Wednesday, December 31, 2008

NIMEANZA KUZISHITUKIA HIZI DINI

Kabla sijaendelea kuandika kile ninachotaka kuandika humu, ningependa kuwaomba radhi wale wote ambao nitawakwaza kutokana na makala hii.
Naamini kila mtu anao uhuru wa kusema kile anachokiamini, hivyo nimeona na mimi nitumie uhuru wangu kusema kile ninachokiamini.
Ningependa kuchukuwa nafasi hii kuwaomba radhi, dada Yasinta, kaka Mpangala, kaka Kamala, kaka Mbilinyi, kaka Mtanga, kaka Mtwiba, kaka Bwaya, kaka Fita aka mzee wa Theolojia na wengine ambao sikuwataja lakini huenda habari hii ikawakera, kutokana na labda kugusa imani zao.

Hivi karibuni nimetofautiana sana na marafiki zangu kwa sababu eti siendi kanisani.
Kwani ni muda mrefu sasa nimekuwa siendi kanisani.

Kwa nini?

Ni kwa sababu nimepambazukiwa, nimeanza kutilia mashaka imani yangu ya kidini.
Familia yangu ni ya Kikristo wa dhehebu la Seventh Day Adventist (SDA) maarufu kama Wasabato, na tumekuwa tukihudhuria ibada tangu utoto wangu.

Nilivyozidi kukuwa ndivyo familia yetu ilivyozidi kutokuwa na mahudhurio mazuri kanisani. Kipindi hiki cha makuzi yangu akili yangu ilianza kujiuliza baadhi ya maswali yasiyokuwa na majibu.

Nilipofika kidato cha sita mahudhurio ya familia yangu kanisani yalipungua kabisa ikabaki kwenda mara moja au mbili kwa mwaka hasa labda kipindi cha Makambi.

Ni katika kipindi hiki ndipo nilipohudhuria ibada moja katika kanisa la Roman Catholic, nikiwa na rafiki zangu, niliamua kuungana nao ili kuwapa kampani.

Hili ni dhehebu la Kikriso kama la kwangu, lakini mbona lina taratibu nyingi tu ambazo ni tofauti na za kwetu sisi Wasabato?

Haya ndio maswali ambayo yalikuwa yakigonga katika kichwa changu kila wakati. Baada ya uzoefu na kuanza kukomaa nilianza kutafuta chimbuko la hii dhana ya dini. Nilianza kupata wasiwasi baada ya kugundua kwamba kila mtu amefuata dini ya wazazi wake na mababu zake.

Naamini ni watu wachache sana wanaoweza kusimama na kusema kwamba wamejichagulia wenyewe imani zao za kidini au hata madhehebu wanayokwenda kuabudia, nje ya dini au madhehebu ya wazazi wao.
Na kama walifanikiwa kufanya hivyo nadhani uhusiano na wazazi wao utakuwa una mashaka makubwa kama sio kuvunjika.

Kwa mfano mimi nilikuwa katika dhehebu la wasabato kwa sababu wazazi wangu ni Wasabato, kwa kuwa walinipeleka kanisani tangu nikiwa mdogo basi nikajikuta ni Msabato. Sikutakiwa kuhoji.

Jambo hili la kutokuwa na uhuru wa kuchagua dini lilianza kunitia wasiwasi kwa kiasi kikubwa.
Kwa jinsi nilivyozidi kukua ki umri na kimo ndivyo nilivyozidi kuyajua mambo kwa mapana zaidi, niligundua kwamba, kumbe dini zilikuwa zinatofautiana sana katika imani kiasi cha kufikia kurushiana maneno ya kejeli au wakati mwingine hata kupigana, hii iliendelea kunichanganya zaidi.

Hivi kwa mfano kama mimi ningezaliwa nikakuta wazazi wangu ni waislamu, kwa hiyo na mimi ningekuwa ni muislamu.
Na labda ningekuwa nawakejeli wakristo kwa kuwaona kama hawafuati dini ya kweli, bali dini yangu ndio ya kweli! Hii niliona haileti mantiki.

