Saturday, January 30, 2010

KUELEKEA UCHAGUZI MKUU: NAOMBA NIWE MTABIRI

Mojawapo ya vikao vyao

Nathubutu kukubaliana na mtaalamu wa sayansi ya siasa Harold Laswell katika taaluma hiyo. Mwanazuoni huyu alikwisha kusema maana halisi ya siasa na wanasiasa, kwamba ‘Politics is the Art of Possible”. Pale ambapo mwanasiasa anatarajiwa kutenda jambo fulani, hatendi lakini asipotarajiwa hutenda. Na hili limekuwa zuri kwa wanasiasa hata Harold Laswell akawachambua katika maana nzima ya siasa.

Karl Marx naye hakubaki nyuma, alishaeleza kuwa siasa na wanasiasa kuwa ni watu wanaofanya mambo kwa matakwa yao,mahitaji yao kwa faida zao. Tunaweza kuwa na maoni tofauti lakini msingi wetu ni kuchambua jambo lilelile.

Endapo wewe ni mfuatiliaji wa siasa za hapa nchini, ninahakika huhitaji kuwa na taaluma kama ya yule Shehe wa Mwembechai yaani Shehe Yahya Hussein, kutabiri siasa za hapa nchini. Au kumaizi na kuwa kama Harold Laswell. Inahitaji uelewa mdogo tu kuchanganua matukio ya kisiasa yanayotokea hapa nchini, kisha kubaini kitakachotokea.

Kwa msingi huo, leo naomba niwe mtabiri wa kile kitakachotokea katika uchaguzi mkuu ifikapo Oktoba 25 mwaka huu. Hivi karibuni tumeshuhudia chama kipya cha siasa kinachoitwa Chama cha Jamii (CCJ) kimepewa usajili wa muda, wengi wamekihusisha chama hicho na Vigogo wa kupiga vita ufisadi ndani ya chama tawala yaani CCM almaarufu ‘Mitume 12’. Inaelezwa kuwa ‘mitume hawa 12’ ndiyo waanzilishi wa chama hicho.

Yamesemwa mengi na kukifanya chama hicho kuwa gumzo katika medani za kisiasa. Ni aghalabu ikapita siku pasipo vyombo vyetu vya habari hususan magazeti kuandika juu ya CCJ. CCM nacho katika nyakati tofauti viongozi waandamizi wakiongozwa na katibu wake mwenezi Kapteni mstaafu John Chiligati na Katibu wake mkuu Luteni Yusuph Makamba ambao awali walionekana kukibeza chama hicho, lakini sasa inaelekea kuwatikisa.

Jana katibu mwenezi Kapteni mstaafu John Chiligati, amesambaza waraka kwa wana- CCM nchi nzima kuwatahadharisha kujiepusha na chama hicho, vinginevyo wataharibikiwa.
Hiyo ni ishara tosha kuwa joto la CCJ limeanza kuitikisa na kuitekenya CCM.

Kwa Wasomaji wa Biblia watakumbuka kisa cha Goliath na Daudi. Goliath alikuwa ni pandikizi la mtu lililoshiba haswa, lakini alipigwa na mtoto mdogo sana Daudi. Hivyo basi CCM nayo kwa upande wake inaonekana kung’amua nguvu za chama cha CCJ,na hivyo kuogopa kupigwa kama ilivyotokea kwa Goliath na Daudi, na ndio sababu ya kuanza kuweweseka mapema.

Nirejee kwenye utabiri wangu, nionacho ni kwamba, tumeshuhudia Makundi ndani ya CCM, ambayo yamesababishwa na vita ya ufisadi ambayo ilianzishwa na Chadema. Lakini bila soni baadhi ya wabunge wa CCM wakaiteka nyara na kuigeuza mtaji wao wa kisiasa. Wakajivika jina la ‘mitume 12 wa kupambana na ufisadi’, huku wakishindwa kuitoa orodha ya mafisadi hao kama ilivyofanywa na Dk Wilbroad Slaa pale Mwembe Yanga, ambaye anastahili pongezi kwa ujasiri wake.

Ingawa wapo baadhi ambao wanania ya dhati kabisa kupiga vita ufisadi, lakini nasikitika kusema kuwa miongoni mwao wapo mafisadi ambao wamejivika dhamana ya kuupiga vita ufisadi ilhali na wao sio wasafi kabisa. Mafisadi wanayo nguvu kubwa ndani ya CCM, na kwa sehemu kubwa wanashiriki vikao muhimu vya kamati za CCM ikiwemo Kamati kuu ya taifa ya chama(NEC). Hawa ni wajumbe wa kamati kuu na wana uwezo mkubwa wa kupitisha maamuzi wanayoyataka, na hili tulishuhudia walipotaka kumng’oa Spika wa Bunge Mheshimiwa Samwel Sitta.

Ni busara za wazee hasa rais mstaafu wa awamu ya pili Mzee Ali Hassani Mwinyi na Rais mwenyewe Jakaya Mrisho Kikwete, ndizo zikaweza kumnusuru na rungu la mafisadi, vinginevyo hatma ya Spika wa bunge ingekuwa mashakani.

Hawa ndio ambao watakuwa na maamuzi ya kupitisha majina ya wabunge watakaogombea ubunge kupitia CCM, hata baada ya kupita katika kura za maoni, kamati kuu ya CCM chini ya mwenyekiti wake Rais Jakaya Kikwete inayo maamuzi ya kupitisha majina ya walioshinda katika kura za maoni katika kinyang’anyiro cha kugombea ubunge kupitia CCM.

Hapa ndipo penye hekima na akili, hapo ndipo kwenye mashaka makubwa kwani mwanachama anaweza kushinda katika kura za maoni lakini jina lake likaondolewa katika kikao hicho pale ambapo wajumbe wasiporidhishwa na jina la mgombea aliyeshinda. Hapo inategemea zaidi maoni ya wajumbe wa kamati kuu ya chama. Hili ndilo alilofanyiwa Dk Slaa aliyeamua kujiunga Chadema au hata Stephen Wassira(kabla hajarejea CCM), wawili hawa walikumbana na ‘mkono wa kamati kuu’.

Ikumbukwe kuwa kuna wabunge ndani ya CCM ambao wameisumbua sana serikali hasa katika sakata la kashfa ya kampuni ya Richmond, ambayo hata hivyo mpaka sasa maamuzi yaliyofikiwa na kushauriwa na kamati ya bunge, bado hayajatekelezwa na serikali imeendeleza ngonjera na kupiga danadana.

Ngonjera hizo ndizo zinazowafanya baadhi ya waandamizi washindwe kumwelewa mwenyekiti wao, licha ya kuwa mwenyekiti wa baraza la mawaziri(kwa maana alijua zabuni hiyo na kuidhinisha), lakini amekuwa kimya huku taarifa za kiserikali kwa mujibu wa waziri wa nishati na madini, William Ngeleja zikisema watuhumiwa wameonywa tu.

Ninachokiona, ni kwamba CCJ, imeundwa kama kimbilio la wabunge wa CCM iwapo wataenguliwa na kamati kuu baada ya kushinda katika kura za maoni au wakifanyiwa mizengwe ili wasishinde katika kura za maoni. Mtu anaweza kujiuliza, ni kwanini wasikimbilie chama kingine cha siasa cha upinzani ambacho kimekomaa, mpaka waanzishe chama kingine cha siasa?, kama utakuwa ni mfuatiliaji wa mambo ya kisiasa hapa nchini naamini unafahamu kilichompata Mwenyekiti wa TLP Augustine Lyatonga Mrema ‘mzee wa Kiraracha’.

Kama ambavyo nimedokeza mwanazuoni Harold Laswell, ni dhahiri wanasiasa ni wataalamu wazuri wa kusoma alama za nyakati, na wanajua huko nje katika vyama vya siasa ni vigumu kupata ushawishi wa kuweza kumpitisha kuwa mbunge kwa kuwa vyama vya upinzani vilivyopo navyo vina shiranga zao. Ndiyo maana tunashudia waanzilishi wa chama cha Jamii(CCJ) siyo watu mashuhuri katika medani za kisiasa, bali wale wametangulizwa tu.

Kelele za wabunge wa CCM hususan wale vinara wa vita vya ufisadi kukikana chama hicho hadharani ni kauli za kisiasa tu katika kuweka mambo yao sawa ndani ya CCM. Nani anayeweza kuukata mkono wake unaomlisha?, ni vigumu kukiri hadharani kukiunga mkono chama fulani ukiwa ndani ya CCM. Hilo ameweza kufanya mbunge wa Kigoma kwa tiketi ya Chadema Mheshimiwa Zito Kabwe peke yake ambaye siyo mnafiki.

Nina hakika hawa wabunge wa CCM wanaokikana chama cha CCJ leo hii, lakini wakienguliwa na kukimbilia katika chama hicho watasema wameombwa na wapiga kura wao hapo ndipo unapokutana na msemo wa ‘Politics is art of possible’. Ni nani asiyejua kuwa wanasiasa ni watu wasiotabirika, wanaweza kuahidi kujenga daraja mahali pasipo na mto, wanaweza kudondosha machozi kana kwamba wanauchungu, lakini wakipewa kura hutimka na hapo kuonekana ni mwaka wa uchaguzi.

Mwanasiasa anaweza kukuonesha bakuli akakwambia ni bilauri, mkabishana kweli kweli lakini ukimthibitishia kwa kutumia hata mashahidi atakwambia kuwa ni kweli ulikuwa sahihi kuwa ile ni bakuli, lakini kama ukikosa bilauri unaweza kuitumia bakuli hiyo kama bilauri. Naomba nimalizie kwa kusema kuwa Mwaka huu tutashuhudia matukio mengi ya kushangaza na haya ni majilio tu.

Wednesday, January 27, 2010

VYOMBO VYETU VYA HABARI NA MAJINA YA VIGOGO NA WATOTO WAO


Hivi karibuni Gazeti la Mwananchi liliandika juu ya habari ya mtoto wa Kigogo mmoja huko Moshi kukamatwa kwa kosa la kulawiti. Mtoto huyo anatuhumiwa kumlawiti mtu mmoja aliyekamatwa ugoni katika Hoteli ya KNCU, akishirikiana na watu wengine.

Katika Gazeti hilo waliwataja watuhumiwa waliofikishwa mahakamani akiwemo mume mshika ugoni na mke wake ambao naamini ni makabwela kwa kosa la kumlawiti mtuhumiwa wa ugoni, lakini jina la mtoto wa kigogo huyo bado lilikuwa halitajwi pamoja na kuwa alifkishwa mahakamani.

Sswali ninalojiuliza ni hili, Je kuna sheria maalum inayowalinda watoto wa vigogo kutajwa katika vyombo vya habari pale wanapotuhumiwa kwa makosa na kufikishwa kwenye vyombo vya sheria?

