Tuesday, April 19, 2011

BALAA GANI HILI!?

Msinielewe vibaya waungwana, hata mie nashangaa tu!!!!!!

Saturday, April 16, 2011

MPIGA DEBE WA DALADALA AMWAGA NGELI NA KUWASHANGAZA WENGI………





Leo asubuhi nimekutana na kituko cha mwaka, naomba nikiri kwamba hata mimi nilikuwa ni mjinga kwani sikutarajia kwamba jambo hilo nililolishuhudia linawezekana. Naomba nikiri kuwa hata mie nilikuwa nawapa watu hawa mtazamo tofauti kabisa nikidhani labda mie ni mjanja kuliko wao, lakini hili nililolishuhudia asubuhi ya leo, nimenifunza jambo moja muhimu sana maishani, kwamba kamwe usimhukumu mtu kutokana na muonekano wake.


Ilikuwa ni majira ya saa kumi na mbili alfajiri, niko maeneo ya Msasani, nikisubiri daladala la kuelekea Kariakoo, mara likaja basi moja hivi aina ya Toyota Coster. Kama kawaida abiria wakiwemo wanafunzi tulilikimbilia na kuanza kugombea kupanda kila mtu akijaribu kuwahi kiti. Japokuwa hatukuwa wengi, lakini nilishangazwa na jinsi abiria walivyokuwa wakigombea kupanda utadhani watakosa nafasi ya kukaa. Lakini cha kushangaza ni kwamba vurugu zote zile ilikuwa ni ili kuwahi viti vya Dirishani!


Pale mlangoni alisimama mpiga debe mmoja ambapo kwa hapa Dar hujulikana kama Mateja, yaani watumia madawa ya kulevya, ambaye alikuwa amevaa nguo kuu kuu na zilikuwa chafu ajabu. Alikuwa pale mlangoni kuzuia wanafunzi wasipande. Kwa hapa Dar ni jambo la kawaida wanafunzi kuzuiwa wasipande kwenye basi na abiria wakabaki wakiangalia tu, kama vile haiwahusu. Kule Arusha mambo ni tofauti kidogo, wanafunzi huwa hawaachwi, tena kama hajavuka barabara, hasa watoto wadogo, kondakta anamfuata na kumvusha ili apande kwenye basi, kwa kweli nilishangazwa na ustaarabu wa makondakta wa daladala za Arusha.


Baada ya abiria wote kupanda, yule mpiga debe aliwaambia wale wanafunzi kuwa atachukua wanafunzi sita tu, wengine waende kwenye mabasi mengine. Pale chini kulikuwa na wanafunzi zaidi ya kumi na tano hivi na wote walionekana wakitaka kupanda kwenye hilo basi ili kuwahi shule. Yule kijana mpiga debe aliongea kwa usataarabu akiwaelewesha wale wanafunzi, akiwaambia kuwa hata yeye anajua adha ya usafiri kwa wanafunzi lakini ile gari ina Hesabu, yaani wanatakiwa wafikishe kiwango fulani cha hela kwa mwenye gari na wao wabaki na chochote, na kwa kuzingatia kuwa leo ni Jumamosi, ni ngumu sana kupata hesabu ya tajiri.


Lakini kulitokea kutoelewana kati ya wale wanafunzi na yule mpiga debe, wanafunzi walimjia juu wakimwambia aache siasa, wao wanataka kuwahi shule na hawahitaji Lecture pale. Kulitokea kutoelewana, lakini yule mpiga debe alisisitiza msimamo wake wakutaka wapande wanafunzi sita tu. Ni kweli walipopanda wanafunzi sita, aliwazuia wengine wasipande na kuruhusu dereva aondoe gari. Baadhi ya wanafunzi walioachwa pale chini walilazimisha kuning’inia mlangoni, lakini yule mpiga debe aliendelea kuwazuia huku gari likianza kuondoka mdogo mdogo..


Wakati zogo kati ya wanafunzi na yule mpiga debe likiendelea, ghafla akaibuka abiria mmoja, akaanza kumfokea yule mpiga debe, akimuonya kwamba kama hatawaruhusu wale wanafunzi wapande basi atalipeleka basi lile Polisi, yule Mpiga debe hakumjibu alikuwa akiendelea kuzozana na wanafunzi.