Kama wewe ni muislamu unaamua kupigana na mkristo kwa sababu ya imani yake au Mkristo unaamua kupigana na Muislam kwa sababu ya imani yake, Je kama unapigana na mjomba, shangazi, au binamu yako?

Nilipokuwa kidato cha sita masomo niliyokuwa nikiyapenda sana yalikuwa ni ya Sayansi. Niliona kwamba baadhi ya mambo ambayo nilikuwa nikiyasoma katika sayansi yalikuwa yakipingana na mambo niliyojifunza kanisani. Niliamua nisiendelee kutilia mkazo sana maneno ya mchungaji, nikaona nichunguze mgongano huu wa dini kwa dini pamoja na ule mgongano wa dini na sayansi.

Ukweli ni kwamba sitaeleza mgongano wa dini na sayansi kwa sababu bwana Mtambuzi na kaka Bwaya waliwahi kulieleza hilo kwa kirefu, sidhani kama maelezo yangu yatatofautiana na ya kwao. Rejea makala zao kama unahitaji ufafanuzi zaidi.

Nilipoenda chuoni mahudhurio yangu kanisani yalikoma kabisa na tafakuri yangu kuhusu dunia ndiyo ikawa imepamba moto. Sasa nilikuwa nimeenda mbali zaidi, na kwamba, kumbe kulikuwa na watu ambao walikuwa wanaamini kwamba mungu hayupo, pia nikaangalia katika dini mbalimbali za mashriki ya kati, mambo niliyokutana nayo sikuwahi kuyasikia hapo kabla.
Kumbe migogoro kati ya dini na dini na kati ya dini na watu wasiomwamini Mungu ni kutokana na kila kundi kutokubaliana na nadharia ya mwenzake!

Kufikia hapo nilianza kuiangalia dini yangu kwa mtazamo tofauti, mimi sio mtoto tena.
Nilisoma habari za wale wanaoamini kwamba hakuna mungu mtandaoni, nikagundua sababu ya wao kuamini hivyo. Kitendo cha kusoma habari zao katika kuutafuta ukweli kumenisaidia kuelewa kwamba siasa ilihusika kwa kiasi kikubwa katika dini.
Niligundua kwamba vitabu vya Biblia viliunganishwa pamoja kutokana na maandiko ya awali ya viongozi wa serikali za wakati huo na kanisa kwa ajili ya malengo yao.

Nimegundua kwamba viongozi wengi wa dini hutumia vitisho vya moto wa milele wa mungu ili kuwafanya watu wanywee na kujiunga na dini zao, kwa hofu kuwa wasipofanya hivyo watakuja kuungua na huo moto wa milele!!!.

Mambo haya, pamoja na kukosekana ushahidi wa kuwepo mungu ilikuwa ni rahisi kwangu kukubaliana na nadharia ya watu wasioamini uwepo wa mungu.

Dini za Kimashariki zinaonekana kuleta mawazo mapya ya mtazamo wa kisasa. Kwani hazina mlolongo wa vitisho na msululu wa mambo magumu ya kufanya ili kuweza kufika mbinguni,. Dini hizi zinasisitiza mtu kujitambua.

Tatizo moja kubwa linalozikabili dini zetu nitabia ya dini moja kuihukumu dini nyingine kwamba haifai. Wengine wanadai wasioamini hata wale wenye mioyo safi na wadilifu hawafai na wataishia Jehanam. Lakini watu wenye roho mbaya, mradi tu ni waumini na wanatoa sadaka basi wataishi katika utukufu wa milele!

Kitu cha kushangaza ni kwamba katika biblia imeandikwa kwamba tusihukumiane, lakini wakristo wanawahukumu wasioamini, kwamba hawafai. Wasioamini nao wanatakiwa kumkubali kila mtu kwa imani yake, lakini utakuta wanadharau waumini wanaoamini uwepo wa mungu. Inabidi kila upande ukubali imani ya mwenzake, kwani kila upande una watu wengi tu wa kutosha.
Hivi inawezekana watu wote hao wakawa ni wajinga?

Mimi kwa upande wangu naamini kila upande unategemeana na wa mwenzake, kama ukichunguza kwa makini imani ya kila mmoja.
Ingawa nimegundua kasoro ya dini yangu lakini sijawahi hata siku moja kuiponda. Ni moja ya urithi wangu, na imehusika kwa kiasi kikubwa katika malezi yangu.