Mimi naamini sheria hiyo ipo, na inafanya kazi. Kwa nini nisiamini wakati mara nyingi vyombo vya habari vimekuwa vikitumia msamiati wa “Mtoto wa Kigogo fulani” bila kutaja jina huku walioshirikiana naye wakitajwa waziwazi?

Nimekuwa nikishuhudia ubaguzi wa waziwazi katika vyombo vyetu vya habari kwa kuwataja baadhi ya watuhumiwa kwa majina na kuficha majina ya watoto wa hao wanaoitwa vigogo au vigogo wenyewe, hivi kwani Vigogo ni akina nani hasa?
Je wako juu ya sheria? Wanalindwa kwa maslahi ya nani?

Naomba wajuzi wa Sheria watuelimishe juu ya hili.

Friday, January 22, 2010

RAISI AMANI KARUME NA MKAKATI WA MARIDHIANO

Rais Amani Karume na Katibu Mkuu wa CUF Seif Shariff Hamad na urafiki wa mashaka

Aristotle – yule mwanafalsafa wa kale wa Kigriki aliwahi kusema kwamba “man is a political animal”. Japo kumekuwa na mjadala mrefu (ambao bado unaendelea) kuhusu alichokimaanisha hasa aliposema maneno haya, tunaweza kuchukulia kijuujuu tu hapa kwamba pengine alichokimaanisha Aristotle ni ukweli kwamba binadamu ni mnyama ambaye anajulikana kwa kujiundia mifumo tata ya kisiasa na kijamii, mifumo ambayo ipo hasa kwa lengo la kuhakikisha kwamba anaishi kwa amani kulingana na sheria na amali alizojiwekea. Kutokana na ukweli huu, binadamu pia inamlazimu awe na “watawala” ambao kimsingi kazi yao ya msingi ni kuhakikisha kwamba sheria na amali zilizokubaliwa kufuatwa na jamii zinatekelezwa na kuwa kila mwanajamii anaishi kwa utangamano katika nyanja zote. Inavyoonekana, kama Historia inavyotuonyesha, utawala ni mtamu na tabaka linalofanikiwa kushika nafasi hii mara nyingi huwa halipendi kuiachia kirahisi. Ndiyo maana Historia imejaa wafalme (wa maisha), maraisi wa kudumu na hata madikteta. Ndiyo maana wengine hujaribu hata kubadili katiba ili waweze kuendelea kuwa watawala. Hata katika nchi zinazojidai kuwa na ukomavu wa kidemokrasia, tamaa ya tabaka (au chama) tawala daima ni kubakia madarakani kwa mbinu na gharama yo yote ile.

Leo nitazungumzia suala hili kwa kuangalia mbinu na ujanja unaotumiwa na chama tawala cha Tanzania (CCM) kinapojaribu kung’ang’ania madarakani kwa kuangalia kiinimacho cha maridhiano kule Zanzibar. Sina ugomvi na CCM, na kama nilivyodokeza hapo juu, hata kama chama kingine cha upinzani kingekuwa madarakani leo (mf. CUF, CHADEMA au UDP), kingejaribu pia kutumia mbinu ili kiweze kung’ang’ania madarakani. Tayari tumeshaona baadhi ya viongozi wa vyama hivi vinavyoitwa vya upinzani wanavyoupenda Uenyekiti, Umakamu Mwenyekiti na Ukatibu Mkuu wa vyama vyao kiasi kwamba hawataki kuwaachia wanachama wengine. Unafikiri wakiingia madarakani watakubali kuondoka kwa urahisi hawa? Thubutu! Hebu turudi kwenye mada yetu kuu ya leo - kiinimacho cha maridhiano Zanzibar.

Kama kuna chama ambacho unaweza kukiita chama cha watu wenye kujua kuchezea watu shere basi chama hicho ni CCM. Ndiyo maana kuna kitengo cha Propaganda kinachoongozwa na Hizza Tambwe.

Mimi siyo mfuatiliaji sana wa masuala ya kisiasa, lakini matukio yaliyojitokeza hivi karibuni katika duru za siasa hapa nchini, nimejikuta nikikaa na kutafakari sana, na hatimaye nikajiwa na kitu kama maono.

Kwa wale wanaofanya ‘meditation’ kama rafiki yangu Kamala, anafahamu nazungumzia kitu gani. Ilianza kama masihara, Rais Amani Abeid Karume akamwalika hasimu wake kisiasa Katibu mkuu wa CUF, Maalim Seif Shariff Hamadi pale ikulu ili kupata staftahi.

Lakini pamoja na mambo mengine Rais Karume akaja na agenda ya kutafuta suluhu baina ya vyama hivyo viwili, kule Zanzibar, yaani CCM na CUF.

Katika stafutahi hiyo Mheshimiwa Amani Karume akaja na msamiati wa “Maridhiano”. Kama kuna chama kinachojua kucheza na misamiati ya ghiliba za kisiasa zisizo na ukomo, basi CCM inaongoza.

Awali chini ya uongozi wa Rais mstaafu Dk. Salmin Amour waliunda tume ya kutafuta ‘suluhu’ ikiwa inaongozwa na aliyekuwa katibu mkuu wa jumuiya wa madola Chifu Emeka Anyaoku, mnamo mwaka 1999, ikiwa ni mwendelezo wa mtafaruku wa chama cha CUF kupinga matokeo ya uchaguzi wa mwaka 1995 ambapo Salmin Amour akaukwaa urais kwa mara ya pili.

Rais Benjamin Mkapa akishiriki moja kwa moja katika msamiati huo wa “Suluhu”. Hata hivyo baada ya mauaji ya Januari 27, 2001, serikali ililazimika kuamuru jeshi la polisi kutumia risasi za moto kuzima maandamano ya wafuasi wa CUF waliokuwa wakipinga matokeo ya mwaka 2000 yaliyompatia uongozi Rais Karume.

Hapo ndipo ukazuka msamiati wa pili wa ‘muafaka’ baina ya CUF na CCM kutoka msamiati wa ‘suluhu’ chini ya Dk Salmini Amour. Ikumbukwe ‘muafaka’ huo ulishindwa kutekelezwa kutokana na danadana nyingi. Baada ya hapo sasa upo mikononi mwa Rais wa awamu ya nne mheshimiwa Kikwete.

Jitihada za Rais Kikwete kutanzua mzozo huo uliwafikisha hadi kijijini Butiama alikozikwa baba wa Taifa, Mwalimu Nyerere. Na hapo ndipo wakazuka na msamiati mwingine wa ‘kura ya maoni’ kama wananchi wanaridhia serikali ya mseto itakayoundwa na vyama hivi viwili(CCM na CUF).

Kwa maana nyingine ‘muafaka’ ulioafikiwa katika kamati za vyama hivyo haukutekelezwa, ndiyo maana tukaona malumbano yasiyo na tija huku CUF wakigomea mazungumzo mengine na CCM kwakuwa maazimio ya awali hayakutekelezwa.
.
Waama! sasa Mheshimiwa Amani Karume kazuka na msamiati mwingine wa nne “Maridhiano”. Hapa kama ni ndoano basi imenasa Jodari. Kwasababu ukihesabu unaona huu ni msamiati wa nne wa kulijadili jambo lilelile na watu walewale………….

Naam! wakati wa hiyo stafutahi ndipo mzee mzima Rais Karume akamweleza Bwana Shariff Hamad, ‘Bwanae!, hii Zanzibari ni yetu sote kwa nini tugombane atii?!!!... huu sio wakati wa maugomvi yakhe!!.., tuijenge nchi yetu ili watu waendelee …kulima na kuvuna Karafuu bila ghasiaaa, au wewe wasemaje?”

Sharrif Hamad naye, akajibu….’Bwana Amani Karume, (Hapo ilikuwa bado kumtambua kama Raisi), umegusa pale ninapopataka, unajua naona sasa wananchi watafikia mahali watachoka na haya mambo ya Unguja na Pemba, huu si wakati wa kuwachezea shere ati, wanifahamu?

….Huu ni wakati wa kuyamaliza mambo haya ili tuishi kama enzi zileee! tukicheza ngoma ya mbwa kachoka na Kibati wan’kumbuka sawasawa?”…

Mheshimiwa Amani Karume naye akaongeza…..‘Nakumbuka shehe wangu, sasa wewe kawakusanye wana-CUF wote pale Kibanda Maiti na kisha katangaze kun’tambua mie kama rais wa Zanzibar nami nitawakusanya wana-CCM wote pale Jambiani kisha nitatangaza kuwa tumeamua kufanya ‘maridhiano’,… waonaje hapo”??!

Seif Shariff Hamadi akajibu, ‘Hapo umenena, lakini shehe wangu, (akainamisha kichwa chini) wewe wawajua hawa Wapemba, ni wakorofi mno hawa, waweza kun’piga hawa. Itakuwaje ulinzi sasa?”…

‘Hapo shehe wangu sina nsaada, kwani nikisema nitumie polisi itakuwa vita, wataona hawa ni njama ya CCM, kwa nini usitumie wale Blue Guard wenu?!’

‘Basi ngoja nikajaribu kisha wewe utaona na kitakachotokea, lakini usisahau kunilinda shehe wangu sawa?’……

Basi huo ndio ukawa mwanzo wa kuanzishwa kwa mchakato wa ‘Maridhiano’. Kilichotokea katika mkutano wa CUF kila mtu anakifahamu, ilikuwa chupuchupu Seif Shariff Hamad atolewe ngeu na Wapemba wenye msimamo mkali, lakini akaokolewa na Blue Guard.

Baadaye Rais Amani Karume naye akaitisha mkutano na kueleza mkakati huo wa kuanzisha maridhiano na CUF. Serikali yetu ikapongeza jitihada hizo na Mataifa mbalimbali nayo yakapongeza hatua hiyo.

Huo ukawa mwanzo mpya kuelekea katika ‘Maridhiano’. Wakati wananchi wakiendelea kutafakari mwanzo huo mpya kati ya CCM Zanzibar na CUF, huku Bara akaibuka mpiga ramli mmoja anayeishi pale Magomeni Mwembe Chai.

Huyu akaja na kali kuliko zote. Kwa umaridadi kabisa bila soni akasema endapo mwana-CCM yeyote atakayechukua fomu za kumpinga Kikwete katika uteuzi wa kugombea urais ndani ya CCM atakufa ghafla.

Hii ni kwa mujibu wa utabiri wa huyu mpiga ramli anayedai kusifika Afrika Mashariki na Kati. Duh!.. watu wakataharuki, kulikoni jamani uchuro huu?. Mpaka sasa bado mjadala huu unaendelea.

Katika duru za siasa kuna watu wanaojulikana kama Political Thinkers (Wataalamu wa sayansi ya siasa au wachunguzi/wachambuzi wa masuala ya kisiasa).

Hawa Political Thinkers ndiyo hasa huwaongoza watawala wetu katika nadharia za mienendo ya wapinzani wao na wananchi(Political Behavourism au Political Behavoralism), na siku hizi wamekoleza kwa kusema ‘Post Behavoralism’. Wenyewe husema eti ni ‘The Mass’(wananchi) na ‘Political Elite’(wanazuoni wa kisiasa).

