Saturday, January 9, 2010

DICKSON, KWA NINI ULINITENDEA HIVI?

Ni saa kumi jioni, ndio nimeamka kutoka katika usingizi wa mchana. Hapa nilipo nimesimama dirishani, nikitazama mandhari ya huko nje, kuna manyunyu kiasi na ngurumo za hapa na pale.

Hali ya hewa imebadilika katika jiji hili la Dar na kuna hali ya kijiubaridi kwa mbali na hali ya mvua za kiasi na hivyo kupunguza hali ya joto ambalo limekuwa ni la kutisha lisilo na mfano utadhani tupo katika nchi ya Sudan au Chad, naambiwa kuwa hali ya joto imefikia kiasi cha digrii 37, hiki ni kiwango cha kutisha sana tofauti na miaka ya nyuma.

Siku ya leo sikwenda kazini nilijihisi kuwa na homa ya malaria , nikaona ni vyema nikapate matibabu, na baada ya matibabu nikaona nijipumzishe.Kupitia dirishani, nawaona watoto wakicheza mpira, huku wakifurahia hii hali ya manyunyu. Wanacheza kwa furaha huku wakicheka, nadhani ni kutokana na hii hali ya hewa. Nikiwa bado nimewatumbulia macho, mtoto mmoja anaupiga mpira na kuingia ndani ya uzio wa nyumba yangu, kutokana na kuvutiwa na mchezo wao nikaamua kutoka na kuwarudishia mpira wao, nilitamani waendelee kucheza, kwani nilivutiwa sana na watoto wale kwa jinsi walivyokuwa wakicheza kwa furaha.

Baada ya kuwarudishia mpira wao, walinishukuru na kunishangilia kisha wakaendelea na mchezo wao. Ilionekana walifurahishwa na kitendo changu hicho.

Dickson, nimeamua kuchukua karatasi na kalamu ili kukusimulia haya kutokana na uchungu nilio nao, uchungu ambao kamwe sijui kama nitakuja kuusahau. Kidondo ulichoniachia bado hakijapona na kila uchao maumivu yako pale pale. Kwa kifupi sijapata tiba na sijajua ni lini kidonda hiki kitapona.

Dk, kama nilivyozoea kukuita wakati ule wa kilele cha mapenzi yetu, naomba nikuite kwa jina hili katika waraka huu, naamini haitakuwa ni tatizo kwako. Ni mwaka wa kumi sasa tangu uliponiacha na kuoa mwanamke mwingine eti kwa sababu sikubahatika kukuzalia mtoto. Pamoja na kunieleza kuwa ilitokana na shinikizo la wazazi wako, lakini naamini wewe ndiye uliyekuwa na uamuzi wa mwisho wa kuamua hatima ya mapenzi yetu. Kuwasingizia wazazi na ndugu zako naamini haikuwa ni sababu stahili ya kukwepa lawama. Dk, naomba ukumbuke kiapo chetu, uliniambia kuwa mimi na wewe mpaka kufa, lakini mbona bado tuko hai, lakini umeniacha, Dk, kwa nini lakini?

Kumbuka kwamba matatizo niliyokuwa nayo, wewe ndiye chanzo chake, na ni wewe uliyenishawishi hadi kufikia uamuzi ambao ndio uliosababisha mie kutopata mtoto.
Ilikuwa ni mwaka 1990, tulikuwa ndio tumengia kidato cha sita, na tulikuwa katika kilele cha mapenzi yetu. Ni katika kipindi hicho ndipo nilipojihisi kuwa mjamzito. Nilipokueleza ulishtuka sana, na ulinieleza kuwa hutarajii kuitwa baba kabla ya kumaliza masomo, ulinishawishi tuutoe ujauzito ule ili kuninusuru niendelee na masomo, ulidai kuwa isingekuwa vyema nisimamishwe shule kwa kuwa mjamzito halafu wewe uendelee kusoma peke yako. Tulikuwa tumejiwekea malengo, kuwa tuhakikishe tunasoma mpaka chuo kikuu, hukutaka tutibue malengo yetu.

Nilikupinga kwa maelezo kuwa hata nikisimama shule bado nitakuwa na nafasi ya kudurusu kidato cha sita baada ya kujifungua na nikakuhakikishia kuwa hata kama ukinitangulia sio vibaya, nitahakikisha namaliza chuo kikuu na kutimiza ndoto zetu. Ulinipinga sana, na baada ya kuvutana kwa muda mrefu huku miezi ikiendelea kuyoyoma hatimaye niliamua kukubaliana nawe, na tukiwa pamoja tulikwenda kuutoa ujauzito ule uliokwisha fikisha miezi minne.

Haikuwa kazi rahisi, kwani daktari aliyefanikisha operesheni ile hakuifanya kwa ufanisi kwani hata baada ya kurudi nyumbani hali yangu haikuwa nzuri, niliendelea kusumbuliwa na tumbo. Tuliporudi hospitali nilisafishwa na kuruhusiwa kurudi nyumbani. Tulirejea shuleni na kuendelea na masomo hadi tukamaliza kidato cha sita. Kwa bahati nzuri wote tulichaguliwa kujiunga na chuo kikuu mlimani, wewe ukisomea fani ya uhasibu na mimi nikisomea fani ya sosholojia.

Tulifanikiwa kumaliza pamoja na kufaulu, tulifanya sherehe ya pamoja na kuingia katika ajira pamoja, mimi nikiajiriwa serikalini na wewe ukiajiriwa katika shirika la Umoja wa Mataifa {UN}.