Huu ni mtazamo wangu tu, naomba msinijengee chuki!!!!!!

Tuesday, December 30, 2008

HIVI KWA NINI TANGU MWAKA 1947 HADI LEO MGOGORO HUU HAUISHI?

Juzi wakati naangalia taarifa ya habari kwenye Luninga nilikutana na habari inayohusu mashambulizi ya anga yanayofanywa na na Israel katika ukanda wa Gaza ambao unamilikiwa na kundi la Kipalestina la Hamas.

Mpaka wakati huo naangalia taarifa ya habari kuliripotiwa kuwa mashambulizi hayo yaliyorindima kwa takriban masaa 24 yamesababaisha vifo vya Wapalestina wapatao 271, huku Israel ikiwa imepoteza askari wake mmoja tu! Kwa kuwa mashambulizi hayo bado yalikuwa yanaendelea sijui ni roho za watu wangapi zisizo na hatia zitakuwa zimepotea.

Hata hivyo Israel imejitetea kwamba imefanya mashambulizi hayo kwa nia ya kujilinda dhidi ya mashambulizi ya Hamas.

Wakati huo huo Umoja wa mataifa ulikemea mashambulizi hayo na kuitaka Israel kukomesha mashambulizi hayo mara moja.

Wakati nikiwa sekondari mwalimu wetu wa somo la Historia aliwahi kutufundisha kwamba kabla ya mwaka 1800 hakukuwa na taifa linaloitwa Israel.
Nakumbuka kwamba topiki hiyo sikuipa uzito unaostahili wakati ule, nadhani ilitokana na sijui utoto au kutokuchukulia mambo kwa uzito unaostahili.

Siku hizi nimekuwa ni mdadisi sana, kwa hiyo natumia muda mwingi kwenye maktaba ya baba nikipekua pekua ili kupanua wigo wa uelewa wangu.

Hata baba yangu huwa ananishangaa kwani tabia hii niliyoianzisha sikuwa nayo hapo kabla, lakini nadhani imetokana na kukua na kupambazukiwa, kwani ukishafika ngazi fulani ya elimu unakutana na nadharia nyingi za watu waliokufa ambazo nyingine hazikupata kuhojiwa wala kuchunguzwa.

Hebu ngoja niachane na hilo nisije nikakuchosha wewe msomaji wa blog yangu hii isiyokosa vituko kila uchao.

Basi baada ya kuangalia taarifa hiyo ya habari niliingia katika maktaba ya baba kutafuta kitabu chochote cha kujisomea, katika pekua pekua yangu nikakutana na kijitabu kilichoandikwa historia ya Israel, kwa bahati mbaya kijitabu hicho hakina hata jalada lake la juu hivyo msije mkaniuliza kinaitwaje.

Kutokana na kile nilichokiona kwenye taarifa ya habari muda mfupi uliopita nilivutiwa kukisoma kile kitabu.

Kumbe kwenye miaka ya 1800 ndipo kulipozuka swali la ni kwa namna gani wayahudi wataepuka kuuwawa kwa sababu ya chuki kule Ulaya?
Kwani wakati huo wayahudi hawakuwa na makazi, isipokuwa walikuwa wakitangatanga kule Ulaya.

Basi yale maandiko ya Biblia ya nchi ya ahadi, yakageuka harakati za kisiasa ya kutafuta makazi ya kudumu kule Mashariki ya Kati, kwenye eneo ambalo lilikuwa likikaliwa na wapalestina.

Kutokea mwaka 1920 hadi mwaka 1947, himaya ya Waingereza ndiyo iliyokuwa na mamlaka na Palestina. Wakati huo Palestina ilikuwa ni eneo lote la Israel ya sasa na maeneo yote yanayokaliwa kimabavu hivi leo na Israel. Maeneo hayo ni Gaza na Kingo za Magharibi.