Inaeleweka kuwa ushauri wa kujenga mitandao ndani ya vyama ulikuwa wa hawa Political Thinkers ambao baadhi yao sasa wanaongoza taasisi kubwa za serikali ikiwemo chuo kikuu cha Dar es salaam.

Hawa ni watu hodari sana katika kusoma hali ya kisiasa na kutengeneza propaganda pale ambapo viongozi wa kisiasa wanapotaka kutekeleza agenda zao, ni watu ambao wakati mwingine hueneza uvumi ili kupima uelekeo wa umma(Public reaction) kabla ya maamuzi kamili.

Na maamuzi mengine hufanywa hata pale maandamano ya kupinga jambo lolote katika nchi au mgongano wa wananchi na serikali yao. Wenyewe huita ‘Divide and rule’, wagawanye na uwatawale. Kwa maana nyingine msingi mkubwa hapa ni kwamba kitendo cha wananchi kuridhia ‘maridhiano’ yale ndiyo majilio ya kuongezewa muda wa kutawala kwa Rais Karume.

Political Thinkers hawa kuna wakati pia huwatumia wapiga ramli kama Shehe wa Magomeni Mwembe Chai, yaani Shehe Yahya Hussein. Hupima uelekeo wa kisiasa na kutoa ushauri kuwa nini kifanyike pale panapotokea ombwe la kisiasa.

Sote tunajua kuwa huu ni mwaka wa uchaguzi. Kwa upande Bara, Rais aliyepo madarakani bado anataka kumaliza kipindi chake cha pili cha miaka mitano.

Lakini kwa upande wa Zanzibar, Rais Karume anamaliza ngwe yake ya miaka kumi na anatakiwa kuondoka, ili aje raisi mwingine, bila kujali atatokea CCM au CUF.

Maswali ninayojiuliza ni haya; kwanini suala la ‘maridhiano’ lijitokeze wakati huu wakati Rais Amani Karume anamaliza muda wake? Je kipindi chote cha miaka tisa alikuwa wapi? Ni kwanini Seif Hamad akubali kumtambua Rais Karume kipindi hiki?

Hivi nitakosea nikisema kuwa agenda hii ya maridhiano imekuja wakati huu, mahsusi ili kutengeneza mazingira ya Rais Amani Karume kuongezewa muda wa Urais kwa kisingizio cha kuweka sawa haya maridhiano?

Kwa nini nisiamini hivyo wakati tayari Wanachama na Viongozi wa vyama vyote viwili wameshafanya maandamano ya pamoja na kumuomba Raisi Karume akubali kuongezewa muda wa Uraisi ili aweze kuyaendeleza haya Maridhiano.

Hata hivyo wakati wa Kilele cha Sherehe za Mapinduzi, Rais Amani Karume akatangaza kuwa Uraisi wa Zanzibar ni miaka kumi tu kwa mujibu wa katiba, hivyo hatagombea tena.

Hii siyo danganya toto kweli? Kwanini wamsemee eti aongezewe muda halafu mwenyewe anajidai kukataa? Je iwapo katiba itarekebishwa na kuombwa aendelee tena na Urais atakataa?.

Hili tunaomba alijibu kwa yakini ili historia imhukumu. Upande wa Bara, CCM ikiongozwa na Katibu wake mkuu Luteni mstaafu Yusuf Makamba na katibu mwenezi Kapteni mstaafu John Chiligati, wakahamaki na kudai kuwa haiwezekani katiba ya Zanzibar kuchezewa, urais mwisho ni miaka 10.

Huu sio mkakati kweli wa kujaribu kupima upepo, naamini hapo baadaye Wazanzibari wakidhamiria katiba irekebishwe ili Rais Amani Karume aendelee kuongoza, hawa kina Makamba na Chiligati hawatatueleza mambo ya Wazanzibari waachiwe wenyewe????.

Je mpaka hapo lengo halijatimia na kuongezwa muda wa kututawala??? Jamani mimi siyo Mnajimu, au msoma elimu ya nyota, bali hizi ni Porojo zangu tu! Tukumbuke kwamba, kama alivyosema Aristotle, “man is a political animal” na kwamba madaraka ni matamu. Wenye nayo wanayakumbatia na kuyaengaenga ili wayahodhi daima dumu. Nadhani hiki ndicho kinachojaribu kufanywa kupitia hiki kiinimacho cha Maridhiano!
Mwaonaje waungwana??!!

Saturday, January 16, 2010

DADA YASINTA NIMEISHITUKIA JANJA YAKO

Dada yangu akiweka mikakati
Kwa dada yangu Yasinta,

Nimesikitishwa sana na kile ulichobandika katika blog yako ukidai kuwa wewe hutaki kuwa mwanaharakati wa kututetea sisi wanawake na watoto zetu, kama nilikunukuu vizuri umesema kuwa kuandika kwako makala za kutetea haki za wanawake sio kwamba unayo dhamira ya kuanzisha NGO.

Umedai kuwa hujawahi kuota na wala kuwaza kufanya kazi hiyo, bali unaamini kwamba, kuwa mwanaharakati haimaanishi kuwa na Organization. Kwamba huwezi kuwatetea wanawake na watoto isipokuwa mpaka uwe na NGO.

Pia ukabainisha kuwa umeamua kuweka mambo hadharani maana kuna vimbelembele washaanza kujifanya yule shehe wa Mwembe chai aliyetabiri kuwa mwana CCM yeyote atakayechukua fomu za kutaka kugombea urais kwa kumpinga Rais wa sasa Muheshimiwa Kikwete basi atakufa ghafla kwa kubanwa na ngiri. Vimbelembele hao wamekutabiria kuwa kwa kuandika kwako vimakala vya kujifanya una huruma sana na wanawake wanaonyanyaswa na waume zao ni kamchakato kako ka kuelekea kuanzisha Organization ya kuwatetea wanawake nchini.

Duh! Samahani dada nilisahau kukupa heshima yako. Nakupa shikamoo zako wewe na mumeo. Habari za huko ughaibuni mlipo, nasikia kuwa kuna baridi sana kiasi kwamba mabarafu yamejaa kila mahali mpaka chooni. Samahani kwa kutaja chooni, nimesahau kuwa hilo sio neno la kistaarabu, nilikuwa namaanisha toilet.

Dada kama nilivyoanza katika utangulizi wa barua hii, ni kwamba nimeishitukia janja yako. Unajua tangu uhamie ughaibuni dada umekuwa na akili sana.

Sio wewe mwaka juzi ulipokuja huku nyumbani ulianzisha NGO ya kutetea haki za wanawake na watoto kwa kushirikiana na yule binamu yako anayezaliwa na yule shangazi, ambaye analazimisha undugu baada ya kusikia kuwa umeolewa na mzungu kwa kudai kuwa eti zamani alikuwa akimbeba baba yako wakati bibi na babu yako wakienda shamba.

Huyu binamu yako ambaye inasemekana alifeli zaidi ya mara saba kuingia kidato cha pili huko Songea katika ile shule iliyoko pale Mfaranyaki, karibu na ule muembe dodo unaotumiwa na mafundi baiskeli ndiye uliamua kumshirikisha kuanzisha NGO yenu wenyewe ambayo mliipa jina la Ruhuwiko NGO for woman and children crying everyday.
Taasisi hiyo ambayo imesajiliwa na katibu kata ilikuja kwa kasi ya ajabu na inatishia kuvunja ndoa za watu, na mojawapo ya ndoa iliyovunjika ni ile ya yule mzee Ngatura mwenye wake saba.

Ndao iliyovunjika ni ya yule binti machepele wa saba kuolewa na yule mzee. Nadhani unamkumbuka yule binti aliyewahi kufumaniwa na mke wa mwalimu wa kufundisha ngoma za asili pale shuleni, na kutokana na umahiri wa kucheza lizombe yule binti alipewa Umanju wa kuongoza ngoma na mwalimu na kutokana na kupewa cheo hicho mwalimu wa ngoma akamgeuza kuwa kijumba kidogo chake na makutano yao yakawa kule kwenye shamba la kijiiji, na kama unavyojua wambea wa kijiji wakamjuza mke wa mwalimu wa ngoma na hivyo kuwekewa mtego na kufumaniwa. Si unakumbuka jinsi alivyopigwa mpaka akachaniwa nguo zote? Basi kutokana na aibu si ndio akahamishiwa katika shule ya jirani na baba yake ili kukwepa aibu.

Basi huyu binti baada ya kuachika huku akiongozwa na binamu yako wanataka mali za yule mzee zigawanywe sawa kwa sawa la sivyo kesi inapelekwa mahakaam kuu.
Hivi ninavyo kuandikia kuna mashauri zaidi ya wanawake 30 wanaotaka kuachana na wanaume zao kwa kutegemea kugawana mali walizochuma na wanaume zao. Kampeni hiyo ya kuachanisha wanandoa inaongozwa na hiyo NGO yenu na anayeingoza uasi huo wa kuvunja ndoa za watu ni huyo binamu yako.

Hivi sasa hali ni tete pale kijijini na wazee wa kijiji wameitisha kikao cha dharura kujaldili hali hiyo na wanatishia kuchangishana nauli ili waje Dar kumuona muheshimiwa rais ili anusuru ndoa zao zinazoelekea shimoni. Pia wanataka binamu yako huyo aondolewe haraka pale kijijini kwa ile staili ya kuwekewa karantini asikanyage tena pale kijijini iwe ni kwa sherehe au misiba.

Hata hivyo katika utetezi wake binamu yako huyo amejitetea kuwa eti hiyo kampeni ya kuachanisha ndoa za watu ni idea yako yaani kwa kiingereza suggestion yako maana alidai kuwa yeye siye msemaji mkuu wa hiyo NGO, bali ni mtekelezaji wa kile unachokiagiza ukiwa huko ughaibuni.

Sasa dada kwa kutaka kutuchota akili unajidai kuwa hutaki kuwa mwanaharakati wakati tayari ulishakuwa mwanaharakati tangu mwaka juzi. Kwa kuwa unatafuta umaarufu ili kutengeneza mazingira ya kupanua wigo wa hiyo NGO yako kutoka kijijini hadi kuwa NGO ya kitaifa baada ya kuona kule Ruhuwiko umeanza kupoteza umaarufu na ndio maana unataka kupata maoni ya wasomaji wako katika ile staili ya mchomeko, yaani ku bip kwa kiingereza.

Dada samahani naomba univumilie kwa haya ninayoyasema maana mie sitaki uje kuumbuka baadae, kwani Dar es salaamu sio sawa na Ruhuwiko, huku kuna ushindani wa hii biashara ya NGO, usipoangalia utatapeliwa wewe, kuna watu huku ni wasanii ile mbaya, anaweza kuja mwanamke akajidai amegombana na mumewe, na akipata msaada huyooo anaenda kuendelea na ndoa yake kama kawaida. Ukitaka kupanua wigo wa NGO yenu ihamie huku Dar inabidi utafute mganga ambaye anaweza kumwangalia mteja akajua kama huyu ana matatizo kweli au msanii tu.
Dada huku Dar NGO ni mradi wa watu wajanja ambao hutumia staili ya matatizo yenu ndio tijara yetu, na wengi wao ni wale walioshindwa kutofautisha ile dhana kujiajiri na kujitolea. Kwa wao kuitolea maana yake ni kuwekeza kwa kutumia matatizo ya wengine.

