Sunday, September 27, 2009

VUA NGUO NIKUPE UTAMU!!!!!!!!

Jamani hii sio falsafa ya kaka yangu Simon Mkodo wa Kitururu, kwa hiyo naomba msistushwe na kichwa cha habari hapo juu. Jana nikiwa nimejipumzisha nyumbani baada ya kutoka kanisani, niliamua kufungulia redio ili kusikiliza habari mbali mbali.

Nilipofunga redio nilikutana na kipindi cha watoto kilichokuwa kikirushwa hewani na Redio One, wakati huo ilikuwa ni wakati wa vitendawili, nilijikuta nikivutiwa na kile kipindi kwani kilinikumbusha enzi zile nikiwa mwanafunzi, nilitulia kwenye kiti na kusikiliza kipindi kile.

Mara mwanafunzi mmoja aliyetakiwa kutoa kitendawili chake akasema ‘Kitendawili’
Wenzake wakajibu ‘tega’, na ndipo akasema ‘Vua nguo nikupe utamu’
Yule mwendesha kipindi ambaye alikuwa ni miongoni mwa wale wanafunzi alimkata yule mwanafunzi kalma, na kumuonya yule mwanafunzi, kwa maneno yake mwenyewe alisema, ‘Jamani hivyo vitendawili haviruhusiwi, kwa nini huwaulizi wenzio, muwe mnawaelimisha wenzenu’

Akamchagua mwanfunzi mwingine na kipindi kikawa kinaendelea. Hata hivyo mimi bado nilibaki na swali, Je yule mwanafunzi alimaanisha nini katika kitendawili chake?
Kwa nini hakupewa nafasi ya japo kutoa jibu akiwa Off Air na kisha muongoza kipindi akatoa ufafanuzi? Je watoto walioko majumbani ambao walikuwa wakisikiliza kile kipindi watakuwa na picha gani juu ya kile kitendawili?

Unajua siku hizi kiswahili kimegeuzwa sana kiasi kwamba kila neno siku hizi limegeuka kuwa matusi.

Kwa kawaida watoto ni wadadisi sana na hicho kitendawili huenda watoto wengine waliokuwa kwenye kipindi na wale waliokuwa wakisikiliza majumbani mwao wamewauliza wazazi wao, na kwa bahati mbaya sana mwenye jibu la kitendawili kile alinyimwa haki ya kutoa jibu, Je wazazi watajibu nini?

Mpaka leo bado natafuta jibu la kitendawili kile, mwenye nalo anisaidie……

Saturday, September 19, 2009

HUYU NDIYE KAMALA LUTATINISIBWA

Kamala Lutatinisibwa,
Picha kwa hisani ya Blog ya Kijiwe cha Nyegerage.

Ni kijana wa kutoka kabila la Kihaya, na mzaliwa wa kule Bukoba mkoani Kagera. Alizaliwa miaka 28 iliyopita, tarehe 30 July.

Maisha yake ya udogoni hayakuwa mazuri sana kwani hakuwahi kufurahia upendo wa mama kwani inasemekana baba na mama walitengana mwaka mmoja tu baada ya yeye kuzaliwa akiwa ni mtoto wa mwisho hivyo akalelewa na bibi yake akishirikiana na shangazi zake kadhaa na binamu zake.

Binamu na baadhi ya ndugu alioishi nao kwa upendo na anaowakumbuka ni Jennifer Lukambuzi, Jovian na Elivida Binomutonzi, na dada yake Julieth na kaka yake Japhet ambao walikua pamoja wakicheza na kufurahia maisha ya utotoni. Alibatizwa tarehe 12/12/1982, rasmi bila ridhaa yake na kuwa mkirsto mfuasi wa ulutheri na kupewa jina la James.

Anakiri mwenyewe kuwa mpaka leo hajaweza kuelewa falsafa ya dhehebu hilo wala malengo yake na hivyo alibadili jina na kujiita Kamala Lutatinisibwa, na kubadili falsafa yake kutoka ile ya kimapokeo na kuhamia katika falsafa ya Spiritual yaani kujitambua.

Mwishoni mwa miaka ya 1980 kijana huyu akaanza shule ya awali maarufu kama vidudu au chekechea iliyokuwa ikimilikiwa na kanisa.

Anakiri kwamba hakuwa na mapenzi na shule hiyo ya awali kwani kuna wakati alikuwa akiishia njiani badala ya kwenda shuleni hivyo kuchapwa bakora kwa utoro. Alipokuwa darasa la tatu, alisomeshwa kipaimara na kuanza kula mkate kanisani ambao hujulikana kama kushiriki meza takatifu, ingawa hakuwahi kupenda kula mikate hiyo.