Ongezeko la Waisrael kwenye eneo ambalo wenyewe wanaamini ni nchi yao ya ahadi, kwa mujibu wa maandiko ya Biblia takatifu, kitabu kisichohojiwa ingawa kiliwahi kukosewa mara kadhaa katika kuchapishwa kwake, kulianza kujenga hofu na wasi wasi kwenye eneo hilo.

Kwa hiyo ukichunguza sana utagundua kwamba hawa wanafiki Waingereza wamehusika sana katika kujenga mashariki ya kati ya leo isiyoisha migogoro, kisirani na wendawazimu ambao binadamu wa karne ya 21 kuushudia ni jambo la aibu isiyo na mfano.

Kwa ujumla migogoro ya kijiografia na kisiasa iliyozikumba na nchi za mashariki ya kati imechangiwa kwa kiasi kikubwa na nchi za Ulaya pamoja na Marekani.

Baada ya vita kuu ya pili ya dunia, umoja wa mataifa ambao ndio kwanza ulikuwa umeundwa ukiwa na nchi chache changa, uliamua kwamba, Palestina igawanywe na kuwa mataifa mawili.

Katika mgawanyo huo wayahudi wachache walipewa eneo kubwa kuliko wenye nchi, yaani Wapalestina.

Katika mgawanyo huo Wayahudi walipata asilimia 57 ya eneo, huku Wapalestina wakiambulia asilimia 43. Na Mji wa Jerusalem uliwekwa chini ya umoja wa mataifa.

Marekani ndio iliyokuwa kinara wa mpango huo na iliutilia nguvu na kuushabikia sana, Rais wa wakati huo Harry Truman, ambaye ndiye aliyeruhusu matumizi ya kwanza ya bomu la Atomic lililopigwa Hiroshima na Nagasaki nchini Japan hapo mnamo tarehe 6 na 9 mwaka 1945, na kusababisha kumalizika kwa vita vya pili vya dunia.

Rais huyu alionekana kuguswa na maisha ya ukimbizi ya Wayahudi na aliseam wazi kwamba Wayahudi kugaiwa eneo ambalo sio lao ilikuwa ndio muarobaini wa madhila waliyokuwa wakiyapata huko Ulaya.

Hata hivyo Rais huyo alipingwa sana na wasaidizi wake wa masuala ya kigeni kuhusu kuunga kwake mkono jambo hilo. Wasaidizi hao walikuwa wanaogopa kuharibu uhusiano kati ya Marekani na nchi za kiarabu na walihofia kwamba Urusi inaweza kuteka nchi za Kiarabu.

Labda niwakumbushe kwamba wakati ule Dunia iligawanywa kati ya Urusi (Ukomunisti) na Marekani (Ubepari)

Taifa la Israel lilitangazwa au kujitangaza rasmi hapo mnamo Mei 14, 1948, lakini mataifa ya Kiarabu yalipinga kugawanywa kwa Palestina na kukataa kulitambua taifa hilo la Israel.
Majeshi ya Iraq, Syria, Lebanon, Saudi Arabia, Yemen na Misri, Yaliishambulia Israel, lakini yalishindwa na Wamarekani.

Israel isingeweza kuyashinda majeshi hayo, kwani ilikuwa bado ni kanchi kachanga.

Wakati Waisrael wakiendelea kujiimarisha, Wapalestina walijikuta wakiwa ni wageni kwenye ardhi yao, na suala la Jerusalem kuwa mji wa Kimataifa, yaani kusimamiwa na umoja wa mataifa nalo likafa.

Mwaka huo huo wa 1948 Wapalestina walitimuliwa kutoka katika maeneo yao na kulazimishwa kuishi ukimbizini kwenye nchi za Jordan, Misri, Lebanon na nchi nyingine.
Inadaiwa kwamba, zaidi ya Wapalestina 750,000 wanishi ukimbizini.

Historia ya mgogoro huu ni ndefu na nikisema nisimulie yote kama nilivyosoma katika kijitabu hicho pamoja na mtandaoni vile vile, nitawachosha.

Lakini swali ninalojiuliza hapa, ni kwamba ina maana dunia hii imekosa wastaarabu kadhaa wanaoweza kumaliza mgogoro huo.

Jamani yaani kizazi na kizazi bado tunaendelea kushuhudia ujinga huu wa mgogoro usioisha!!!