Yule abiria alianza kumtolea yule mpiga debe maneno ya kashfa huku akimtisha kuwa atampiga. Basi liliondoka na baadhi ya wanafunzi waliachwa pale kituoni, ndipo yule mpiga debe akamgeukia yule abiria na kumuuliza kisa cha kumkashifu wakati yuko kazini.


Yule abiria akawa kama amechokozwa, alimshambulia yule mpiga debe kwa maneno makali na kumkashifu kuwa hajasoma na ni mvuta unga tu na kibaka wa mtaani.


Yule mpiga debe akamwambia, ni kweli hajasoma, kwa sababu ingekuwa ni jambo la kustaajabisha kukuta mpiga debe msomi, hata hivyo hakuishia hapo, akamtupia swali yule abiria………


"inaonekana mwenzangu umesoma sana eh!….. hivi una degree ngapi mpaka sasa, au una masters?” Yule abiria aliendelea kumtolea maneno ya kashfa yule mpiga debe huku akisisitiza kuwa hajasoma na ni mjinga tu.


Yule Mpiga debe akaonekana kukerwa na yale maneno kutoka kwa abiria mkorofi, akamgeukia na kumwambia, kwa kiingereza, ngoja nimnukuu hapa……..


“Listen my friend, don’t judge me because of what I am doing, I have good education background than you. To be a Daladala tout does not justify that I am ignorant. For your information, I am educated enough to work for a white-collar job. I am here because of frustration, after being fired from my job; I had a nice job with a lot of benefits and privileges, I am not a fool ok!”


Wakati anamwaga kiingereza, kwanza abiria walishikwa na butwaa, na baadae wakaanza kumshangilia wakiwemo wale wanafunzi waliokuwa wakitetewa na yule abiria mkorofi. Hata hivyo yule abiria aliposikia jamaa anamwaga kiingeza, alikaa kimya asiamini masikio yake,hakujibu kitu.


Abiria waliendelea kumchagiza mpiga debe aendelee kutoa dozi kwa mshkaji, na yeye ili kupata ujiko zaidi akaendelea kumwaga ma-vitu, palikuwa ni patamu hapo…….


“You know sometimes people think all daldala touts are drug users and they are not educated ……..… No, you are totally wrong my friend, for this job I am earning more than enough, I can make your salary which you get from you Boss Indians for 10 days. Although I have been fired but I decided to work as a daladala touts rather than stealing someone’s money.”


Kisha akaendelea…..


“Why you are quiet, talk now Mr. Educated” ………… “You see,” akatugeukia sisi abiria na kutuambia ……….. “Mr. Educated have failed to speak even two English words”


Jamaa akajikakamua na kumjibu,


“Hebu ondoka na kiingereza chako cha kuombea maji, mwenyewe unajiona umeongea kiingereza hapo, hamna kitu,unachapia tu”


Mpiga debe hakumkawiza akamjibu…….


“Ok, my English is just for begging water, where is yours, if you can speak only two English words, I will give you ten thousand, right now, in front of passengers, I am not joking”


Yule mpiga debe akatoa elfu kumi na kumpa abiria mwingine aishike, ili kuthibitisha kuwa hatanii. Kumbe jamaa alikuwa ni mweupe, hajui Ngeli, yaani ilikuwa ni aibu, karibu abiria wote wakawa wana mzodoa kwa maneno ya kejeli.


Tulipofika kituo cha Namanga jamaa akashuka kwa aibu na ninadhani alikuwa hajafika safari yake, naona alishuka ili kujisitiri na aibu iliyomkumba mle ndani ya basi.


Nakwambia ilikuwa ni gumzo ndani ya basi lile kila mtu akisema lake wapo waliosema kuwa yule mpiga debe ni mpelelezi wa Polisi, wapo waliosema ni shushushu yaani anafanya kazi usalama wa Taifa. Na hilo ndilo tatizo tulilonalo Watanzania, yaani mtu akijibainisha tofauti na muonekano wake basi ataitwa shushushu…….. Basi na yule mpiga debe akapewa cheo cha ushushushu pale pale, kisa kaongea Kiingereza, kuna wengine walisema sio Mtanzania bali ni Mkenya, kwa kuwa hakuna Mtanzania anayejua Kiingereza kama vile halafu afanye kazi ya kupiga debe, ili mradi kila mtu alisema lake.


Tulifika Kariakoo kilamtu akashika hamsini zake, nimerejea nyumbani jioni hii nikaona niwashirikishe wasomaji wangu katika kisa hiki ambacho hata mie kiliniacha mdomo wazi.

