Friday, March 9, 2012

MIKOBA YA MANUNUZI INAPOKUWA NA VIJIDUDU GEMS





Utafiti uliofanywa na profesa Charles Gerba wa chuo kikuu cha Arizona nchini Marekani umebaini kwamba wengi wetu hususan sie kina mama hatusafishi mikoba yetu tunayotumia kufanyia manunuzi sokoni. Kuna hii mifuko maarufu kwa jina la mifuko ya Rambo au wakati mwingine tunayo mikoba maalum ya Canvas ambayo tunaitumia kufanyia manunuzi. Mikoba hii huwa tunaitumia na kisha kuihifadhi kwa matumizi wakati mwingine.


Je huwa tunaisafisha mikoba hiyo au tunaitumia mara kwa mara bila kuifanyia usafi kwa usalama wetu?


Profesa Gerba ambaye ni mtaalamu wa masuala ya udongo, maji na mazingira, alichunguza na kupima zaidi ya mikoba 100 kwenye miji ya California na Arizona, na katika utafiti huo aligundua kwamba ni asilimia 3 tu ndio wanaosafisha mikoba yao. Katika utafiti huo aligundua mikoba mingi ikiwa na vijidudu hatari vya Coliform asilimia 50 na E. Coli asilimia 8

“Inashangaza kidogo kuona mtu anatumia mikoba hiyo kubebea nyama, mayai, mboga mboga ambazo hata hazijaoshwa vyema na makorokoro mengine ambapo yamesheheni vijidudu vya maradhi lakini haifanyii usafi mikoba hiyo, bali huiweka kwa matumizi wakati mwingine.” Alisema Mtaalamu huyo wa masuala ya udongo, maji na mazingira,

Profesa Gerba alishauri watu wawe wanaosha mifuko yao kwa sabuni na maji ya moto baada ya matumizi.



Saturday, March 3, 2012

SASA MIMI NI MKE WA MTU!




Asalaamu Aleikhum mabibi na mabwana – hii ni kwa ndugu zangu Waislamu

Shaloom – Hii ni kwa ndugu zangu Wakristo

Ni matumaini yangu nyote hamjambo na mnaendelea vyema na shughuli zenu za kila siku. Ni muda sasa sijaonekana humu Jamvini, na hiyo ilitokana na kutingwa na shughuli nyingi za kujiandaa na harusi yangu ambayo ilifanyika mwaka jana mwezi wa kumi.

Ni masikitiko yangu kwamba sikuweza kuwasiliana na wanablog wenzangu pamoja na wasomaji wa blog hii ya VUKANI, na hiyo ilitokana na kutingwa na mambo mengi yaliyojitokeza kwa kipindi hicho. Huyu mume wangu ni mtu anayependa usiri, hivyo hakutaka jambo hilo tulikuze saaana na kulifanya kwa mbwembwe. Tulifanya kasherehe kadogo sana ambako kaliwakutanisha ndugu wa pande mbili tu na baadhi ya marafiki wa karibu sana. Lakini pia ni vyema mkafahamu kwamba nimeolewa mkoani Kilimanjaro huko Marangu.

Baada ya harusi nilirejea kwenye pilika zangu za kusaka mkwanja, na kama mjuavyo kwamba biashara hapa nchini imebana sana, na watu wanakimbizana kutafuta masoko na hapo hapo tunapambana na TRA ilimradi shida mtindo mmoja.

Mume wangu alinishauri niache kublog, kitu ambacho sikuafiki, lakini baada ya kujadiliana kwa kina, tulikubaliana niendelee kublog, lakini nisimame kwa muda kwanza ili tuweze kusimama kibiashara na kuweka msingi wa maisha yetu kwani tulikuwa tunahitaji muda wa kuwa pamoja zaidi. Kwa sasa naitwa mama kijacho na niko mapumziko (Bed Rest) na ndio sababu nikapata muda wa kuandika na kuweka kitu hapa VUKANI.

Naomba mniwie radhi wote mliokwazika na kutowahabarisha juu ya harusi yangu, lakini nataka kuwahakikishia kwamba tupo pamoja.