Baada ya miaka miwili tangu kuingia katika ajira, tuliamua kufunga ndoa ambayo ilikuwa na mbwembwe nyingi. Maisha yetu ya ndoa yalikuwa ni ya upendo na amani. Sio kwamba tulikuwa hatugombani, la hasha, tulikuwa tunagombana lakini hiyo ilikuwa ni njia mojawapo ya kustawisha mapenzi yetu, kwani kupitia kugombana kwetu, tulipata fursa ya kila mmoja kufahamu hisia za mwenzie.

Mwaka mmoja tangu tufunge ndoa tuliamua kuzaa mtoto, na baada ya majaribio kadhaa kushindikana tuliamua kwenda kwa watalamu wa tiba ili kupata ushauri. Ni katika kipindi hicho ndipo tulipopata taarifa ambazo zilinipenya moyoni kama msumari wa moto. Tuliambiwa kuwa siwezi kupata mtoto milele kwa kuwa mirija yangu ya uzazi imeathirika baada ya kile kitendo cha kutoa mimba tulichokifanya wakati ule.

Hatukata tamaa, tuliwatembelea wataalamu kadhaa wa tiba wakiwemo wa tiba za asili lakini hatukufanikiwa kupata mtoto. Miaka minne baadae tangu tuoane ndugu zako walianza manung’uniko ya chinichini, lakini hata hivyo walifikia hatua ya kunieleza waziwazi kuwa mimi ni mgumba siwezi kukuzalia mtoto, maneno hayo yalinichoma rohoni, lakini nashukuru ulikuwa pamoja nami na uliniahidi kunilinda. Hukuishia hapo ulifikia hatua ya kula kiapo kuwa mimi na wewe mpaka kufa.

Nilifarijika na msimamo wako, na ulinipa nguvu kila wakati. Mwaka mmoja baada ya kiapo chako ulianza kubadilika, ulikuwa ukichelewa kurudi nyumbani na nikikuuliza majibu yako yalikuwa ni ya mkato. Chakula ulikuwa huli nyumbani na kama hiyo haitosh ulifikia hatua ya kunipiga kwa sababu ya kukumbusha kule tulipotoka. Mateso yalizidi sana na ndugu zako walikuja kunieleza wazi kuwa unarajia kuoa hivyo nijiandae kuwa na mke mwenza, kwa kuwa huyo mchumba wako ameshakuzalia mtoto wa kiume.
Dk, umesahau kuwa hata mie kama nisingetoa ule ujauzito ningekuwa na mtoto wa kiume kama alivyotueleza yule daktari, na uamuzi wa kutoa ule ujauzito haukuwa ni wangu bali ilitokana na shinikizo lako.

Nilipokuuliza kuhusu wanavyosema ndugu zako, ulinijibu kwa mkato kuwa ni kweli na ulidai kuwa haikuwa na ubaya wowote kwa kuwa amekuzalia mtoto, kitu ambacho mimi nimeshindwa.

Nililia kwa uchungu sana na niliamua kuondoka, sikutaka kuishi na mke mwenza kwa kuwa hiyo ni kinyume na mafundisho ya dini yetu ya kikristo. Nilifanya juhudi za kutafuta suluhu kupitia kwa mchungaji wetu lakini haikuzaa matunda na hatimaye tukatengana, na wewe kumuoa huyo binti aliyekuzalia mtoto.

Sikukata tamaa, niliamini tu kuwa iko siku nitakuja kupata mtoto siku moja. Mwaka jana niliamua kwenda nchini Afrika ya Kusini, hiyo ni baada ya kushauriwa na baadhi ya madaktari bingwa, na nilipofika kule nilipatiwa matibabu na kupandikizwa ujauzito. Hivi ninavyokuandikia waraka huu ninao ujauzito wa miezi saba, na ninatarajia kupata mtoto wa kiume mungu akinijaalia.

Hiyo yote ni kutaka kukuthibitishia kuwa kwa mungu kila jambo linawezekana. Nilipokuwa nikiwaangalia wale watoto waliokuwa wakicheza mpira, nilikuwa nimeshika tumbo langu na nilihisi mwanangu na yeye akirukaruka kwa furaha akifurahia kile ninachokiona kupitia kwangu. Naamini na yeye atakuwa ni mchezaji mpira mahiri, kwa kuwa mama yake pia ni mshabiki wa mpira wa miguu.

Naomba nihitimishe waraka huu kwa kukutakia maisha marefu ili uje kushuhudia miujiza ya Mwenye enzi mungu, kwamba kwake yeye kila jambo linawezekana.

Ni mimi mke wako wa zamani.

Kolambo Kiangi

Ndugu Msomaji, jana nilimtembelea shangazi yangu, nilimkuta amesimama dirishani akiangalia watoto wakicheza mpira. Shangazi yangu huyu amepambana na mikasa ya dunia, na baada ya kuzungumza naye ndio nikaona niandike huu waraka.

Ni mkasa wa kweli uliompata shangazi yangu, nami kwa kutaka kufikisha ujumbe kwa njia ambayo itamuwezesha msomaji kujifunza, ndio nikaandika waraka kwa mtindo huo.

NB: Jina la Dickson sio la muhusika.

2 comments:

Yasinta Ngonyani said...

Ni habari ya kusikitisha na kusisimua, ni ajabu kuona watu hawawezi kutunza ahadi zao. Namsifu shangazi kwa kutokata tamaa ya mtoto pia namsifu sana kwa kuwa na imani aliyo nayo. Nimeguswa sana na habari hii.Ila nasikitika sana kwa kitendo alichotenda bwana Dickson kwa kumshawishi shangazi yetu na baadae kuoa mke mwingine. Sijui wanaume wanadhani wao wanaweza tu kuamua watakavyo? Wanajifikiria wo tu na pia wanadhani wanaweza tu kubadili wanawake kama shati.

MARKUS MPANGALA said...

Niambie penzi bandia,
wapi linapoanzia,
kichwani au mdomoni?