Yaani siamini kuwa na wewe umeingia katika kamtindo hako kwa kutafuta fedha kwa kutumia matatizo ya wengine. Nashawishika kuamini kuwa na wewe umefulia kimawazo, kwani hiyo mbinu yako nimeishitukia dada. Hapa Dar humpati mtu labda Kamala na Chacha kwani nao eti ni wanaharakati wa kuwatetea vijana…….LOL

Kwa leo naomba niishie hapa nikipata muda nitakujuza mengi juu ya NGO za hapa Dar.

Nakutakia siku njema.

Friday, January 15, 2010

NAJIVUNIA KUMFAHAMU

Alikuwa ndiye mtu wa kwanza kuniandikia email binafsi akinikaribisha katika ulimwengu huu wa blog, hiyo ni baada ya kusoma ujio wa blog yangu na kutoa maoni yake akinitia moyo.
Kama haitoshi kaka yangu huyu alidiriki kuitangaza blog hii ya Vukani kupitia blog yake ili kuiweka katika ramani ya ulimwengu wa wanablog,
Alizaliwa Aug 10, miaka thelathini iliyopita katika hospitali ya Brackenridge iliyopo AUSTIN, TEXAS. U.S.A
Brackenridge Hospital. Austin, TX (kama ilivyoonekana Aug 1980)
Ni mtoto wa tatu kati ya watano katika Familia ya Mzee Simon na Mama Paulina. Ametanguliwa kuzaliwa na Dada wakubwa wawili na kufuatiwa na kaka zake wadogo wawili (mapacha)

Familia nzima atokayo kijana huyu.
Alianza shule ya awali maarufu kama "vidudu" Lutheran Junior Seminary mpaka alipojiunga darasa la kwanza Shule ya Mazoezi Kigurunyembe. Baadae alihama na wazazi wake kwenda Nachingwea Lindi na kujiunga na Shule ya Mazoezi Nambambo, shule ambayo ndipo alipomaliza elimu ya msingi.
Elimu yake ya Sekondari aliipata katika shule za Ndanda Masasi Mtwara na Ihungo na Iluhya zilizopo Bukoba Kagera. Kisha akaenda Dodoma kwa mafunzo ya ufundi katika fani ya ufundi mitambo, utengenezaji vipuri na ukerezaji (Fitter Mechanics) ambayo aliisomea kwa miaka minne na kupata Grade One. Pia akiwa hapo chuoni alijifunza Ufundi Magari (Motor Vehicle Mechanics)
Alirejea Dar na kuendelea na pilika nyingine na mwaka 2001 alipata kazi katika kituo cha redio maarufu cha 100.5 Times Fm ambapo alikaa mpaka mwaka 2003.

Kaka yangu huyu hakuridhika na maaarifa aliyokuwa nayo hivyo aliondoka nchini na kuelekea nchini Marekani, nchi ambayo ndipo alipozaliwa ili kutafuta maarifa zaidi.
Kwa sasa yuko shule nchini humo akichukua masomo ya awali ya fani ya UHANDISI, huku pia akifanya kazi ambayo haiko mbali na fani hiyo. Ni mtengeneza vipuri katika kiwanda kinachojishughulisha na vipuri vya ndege cha Eaton Aerospace kilichopo Beltsville Maryland.
Nilipofanya mahojiano naye alikiri kuipenda zaidi fani ya uandishi wa HABARI na UHANDISI na anajitahidi kuchukua masomo ya wali yatakayomuwezesha kuunga fani zote.
Kwa upande wa starehe alisema kuwa yeye sio aina ya vijana wanaopenda kujirusha au kuendekeza starehe, bali ni kijana mwenye kipaji halisi cha uandishi wa habari za kijamii, uchambuzi katika medani ya kisiasa na kiuchumi pamoja na habari za kisaikolojia kupitia ukurasa wake binafsi maarufu kama Blog na kama akikereka, kufurahi, kusikitika au akiwa katika mood yoyote ile anapenda zaidi kusikiliza muziki wa kihisia, maarufu kama Reggae.
Anasema muziki huu HUFUNZA, HUBURUDISHA NA KUIKOMBOA JAMII TOKA UTUMWA WA KIAKILI.
Pia alikiri kuwa kwa sasa anayo familia, akiwa na mpenzi wake wa tangu mwaka 2001 aitwae Esther na hivi karibuni wamepata baraka ya mtoto mmoja aitwae Paulina Arianna.
Katika maisha tunayoishi yapo matukio ambayo hututokea, yapo ya kufurahisha na ya kukera au ya kuhusunisha. Mengine unaweza kuyasahau na mengine ni vigumu kuyasahau. Tukio ambalo kaka yangu huyu itakuwa ni vigumu kulisahau ni lile la ajali aliyoipata Disemba 22, 1999 nchini Kenya katika eneo la Nakuru kilomita chache kutoka jijini Nairobi, wakati alipokuwa akisafiri kuelekea Bukoba kula sikukuu na wazazi wake.
Ajali hiyo ambayo ilihusisha basi la Tawfiq na lori ambalo lilipaki njiani ilisabababisha vifo vya watu zaidi ya 20 na kuacha majeruhi kadhaa akiwepo yeye ambapo amekuwa akisumbuliwa na maumivu ya mgongo hadi leo, unaweza kuBOFYA HAPA ili kujua yaliyomkuta kaka yangu huyu.
Ni jambo la kujivunia kwamba pamoja na ajali hiyo ameweza kusimama na kuendelea na shughuli zake huko ughaibuni huku akiendelea kubukua kwa ajili ya kujikusanyia taaluma ili aweze kuisaidia jamii hii ya Kitanzania na dunia kwa ujumla.
Najivunia sana kumfahamu na najivunia kupendwa na yeye kwani kwangu mimi huyu ni zaidi ya kaka na nimenufaika sana na mchango wake, kwani ametumia muda wake mwingi kunikuza katika tasnia hii ya blog.
Napenda kumuombea maisha marefu yenye baraka na fanaka ili atakaporejea nchini tupate kufurahi kwa pamoja na kumshukuru mungu, maana neema zake ni za milele.
Ahsante sana kaka Mubelwa Bandio nashukuru kukufahamu

Monday, January 11, 2010

ILIKUWA NI SAFARI ILIYOJAA VITUKO

Ni mara yangu ya kwanza kusafiri kwa ndege kwenda nchi ya mbali, kwani nchi ambayo niliwahi kwenda kwa ndege ni Afrika ya Kusini tu. Ni safari ya ghafla mno ambayo sikuitarajia. Niliondoka jijini Dar mida ya saa nne usiku na ndege ya KLM, hadi Amsterdam, pale niliunganisha ndege nyingine hadi Stockholm Sweden katika uwanja wa ndege wa Arlanda. Hali ya hewa hapa ni ya baridi kweli na ingawa nilibeba makoti mazito ya baridi lakini nilihisi baridi ikipenya katika maungo yangu barabara.

Nilichukua taxi hadi kwenye Hoteli ambayo baba yangu alinifanyia booking. Safari yenyewe ilikuwa haijafika ukingoni kwani nilitakiwa kesho yake nisafiri kwa treni kwenda mji wa Uppsala ambapo ndipo chuo nilichotarajiwa kujiunga nacho kilipo.

Nililala pale na siku ya pili niliondoka na taxi hadi kituo cha treni ambapo kwa msaada wa dereva wa taxi nilikata tiketi yangu na kuingia kwenye treni. Ilituchukua takribani dakika arobaini na tano kufika katika huo mji, naambiwa kuwa kwa kawaida ni nusu saa tu, lakini kutokana na hali ya barafu iliyojaa katika njia ya reli ilibidi tutumie hizo dakika arobaini na tano.
Nilifika katika huo mji wa Uppsala na kuchukua taxi ambayo ilinipeleka hadi chuoni, na nilipoangalia saa yangu ilinionyesha kuwa ni saa sita za mchana, niliopokelewa na kupelekwa ofisini kwa mkuu wa chuo ambapo nilipata maelekezo yote ya pale chuoni kisha nikakabidhiwa kwa mama mmoja wa makamu ambaye nadhani ndiye msimamizi wa zile apartment pale chuoni, alinipeleka hadi kwenye chumba changu ambapo nilimkuta binti mwingine ambaye alijitambulisha kwangu kuwa ni raia wa Finland, tulisalimiana na akapewa maelekeza kuwa tutakuwa tukiishi pamoja katika chumba kile hadi tutakapomaliza masomo. Kusema kweli alinipokea kwa bashasha, na kutokana na kusikia sifa nyingi juu ya nchi yangu ya Tanzania pamoja na sifa za mlima Kilimanjaro, binti huyu alikuwa ana hamu ya kutaka kujua mengi juu ya mlima huo na pia mbuga zetu za wanyama.
Binti wa kizungu akaanza maswali yake akitaka kujua habari za mlima huo uko upande gani wa nchi yetu, una urefu gani, ukitaka kupanda itakuchukua muda wa siku ngapi, je mbuga za wanyama nazo, ziko ngapi, ukitaka kwenda utafikaje, na itakugharimu kiasi gani kulipia kiingilio ili mradi yalikuwa maswali lukuki.

He! wenzangu nikaona naumbuka sasa, nilichojibu ni upande ambapo mlima Kilimanjaro upo ambapo ni mashariki mwa nchi yetu yaani mkoani Kilimanjaro, mengine nilitoka kapa, na kuhusu mbuga za wanyama nilizungumzia tu mbuga ya Ngorongoro ambayo niliwahi kuitembelea mwaka jana mwanzoni, zaidi ya hapo maswali mengine nilimwahidi kumjibu wakati mwingine, kwani nilijifanya kuwa nimechoka na safari, lakini moyoni nilipanga nikipata muda niende ubalozini kwetu nikatafute zile taarifa ili kuepuka fedheha ugenini, maana hawa wazungu wanadhani kwa kuwa nimezaliwa Tanzania basi nafahamu kila kitu.

Kwa kuwa ilikuwa ni ijumaa hapakuwa na ratiba yoyote kwa sababu chuo ndio kilikuwa kikiendelea kupokeaa wanafunzi kutoka nchi mbalimbali. Niliamua kujipumzisha kidogo.Niliamka majira ya saa kumi jioni, nikaelekea katika café ya pale chuoni ili kupata kahawa kupunguza baridi, nilipofika pale café niliona call box, nikaona huo ndio wakati muafaka wa kumpigia dada yangu Yasinta simu ili kumjulisha kuwa niko Sweden kwa masomo.

