Thursday, January 7, 2010

MAJIBU YA DADA SUBI KWA BARUA YANGU

Dada Subi

Kama kumbukumbu zenu haziko mbali, ni kwamba mwaka jana nilimuandikia dada yangu Subi barua ya siri nikimjuza hali halisi ya huku nyumbani na maandalizi ya uchaguszi mkuu octoba mwaka huu, kwa yule asiyekumbuka anaweza kujikumbusha kwa kubofya hapa.

Na haya ndiyo majibu ya dada Subi katiaka kujibu bara yangu. Ni jambo la kujivunia kuwa kumbe dada yangu huyu aliipata barua yangu na kupata muda wa kukaa chini na kunijibu barua yangu.

Naomba muunganr nami katia kuisoma barua hii……………………

Mpendwa mdogo wangu Koero,
Salam sana. Na baada ya salam, natumai u mzima wa afya. Ni matumaini yangu kuwa ndugu na jamaa zetu hapo Kijijini ni wazima na wanaendelea vizuri kwa kudra za Mwenyezi Mungu.

Dhumuni la kuandika barua hii ni kupenda kukushukuru sana kwa barua yako uliyoniandikia tarehe 16 mwezi wa Disemba 2009 na kunieleza mengi ya hapo Kijijini. Mara ya mwisho nimepata ujumbe toka nyumbani ni pale kaka Mtoahanje aliponitumia ujumbe kuwa ametindikiwa fedha kiasi za kulipia ada ya shule, nikaahidi kumsaidia kadiri ambavyo ningeweza. Sasa umenieleza tena kuhusu hali ya henia ya babu, nilijitahidi sana kuwasiliana na Mbega kuhusu suala hilo siku mbili tu baada ya kusoma ujumbe wa Mtoahanje lakini kwa habati mbaya, Mbega amekuwa msemaji sana siku hizi kuliko mtendaji, si kama vile alivyokuwa kijana mdogo na mchapakazi. Nitajitahidi sana niwasiliane na rafiki yangu Mwelumbini, yule mototo wa mzee Shelukindo tuliyesoma naye wote Mazoezi, angalao aweze kufika na kumwona Mzee na kutafuta tiba inayofaa.

Nimefurahishwa sana na maendeleo ya usafiri kutoka baiskeli hadi pikipiki lakini nimehuzunishwa sana na mambo vijana wa mtaani wanayowatendea dada na mama zetu huko njiani. Juzi juzi hapa, rafiki yangu alipiga simu akaongea na Bibi yake ndipo aliposimuliwa masahibu yaliyompata siku moja akirejea toka shambani alikokuwa amekwenda kufunga majani ya wale ng’ombe wake (hawa wazazi wetu na ng'ombe hawaachani hata uwaagizie pikapu ya maziwa kila siku asubuhi). Basi alipokuwa katika kijia pale Komkonga, ghafla akatokea kijana mmoja wasiyefahamiana, na katika kupishana, salam akampa, ‘emcheku, urevedi?’, bibi akaitika, ‘ni jedi’, huku wakipishana kila mtu kuelekea upande wake. Sasa kwa kuwa wazazi wetu huwa na hisia za ziada, baada ya mwendo wa hatua chache, bibi alihisi kuwa kuna mtu anamfuata nyuma, lakini akapuuzia kidogo, Kabla ya kuendelea na umbali wowote wa kuhesabika, Bibi akastukia kanigwa shingoni na kupigwa ngwala, akaanguka chini pu! Majani aliyokuwa amebeba kichwani yakaanguka na kunde alizokuwa amefungia humo zikamwagika na kusambaa majanini. Kumbe kijana alikuwa amejiandaa tayari kwa kumbaka BIbi. Kwa bahati Bibi ujasiri ukamjia, akajitahidi akafungua mdomo wake kisha akamuuma kwa nguvu kweli sehemu ya mkono (kwa kuwa alizibwa mdomo na yule kijana kwa kutumia sehemu ya mkono), ndipo yule kijana alipoondoa mkono wake na kuugulia maumivu, Bibi akabeba jiwe moja la moram lililokuwa pembezoni hapo kijiani, akamkoboa nalo yule kijana kwenye kipaji cha uso upande wa kushoto. Bibi naye amekula chumvi nyingi, hivyo alijua haswa pa kuumiza, wala hakufanya ajizi. Baada ya hapo akajitahidi kupiga ukelele kwa sauti kubwa, ndipo kijana akaogopa na kwa haraka akajivuta na kukimbia, akatokomea katikati ya shamba la mahindi. Ndipo bibi akanyanyua mzigo wake wa majani, akaufunga tena vizuri pamoja na kunde chache azizoweza kusomba pale kijiani, akaendelea na safari ya kurudi nyumbani. Hivi ninavyokueleza, si kisa cha kutunga hiki, ni kweli kimemtokea huyu Bibi na alama ya jino lake dhaifu kumeguka baada ya purukushani na kumuuma yule kijana bado ipo, ndiyo sababu ya maumivu yake ya jino na kichwa hadi leo.