Thursday, April 14, 2011

MHUBIRI WA INJILI KITAANI ADUNDWA

Mhubiri akiwa kazini




Hii niliishuhudia katika viunga vya pale Mwenge jiji Dar jana wakati naenda Hospitali. Nilikuwa nimesimama kwenye duka moja la kuuza Dawa kuulizia dawa fulani ambayo niliandikiwa hospitalini. Upande wa pili wa barabara kutoka katika duka hilo kulikuwa na jamaa mmoja aliyejitambulisha kama Mtumishi wa Mungu, alikuwa akimwaga neno la Mungu, kuwaasa watu waache matendo ya Dhambi, na kumrejea Mungu.


Jasho lilikuwa likimtoka kwelikweli na alikuwa akiongea kwa jazba kama vile anagombana, lakini katika mahubiri yake alikuwa akiwananga wapita njia hususan wanawake ambao walivaa vimini au suruali za kike.


Ilikuwa kila akipita mwanamke mwenye kimini au suruali ya kike alikuwa akimwambia…….. ngoja nimnukuu hapa. ‘wewe mwanamke mwenye suruali acha dhambi, hayo mavazi uliyovaa hayampendezi mungu kamwe na ninakuhakikishia utakwenda motoni, na wewe mwanamke mwenye kimini na hakika hutauona uzima wa milele, utaishia motoni’ mwisho wa kunukuu.


Kibaya zaidi alikuwa akitumia kipaza sauti na alikuwa akiwafuata nyuma (hao wanawake) huku akiwamwagia maneno makali na ya kudhalilisha


Wakati akiendelea na mahubiri yake akapita dada mmoja ambaye alikuwa amefuatana na mvulana, sikuweza kujua kama walikuwa na uhusiano wa kimapenzi au walikuwa ni ndugu, yule mhubiri kama kawaida yake akaendelea kumwaga maneno ya kuwakashifu wanawake wenye kuvaa suruali.


Kutahamaki nikamuona mhubiri kakunjwa shati na yule kijana, aliyekuwa na yule binti, mara ghafla yule kijana akaanza kumchapa makonde yule mhubiri mara kichwa, hajakaa sawa akalambwa mtama, mhubiri chali……………..


Kisha yule kijana akamshika mkono yule dada, wakaondoka wakimuacha mhubiri akijizoa zoa pale chini. Niliondoka katika eneo lile maana umati wa watu ulianza kusogea katika eneo hilo ili kujua kulikoni.


Kilichojiri nyuma yangu sijui.


Tuesday, April 12, 2011

BODA BODA ILIPONITEGUA MGUU.

Juzi katika harakati zangu za kutafuta mikwanja, nikajikuta nikipigwa defrao na Bodaboda maeneo ya Msasani.

Niliwahishwa Hospitali na ikaonekana nimeteguka kifundo cha mguu wa kushoto. nimefungwa POP na sasa naendelea vyema.

Friday, April 1, 2011

BIBI KOERO NA KIKOMBE CHA BABU AMBILIKILE

Misitu kama hii ni hazina kubwa kwa dawa za miti shamba



Hivi karibuni nilimtembelea bibi Koero kule kijijini, nilipitia huko wakati nikitokea Arusha kurudi Dar. Nilimkuta yu buheri wa Afya, na kama kawaida yake alinipokea kwa bashasha kubwa pamoja na tabasamu pana usoni pake.


Mara zote anajua mjukuu wake nina hamu ya simulizi zake zinazonipa tanuri la fikra, kwa kweli Bibi yangu huyu ananipenda sana.Daima napenda sana udadisi,napenda kuchokonoa, kudadavuliwa na kudadavua niwapo na bibi Koero, kama vile alivyo Yasinta na mie siko nyuma katika Ukapulya.


Yaani ni zaidi ya falsafa na wazo ndani ya neno ya kaka Kitururu pamoja na chakula kitamu kiliwacho.


Basi katika hali ya utani nikamuuliza kuwa kwa nini na yeye asiende Loliondo kwa Babu Ambilikile Mwasapile kupata Kikombe? Nilimuuliza hivyo baada ya kuniambia kuwa juma lililopita alikuwa anasumbuliwa na maumivu ya mgongo na kichwa.