Nadhani kuna haja ya Wapalestina na Waisrael yakiwemo Mataifa makubwa pamoja na umoja wa mataifa kuona haya na kuangalia mustakabali wa Taifa hilo.

Kwani damu imemwagika sana, He! tangu mwaka 1947!!!!

Sunday, December 28, 2008

JAMANI HIVI HALI HII MPAKA LINI?

Kuna jambo moja lilinikwaza sana wakati fulani. Hivyo nimeona ni vyema nikasema hisia zangu humu ili wanablog wenzangu wanisaidia mawazo.

Mimi ni miongoni mwa wanafunzi wa vyuo vikuu waliorudishwa majumbani kutokana na migomo iliyovikumba vyuo vikuu vingi hapa nchini kutokana na madai mbali mbali.

Sitaki kujadili kuhusu hilo kwa sababu si sababu ya kero niliyokumbana nayo.

Baada ya kurudishwa nyumbani baba alinishauri nikaripoti ofisini kwake anipangie kazi ya kufanya, kwani kuna kazi nyingi na anahitaji msaada wangu.

Labda niweke wazi kuwa baba yangu anamiliki kijikampuni chake kinachojishughulisha na utoaji huduma mbalimbali za kijamii.

Ukweli sikukubaliana na wazo la baba kwa sababu sikupenda kufanya kazi karibu na baba na badala yake nilitaka nitafute kazi ili baadae na mimi niwe na kitu changu mwenyewe kama vile na yeye alivyotafuta na kuwa na kitu chake mwenyewe.

Pia sikupenda kuwa kuajiriwa na baba kwani nadhani baadhi ya wafanyakazi wa mzee hawatajisikia vizuri na uwepo wangu pale ofisini.

Basi baada ya kubishana sana na baba, ilibidi akubaliane na mimi.
Ukweli ni kwamba baba yangu ananiheshimu sana kwani mimi ni mtaalamu wa kujenga hoja na kuitetea, ni mara chache sana alikuwa akinishinda linapokuja suala la kutofautiana kimtazamo.

Hivyo niliamua kutafuta kazi, niliamua kutumia muda wangu mwingi nikiwa kwenye mtandao pale nyumbani nikijaribu kutuma maombi yangu ya kazi kwenye mashirika tofauti tofauti na wakati mwingine nilipeleka maombi yangu kwa mkono au kwa njia ya Posta, ilimradi kutaka kujaribu kila mahali.

Kuna wakati nilipokea simu moja kutoka kwa mtu nisiyemfahamu, alinijulisha kwamba ameona maombi yangu ya kazi na anataka kunisaidia, hivyo alitaka tukutane tuzungumze kabla ya kufanya usaili ili aweze kunisaidia mambo fulani.

Nilijaribu kumuuliza kwa nini ameamua kunisaidia mimi, mtu ambaye hanifahamu na si ndugu yake, au mtu mwingine, alinijibu kwamba ameona anisaidie kwani amevutiwa sana na CV yangu na ameona kuwa ni mtu ambaye ninafaa kuajiriwa katika shirika lao.
Alitumia muda mwingi kujieleza na kunihakikishia kwamba anayo nia nzuri ya kutaka kunisaidia.

Nilipomuuliza tukutane wapi, alinitaka tukutane kwenye hoteli moja maarufu iliyoko maeneo ya katikati ya jiji.
Nilisita kumkubalia , lakini baada ya kutafakari niliona nimkubalie, hivyo nilikubali ule mwaliko wa yule mtu aliyejitambulisha kwamba ni mmojawapo wa wakurugenzi waandamizi wa lile shirika nilikopeleka maombi yangu.

Siku iliyofuata majira ya jioni nilikwenda pale Hotelini kama tulivyo ahidiana, sikuwa mgeni na mahali na ile Hoteli kwa sababu nilishawahi kwenda pale mara kadhaa kuhudhuria semina wakati nilipokuwa nafanya kazi kwa muda kwenye NGO moja kabla sijajiunga na Chuo kikuu.

Nilipofika pale nilimpigia simu na alinielekeza mahali alipo, nilipofika nilikutana na baba mtu mzima anayeweza hata kunizaa mara tano.