Kwanza dadaYasinta hakuamini alidhani namtania, lakini baada ya kumweleza mahali nilipo yaani Uppsala aliniamini na aliniahidi kunifuata siku inayofuata yaani jumamosi ili anipeleka kwake. Dada Yasinta alifurahi sana na hata baada ya kuongea naye kwa simu nilipotoka pale nilirudi chumbani kwangu na kwa kuwa pale chumbani kwetu kuna computer room, niliingia hapo tukachat kwa takriban masaa matano, tulizungumza mengi na aliniambia kuwa familia yake imefurahia ujio wangu kwani hatimaye sasa watamuona Koero live.

Ni kweli siku iliyofuata majira ya saa nne, nilikuwa bado niko chumbani kwangu nikipitia makabrasha ya maelekezao ya namna ya kuishi pale chuoni pamoja na malezo mengine juu ya kozi yangu nitakayoichukua. Ghafla nikapigiwa simu na sekretari wa mkuu wa chuo kuwa nina wageni wako mapokezi.
Nilitoka haraka kwani nilijua tu kuwa huyo angekuwa ni dada Yasinta. Anitembeee nani hapa Sweden zaidi yake? Nilipokaribia mapokezi nilimuona dada Yasinta akiwa na mumewe na nyuso zao zilikuwa zimepambwa na tabasamu pana, walikuwa wamesimama mahsusi kunipokea na nilipowafikia dadaYasinta hakusubiri, alinirukia kwa furaha na kunibeba, na hivi nina kamwili kadogo , alinibeba utadhani mama aliyembeba mwanaye, kila mtu pale mapokezi alishangaa, lakini mumewe yaani baba Camilla alisema kitu kwa kiswidish, nadhani alikuwa akiwaeleza jambo kuhusu mimi.

Tulizungumza kwa kifupi na bila kupoteza muda niliomba fomu maalum ya kuomba ruhusa ya kutoka nje ya chuo na baada ya kuijaza fomu hiyo tuliondoka pale chuoni na gari walilokuja nalo wenyeji wangu. Njiani tulizungumza mambo mengi sana juu ya blog zetu, tuliwazungumzia wana blog wenzetu kina kaka Mubelwa, Kamala, Kitururu, Markus aka Mcharuko, Da’ Subi, Da Mija, Da Schola Mbipa, kaka Bwaya, Da’ My little world, Ka Godwin Meghji, na wengine weeeengi tu.
Ingawa safari ilikuwa ni ndefu kiasi, lakini niliiona fupi kutokana na mazungumzo. Tulipofika nyumbani nilipokelewa na Camilla na Erik kwa bashasha na walinifurahia sana. Nyumba yao ni nzuri ikiwa imezunghushiwa uzio mfupi hivi huku ikiwa imenakshiwa na maua ambayo yalikuwa yameanza kunyauka kutokana na barafu, tulipoingia ndani nilikutana na hali ya joto kutokana na hita zilizowashwa ili kupunguza baridi.
Dada Yasinta alitengeneza chai haraka haraka na tukajumuika pale mezani kupata chai huku tukiendelea na mazungumzo, pamoja na kwamba kuna dinning room lakini jiko la dada Yasinta ni kubwa kiasi kwamba kulikuna na meza kubwa na viti ambapo hutumika wakati mwingine kwa ajili ya kulia chakula pale pale jikoni.

Nililipenda sana jiko lao na mpangilio mzima wa nyumba yao. Tulizungumza sana na kutaniana na shemeji yangu huku dada Yasinta akiandaa chakula cha mchana.Dada Yasinta alinifahamisha kuwa jioni walikuwa na mpango wa kwenda kucheza mchezo wa kuteleza kwenye barafu, yaani skiing, waliniuliza kama nitaongozana nao, niliwakubaliana na walifurahi sana.

Jioni ilipofika tulifungasha mizigo yetu ambapo ilikuwa ni vifaa vya kutelezea katika barafu, kisha tukaondoka na gari hadi kwenye eneo linalotimika kwa mchezo huo, tulipofika tulikuta watu wengi sana wakicheza mchezo huo, Muafrika nilikuwa ni mimi na dada Yasinta pekee wengine walikuwa ni wazungu watupu. Tulivaa vifaa vyetu na kutokana na kuwa mgeni wa mchezo huo, Dada Yasinta alinielekeza namna ya kutumia vifaa hivyo , kisha tukaanza kuteleza.

Ingawa nilikuwa nikianguka mara kwa mara, lakini shemeji yangu Torbjorn alikuwa akinisaidia kuninyanyua na kuniekeleza namna ya kutumia vifaa hivyo, mpaka nikamudu. Nilikuwa nateleza kwa uhodari mpaka kila mtu akawa ananishangaa.

Nilikuwa nateleza kwa kasi sana, mara nikajikuta nikiwaacha wenzangu hatua kadhaa nyuma, mara ghafla nikajikuta nikielekea kwenye mteremko mkali, nilishindwa kujizuia, kumbe kulikuwa na kibao kilichokuwa kikitahadharisha kuwa mbele ya lile eneo kuna bonde na ilikuwa hairuhusiwi kuvuka pale, nilisikia watu wakipiga kelele nyuma yangu lakini nilishindwa kujizuia, nikajikuta naelekea bondeni , “ mama wee nakufaaaaaa” nilipiga kelele, lakini ghafla nilisikia mtu akiniita kwa sauti “Koero nini” Nilishtuka na kuamka, huku mapigo ya moyo yakinienda mbio na jasho likinitoka, nilimuona mama akiwa pembeni yangu.
Kumbe nilikuwa nimelala na ile ilikuwa ni ndoto tu. Mama alinijulisha kuwa nilikuwa nikipiga kelele mpaka wakaamka wakidhani labda nimevamiwa. Kwa kuwa huwa sifungi mlango wangu wa chumbani. ilikuwa ni rahisi kwake kuingia chumbani kwangu ili kuangalia kama nimepatwa na nini.

Nilipoangalia nje kulikuwa kumepambazuka, nilimuomba mama maji ya kunywa na na baada ya kunywa, nikamsimulia juu ya ile ndoto. Mama alicheka sana akanimbia kuwa ni kweli baba amenitafutia chuo nje ya nchi na si muda mrefu nitaondoka nchini kwenda kukariri ujinga wa wengine.

Saturday, January 9, 2010

DICKSON, KWA NINI ULINITENDEA HIVI?

Ni saa kumi jioni, ndio nimeamka kutoka katika usingizi wa mchana. Hapa nilipo nimesimama dirishani, nikitazama mandhari ya huko nje, kuna manyunyu kiasi na ngurumo za hapa na pale.

Hali ya hewa imebadilika katika jiji hili la Dar na kuna hali ya kijiubaridi kwa mbali na hali ya mvua za kiasi na hivyo kupunguza hali ya joto ambalo limekuwa ni la kutisha lisilo na mfano utadhani tupo katika nchi ya Sudan au Chad, naambiwa kuwa hali ya joto imefikia kiasi cha digrii 37, hiki ni kiwango cha kutisha sana tofauti na miaka ya nyuma.

Siku ya leo sikwenda kazini nilijihisi kuwa na homa ya malaria , nikaona ni vyema nikapate matibabu, na baada ya matibabu nikaona nijipumzishe.Kupitia dirishani, nawaona watoto wakicheza mpira, huku wakifurahia hii hali ya manyunyu. Wanacheza kwa furaha huku wakicheka, nadhani ni kutokana na hii hali ya hewa. Nikiwa bado nimewatumbulia macho, mtoto mmoja anaupiga mpira na kuingia ndani ya uzio wa nyumba yangu, kutokana na kuvutiwa na mchezo wao nikaamua kutoka na kuwarudishia mpira wao, nilitamani waendelee kucheza, kwani nilivutiwa sana na watoto wale kwa jinsi walivyokuwa wakicheza kwa furaha.

Baada ya kuwarudishia mpira wao, walinishukuru na kunishangilia kisha wakaendelea na mchezo wao. Ilionekana walifurahishwa na kitendo changu hicho.

Dickson, nimeamua kuchukua karatasi na kalamu ili kukusimulia haya kutokana na uchungu nilio nao, uchungu ambao kamwe sijui kama nitakuja kuusahau. Kidondo ulichoniachia bado hakijapona na kila uchao maumivu yako pale pale. Kwa kifupi sijapata tiba na sijajua ni lini kidonda hiki kitapona.

Dk, kama nilivyozoea kukuita wakati ule wa kilele cha mapenzi yetu, naomba nikuite kwa jina hili katika waraka huu, naamini haitakuwa ni tatizo kwako. Ni mwaka wa kumi sasa tangu uliponiacha na kuoa mwanamke mwingine eti kwa sababu sikubahatika kukuzalia mtoto. Pamoja na kunieleza kuwa ilitokana na shinikizo la wazazi wako, lakini naamini wewe ndiye uliyekuwa na uamuzi wa mwisho wa kuamua hatima ya mapenzi yetu. Kuwasingizia wazazi na ndugu zako naamini haikuwa ni sababu stahili ya kukwepa lawama. Dk, naomba ukumbuke kiapo chetu, uliniambia kuwa mimi na wewe mpaka kufa, lakini mbona bado tuko hai, lakini umeniacha, Dk, kwa nini lakini?

Kumbuka kwamba matatizo niliyokuwa nayo, wewe ndiye chanzo chake, na ni wewe uliyenishawishi hadi kufikia uamuzi ambao ndio uliosababisha mie kutopata mtoto.
Ilikuwa ni mwaka 1990, tulikuwa ndio tumengia kidato cha sita, na tulikuwa katika kilele cha mapenzi yetu. Ni katika kipindi hicho ndipo nilipojihisi kuwa mjamzito. Nilipokueleza ulishtuka sana, na ulinieleza kuwa hutarajii kuitwa baba kabla ya kumaliza masomo, ulinishawishi tuutoe ujauzito ule ili kuninusuru niendelee na masomo, ulidai kuwa isingekuwa vyema nisimamishwe shule kwa kuwa mjamzito halafu wewe uendelee kusoma peke yako. Tulikuwa tumejiwekea malengo, kuwa tuhakikishe tunasoma mpaka chuo kikuu, hukutaka tutibue malengo yetu.

Nilikupinga kwa maelezo kuwa hata nikisimama shule bado nitakuwa na nafasi ya kudurusu kidato cha sita baada ya kujifungua na nikakuhakikishia kuwa hata kama ukinitangulia sio vibaya, nitahakikisha namaliza chuo kikuu na kutimiza ndoto zetu. Ulinipinga sana, na baada ya kuvutana kwa muda mrefu huku miezi ikiendelea kuyoyoma hatimaye niliamua kukubaliana nawe, na tukiwa pamoja tulikwenda kuutoa ujauzito ule uliokwisha fikisha miezi minne.

