Saturday, May 8, 2010

TAFAKARI YA LEO: TUENDELEE NA SOMO LA IMANI

Akaukemea upepo, akaiambia bahari, nyamaza utulie. Upepo ukakoma, kukawa shwari kuu.

Katika mfululizo wa tafakari ya leo nimeona tuendelee na somo letu la imani.
Ningependa leo tusome Marko Mtakatifu 4:35-41

Siku ile kulipokuwa jioni, akawaambia. Na tuvuke mpaka ng’ambo. Wakauacha mkutano, wakamchukua vile vile alivyo katika chombo. Na vyombo vingine vilikuwako pamoja naye. Ikatokea dhoruba moja kuu ya upepo, mawimbi yakakipiga chombo hata kikaanza kujaa maji. Naye mwenyewe alikuwepo katika shetri, amelala juu ya mto; wakamwamsha, wakamwambia, Mwalimu, sikitu kwako kuwa tunaangamia? Akaamka, akaukemea upepo, akaiambia bahari, nyamaza utulie. Upepo ukakoma, kukawa shwari kuu. Akawaambia, Mbona mmekuwa waoga ? Hamna imani bado? Wakaingiwa na hofu kuu, wakaambiana, ni nani huyu, basi, hata upepo na bahari humtii?

Mara nyingi Bwana Yesu alikuwa akifundisha kwa mifano, na haiyumkini kuna matukio ambayo yalikuwa yanamtokea ili wanafunzi wake wapate kujifunza kupitia kwake.

Hebu tuangalie mfano huo hapo juu, wanafunzi hawa wamekuwa wakitembea na Yesu kutwa nzima na walikuwa wakimuona akitenda miujiza mbalimbali kwa kuponya watu, kufufua wafu na miujiza mingine mingi tu.

Na hata kufikia kuwaeleza kuwa hata wao wanaweza kutenda miujiza iwapo watakuwa na imani. Lakini wanafunzi hawa pamoja na kuwa walikuwa na Yesu mle chomboni lakini bado walikosa imani kuwa wanaweza kuukemea upepo ule na ukatulia. Walikuwa wamekata tamaa kabisa ikabidi wamwamshe Yesu ili awaokoe.

Naye Yesu kwa kutambua kuwa wanafunzi wake hawajaiva katika somo la imani akaamka na kuukemea upepo ule hadi ukatulia, lakini hakuwaacha hivi hivi, akawaambia ‘Mbona mmekuwa waoga ? Hamna imani bado?’

Yesu aliwashangaa wanafunzi wale, kuwa pamoja na kufundisha kote lakini bado tu somo hili la imani halijawaingia? Ajabu kweli!

Leo Yesu hayupo, lakini ametuachia somo hili kubwa kabisa la kuwa na imani.

Tukio hilo la Baharini, naweza kulifananaisha na misukosuko iliyopo hapa duniani.
Dunia yetu hii imejaa misukosuko mingi sana ya kimaisha, kama ilivyo misukosuko ya baharini, kuna matukio mengi ya kukera na kukatisha tamaa.

Kama ilivyo bahari kukumbwa na upepo mkali na mawimbi, na wakati mwingine kuwa shwari na ndivyo maisha yetu yalivyo.

Kuna wakati tunakuwa na furaha na amani lakini kuna wakati hali hugeuka na kuwa ya kukatisha tamaa kutokana na misukosuko ya kimaisha.

Hali hiyo hatuwezi kuiepuka, hadi tutakapoiacha hii miili yetu (tutakapokufa). Hatuwezi hata siku moja kuishi bila kukabiliana na changamoto za hapa duniani. Kama Yesu aliweza kukabiliana na cnagamoto mbalimbali za kimaisha iweje sisi tusikabiliane na changamoto hizo.

Kwa kulitambua hilo, ndipo bwana Yesu anapotueleza kuwa sisi pia tunaweza kufanya miujiza pale tunapokabiliana na changamoto za kimaisha.

Kama wewe ni ni mwanafunzi na una wasiwasi wa kufaulu mtihani, basi amini tu kuwa unaweza kufaulu, kwa kusoma kwa bidii na kuzingatia masomo, jitihada hizo na imani inaweza kukuvusha. Kama umetafuta kazi kwa muda mrefu bila mafanikio, umelima kwa muda mrefu bila kupata mazao ya kutosha au kukosa kabisa, umefilisika katika biashara zako au umepata hasara katika bishara zako, maisha yako yamekuwia magumu, umempoteza mwenzi wako, umeachwa na mchumba wako, usikate tamaa, weka imani yako kwa mungu, hakika kila utakaloomba na kuamini litawezekana.

Tunaweza kuvuka vikwazo na viunzi mbalimbali vya kimaisha kwa kuamini tu kuwa hayo ni mapito. Hatuna haja ya kusononeka wala kukata tamaa.

Tukutane Jumamosi ijayo……………..

3 comments:

Fadhy Mtanga said...

Mchungaji Koero,
Ahsante kwa mada nzuri.
Wasalaam,
Askofu Fadhy

o'Wambura Ng'wanambiti! said...

Mama Mchungaji,

Aksante kwa hili somo. Laiti tungekuwa na imani kama punje ya haradari tusingekuwa na maradhi wala ufisadi

Yasinta Ngonyani said...

Nanukuu "Kuna wakati tunakuwa na furaha na amani lakini kuna wakati hali hugeuka na kuwa ya kukatisha tamaa kutokana na misukosuko ya kimaisha." Nakubaliana bila imani huwezi kufanikiwa ombi lako. Asante kwa somo la leo. Sista Yasinta