisikia hiyo emcheku, wanajua kuwa ni bahati imewajia, kumbe hakuna lolote ni wavulana mafisadi tu wenye uchu wanataka kuwaonja na kisha kutoweka.

Sasa sijui na mimi nilipigiwa hiyo emcheku ili kuonjwa……LOL

Sunday, November 15, 2009

MUNGU ALINIONYESHA MSIBA ULE!


Kwanza ningependa kuchukua nafasi hii kuwashukuru wasomaji na wanablog wenzangu wote mlionipa pole kwa msiba uliotupata. Kusema kweli kama walivyosema baadhi ya wanablog kuwa ule ulikuwa ni msiba wa taifa kwani roho za watu zaidi ya 20 zimepotea wakiwemo watoto ambao bado walihitaji kuishi na kutimiza ndoto zao.

wakati mwingine unaweza kukufuru mungu kw kuhoji kile kilichotokea, lakini kama maandiko matakatifi katika vitabu vya dini hususana hizi dini zetu mbili ambazo ndizo dini kuu hapa nchi yaani ukristo na uislamu, vilivyoeleza kuwa yote mema na mabaya yanatoka kwake yeye na hatupaswi kuhoji mamlaka yake.
Lakini kama si hivyo naamini tungekuwa tunamlaani sana Mungu pale tunapoondokewa na wapendwa wetu.

Ukweli ni kwamba msiba ule uliotupata nilionyeshwa kabisa na mwenyezi Mungu katika njia ya ajabu sana. Ni kiasi cha wiki nilikuwa nasumbuliwa na malaria kiasi cha kulazwa Hospitalini na kutundikiwa Drip za Kwinini. Nakumbuka siku mbili kabla yakupata msiba ule niliota ndoto ya kustaajabisha sana, niliota kuwa nimeenda kijijini kwa bibi Koero kumtembelea na nilipofika kule kijijini nilipokewa na bibi Koero lakini hakuwa na furaha sana kama nilivyokuwa nimemzoea, nilipomdadisi sababu ya kutofurahishwa na ujio wangu, alinijibu kwa kifupi tu kuwa anajisikia vibaya.

Siku iliyofuata aliniomba nimsindikize shambani kwake ili akanioneshe mazao aliyolima, tulipofika shambani nilishangaa kukuta matuta mengi ya viazi vitamu yakiwa yamestawi barabara, niliruka kwa furaha, kwani mimi huwa napenda sana viazi vitamu, bibi alionekana kunishangaa, nilipomdadisi kuwa kwanini haonekani kufurahia mazao yake, aliniambia kuwa, sina haja ya kufurahia kustawi kwa vile viazi kwani havina ishara nzuri katika familia yetu. nilimdadisi anifafanulie maana ya kusema vile, aliniambia tukae chini anieleze.

Aliniambia kuwa hapo zamani enzi za mababu zao, ilikuwa kama mtu akilima viazi kisha vikastawi sana na kuonesha ishara ya mavuno ya kutosha, waliamini kuwa hiyo sio ishara nzuri katika familia husika, kwani ni lazima pangetokea maafa makubwa au kupata msiba wa mtu mzito katika familia, kwa hiyo hata yeye hawezi kufurahia kustawi kwa yale mazao kwani sio ishara nzuri katika ukoo wetu.

Nilijikuta nikilia kwa sauti, baada ya kusimuliwa habari ile na bibi Koero, nilishtuliwa na mama, alipokuja kuniamsha baada ya kusikia kilio changu. Ilikuwa ni saa kumi za alfajiri, nilimsimulia mama na bada ya kumweleza juu ya ile ndoto aliniambia kuwa sina haja ya kuamini kwani ni mambo ya kishetani, hata hivyo tulisali na mama kisha nikarudi kulala, lakini sikupata usingizi kutokana na kuogopa, ikabidi niamke na kuanza kusoma mtandao na baadae ndio nikaandika ile habari ya siku ya kufa kwangu, nilijikuta tu nikiandika na kuiweka hapa kibarazani kwangu.