Alijitambulisha na mimi nikajitambulisha, mara akamuita muhudumu na kunitaka niagize kinywaji chochote ninachotaka, niliagiza maji tu, alinitaka nagize mvinyo au pombe yoyote ambayo ninakunywa, lakini nilimkatalia.

Hata hivyo nilimuomba afupishe maongezi kwa sababu baba yngu huwa anapenda sana kufika pale Hoteli na marafiki zake, kusikia hivyo akadakia na kunijulisha kuwa ameandaa mahali pa faragha kwani amechukuwa chumba tutachofanyia maongezi, kisha akanikabidhi kadi ya kufungulia mlango ambayo ilikuwa imeandikwa namba ya chumba.
Nikamuuliza, kwani hatuwezi kufanyia mazungumzo yetu pale mpaka twende chumbani?
Akadai kwamba anataka kunilinda kwa hiyo nisihofu nitakuwa salama.
Nitakuwa salama!!!? mimi na yeye chumbani!!!? Nilimkatalia na kumtaka tufanyie mazungumzo yetu pale la sivyo niondoke zangu, alikubali japo kwa shingo upande.
Mara akaanza kujiongelesha, “ooh unajua wewe ni mzuri sana na una sifa zote za kupata kazi pale lakini unaweza kukwamishwa kwa sababu utatakiwa utoe kitu kidogo, kwani kazi yenyewe imeombwa na watu wengi, na wote wanasifa, lakini nilipoona CV yako nikavutiwa na wewe, hivyo naomba ukubaliane na mimi kiutu uzima ili na mimi nikusaidie”

Nilipomuuliza nikubaliane na yeye kiutu uzima kivipi? kwani kama ni rushwa mimi siwezi kutoa kwa sababu si lazima nifanye kazi kwenye shirika lao.

Ndipo akaniambia nikubaliane nae tukafanye mapenzi, ili aweze kunisaidia.
Nilibaki nikiwa nimeduwaa kwenye kiti, nisiamini kile nilichosikia kutoka kwa yule mzee, alionekana kutokuwa na wasi wasi kabisa wakati akitamka neno lile, na hiyo iliashiria kwamba hiyo ndio tabia yake.

“Unashangaa nini?” aliniuliza bila hata kuonesha dalili ya aibu usoni pake. Nisaidia na mimi nikusaidie, kwani ulimwengu tulionao ni wa kusaidiana, wewe unahitaji kazi na mimi nahitaji mwili wako tatizo liko wapi?

Niliimkatalia, kata kata na kumuonya kwamba asirudie tena kunipigia simu la sivyo nitamuadhiri mpaka ashangae, kwani mimi sio malaya kama anavyofikiria.

Huo ulikuwa ndio mwanzo wa matukio mengine yanayofanana na hayo kunitokea, kwani katika baadhi ya makampuni au mashirika niliyoomba kazi nilikutana na viashiria au mazingira ya kuombwa rushwa ya ngono.
Wengine walikuwa makini sana walikuwa wanatumia njia ya mzunguko katika kufikisha ujumbe kwamba wanachohitaji kutoka kwangu ni Ngono!!!!.

Jamani hivi ni kwa nini hali hii?

Najaribu kuangalia wale wasichana wenzangu ambao wanatoka katika familia duni ambazo mustakabali wa kuendesha maisha yao na ya familia zao ni wao kupata vibarua.

Je kwa hali hii watapona?

Mimi si mtetezi wa haki za wanawake na watoto, ila nimelisema hili kwa sababu limenikuta, nikamudu kukabiliana nalo, kwa sababu mimi ni zaidi ya mwanamke.

Hivi sasa nimefungua kijimradi changu sikosi shilingi mbili tatu, huku nikisubiri mustakabali wa kurudi chuoni kuendelea kukariri kile mtambuzi alichoita maarifa ya wengine pasipo kubuni maarifa yetu wenyewe.




Friday, December 26, 2008

MWANASAYANSI LONGO LONGO.

Jana katika kupitia Blog mbalimbali ili kupata hekima za wenzangu, nimekutana na Blog mbili zinazoshabihiana kimtazamo, Yaani ile ya Utambuzi na ya Jielewe.