Haikuwa kazi rahisi, kwani daktari aliyefanikisha operesheni ile hakuifanya kwa ufanisi kwani hata baada ya kurudi nyumbani hali yangu haikuwa nzuri, niliendelea kusumbuliwa na tumbo. Tuliporudi hospitali nilisafishwa na kuruhusiwa kurudi nyumbani. Tulirejea shuleni na kuendelea na masomo hadi tukamaliza kidato cha sita. Kwa bahati nzuri wote tulichaguliwa kujiunga na chuo kikuu mlimani, wewe ukisomea fani ya uhasibu na mimi nikisomea fani ya sosholojia.

Tulifanikiwa kumaliza pamoja na kufaulu, tulifanya sherehe ya pamoja na kuingia katika ajira pamoja, mimi nikiajiriwa serikalini na wewe ukiajiriwa katika shirika la Umoja wa Mataifa {UN}.

Baada ya miaka miwili tangu kuingia katika ajira, tuliamua kufunga ndoa ambayo ilikuwa na mbwembwe nyingi. Maisha yetu ya ndoa yalikuwa ni ya upendo na amani. Sio kwamba tulikuwa hatugombani, la hasha, tulikuwa tunagombana lakini hiyo ilikuwa ni njia mojawapo ya kustawisha mapenzi yetu, kwani kupitia kugombana kwetu, tulipata fursa ya kila mmoja kufahamu hisia za mwenzie.

Mwaka mmoja tangu tufunge ndoa tuliamua kuzaa mtoto, na baada ya majaribio kadhaa kushindikana tuliamua kwenda kwa watalamu wa tiba ili kupata ushauri. Ni katika kipindi hicho ndipo tulipopata taarifa ambazo zilinipenya moyoni kama msumari wa moto. Tuliambiwa kuwa siwezi kupata mtoto milele kwa kuwa mirija yangu ya uzazi imeathirika baada ya kile kitendo cha kutoa mimba tulichokifanya wakati ule.

Hatukata tamaa, tuliwatembelea wataalamu kadhaa wa tiba wakiwemo wa tiba za asili lakini hatukufanikiwa kupata mtoto. Miaka minne baadae tangu tuoane ndugu zako walianza manung’uniko ya chinichini, lakini hata hivyo walifikia hatua ya kunieleza waziwazi kuwa mimi ni mgumba siwezi kukuzalia mtoto, maneno hayo yalinichoma rohoni, lakini nashukuru ulikuwa pamoja nami na uliniahidi kunilinda. Hukuishia hapo ulifikia hatua ya kula kiapo kuwa mimi na wewe mpaka kufa.

Nilifarijika na msimamo wako, na ulinipa nguvu kila wakati. Mwaka mmoja baada ya kiapo chako ulianza kubadilika, ulikuwa ukichelewa kurudi nyumbani na nikikuuliza majibu yako yalikuwa ni ya mkato. Chakula ulikuwa huli nyumbani na kama hiyo haitosh ulifikia hatua ya kunipiga kwa sababu ya kukumbusha kule tulipotoka. Mateso yalizidi sana na ndugu zako walikuja kunieleza wazi kuwa unarajia kuoa hivyo nijiandae kuwa na mke mwenza, kwa kuwa huyo mchumba wako ameshakuzalia mtoto wa kiume.
Dk, umesahau kuwa hata mie kama nisingetoa ule ujauzito ningekuwa na mtoto wa kiume kama alivyotueleza yule daktari, na uamuzi wa kutoa ule ujauzito haukuwa ni wangu bali ilitokana na shinikizo lako.

Nilipokuuliza kuhusu wanavyosema ndugu zako, ulinijibu kwa mkato kuwa ni kweli na ulidai kuwa haikuwa na ubaya wowote kwa kuwa amekuzalia mtoto, kitu ambacho mimi nimeshindwa.

Nililia kwa uchungu sana na niliamua kuondoka, sikutaka kuishi na mke mwenza kwa kuwa hiyo ni kinyume na mafundisho ya dini yetu ya kikristo. Nilifanya juhudi za kutafuta suluhu kupitia kwa mchungaji wetu lakini haikuzaa matunda na hatimaye tukatengana, na wewe kumuoa huyo binti aliyekuzalia mtoto.

Sikukata tamaa, niliamini tu kuwa iko siku nitakuja kupata mtoto siku moja. Mwaka jana niliamua kwenda nchini Afrika ya Kusini, hiyo ni baada ya kushauriwa na baadhi ya madaktari bingwa, na nilipofika kule nilipatiwa matibabu na kupandikizwa ujauzito. Hivi ninavyokuandikia waraka huu ninao ujauzito wa miezi saba, na ninatarajia kupata mtoto wa kiume mungu akinijaalia.

Hiyo yote ni kutaka kukuthibitishia kuwa kwa mungu kila jambo linawezekana. Nilipokuwa nikiwaangalia wale watoto waliokuwa wakicheza mpira, nilikuwa nimeshika tumbo langu na nilihisi mwanangu na yeye akirukaruka kwa furaha akifurahia kile ninachokiona kupitia kwangu. Naamini na yeye atakuwa ni mchezaji mpira mahiri, kwa kuwa mama yake pia ni mshabiki wa mpira wa miguu.

Naomba nihitimishe waraka huu kwa kukutakia maisha marefu ili uje kushuhudia miujiza ya Mwenye enzi mungu, kwamba kwake yeye kila jambo linawezekana.

Ni mimi mke wako wa zamani.

Kolambo Kiangi

Ndugu Msomaji, jana nilimtembelea shangazi yangu, nilimkuta amesimama dirishani akiangalia watoto wakicheza mpira. Shangazi yangu huyu amepambana na mikasa ya dunia, na baada ya kuzungumza naye ndio nikaona niandike huu waraka.

Ni mkasa wa kweli uliompata shangazi yangu, nami kwa kutaka kufikisha ujumbe kwa njia ambayo itamuwezesha msomaji kujifunza, ndio nikaandika waraka kwa mtindo huo.

NB: Jina la Dickson sio la muhusika.

Thursday, January 7, 2010

MAJIBU YA DADA SUBI KWA BARUA YANGU

Dada Subi

Kama kumbukumbu zenu haziko mbali, ni kwamba mwaka jana nilimuandikia dada yangu Subi barua ya siri nikimjuza hali halisi ya huku nyumbani na maandalizi ya uchaguszi mkuu octoba mwaka huu, kwa yule asiyekumbuka anaweza kujikumbusha kwa kubofya hapa.

Na haya ndiyo majibu ya dada Subi katiaka kujibu bara yangu. Ni jambo la kujivunia kuwa kumbe dada yangu huyu aliipata barua yangu na kupata muda wa kukaa chini na kunijibu barua yangu.

Naomba muunganr nami katia kuisoma barua hii……………………

Mpendwa mdogo wangu Koero,
Salam sana. Na baada ya salam, natumai u mzima wa afya. Ni matumaini yangu kuwa ndugu na jamaa zetu hapo Kijijini ni wazima na wanaendelea vizuri kwa kudra za Mwenyezi Mungu.

Dhumuni la kuandika barua hii ni kupenda kukushukuru sana kwa barua yako uliyoniandikia tarehe 16 mwezi wa Disemba 2009 na kunieleza mengi ya hapo Kijijini. Mara ya mwisho nimepata ujumbe toka nyumbani ni pale kaka Mtoahanje aliponitumia ujumbe kuwa ametindikiwa fedha kiasi za kulipia ada ya shule, nikaahidi kumsaidia kadiri ambavyo ningeweza. Sasa umenieleza tena kuhusu hali ya henia ya babu, nilijitahidi sana kuwasiliana na Mbega kuhusu suala hilo siku mbili tu baada ya kusoma ujumbe wa Mtoahanje lakini kwa habati mbaya, Mbega amekuwa msemaji sana siku hizi kuliko mtendaji, si kama vile alivyokuwa kijana mdogo na mchapakazi. Nitajitahidi sana niwasiliane na rafiki yangu Mwelumbini, yule mototo wa mzee Shelukindo tuliyesoma naye wote Mazoezi, angalao aweze kufika na kumwona Mzee na kutafuta tiba inayofaa.

Nimefurahishwa sana na maendeleo ya usafiri kutoka baiskeli hadi pikipiki lakini nimehuzunishwa sana na mambo vijana wa mtaani wanayowatendea dada na mama zetu huko njiani. Juzi juzi hapa, rafiki yangu alipiga simu akaongea na Bibi yake ndipo aliposimuliwa masahibu yaliyompata siku moja akirejea toka shambani alikokuwa amekwenda kufunga majani ya wale ng’ombe wake (hawa wazazi wetu na ng'ombe hawaachani hata uwaagizie pikapu ya maziwa kila siku asubuhi). Basi alipokuwa katika kijia pale Komkonga, ghafla akatokea kijana mmoja wasiyefahamiana, na katika kupishana, salam akampa, ‘emcheku, urevedi?’, bibi akaitika, ‘ni jedi’, huku wakipishana kila mtu kuelekea upande wake. Sasa kwa kuwa wazazi wetu huwa na hisia za ziada, baada ya mwendo wa hatua chache, bibi alihisi kuwa kuna mtu anamfuata nyuma, lakini akapuuzia kidogo, Kabla ya kuendelea na umbali wowote wa kuhesabika, Bibi akastukia kanigwa shingoni na kupigwa ngwala, akaanguka chini pu! Majani aliyokuwa amebeba kichwani yakaanguka na kunde alizokuwa amefungia humo zikamwagika na kusambaa majanini. Kumbe kijana alikuwa amejiandaa tayari kwa kumbaka BIbi. Kwa bahati Bibi ujasiri ukamjia, akajitahidi akafungua mdomo wake kisha akamuuma kwa nguvu kweli sehemu ya mkono (kwa kuwa alizibwa mdomo na yule kijana kwa kutumia sehemu ya mkono), ndipo yule kijana alipoondoa mkono wake na kuugulia maumivu, Bibi akabeba jiwe moja la moram lililokuwa pembezoni hapo kijiani, akamkoboa nalo yule kijana kwenye kipaji cha uso upande wa kushoto. Bibi naye amekula chumvi nyingi, hivyo alijua haswa pa kuumiza, wala hakufanya ajizi. Baada ya hapo akajitahidi kupiga ukelele kwa sauti kubwa, ndipo kijana akaogopa na kwa haraka akajivuta na kukimbia, akatokomea katikati ya shamba la mahindi. Ndipo bibi akanyanyua mzigo wake wa majani, akaufunga tena vizuri pamoja na kunde chache azizoweza kusomba pale kijiani, akaendelea na safari ya kurudi nyumbani. Hivi ninavyokueleza, si kisa cha kutunga hiki, ni kweli kimemtokea huyu Bibi na alama ya jino lake dhaifu kumeguka baada ya purukushani na kumuuma yule kijana bado ipo, ndiyo sababu ya maumivu yake ya jino na kichwa hadi leo.