Jioni nilipata email kutoka kwa kaka Shabani, Mzee wa Utambuzi. Email yake ilinifumbua macho na kuuona ukweli mpana zaidi, kwamba ile makala yangu haikuashiria jambo jema. kwani baada ya kusoma ile makala yangu niliyoipa kichwa cha habari kiisemacho SIKU YA KUFA KWANGU, kaka Shabani aliniandikia akiniambia kuwa ile makala imemtisha sana na aliniambia kuwa haiashirii jambo jema. Alitaka kujua zaidi hali yangu na pia kujua niliwaza nini mpaka kuandika makala ile.

Sikuweza kumjibu kutokana na kutingwa, lakini siku iliyofuata wakati najiandaa kumjibu na labda kumtaka ushauri juu ya ile ndoto niliyoota ndipo tukapokea taarifa za maafa yaliyotokea kijijini kwa mama ya kuporomoka kwa mlima kulikosababishwana mvua kubwa na kusababisha vifo vya watu zaidi ya 20 wakiwemo shangazi na mjomba wake na mama pamoja na watoto wao.
Ulikuwa ni msiba mzito sana kwetu kwani alikuwa ndiye shangazi yake mama pekee aliyebaki, baada ya shangazi zake watatu kufariki miaka kumi iliyopita.

Safari yetu nayo ya kuelekea msibani iligubikwa na mauzauza mengi, kwani wakati tunakwenda, mimi ndiye niliyekuwa nikiendesha gari na tulipofika Korogwe kwenye kona za msambiazi niligonga Kondoo ambapo alikufa pale pale, nilibabaika kidogo ikabidi dada yangu anipokee na kuendesha yeye.

Leo wakati tunarudi tulisimama Korogwe ili kupata chakula cha mchana, na baada ya kupata chakula tukarejea kwenye gari ili kuendelea na safari, ni hapo ndipo tukagundua kuwa kitasa cha mlango kimevunjwa na mkoba wa mama uliokuwa na fedha, simu zake mbili za mkononi na Kamera umeibwa, tulijaribu kuwauliza watu waliokuwa jirani na gari letu, lakini hatukupata ushirikiano, tuliamua kuondoka lakini tulipofika ya maeneo ya Kwedikwazu, mdogo wangu Jarome ambaye ndiye aliyekuwa akiendesha gari akagonga mnyama jamii ya kicheche au sijui ni fungo, hata sijui alikuwa ni mnyama gani maana alikuwa akiendesha kwa spidi kubwa kidogo. Ilibidi tumshauri apunguze mwendo hadi tukafika Dar.
Kilichotuuma ni kuibiwa kwa kamera ya mama ambayo ilikuwa na picha nyingi za kumbukumbu ya mazishi ya wale wahanga wa maporomoko ya mlima. Ni jambo ambalo lilitufadhaisha sana.
Tumerejea salama, na wote tuwazima wa afya

Wednesday, November 11, 2009

SIKU YA KUFA KWANGU!


Wengu tunaogopa kifo!

WAKATI NASOMA HIKI KISA KWA MARA YA KWANZA NILIOGOPA SANA, LAKINI KUNA KITU NILIJIFUNZA, HATA WEWE UNAWEZA KUJIFUNZA PIA.



Naomba wakati unasoma hii habari uwe peke yako na uwe umetulia, bila kubughudhiwa.
Hakikisha hakuna unaloliwaza wakati unapoanza kusoma kwani hiyo itakusaidia kung’amua kile ninachomaanisha katika habari hii.


Naomba usiwe mwoga, kwani ni habari ambayo itakufunza jambo fulani katika maisha.
Haya ungana nami katika kusoma habari hii.