Kuna wakati alipenda mambo ya dini na kutaka kusomea uchungaji lakini baadaye alibadilisha uamuzi wake huo na kuamua kuishi kwa misingi ya falsaya ya Spiritual baada ya kuvutiwa na falsafa ya Budha na Osho.

Mnamo August 1, 1998 akiwa kidato cha pili kijana huyu alimpoteza baba yake mpendwa Omwami Ta Jasson Lutabwasibwa Kamala.

Baada ya kumaliza masomo yake ya Sekondari mnamo mwaka 2004 alihamia rasmi jijini Dar es salaam na kujiunga na vyuo mbalimbali ili kujifunza taaluma tofauti tofauti ambapo mpaka sasa ameweza kuwa mtaalamu wa Kompyuta, ingawa mwenyewe anakiri kuwa haipendi taaluma hiyo bali anapenda uandishi wa habari taaluma ambayo anaiendeleza kupitia kibaraza chake cha kublog akifundisha maarifa ya Utambuzi na stori za hapa na pale ili mradi maisha yanaendelea.

Ni mchangiaji mzuri katika blog za wengine ila msomaji asipokuwa makini anaweza kumuona kama mpotoshaj. Ni mkweli na hafichi kile anachokiamini bila kujali kama utakasirika au utafurahi.

Mara nyingi watu wasioelewa wanaweza kudhani labda ninapolumbana nae ninakuwa niko katika kiwango cha juu cha hasira, la hasha, ni katika kupendezesha mada husika na kuleta changamoto kuhusiana na mada hiyo.

Naomba nikiri kuwa Kamala ni mmoja kati ya wanablog ninaoheshimu sana misimamo yao, pamoja na kuonekana kuwa huwa natofautiana nae, lakini naomba nikiri kuwa sio kwamba nafanya hivyo kwa kuwa simpendi au sipendi misimamo yake. Ukweli ni kwamba napenda na ninaheshimu sana misimamo yake na maoni yake binafsi yawe ni mabaya au ni mazuri.

Hata hivyo naomba nikiri kuwa yapo mengi nimejifunza kutoka kwake na pia naamini kuwa

wasomaji wa blog hizi watakubaliana na mimi kuwa Kamala anao mchango mkubwa sana juu ya uwepo wa blog zetu kutokana na kutia hamasa kila achangiapo mada.

Naomba niishie hapa nisije nikatia chumvi sana na mchuzi ukachachuka.

Huyu ndiye Kamala Lutatinisibwa Omwami Ta Jasson Lutabwasibwa.

Bofya hapa kumsoma zaidi

Friday, September 18, 2009

SALAAM ZA MAKABILA YETU

Kijijini kwetu

Wasomaji wapendwa wa blog hii isiyoisha vituko, Kwa sasa niko jijini Dar es salaam nimerejea kimya kimya na leo nilikuwa najaribu kufanya utafiti wa lugha za makabila yetu hapa nchini. Kwa mujibu wa tafiti inasemekana kuna makabila zaidi ya 120 hapa nchini.Niliamua kuangalia zaidi salaam, hususan za asubuhi, Kutokana na utafiti wangu nimepitia makabila kadhaa na kukutana na maneno yanayotumiaka katika salaam za asubuhi ambayo yanafanana kidogo, hebu tuone maneno hayo ni yapi:


KINGONI: Uyimwiki = Habari za asubuhi

KIZIGUA: Kugona vihi = Habari za asubuhi

KINYAKYUSA: Ughonile = Habari za asubuhi

KIYAO: kwimukaga = Habari za asubuhi

KIPARE: Murevuka = Habari za asubuhi

KIUNGUJA: wambaje = Habari za asubuhi

KISAMBAA: Onga makeo = Habari za asubuhi

KIANGAZA: Mwalamtse = Habari za asubuhi

KINYAMWEZI: Mwangaluka = Habari za asubuhi

KICHAGA: Shimbonyi = Habari za asubuhi

KIMERU: Konumbware = Habari za asubuhi

KIMASAI: Sopai = Habari za asubuhi

KISUKUMA: Mwadila = Habari za asubuhi

KIHEHE: Kamwene = Habari za asubuhi

KIBENA: Kamwene = Habari za asubuhi

KIKINGA: Ulamwihe = Habari za asubuhi

KINYIRAMBA: Ulalaliani = Habari za asubuhi

KIHAYA: Wabonaki = Habari za asubuhi


Kwa leo naishia hapa mwenye nyongeza anaweza kuongeza ili tujifunze pamoja.
Tukutane wakati ujao