Wednesday, November 18, 2009

NIKAPIGIWA “EMCHEKU”

Usiku ndio muda muafaka

Ni usiku wa saa tatu hivi, niko kijijini kwa bibi Koero, na tuko jikoni tunaota moto, huku akinisimulia simulizi mbalimbali juu ya maisha. Bibi Koero ni hodari wa kutoa simulizi zenye kufundisha na za kusisimua.

Tukiwa katikati ya mzungumzo, mara tukasikia michakato ya miguu huko nje kuashiria kuwa kuna mtu huko, “Emcheku aha” ilikuwa ni sauti ya kiume kutoka nje, bibi aliniambia nitoke ili kuangalia kuwa ni nani.

Nilipotoka, kwa kuwa kulikuwa na giza, niliona kivuli cha mtu, lakini alikuwa na kurunzi yenye mwanga hafifu, na alikuwa akiiwasha na kuizima, nilirudi ndani kwa hofu na kumweleza bibi Koero mauzauza niliyokutana nayo huko nje.

Bibi Koero alicheka sana, na kuniambia kuwa, huyo ni mgeni wangu, kaja pale kuposa, na mlengwa ni mimi kwa kuwa hakuna binti mwingine pale nyumbani bali ni mimi.
Nililishangazwa na aina ule ya posa, kwangu mimi ile ilikuwa ni habari, na ili kujua mengi zaidi, nilimdadisi bibi Koero ili anisimulie juu ya utaratibu huo.

Bibi Koero anasimulia kuwa enzi zao, binti akivunja ungo, vijana huanza kufika pale mida ya usiku kupiga hiyo “Emcheku” inawezekana wakafika zaidi ya wavulana kumi kwa usiku mmoja kulingana na uzuri na tabia ya binti huyo.
Emcheku ni salaam ya heshima anayotoa mvulana anapokwenda kuchumbia.

Kwa kawaida wavulana hao wakifika kila mmoja kwa muda wake na kupiga hiyo Emcheku, Binti husika huambiawa atoke nje kuonana na mvulana huyo na kama hajampenda basi humweleza na huyo kijana huondoka zake, na akitokea mvulana anayempenda, basi hupewa ruhusa na binti huyo ili alete Posa na hapo ndio milango hufunguliwa kwa mvulana huyo kumtembela mchumba wake.

Mara nyingi matembezi hayo hufanywa usiku na mvulana akifika binti huruhusiwa na wazazi kutoka nje ili kuzungumza na mchumba wake, lakini walikuwa hawaruhusiwi kukutana kimwili au kuonjana mpaka utakapofika muda muafaka watakapofunga ndoa takatifu.

Tofauti na zamani, bibi Koero, anasimulia kuwa, siku hizi vijana wamebadilika sana na wengi wameuharibu utaratibu huo na kuugeuza kuwa kichaka cha kufanyia ngono. Wavulana siku hizi kama anamtaka binti, hupiga hiyo Emcheku na binti akiridhia, humhadaa, mpaka amuonje na akifanikiwa kuingia mitini na posa inaota mbawa.

Unaweza kukuta mvulana anawahadaa wasichana zaidi ya kumi lakini aisoe hata mmoja baada ya kuwaonja.

Wasichan nao wamekosa subira, kila wakisikia hiyo emcheku, wanajua kuwa ni bahati imewajia, kumbe hakuna lolote ni wavulana mafisadi tu wenye uchu wanataka kuwaonja na kisha kutoweka.

Sasa sijui na mimi nilipigiwa hiyo emcheku ili kuonjwa……LOL

Sunday, November 15, 2009

MUNGU ALINIONYESHA MSIBA ULE!


Kwanza ningependa kuchukua nafasi hii kuwashukuru wasomaji na wanablog wenzangu wote mlionipa pole kwa msiba uliotupata. Kusema kweli kama walivyosema baadhi ya wanablog kuwa ule ulikuwa ni msiba wa taifa kwani roho za watu zaidi ya 20 zimepotea wakiwemo watoto ambao bado walihitaji kuishi na kutimiza ndoto zao.

wakati mwingine unaweza kukufuru mungu kw kuhoji kile kilichotokea, lakini kama maandiko matakatifi katika vitabu vya dini hususana hizi dini zetu mbili ambazo ndizo dini kuu hapa nchi yaani ukristo na uislamu, vilivyoeleza kuwa yote mema na mabaya yanatoka kwake yeye na hatupaswi kuhoji mamlaka yake.
Lakini kama si hivyo naamini tungekuwa tunamlaani sana Mungu pale tunapoondokewa na wapendwa wetu.