Hali hiyo imenishangaza sana kwani bado inaendelea japo viongozi wapo. Kwani Mzee Mkiramweni siku hizi hawamsikilizi tena anapotoa maagizo? Na vijana wanashindwa kwenda mashambani kulima au katika biashara sokoni wao wanakalia kusubiri wasafiri tu na kisha kuwabaka? Hali haikuwa nzuri wakati sisi tunakua, nakumbuka hivi vituko vya kubaka tulikuwa tukivisikia kwenye vile vikao vya wazee na akina mama mara kwa mara jioni pale kwa Mzee Mkiramweni kila kilipotokea kituko. Walikuwa wakiitwa vijana waliotenda haya makosa na kukalishwa kikao na kuadabishwa, sisi watoto tulikuwa tunasikia tu lakini hatuelewi yanayojiri kikaoni. Ila kwa wakati huu, hali inazidi kuwa mbaya na cha kusikitisha zaidi, hakuna anayewasikiliza akina Mzee Mkiramweni tena. Tunakoelekea nako yaonesha ni kubaya zaidi.

Sasa leo mdogo wangu Koero, wacha niishie hapa. Haya mengine nitayajibu nitakapopata nafasi ya kuketi tena chini kitako kwani muda huu zimebaki dakika chache kabla ya muda wa kwenda kibaruani haujawadia. Huku ng’ambo inabidi kufanya kazi kwa juhudi kweli na maarifa mengi ili kukwepa hatari ya kupoteza kazi na kukumbwa na adha ya kutafuta kazi, wakati mwingine hata yabidi kufanya kazi tatu kwa siku alimradi kujipatia fedha ya kuweza kumudu mahitaji muhimu kama vile kodi ya pango, gharama za umeme, maji na hata usafi wa mazingira ya nyumba. Kila kitu huku ni pesa na pesa yenyewe ina thamani sana, upatikanaji wake mgumu na kadiri uthamani wake unavyozidi, ndipo upatikanaji wake unavyokuwa mgumu na vitu kuuzwa kwa bei ya kuruka. Siku utakapokuja huku utaweza kujionea mwenyewe na kufahamu ni kwa nini inatuwia vigumu kuwasiliana nanyi mara kwa mara.

Nisalimie sana Babu, Bibi na akina shangazi na mjomba, hasa yule mjomba Eliewaha wa kule bonde la mpunga. Nisalimie pia rafiki zangu hapo kijijini, usisahau kuwaambia kuwa bado ninawakumbuka sana.

NB: Utakapoandika tena, ukumbuke kunitumia namba ya simu ya dukani kwa Mangi ili nikipata nafasi nipige simu niongee nanyi niweze kusikia sauti zenu.

Wasalaam,
Dada yako akupendaye,
Subi

Monday, January 4, 2010

HAIKUWA BAHATI, BALI MKOSI-SEHEMU YA MWISHO


ILIPOISHIA........

Kwa kifupi nilianza uhusiano na yule mzee na alinishauri niache kazi kisha akanitafutia nyumba kubwa nzuri maeneo ta Mikocheni.

ENDELEA KUSOMA HAPA..........

Nililazimika kuacha kazi baada mpenzi wangu kunifungulia miradi ya Duka la nguo (Boutique) maeneno ya Msasani na Salon ya kike kubwa na Mini Super market, na miradi yote hiyo ilikuwa maeneo ya Kinondoni.

Kwa mida mfupi maisha yangu yalibadilika na kuwa ya juu, nilikuwa namiliki magari matatu ya kifahari na na nilinunua Kiwanja maeneo ya Mbezi beach na kuanza ujenzi bila kumshirikisha yule mzee, ambaye ndiye mfadhili wangu.

Siku moja jioni nakumbuka ilikuwa ni Jumapili wakati nikiwa nimejipumzisha nyumbani, nilisikia mlango ukibishwa hodi, nilimtuma mfanyakazi wangu wa pale nyumbani akafungue mlango. Mara aliingia mama mmoja wa makamo hivi.

Alikuwa ni mama wa heshima, nilikmaribisha sebuleni na kumuuliza kama angependa kinyaji gani, alikataa kupewa kinyawaji chochote, lakini alionekana kuzungusha macho huku na huko kama vile alikuw aanakagua kitu, nilimuacha amalize hamu yake kwani nilidhani alivutiwa na mapambo ya pale sebuleni.

Baadae alisema, “Nadhani wewe ndiye Gifti kama sjakosea” nilimjibu kwa utulivu kuwa ndiye mimi….alishusha pumzi na kusema, “Je unamfahamu Mzee Alex?” Nilishtushwa na swali lile na nilijihisi mapigo ya moyo wangu yakienda mbio, lilikuwa ni swali la Kushtukiza sana. Nilijikakamua na kumjibu kuwa simfahamu mtu huyo.

“Sikiliza mwanangu, wewe ni sawa na binti yangu, na sijui wa ngapi, maana unaonekana kuwa bado u binti mdogo sana, kwa umri ulio nao haistahili kutembea na wanaume za watu tena baba zako ambao wanaweza hata kukuzaa, mbona vijana wenzio wako wengi tu, kwa nini usiwatafute hao, mpaka utembee na mume wangu? Nimeishi naye miaka zaidi ya 40, leo hii binti mdogo wa kukuzaa unataka kunivunjia ndoa yangu?” Aliniambia kwa upole kama vile mama aongeae na bintiye

Ukweli ni kwamba maneno yale yalinishtua sana, nilijikuta nikiwa nimemkodolea macho. Nakumbuka niliwahi kumuuliza mzee Alex kuwa familia yake iko wapi na alinijibu kuwa inaishi nchini Malawi na watoto wake wanasoma nchini Uingereza.

Nilikuwa najivinjari na huyu mzee kwa uhuru hasa na sikuwa na wasiwasi kuwa kuna siku nitakuja kukutana na mtu ambaye angekuja kunikabili na kuniambia kuwa natembea na mumewe.

“Mama samahani naona umepotea nyumba huyu mzee simjui na wala sijui unamzungumzia nani hapa,……tena nakuomba uondoke maana mume wangu atarudi hivi punde asije akakufanyia jambo ambalo utalijutia maishani mwako” Nilijikakamua na kumjibu yule mama kwa upole.

"Binti sikiliza, sipendi niingie kwenye kubishana na wewe, wakati ninao ushahidi wa kutosha kuwa unatembea na mume wangu, lakini……..sikutaka kulisema hili, ila kwa kuwa unaonekana mkaidi, nitakueleza,............ mume wangu si salama, ni muathirika, naomba ukapime afya yako, ili uanze kuishi kwa matumaini” alimaliza kusema na kunyanyuka ili aondoke.

Moyo ulinilipuka na nilijikuta nikiropoka, “He, Mzee Alex ni muathirika?” nilijikuta nikiongea kwa sauti.
"Huna haja ya kukata tamaa, bado unayo nafasi ya kuishi, nenda kapime, mimi nilijigundua miaka kumi iliyopita na mpaka sasa ninaishi kwa matumaini, hata wewe unayo nafasi hiyo” Yule mama alinijibu kwa upole na kisha aliondoka zake na kuniacha nikiwa nimeduwaa, nisijue la kufanya, nilikurupuka na kwenda chumbani, nilimeza vidonge vya usingizi na kujitupa kitandani.

Niliamka usiku wa manane kama saa nane za usiku hivi, nilikuwa na njaa, nilikwenda jikoni nikajitengenezea mkate wa nyama na juisi nikala, kisha nikakaa kitandani na kuanza kutafakari maneno ya yule mama. Niliona kama vile ile ilikuwa ni ndoto na huenda ingekwisha muda wowote, lakini hapana haikuwa ni ndoto ulikuwa ni ukweli mtupu.

Siku iliyofuata nilimpigia mzee Alex simu lakini haikupokelewa nilituma ujumbe lakini hakujibu, baadae alinijibu kuwa yuko nchini Uingereza na angerudi baada ya mwezi mmoja, kuanzia siku hiyo namba yake ilikuwa haipatikani na mawasiliano na yeye yakakatika, nikaachiwa segere nilicheze peke yangu.

Namshukuru shangazi yangu aliweza kuniliwaza na kunipeleka kupimwa na kweli niligundulika ni muathirikawa ukimwi, na ninaishi kwa matumaini sasa. Sijaanza kutumia dawa ila najitahidi sana kula vyakula vizuri na kufanya mazoezi.

Kwa kweli nina wakati mgumu sana, kwani kwa jinsi muonekano wangu ulivyo, nasumbuliwa sana na wanaume vijana na wazee, wananitaka kimapenzi na wengine wanataka wanioe, na nikiwaambia kuwa mimi si salama nimeathirika, wanabisha kabisa na wengine wanadiriki kusema hata kama nimuathirika hakuna shida hata akifa powa tu lakini atakuwa amefaidi. Yaani nashindwa kuwaamini wanaume, tena wengine wameoa na wana familia zao, lakini we kutwa kunivizia.

Namshukuru mungu nimemudu kujikubali na kuyakubali matokeo, najua ni lazima nitakufa, siku moja lakini namshukuru mungu kwa kunipa ujasiri huu nilionao mpaka sasa nimemudu kuishi kwa amani na kuepuka vishawishi.

Nawaasa vijana wenzangu hasa mabinti wa shule kuwa sio kila king’aacho ni dhahabu, ukimwi upo na unaua, tujiepushe nao.

***************MWISHO************

Saturday, January 2, 2010

HAIKUWA BAHATI, BALI MKOSI

Nikafunguliwa biashara kubwa

Tunaishi katika maisha yenye vishawishi na matamanio makubwa, kuna wakati mtu anaweza kujikuta akiwa mtegoni asijue hata kujinasua. Ama kweli dunia hii ni hadaa na ulimwengu ni shujaa, wakati unapoamini kuwa umepata bahati unaweza kushangazwa na matokeo ambayo kamwe hukuyatarajia, kuna msemo mmoja unasema kuwa kama mlango mmoja ukifungwa mwingine umefunguliwa. Kuna haja ya kuwa makini kwani kuna uwezekano huo uliofunguliwa ukawa ndio nuksi kuliko uliofungwa.
Naamini kinachohitajika zaidi ni subira kuliko kukimbilia mlango mwingine ulio wazi, kuna uwezekano kuna nyoka humo.

Hivi karibuni nilimtembelea rafiki yangu mmoja, ambaye familia yao ni family friend na familia yetu, nilipofika pale alinitambulisha kwa shangazie ambaye aliwatembelea na kutokana na uchangamfu wangu tulizoeana kwa muda mfupi, tuliongea mengi na katika maongezi yetu alinisimulia mkasa wake aliokumbana nao.
Ungana nami katika simulizi hii ya kusisimua.

Alikuja pale kazini kama mteja, lakini hilo jicho, mwenzangu mpaka niliogopa, maana jicho lake liliniganda mpaka nikaona aibu, hata hivyo alipomaliza shughuli zake aliondoka na kuahidi kurudi eti kunipa lifti nikirudi nyumbani kwangu, mwezangu nikamwambia kuwa mpenzi wangu atanifuata, hakuonekana kujali maneno yangu aliondoka na kusisitiza kurudi.