Bibi Koero aliniangalia, kisha akacheka kwa dharau. Nikajua kuna jambo lenye wazo na chakula kitamu kusimulia. Alicheka kisha akasema kwa dharau, ‘umri huu niende kwa Babu Loliondo kufanya nini?, umri huu nilio nao (Bibi Koero anatimiza miaka 92 mwaka huu) siwezi kujisumbua kiasi hicho, nimeshakula chumvi nyingi na hivyo nasubiri kupumzika’.


Alinishika mkono na kuniambia nimfuate, kwani wakati huo alikuwa kwenye kijishamba chake akipalilia Tangawizi zake. Tukajongea kwenye kivuli cha mti ulioko jirani tukakaa chini. Akaanza riwaya zake zenye maono; sikiliza mjukuu wangu, alisema bibi Koero, kisha akaendelea………..Kuibuka kwa huyo Babu Ambilikile sio jambo la kustaajabisha, ni mambo ya kawaida kabisa, na inawezekana wakaibuka wengine na wengine (wakati tunazungumza ilikuwa bado hazijasikika habari za kuibuka kwa kijana mwingine huko Mbeya, Morogoro na Mama wa Tabora ambao wote wamedai kuoteshwa dawa na Mungu).


Aliendelea, Kabla ya ujio wa tiba za Hospitali, Watu walikuwa wakiugua na kutibiwa kwa miti shamba, na sio kwamba kulikuwa hakuna maradhi kama wakati huu, yalikuwepo, tena maradhi mengine yalikuwa ni ya kutisha, Je watu hao walikuwa wakitibiwa na nani kama sio Mungu? Labda kitu ambacho watu wa kizazi chenu msichokifahamu, ni kutokujua utendaji kazi wa Mungu.


Zamani kulikuwa na imani ya kuamini Mizimu Matambiko au Mizungu na kadhalika na kupitia imani hizo mambo mengi yalifanyika. Ujio wa hizi dini za Mapokeo, ambazo hata hivyo mimi ni mmojawapo ya watu tuliojikuta tukibadilika kutoka katika imani zetu tulizorithi kutoka kwa mababu zetu na kuingia katika imani hizo za dini za mapokeo, tulijikuta tukiziacha na kuzibatiza jina la imani za Kishenzi kwa kuwa tu tulilazimishwa kuzikana. Sasa basi kwa upande wa utendaji kazi wa Mungu, kwa kweli hilo ni jambo ambalo bado linazusha maswali kila uchao. Mungu yupo na anayo namna yake ya kuwasiliana na wanaadamu, kama alivyofanya tangu huko zamani.


Wanaadamu walipitia nyakati tofauti na kila nyakati zilikuwa na kitabu chake, yaani historia yake. Msomaji keti kitako…,..ngoja nikusimulie mkasa huu uliompata baba yetu.Wakati nilipokuwa binti mdogo kigori. Baba yetu aliumwa sana, kiasi cha kulala kitandani kwa mwaka mzima, kama ingekuwa ameugua kipindi hiki labda mngesema kuwa ni huo ugonjwa wenu wa Ukimwi. Tulifika mahali tukakata tamaa, tulimpeleka kwa waganga mbalimbali wa asili wenye sifa za kutibu maradhi yaliyoshindikana lakini hawakuweza kumtibu, tulibaki kumuomba Mungu.


Ilifikia mahali ikabidi sasa tubadilishe sala zetu, kwamba badala ya kumuombea apone, tukamuomba Mungu ampumzishe kwa sababu alikuwa ameteseka sana kwa maradhi hayo.



Ilitokea siku moja Mjomba wake na baba aliyekuwa akiishi Kijiji kingine alikuja nyumbani alfajiri na mapema, na sisi tulijua kuwa amekuja kumuona mgonjwa, lakini alipofika tu, aliomba jembe na panga, kisha akamchukua kaka yetu mkubwa na kwenda naye kwenye Msitu wa Shengena.


Sikiliza hili, msomaji, msitu wa Shengena ni miongoni mwa Misitu yenye maajabu makubwa hapa nchini, msitu huo uko jirani na kijiji alichozaliwa mama yetu yaani hapo Mamba Miamba wilayani Same mkoani Kilimanjaro. Simulizi juu ya maajabu ya Msitu huo yanahitaji makala inayojitegemea. Nitawasimulia nikipata muda.