Ukweli ni kwamba msiba ule uliotupata nilionyeshwa kabisa na mwenyezi Mungu katika njia ya ajabu sana. Ni kiasi cha wiki nilikuwa nasumbuliwa na malaria kiasi cha kulazwa Hospitalini na kutundikiwa Drip za Kwinini. Nakumbuka siku mbili kabla yakupata msiba ule niliota ndoto ya kustaajabisha sana, niliota kuwa nimeenda kijijini kwa bibi Koero kumtembelea na nilipofika kule kijijini nilipokewa na bibi Koero lakini hakuwa na furaha sana kama nilivyokuwa nimemzoea, nilipomdadisi sababu ya kutofurahishwa na ujio wangu, alinijibu kwa kifupi tu kuwa anajisikia vibaya.

Siku iliyofuata aliniomba nimsindikize shambani kwake ili akanioneshe mazao aliyolima, tulipofika shambani nilishangaa kukuta matuta mengi ya viazi vitamu yakiwa yamestawi barabara, niliruka kwa furaha, kwani mimi huwa napenda sana viazi vitamu, bibi alionekana kunishangaa, nilipomdadisi kuwa kwanini haonekani kufurahia mazao yake, aliniambia kuwa, sina haja ya kufurahia kustawi kwa vile viazi kwani havina ishara nzuri katika familia yetu. nilimdadisi anifafanulie maana ya kusema vile, aliniambia tukae chini anieleze.

Aliniambia kuwa hapo zamani enzi za mababu zao, ilikuwa kama mtu akilima viazi kisha vikastawi sana na kuonesha ishara ya mavuno ya kutosha, waliamini kuwa hiyo sio ishara nzuri katika familia husika, kwani ni lazima pangetokea maafa makubwa au kupata msiba wa mtu mzito katika familia, kwa hiyo hata yeye hawezi kufurahia kustawi kwa yale mazao kwani sio ishara nzuri katika ukoo wetu.

Nilijikuta nikilia kwa sauti, baada ya kusimuliwa habari ile na bibi Koero, nilishtuliwa na mama, alipokuja kuniamsha baada ya kusikia kilio changu. Ilikuwa ni saa kumi za alfajiri, nilimsimulia mama na bada ya kumweleza juu ya ile ndoto aliniambia kuwa sina haja ya kuamini kwani ni mambo ya kishetani, hata hivyo tulisali na mama kisha nikarudi kulala, lakini sikupata usingizi kutokana na kuogopa, ikabidi niamke na kuanza kusoma mtandao na baadae ndio nikaandika ile habari ya siku ya kufa kwangu, nilijikuta tu nikiandika na kuiweka hapa kibarazani kwangu.

Jioni nilipata email kutoka kwa kaka Shabani, Mzee wa Utambuzi. Email yake ilinifumbua macho na kuuona ukweli mpana zaidi, kwamba ile makala yangu haikuashiria jambo jema. kwani baada ya kusoma ile makala yangu niliyoipa kichwa cha habari kiisemacho SIKU YA KUFA KWANGU, kaka Shabani aliniandikia akiniambia kuwa ile makala imemtisha sana na aliniambia kuwa haiashirii jambo jema. Alitaka kujua zaidi hali yangu na pia kujua niliwaza nini mpaka kuandika makala ile.

Sikuweza kumjibu kutokana na kutingwa, lakini siku iliyofuata wakati najiandaa kumjibu na labda kumtaka ushauri juu ya ile ndoto niliyoota ndipo tukapokea taarifa za maafa yaliyotokea kijijini kwa mama ya kuporomoka kwa mlima kulikosababishwana mvua kubwa na kusababisha vifo vya watu zaidi ya 20 wakiwemo shangazi na mjomba wake na mama pamoja na watoto wao.
Ulikuwa ni msiba mzito sana kwetu kwani alikuwa ndiye shangazi yake mama pekee aliyebaki, baada ya shangazi zake watatu kufariki miaka kumi iliyopita.

Safari yetu nayo ya kuelekea msibani iligubikwa na mauzauza mengi, kwani wakati tunakwenda, mimi ndiye niliyekuwa nikiendesha gari na tulipofika Korogwe kwenye kona za msambiazi niligonga Kondoo ambapo alikufa pale pale, nilibabaika kidogo ikabidi dada yangu anipokee na kuendesha yeye.

Leo wakati tunarudi tulisimama Korogwe ili kupata chakula cha mchana, na baada ya kupata chakula tukarejea kwenye gari ili kuendelea na safari, ni hapo ndipo tukagundua kuwa kitasa cha mlango kimevunjwa na mkoba wa mama uliokuwa na fedha, simu zake mbili za mkononi na Kamera umeibwa, tulijaribu kuwauliza watu waliokuwa jirani na gari letu, lakini hatukupata ushirikiano, tuliamua kuondoka lakini tulipofika ya maeneo ya Kwedikwazu, mdogo wangu Jarome ambaye ndiye aliyekuwa akiendesha gari akagonga mnyama jamii ya kicheche au sijui ni fungo, hata sijui alikuwa ni mnyama gani maana alikuwa akiendesha kwa spidi kubwa kidogo. Ilibidi tumshauri apunguze mwendo hadi tukafika Dar.
Kilichotuuma ni kuibiwa kwa kamera ya mama ambayo ilikuwa na picha nyingi za kumbukumbu ya mazishi ya wale wahanga wa maporomoko ya mlima. Ni jambo ambalo lilitufadhaisha sana.
Tumerejea salama, na wote tuwazima wa afya

Wednesday, November 11, 2009

SIKU YA KUFA KWANGU!