Hali hiyo imenishangaza sana kwani bado inaendelea japo viongozi wapo. Kwani Mzee Mkiramweni siku hizi hawamsikilizi tena anapotoa maagizo? Na vijana wanashindwa kwenda mashambani kulima au katika biashara sokoni wao wanakalia kusubiri wasafiri tu na kisha kuwabaka? Hali haikuwa nzuri wakati sisi tunakua, nakumbuka hivi vituko vya kubaka tulikuwa tukivisikia kwenye vile vikao vya wazee na akina mama mara kwa mara jioni pale kwa Mzee Mkiramweni kila kilipotokea kituko. Walikuwa wakiitwa vijana waliotenda haya makosa na kukalishwa kikao na kuadabishwa, sisi watoto tulikuwa tunasikia tu lakini hatuelewi yanayojiri kikaoni. Ila kwa wakati huu, hali inazidi kuwa mbaya na cha kusikitisha zaidi, hakuna anayewasikiliza akina Mzee Mkiramweni tena. Tunakoelekea nako yaonesha ni kubaya zaidi.

Sasa leo mdogo wangu Koero, wacha niishie hapa. Haya mengine nitayajibu nitakapopata nafasi ya kuketi tena chini kitako kwani muda huu zimebaki dakika chache kabla ya muda wa kwenda kibaruani haujawadia. Huku ng’ambo inabidi kufanya kazi kwa juhudi kweli na maarifa mengi ili kukwepa hatari ya kupoteza kazi na kukumbwa na adha ya kutafuta kazi, wakati mwingine hata yabidi kufanya kazi tatu kwa siku alimradi kujipatia fedha ya kuweza kumudu mahitaji muhimu kama vile kodi ya pango, gharama za umeme, maji na hata usafi wa mazingira ya nyumba. Kila kitu huku ni pesa na pesa yenyewe ina thamani sana, upatikanaji wake mgumu na kadiri uthamani wake unavyozidi, ndipo upatikanaji wake unavyokuwa mgumu na vitu kuuzwa kwa bei ya kuruka. Siku utakapokuja huku utaweza kujionea mwenyewe na kufahamu ni kwa nini inatuwia vigumu kuwasiliana nanyi mara kwa mara.

Nisalimie sana Babu, Bibi na akina shangazi na mjomba, hasa yule mjomba Eliewaha wa kule bonde la mpunga. Nisalimie pia rafiki zangu hapo kijijini, usisahau kuwaambia kuwa bado ninawakumbuka sana.

NB: Utakapoandika tena, ukumbuke kunitumia namba ya simu ya dukani kwa Mangi ili nikipata nafasi nipige simu niongee nanyi niweze kusikia sauti zenu.

Wasalaam,
Dada yako akupendaye,
Subi

3 comments:

Yasinta Ngonyani said...

Subi umefanya vizuri kuijibu barau hii. Mimi naona aibu sikujibu naona Mdogo wangu kachukia maana mmhhh. Kazi nzuri Subi pia Koero kwa kuiweka hapa ili wasomaji wasome pia.

MARKUS MPANGALA said...

Na kweli

kamala Lutatinisibwa Lutabasibwa said...

lione kwanza,