Bibi Koero aliendelea kusimulia, walirudi baada ya saa kama tatu hivi wakiwa na mizizi na majani ya mti tusioujua. Mjomba alitueleza kuwa siku mbili zilizopita alioteshwa na kuoneshwa dawa itakayomtibu baba, awali alipuuza, lakini kwa mara nyingine siku iliyofuata alioteshwa tena na kuoneshwa dawa hiyo.


Kwa mujibu wa maelezo ya mjomba alidai kuwa akiwa usingizini, aliona kivuli cha mtu pembeni ya kitanda, alikuwa ni mtu mwanaume na alikuwa akimuamsha kwa kumwita kwa jina lake lakini kwa kunong’ona, aliamka na yule mtu akamuonesha ishara kuwa amfuate, alinyanyuka na kumfuata, mjomba alidai kuwa hawakupitia mlangoni, bali kulitokea uwazi kwenye ukuta wakapita na ule uwazi ukajifunga na walipokuwa nje mavazi ya yule mtu yalikuwa yanang’aa kama theluji na hivyo kutoa mwanga.


Kwa kuwa kulikuwa na giza totoro, ule mwanga ulimwezesha kuona njia na waliendelea kutembea kuelekea mahali asipopajua.


Walitembea mwendo mrefu hadi wakafika msituni, na ndipo akaambiwa achimbe mizizi ya mti fulani baada ya kuchimba ile mizizi walienda kwenye mti mwingine na kukata majani ya ule mti kisha wakarudi nyumbani.


Walipofika walipitia pale pale ukutani na walipoingia ndani yule mtu aligeuka kuwa kivuli na kisha akamwambia kwa kunong’ona kuwa ile ni dawa ya kumtibu mjomba wake ambaye ni baba yetu.


Alimwelekeza namna ya kuitayarisha ile dawa kabla ya kumpa mgonjwa kisha akatoweka.Mjomba alistuka usingizini na kumsimulia mkewe, juu ya ndoto ile, shangazi alimshauri aende kwa mtaalamu ili kupatiwa tafsiri ya ile ndoto, lakini alipuuza, siku iliyofuata alioteshwa tena, na ndipo akakata shauri kuitafuta hiyo dawa ambayo kwa kweli ndiyo iliyomtibu Baba.


Baada ya baba kupona hakupata kuumwa tena zaidi ya maradhi madogo madogo hadi alipofarikia akiwa na miaka tisini na ushee.


Muda wote wakati Bibi Koero akinipa simulizi hiyo ya kuvutia nilikuwa nimemtumbulia macho nikiwa nimeshika tama.


Hivyo basi mjukuu wangu, aliendelea Bibi Koero, Mungu amekuwa akiwasiliana na wanaadamu hadi hivi leo, lakini wengi waliokuwa wakioteshwa hapo zamani walikuwa wakifanya siri, na hata hivyo hapakuwepo na wingi wa vyombo vya habari na mawasiliano kati ya eneo moja hadi jingine yalikuwa ni magumu na ndio sababu habari hizo hazikupata kuvuma kama hivi sasa.


Labda jambo lingine na lile la wananchi kukata tamaa na gharama za matibabu katika Hospitali zetu kuwa juu, hiyo nayo ni changamoto nyingine ambayo inaikabili sekta hiyo ya afya sio kwa hapa nchini tu bali dunia nzima kwa ujumla.


Kwa kifupi alinieleza kuwa Mungu yupo na ataendelea kuwasiliana na wanaadamu kwa namna tofauti kulingana na jinsi anavyoona. Lakini hata hivyo, alisema kuwa sio kwamba wote watakaotumia dawa hiyo watapona, haiwezekani, wapo watakaopona na wapo ambao hawatapona kwani kuponya kwa dawa za namna hiyo kunatokana na imani watakayokuwa nayo watumiaji.


Kwa ujumla tuliongea mengi na bibi Koero ikiwemo kutahadharisha juu ya kuibuka kwa Matapeli watakaosingizia nao kuotesha dawa na Mungu kwa ajili ya kujipatia fedha kwa hila na kujijengea umaarufu, kwani katika msafara wa Mamba hata Kenge nao pia wapo.


Hata hivyo msichoke kupitia kibaza hiki maana nikipata muda nitamalizia mazungumzo yetu na Bibi Koero sehemu ya pili ikiwa ni mwendelezo wa kile tulichojadili. Mmmh! Kumbe kikombe cha babu hakikuanza leo!