Wengu tunaogopa kifo!

WAKATI NASOMA HIKI KISA KWA MARA YA KWANZA NILIOGOPA SANA, LAKINI KUNA KITU NILIJIFUNZA, HATA WEWE UNAWEZA KUJIFUNZA PIA.



Naomba wakati unasoma hii habari uwe peke yako na uwe umetulia, bila kubughudhiwa.
Hakikisha hakuna unaloliwaza wakati unapoanza kusoma kwani hiyo itakusaidia kung’amua kile ninachomaanisha katika habari hii.


Naomba usiwe mwoga, kwani ni habari ambayo itakufunza jambo fulani katika maisha.
Haya ungana nami katika kusoma habari hii.


Katika akili yako hebu hisi kama vile unajiona, yaani tengeneza taswira kama vile unajiona ukiwa unaenda kuhudhuria mazishi ya mtu umpendae na unayemfahamu. Jione ukiwa unaendesha gari kuelekea kanisani ambapo ndipo mahali watu wanapokusanyika kuuaga mwili wa marehemu kabla ya mazishi.


Unapofika pale unapaki gari lako na kutoka kuelekea ndani ya kanisa, unapoingia ndani ya kanisa unaona kumepambwa na maua mazuri yenye kunukia na huku ukisikia ala za muziki mororo. Wakati ukielekea kwenye eneo ulilopangiwa kukaa unawapita ndugu, jamaa na marafiki wakiwa na nyuso zenye huzuni na majonzi yenye kuashiria kusikitishwa na kuondokewa na mtu waliyempenda sana.


Unapokaribia kufika kwenye nafasi uliyopangiwa kukaa, unapita karibu kabisa na sanduku lenye mwili wa marehemu na unapotazama mwili ulioko ndani ya sanduku hilo unastuka kuona mwili ulioko ndani ya sanduku hilo ni wa kwako!
Mara kuna sauti inakwambia "haya ni mazishi yako yatakavyokuwa miaka mitatu ijayo kuanzia sasa"


Watu wote walioko pale wamekuja kuonyesha mapenzi yao kwako na kukupa heshima kwa kuuaga mwili wako ili ukapumzike kwa amani.


Duh! Unashusha pumzi na kuketi, ili kusubiri ibada ianze. Unapoangalia ratiba ambayo ulipewa wakati unaingia pale kanisani unakuta wamepangwa wazungumzaji wanne, wazungumzaji wa kwanza wanatoka katika familia yako, mmoja wa watoto wako, mmoja wa kaka zako, dada zako, binamu, shangazi, mjomba, baba mdogo, mama mdogo, bibi, babu na ndugu wengine wa karibu ambao walisafiri maili nyingi ili kuja kushiriki mazishi yako.


Mzungumzaji wa pili ni mmoja wa marafiki zako ambaye mlishibana sana, mzungumzaji wa tatu ni kutoka katika mahali pako pa kazi na mzungumzaji wa nne ni kutoka katika kanisa unalo Sali au kutoka katika taasisi ya kijamii ambayo ulikuwa ukishiriki katika kuihudumia jamii baada ya muda wako wa kazi.


Sasa hebu fikiria kwa makini sana. Ungependa wazungumzaji hawa wazungumze nini juu ya maisha yako hapa duniani? Wewe ni mume, mke, baba au mama wa aina gani? Wewe ni mvulana, msichana, binamu, wa aina gani? Ni rafiki wa aina gani? Ushirikiano wako na wafanyakazi wenzako ulikuwaje?


Ungependa wakuzungumzieje? Ulikuwa ni mtu mwenye tabia gani kwa ujumla? Uliisaidiaje jamii, ulifanikiwa katika lipi? Ungependa wakukumbuke kwa lipi? Hebu waangalie kwa makini watu waliokuzunguka. Kama ungepewa nafasi, ungeyabadili vipi maisha yao?
Kama umesoma kwa makini habari hii naamini kuna jambo utakuwa umejifunza.
Nimegundua kuwa ili ujue kuwa wewe ni mtu wa namna gani ni vyema ukahudhuria mazishi yako mwenyewe………………


Tafakari…………….


Habari hii nimeitoa katika kitabu cha The 7 habits of highly effective people cha Stephen R Covey.

