Monday, May 16, 2011

HARUSI YA WAPEMBA.

Mbwembwe za nini? Kimya kimya tu Mwali akaondoka!



Siku ya Ijumaa ya wiki iliyopita, wakati niko nyumbani majira ya mchana akaja jirani yetu mmoja Mpemba akitaka kumuona baba. Kwa bahati mbaya baba alikuwa hajarudi kutoka katika shughuli zake za kuganga njaa, hivyo akamuachia mama ujumbe kuwa alikuja kutujuza kwamba mdogo wake anaolewa siku hiyo ya Ijumaa majira ya usiku baada ya swala ya Waislamu ya Insha. Alituomba tujumuike nao itakapofika hiyo saa mbili usiku ili kufanikisha shughuli hiyo ya ndoa.


Mie nilishangaa kidogo kwa kuwa tangu asubuhi pale kwa majirani zetu ambao nyumba yao iko mkabala na ya kwetu, kulikuwa kuko swari kabisa na hapakuonesha dalili yoyote kuwa kuna pilika pilika za kufungwa ndoa au Harusi. Kwa kawaida nafahamu kuwa nyumba yenye maandalizi ya Kufungwa ndoa huwa inakuwa bize na pilikapilika za hapa na pale hasa kwa zile shughuli zinazofanyikia nyumbani, kwa kawaida huwa ni lazima kunakuwa na shughuli mbalimbali zitakazowafanya hata majirani wajue kuwa kuna jambo hapo kwa wenzetu, lakini mweh! Kulikuwa kuko shwari tu kutwa nzima.


Ni kweli majira ya saa mbili hivi tukaona majamvi yanatandikwa kibarazani, na sie kama majirani, yaani mie, mama na baba tukaenda kuungana nao. Mie na mama tuliingia moja kwa moja sebuleni ambapo tulikuta pametandikwa majamvi na akina mama kadhaa wakiwemo baadhi ya majirani zetu walikuwa wamekaa na baba alifikia pale kibarazani ambapo aliungana na wazee wengine ambao walikuwa wamekaa pale nje. Kwa kawaida waislamu wanawake hawachangamani na na wanaume kwenye shuguli zao, na ni lazima mjitande ushungi. Waswahili wanasema ukienda kwa waroma basi vaa kama waroma, nasi yaani mie na mama tulijitanda ushungi.


Baada ya muda kidogo, tukasikia watu wakisalimiana huko nje, na mie ili nisipitwe, maana napenda sana kupekua mambo, nikajisogeza karibu na mlango, ili nione yatakayojiri hapo nje. Nilipata sehemu nzuri ambapo niliweza kuwaona watu waliokaa pale nje vizuri tu. Karibu watu wote pale nje walivaa kanzu, akiwemo baba yangu. Mzee mkundi naye anayo kanzu yake ambayo huivaa akipata mialiko ya aina hii.


Basi mara kikaletwa chetezo na ubani ukawekwa, wakanyanyuka wazee kadhaa na wakiongozana na kaka wa binti na kuingia ndani ambapo walielekea katika chumba ambacho alikuwa amewekwa huyo Bi harusi ambaye kiukweli sikumfahamu. Baadae niliambiwa kuwa alikuwa akiishi na dada yake huko Kinondoni na baada ya kupata mchumba ikabidi shughuli za posa na ndoa zihamishiwe kwa kaka yao mkbwa ambaye ni huyo jirani yetu, na ndio maana, wahudhuriaji wengi sikupata kuwafahamu.


Baada ya kitambo kidogo, wakatoka, na kurejea sebuleni. Nilisikia bwana harusi akiulizwa kama mara tatu hivi kuwa amekubali kumuoa huyo Binti ambaye alitajwa kwa jina la Salha kwa mahari ya elfu sabini na tano? Ambapo alishatoa elfu hamsini na kuna deni la elfu ishirini na tano. Bwana harusi mara zote alikubali.


Lakini jambo lililonifrahisha zaidi ni kile kiwango cha mahari, sikujua kama kuna watu bado wanatoza kiwango kidogo cha mahari kiasi kile. Sikusita kuonesha mshangao wangu, na mama mmoja aliyekuwa amekaa jirani namie akaniambia kuwa hata hivyo yule (Yaani bwana harusi) kagongwa, yaani katozwa kiasi kikubwa cha mahari, eti kwa kawaida waislamu hususan Wapembahutoza kiwango kidogo sana cha mahari hata kufikia elfu ishirini na tano!, ndio elfu ishirini na tano!