Katika akili yako hebu hisi kama vile unajiona, yaani tengeneza taswira kama vile unajiona ukiwa unaenda kuhudhuria mazishi ya mtu umpendae na unayemfahamu. Jione ukiwa unaendesha gari kuelekea kanisani ambapo ndipo mahali watu wanapokusanyika kuuaga mwili wa marehemu kabla ya mazishi.


Unapofika pale unapaki gari lako na kutoka kuelekea ndani ya kanisa, unapoingia ndani ya kanisa unaona kumepambwa na maua mazuri yenye kunukia na huku ukisikia ala za muziki mororo. Wakati ukielekea kwenye eneo ulilopangiwa kukaa unawapita ndugu, jamaa na marafiki wakiwa na nyuso zenye huzuni na majonzi yenye kuashiria kusikitishwa na kuondokewa na mtu waliyempenda sana.


Unapokaribia kufika kwenye nafasi uliyopangiwa kukaa, unapita karibu kabisa na sanduku lenye mwili wa marehemu na unapotazama mwili ulioko ndani ya sanduku hilo unastuka kuona mwili ulioko ndani ya sanduku hilo ni wa kwako!
Mara kuna sauti inakwambia "haya ni mazishi yako yatakavyokuwa miaka mitatu ijayo kuanzia sasa"


Watu wote walioko pale wamekuja kuonyesha mapenzi yao kwako na kukupa heshima kwa kuuaga mwili wako ili ukapumzike kwa amani.


Duh! Unashusha pumzi na kuketi, ili kusubiri ibada ianze. Unapoangalia ratiba ambayo ulipewa wakati unaingia pale kanisani unakuta wamepangwa wazungumzaji wanne, wazungumzaji wa kwanza wanatoka katika familia yako, mmoja wa watoto wako, mmoja wa kaka zako, dada zako, binamu, shangazi, mjomba, baba mdogo, mama mdogo, bibi, babu na ndugu wengine wa karibu ambao walisafiri maili nyingi ili kuja kushiriki mazishi yako.


Mzungumzaji wa pili ni mmoja wa marafiki zako ambaye mlishibana sana, mzungumzaji wa tatu ni kutoka katika mahali pako pa kazi na mzungumzaji wa nne ni kutoka katika kanisa unalo Sali au kutoka katika taasisi ya kijamii ambayo ulikuwa ukishiriki katika kuihudumia jamii baada ya muda wako wa kazi.


Sasa hebu fikiria kwa makini sana. Ungependa wazungumzaji hawa wazungumze nini juu ya maisha yako hapa duniani? Wewe ni mume, mke, baba au mama wa aina gani? Wewe ni mvulana, msichana, binamu, wa aina gani? Ni rafiki wa aina gani? Ushirikiano wako na wafanyakazi wenzako ulikuwaje?


Ungependa wakuzungumzieje? Ulikuwa ni mtu mwenye tabia gani kwa ujumla? Uliisaidiaje jamii, ulifanikiwa katika lipi? Ungependa wakukumbuke kwa lipi? Hebu waangalie kwa makini watu waliokuzunguka. Kama ungepewa nafasi, ungeyabadili vipi maisha yao?
Kama umesoma kwa makini habari hii naamini kuna jambo utakuwa umejifunza.
Nimegundua kuwa ili ujue kuwa wewe ni mtu wa namna gani ni vyema ukahudhuria mazishi yako mwenyewe………………


Tafakari…………….


Habari hii nimeitoa katika kitabu cha The 7 habits of highly effective people cha Stephen R Covey.

Saturday, November 7, 2009

MSIONE KIMYA......NAUMWA

Naikumbuka picha hii enzi hizo!

Ndugu zanguni, msione kimya, nimeshambuliwa na anofelesi na sasa najiuguza majeraha ya malaria yapata wiki sasa, nimepata tiba ipasayo lakini majaaliwa ya afya yangu hayaoneshi kutengemaa....nawashukuru sana kwa kunitembelea, na hapo nitakapopona nitarejea kwa kasi ya ajabu...

Nawapenda wote na mungu awabariki..