Katika blog hizo nilikutana na mada mbalimbali, lakini mada iliyonivutia ni hii ya mjadala wa mwanzo wa mwanaadamu. Nimekutana na mjadala mzito wenye rejea za wanasayansi mbalimbali na nadharia zao.

Mimi si mwanasayansi na sitaki kuingia kwenye huo mjadala kwa sababu siipendi sana Sayansi.

Hata hivyo wakati napitia Maktaba ya baba nilikutana na Kitabu kinachozungumzia mambo hayo hayo ya Sayansi, Maana Baba yangu nae anapenda sana kusoma, na ukiingia kwenye Maktaba yake utakutana na vitabu mpaka vya Kilatini.

Tuyaache hayo, ngoja niwasimulie kisa cha mwanasayansi mmoja ambaye nimesoma habari zake kutoka kwenye kitabu hicho cha mzee, ambaye ningependa kumuita Mwanasayansi Longo Longo.

Katika mojawapo ya sijui niite utafiti au utabiri, mwanasayansi huyo wa Ki-Irish,
Dk. Dionysius Lardner aliyeishi kati ta Mwaka (1793-1859) aliwahi kusema kwamba, Garimoshi halitaweza kwenda kasi hata siku moja.
Alisema garimoshi litaendelea kuwa na kasi ndogo sana, kwani likienda kwa kasi kubwa, abiria wataweza kufa kwa tatizo linalifahamika kitaalamu kama Asphyxia, yaani kukosa pumzi.

Pamoja na kwamba alikuwa ni mwanasayansi, Lakini nadhani alikuwa hajui anachokisema kwa wakati ule.

Kwa nini?

Kwa sababu leo hii kuna magari moshi yanayosafiri hata kilomita 500 kwa saa.

Sasa sijui mwanasayansi huyu alikuwa anatumia ubongo huu tulio nao katika tafiti zake au alikuwa anatumia nini, mimi sijui.

Ningependa kuchukuwa nafasi hii kuwatahadharisha kaka
Bwaya na kaka Mtambuzi kuwa wawe makini na nadharia za baadhi ya wanasayansi, kwani pia walikuwepo wanasayansi wengine waongo, kama mwanasayansi huyu wa Ki-Irish.

Hata hivyo nazifagilia kazi zao.

Thursday, December 25, 2008

KUMBE BIBLIA ILIWAHI KUKOSEWA!!!!!!!

Mwaka 1631 toleo fulani la Biblia lilikosewa. Hili lilifahamika kama toleo la Mfalme James. Kwenye kitabu cha Kutoka 20, mstari wa 14 kulikuwa na neno lililoachwa wakati wa kuchapishwa.

Hii ni kwenye amri ya saba, ambapo iliandikwa, “In a thou shall commit adultery”, ikiwa na maana “Mzini”
Neno “not” liliachwa kwa bahati mbaya. Nakala za Biblia hiyo ziliitishwa na kuharibiwa kwa amri ay Mfalme Charles I.

Lakini hadi leo kuna nakala kama 11 ambazo kwa bahati mbaya hazikurudishwa kuharibiwa.
Hivyo ukikutana na moja ya nakala hizo, usije ukaiamini. Biblia hiyo ilijulikana kwa jina la Biblia iliyolaaniwa. Kwenye jengo la kumbukumbu ya Biblia la Branson, kuna nakala moja ya toleo hili.
Mchapishaji wa Biblia hiyo alitozwa faini ya sawa na shilingi 400,000 kwa kosa hilo.

Lakini tena mwaka 1653, neno lingine liliachwa kwenye sentensi katika kitabu cha Wakorintho 6, mstari wa 6 hadi 9. Kuna maneno “Know ye note that, the unrighteous shall inherit the Kingdom of God”. Badala ya “ Know ye note that the unrighteous shall not inherit the Kingdom of God” makosa hayo yalikuwa na maana kwamba waovu wenye dhambi ndio watakaouona ufalme wa mbinguni. Hii nayo ilikusanywa na kwenda kuharibiwa. Hii nayo iliitwa “ Biblia isiyonyoofu”