Ilipofika jioni alirudi lakini nilimkwepa na kuondoka zangu nikimwacha ndani akiongea na Bosi wangu kwani alikuwa namizigo yake na makontena Bandarini ambayo yalikuwa yanashughulikiwa na kampuni yetu kutolewa bandarini.

Siku iliyofuata alifika pale ofisini na kuniahidi kunitoa lunch katika Hoteli ya Kitalii ya Nyota Tano pale Kempinski, nilikataa ofa yake na alionekana kushangaa. Akaniambia kuwa tangu kukua kwake hajawahi kukakataliwa kitu na mwanamke, mimi nitakuwa wa kwanza kumfanyia hivyo, sikumjali sana nilimpuuza.

Baadae Bosi wangu alianza kumsifia yule mzee kuwa ni tajiri ambaye anafanya biashara katika nchi za afrika na mashariki na kati aki-supply bidhaa mbalimbali katika nchi hizo. Bosi wangu aliendelea kusema kuwa toka ameanza kufanya kazi na yeye kampuni imeingiza faida kubwa sana na kuna matarajio mazuri mwakani.

Ilipofika mchana alikuja kijana mmoja akauliza kama anataka kumuona Gift (*sio jina lake halisi) nikamwambia kuwa ni mimi, akatoa bahasha na kunikabidhi, nilipomuuliza kama imetoka wapi akanijibu kwa kifupi tu kuwa imetoka kwa mzee, kisha akaondoka zake.


Niliifungua kwa kiherehere ili kujua ina kitu gani, ndani ya bahasha ile nilkutana na cheni ya dhahabu ya Gram 10 na shilingi laki mbili, na ujumbe unaosema, “Samahani sana Gift, nilikuahidi kukutoa lunchi leo, lakini niko na kikao wizarani, nimeshindwa kutekeleza ahadi yangu, lakini hapajaharibika kitu, hiyo cheni , nilikununulia ili nikupe kama zawadi wakati wa Lunch yetu, lakini kutokana na dharura hiyo, basi pokea zawadi yangu hiyo kama ishara ya upendo nilionao kwako na hizo fedha ndio nilikuwa nimeandaa kwa ajili ya hiyo lunchi yetu, unaweza kuzitumia kwa kununua kitu chochote ukipendacho.

Nilishusha pumzi nikabaki nimeduwaa, kisha nikafyonya kwa dharau, na kuitupia ile bahasha kwenye droo ya mezani kwangu.

Jioni boy friend wangu akanifuata tukaondoka kuelekea kituoni kupanda daldala kurudi nyumbani.Kiukweli Boy friend wangu alikuwa hana kazi bali alikuwaakibangaiza kwenye ofisi ya jamaa yake fulani baada ya kumaliza masomo yake ya International Technology. Akiwa amesoma ngazi ya Diploma.

Nilikuwa na mchanganyiko wa mawazo na kutokana na mawazo hayo nilijikuta nikiwa mbali sana kiasi cha kutosikia yale aliyokuwa akiyasema Boy friend wangu, kuna wakati ilibidi anishtue kwa kuniuliza kama nimemuelewa alichokisema nilimjibu tu ndio lakini kiukweli sikumuelewa kabisa kuwa alikuwa anaongea nini.

Tulipofika Sinza ambapo ndipo ninapoishi tulishuka na kuelekea kwangu lakini karibu na nyumbani tulipisha na gari moja aina ya RAV 4, ilikuwa ikiendeshwa na kijana ninayemfahamu, alinipigia honi na kunipungia mkono, nami nilimpungia mkono. Mpenzi wangu alionekana kutofurahia kile kitendo kwani tulipofika tu nyumbani maswali yakaaza. Yule ni nani? mmejuana lini? ana uhusiano gani na wewe, mbona simfahamu? yalikuwa ni maswali mengi mfululizo ambayo sikuweza kuyajibu yote.


Tatizo la mpenzi wangu ni wivu, yaani bwana yule ana wivu utadhani dume la njiwa. Kama masihara ulizuka mzozo wa maneno kati yangu na mpenzi wangu kiasi cha kufikia kunipiga, na kisha akaondoka zake. Niliwaza sana, kwa kweli sikuwa na uhusiano na yule kijana na nilimfahamu kupitia kwa shoga yangu anayemiliki saluni ambapo ndipo ninapotengenezea nywele na yule kijana ni boy friend wake.

Nililia sana na sikuweza hata kula usiku ule nikalala na njaa. Kesho yake nikiwa ofisini yule mzee alifika tena lakini safari hii hakukaa hata kidogo, alionekana kuwa bize sana,
Ilipofika mchana Boyfriend wangu alinipigia simu lakini sikupokea, alitumia simu ya mtu mwingine kunipigia, lakini nilipopokea na kusikia sauti yake nilikata ile simu alinitumia ujumbe wa simu akiniomba radhi lakini sikumjibu, nilichukizwa sana na kitendo chake cha kunipiga siku ile.

Ilipofika jioni yule mzee akaja kunipitia pale ofisini akiwa na gari lake aina ya GX, niliamua kuondoka naye kwani alinibembeleza sana anipeleke kwangu, wakati tunaondoka nilimuona boy friend wangu akija kunifuata, nilitaka kumuomba yule mzee anishushe lakini nilisita. Yule mzee ambaye ki umri alionekana kuwa sawa na baba yangu alinifikisha nyumbani kwangu, lakini hakushuka kwenye gari, alinipa bahasha nyingine akaniambia ni zawadi yangu, nilipoingia ndani na kuifungua nilikuta dola mia mia kumi, nilishikwa butwaa.......Huyu mzee anataka nini kwangu, hivi anadhani mimi ni wa kutembea na vizee, niliwaza.

Nilishtuliwa na mtu akibisha mlangoni kwangu, nilikwenda kufungua mlango, alikuwa ni mpenzi wangu, nilishtuka sana, aliingia ndani huku akiwa amefura kwa hasira, “niliwaona sana na leo utanieleza” lilikuwa ndio neno lake la kwanza alipoingia ndani, alipitiliza hadi chumbani kwangu na zile dola zilikuwa bado ziko kitandani, nilimfuata kwa nyuma, alipoziona tu akazichukua zote.

Sasa nenda kamwambie nimezichukua na akome kutembea na wachumba za watu. aliniambia huku akizitia zile dola mfukoni, Nilijikuta nikipandwa na hasira, "Safari hii sikubali" nilijisemea moyoni, nilimrukia na kuanguka nae kitandani niliingiza mkono wangu kwenye mfuko wake alipoweka zile dola na kuzichoimoa, na yeye aliukunja mkono wangu kiasi cha kutaka kuuvunja, niliziachia zile dola zikatawanyika kitandani na pale chini, tulipigana hasa na kuvunja vitu mle ndani kosa jirani yetu mmoja kuingilia kati, tungevunja vitu vyote mle ndani.

Nilitoka na kwenda Polisi kuripoti lile tukio na nilipewa PF 3 na RB, sasa mchumba wangu alikuwa akitafutwa na Poilisi, Baada ya kusikia kuwa anatafutwa alitoweka.

Siku iliyofuata nilikwenda kazini,lakini kutokana na hali yangu iliidi niombe ruhusa ili kujiuguza majeraha ya kupigwa na mchumba wangu.

Nilipewa ruhusa ya kupumzika ya siku tatu na Bosi wangu, lakini sikwenda nyumbani kwangu bali nilikwenda kwao na mpenzi wangu Mwenge ili tuyamalize nilipofika nilimkuta shangazi yake anayeishi naye, akaniambia kuwa menzi wangu ameenda Moshi. Lakini hakumwambia shangazi yake kuwa tuligombana.

Nilimsimulia shangazie tukio zima, shangazi yake alishangazwa na habai ile na alijaribu kumpigia simu lakini simu yake ilizimwa. Niliondoka na kurejea nyumbani.
Ilipofika jioni nilisikia mlango wangu ukigongwa na nilipofungua nilikutana uso kwa uso na yule mzee, nilimkaribisha huku nikiw nimetahayari kwani sikutegeme ujio wake, nilimkaribisha ndani.
Alistushwa na hali yangu kwani macho yangu yalikuwa yamevimba na uso wangu pia, alinidadisi, nilimdanganya kama nilikutana na vibaka usiku nilotoka kwenda kununuas chipsi, alitaka kunipeleka katika Hospitali ya rafiki yake lakini nikataa kwa maelezo kuwa natibiwa na kampuni.
Hakukaa sana aliondoka, siku inayofuata alikuja asubuhi kunijulia hali na aliniahidi kunifuata mchana ili tukale lunch pamoja, nilimkubalia.

Nikweli alikuja na tulitoka pamoja hadi katika Hoteli moja iliyoko katikati ya mji, tulikula na kuongea mambop mengi sana, yule mzee a litaka kujua kama nina matarajio gani juu ya maisha yangu ya baadae nilimweleza kuwa nia yangu ni kujiendeleza zaidi kieleimu kwani elimu yangu ya kidato cha sita na diploma ya usekretari sijaridhika navyo aliniuliza kama nataka kusomea nini, nilimjibu kuwa nataka kusomea sayansi ya jamii ngazi ya shahada, aliniuliza kama ningependa kusomea nje ya nchi au hapa hapa nchini.

Nilishangazwa sana na swali lile, nilimjibu kuwa kwa kuwa sina uwezo kifedha nitasomea hapa hapa nchini, alinimabia kwa upole, “ Sikiliza Gift, kwa kuwa mimi nipo, kila kitu kinawezekana, usiwe na wasiwasi nitakusmesham tafuta shule mahali popote nitakusomesha” nilishangazwa na ukarimu wa yule mzee, na aliongea akionekana amedhamiria hasa.

Tulipotoka pale aliniambia kuwa anataka kuni-surprise, sikumuelewa kabisa, alinimbia nisubiri kidogo, tulikuwa tumesimama pale nje ya ile Hoteli na mara ikaja Toyota Rav 4 ya kijivu, na kusimama mbele yetu ilikuwa ni mpya kabisa, na yule dereva akashuka na kumkabidhi yule mzee funguo za lile gari. Yule mzee ambaye alijitambulisha kwangu kuwa anaitwa Alex, aliniuliza kama naweza kuendesha gari, nilimjibu kuwa sijui, alimuita yule dereva aliyekuja na lile gari amabye alionekana ni dereva wake na kumuamuru anipeleke kwangu na kisha anipeleke chuo chochote kizuri nikajifunze udereva.

Aliniambia kuwa lile ni gari langu ameninunulia ili kuniondolea usumbufu wa kugombea daladala.
Nilibaki nimeduwaa sikujua hata niseme nini.

Kwa kifupi nilianza uhusiano na yule mzee na alinishauri niache kazi kisha akanitafutia nyumba kubwa nzuri maeneo ta Mikocheni.
ITAENDELEA..........................