Nilimuangalia mama, nikamkonyeza kwa mbali, naye akatabasamu akijua ninamaanisha kitu gani, kwani wao kwa dada zangu watatu walioolewa, walilamba zaidi ya laki tano kwa kila mmoja! Na hapa nazungumzia tukio la miaka zaidi ya mitano iliyopita!


Sijui kati ya Fadhy, Markus au Kitururu, atakayebahatika kunichumbia atagongwa ngapi, maana kwa jinsi ugumu wa maisha ulivyopanda, sijui kama watamudu dau la Mzee Mkundi…………LOL


Haya baada ya kusomwa dua kadhaa na shughuli ikawa imeisha, na tukatangaziwa kuwa tusubiri Sadaka kabla hatujaondoka.


Mnajua ilikuwa ni nini? Mh! Tuliletewa chai iliyoungwa vizuri na viungo toka Pemba, na vijiandazi vidogo, baada ya hapo, shughuli ikawa imeisha, na jamaa mmoja akaenda barabarani na kudaka Hiace moja ya Kipawa akaikodi na kuja nayo pale, Bwana na Bi harusi walikaa mbele na wapambe walikaa nyuma kisha wakondoka kimya kimya hapakuwa na vigelegele wala nini. Nilipouliza kwa nini hapakuwa na shamrashamra, nilijibiwa kuwa ni kharamu. Mweh! Mwenzenu nilishangaa kweli, maana kusema kweli ile ilikuwa ni mara yangu a kwanza kuhudhuria shughuli ya ndoa ya kimya kimya.



Nimejifunzazjambo kwa kweli.

9 comments:

Simon Kitururu said...

Ndoa za shamrashamra ,...
.... shamra yenyewe nahisi huwa imezidishiwa tu chumvi kama ukiweka na HEADACHE za kuanda sherehe hata kama tukiondoa gharama za shamrashamra!

Mie naona hii HARUSI ilikuwa bomba sana. Simple na cha muhimu kimefanyika!

Na mie ni miongoni mwa wasioelewa ni kwanini VIDUME inabidi walipe mahari au katika jamii kama za Wahindi ni kwanini ni WANAWAKE inabidi walipe mahari ingawa ,...
.... kwa ajili yako KOERO ntalipa chochote kile ili uwe mama watoto wangu ingawa kwa kuwa umewachagua FADHY na MARKUS kabla yangu,...
.... naombea wasikuzalishe sana kabla ya kuja kwangu ili tusaidie kuujaza ulimwengu kwa kuujaza watoto ambao naombea wafananefanane na wewe mtoto mzuri!


Si kama mahari ya Mzee Mkundi ni kubwa sana labda ntaruhusiwa kuiba sehemu ili nilipie ruksa ya kuwa nawe kihalali?

Nami nimejifunza jambo kutoka kwenye uliyoandika Koero!

emu-three said...

Harusi siku huzi zimekuwa ni biashara, biashara ya mpambaji, mtengeneza keki, mtengeneza gauni , ukumbi,....nk...yote haya yametokea wapi!
Kiukweli mengi twajitakia wenyewe, kwangu mimi kama ingewezekana, basi changeni hizo ndululu mumpatie bwana na bibi harusi wakaanzie maisha...!

Anonymous said...

hiyo ndiyo harusi murua ya kiislamu kwa vile katika kila jambo jema linatakiwa lipewe wepesi kwa kadri iwezekanavyo....hayo matarumbeta na nderemo tuzionazo leo ni umajinuni usio na tija wala mashiko. sanasana yanaongeza gharama, kufuru na machukizo kwa mungu. tufuate mfano huo hususan kwa waislam.

Yasinta Ngonyani said...

Ahsante Koero nami pia nimejifunza kitu kutokana na wewe kutokuwa mchoyo!! Harusi hizi kaaazi kwelikweli

Anonymous said...

Hata mimi natarajia kuoa mke wa pili na nikabikra cha kipemba, tumepanga itakua hivyohivyo usiku baada ya inshaa na itakua kimyaaaa hakuna bidaa wala shubha. Mwenyeiz Mungu atufanikishie bado miezi michache tu.

Anonymous said...

nimeopenda hii lakin sikumbuki km kiwango cha mahari kinatajwa wakati wa harusi.. inasemwa tu "kwa mahari muliokubaliana" haitwaji kiwango ni kias gan.....

ddlovato said...

hiyo insha ni nzuri sana lakini kwa size iko kubwa sana hata siwezi ku andika as in copy..
nilipewa insha yakuandika lakina hiyo siwezi lakini nina try
well,asante sana for writing such a beautiful insha

Unknown said...

Best
Insha

Anonymous said...

Great insha can you also write one about SHEREHE YA KRISMASI. Shukran