Saturday, November 7, 2009

MSIONE KIMYA......NAUMWA

Naikumbuka picha hii enzi hizo!

Ndugu zanguni, msione kimya, nimeshambuliwa na anofelesi na sasa najiuguza majeraha ya malaria yapata wiki sasa, nimepata tiba ipasayo lakini majaaliwa ya afya yangu hayaoneshi kutengemaa....nawashukuru sana kwa kunitembelea, na hapo nitakapopona nitarejea kwa kasi ya ajabu...

Nawapenda wote na mungu awabariki..

Saturday, October 31, 2009

LEO TUCHEMSHE BONGO KIDOGO.

Ndugu wasomaji wa blog hii takatifu, leo nataka nijaribu bongo za watu kama zinafanya kazi sawa sawa maana week end hii nimekosa hata cha kuandika kutokana na kuzidiwa na majukumu ya kifamilia.

Nimetenga zawadi za kuwatumia washindi watakaoshinda katika kujibu mafumbo haya yote. Zawadi ya kwanza itakuwa ni Picha yangu kubwa ya ukutani kwa wale walioko ughaibuni au mikoani, au kupata chakula cha usiku mimi na mshindi wa kwanza katika Hoteli maarufu jijini Dar kwa wale walioko hapa Dar. Zawadi ya pili ni kutumiwa zawadi ya kitabu cha The Secret kilichoko online na zawadi ya tatu ni kutumiwa picha ya familia ya mzee mkundi.

Haya tuanze kufumbua mafumbo yafuatayo:


Fumbo la Kwanza:

Mama Yasinta ana watoto watano, wa kwanza anaitwa Nana, wa pili anaitwa Nene, wa tatu anaitwa Nini, wa nne anaitwa Nono, Je wa tano ataitwa nani?

Fumbo la Pili:

Kuna mtu mmoja bubu alikwenda kununua miwani dukani, alipofika alimuonesha muuzaji ishara kama vile anavaa miwani yule muuzaji akamuelewa na kumpatia miwani akaondoka zake, mara akaja kipofu, Je unadhani ataonesha ishara gani ili apatiwe miwani?

Fumbo la Tatu:

Ninazo namba kumi zifuatazo: 1,3,5,7,9,11,13,15,17.19
Kama ukizijumlisha zote yaani 1+3+5+7+9+11+13+15+17+19 unapata 100.
Unachotakiwa kufanya ni kutafuta namba 5 miongoni mwa namba hizo ulizopewa hapo juu na ukizijumlisha unapata 50 yaani nusu ya 100.

Masharti:
Haitakiwa kurudia namba, kwa kuijumlisha mara mbili au kujumlisha namba pungufu ya namba tano zinazotakiwa. kwa mfano: 13+17+15+5 unapata 50. Sio sahihi kwa kuwa idadi ya namba zilizojumlishwa hazifiki 5.

Haya nasubiri majibu yenu…….

Friday, October 30, 2009

HUU NDIO WEMA!

Jirani kala nini?



Huu ndio wema! Unapotenda wema usitegemee fadhila. Unapokuwa na marafiki, ndugu, na jamaa wa karibu, watendee wema bila kudhamiria kupata fadhila kutoka kwao. Ninapoongelea wema na kutoa ninamkumbuka mama Theresa wa Calcutta ambaye kwa umri na maisha yake angelikuwa Bilionea lakini kwa kujitolea kwake alikufa masikini, lakini akiwa ni tajiri wa nafsi. Nina maana alikufa akiwa na ridhiko, kwani kazi aliyotaka kuifanya aliifanya tena kwa kufaulu. Je wewe hufurahii kuwa kama yeye?

Kumbuka amri kuu isemayo “mpende jirani yako kama unavyojipenda” Je unapokula na kusaza huwa unajiuliza kuwa jirani kala nini?

Tafakari………

Wednesday, October 21, 2009

JAMANI HUU NI UTABIRI, UNAJIMU AU DHIHAKA?

Jamani mimi sio mpenzi au mshabiki wa mambo ya Nyota, kwangu mimi nachukulia kama huo ni ushirikina. Jana kuna mdau kanitumia huu utabiri au sijui niite unajimu, akinituhumu kuwa, kwa kuwa nimezaliwa mwezi wa Mei basi ninazo tabia hizi. Ukweli ni kwamba sina uhakika na hicho alichoandika, na siamini kabisa kama ninazo tabia hizo, ila waswahili wanasema Nyani haoni kundule. Kwa hiyo naomba wadau munisaidie kama unajimu huu unanihusu………….maana naona hii ni kaaaaaaaazi kweli kweli.

TABIA ZA WATU WALIOZALIWA MWEZI MEI…….HATA WEWE KOERO UMO

Mtu yeyote ambaye amezaliwa mwezi wa Mei mwaka wowote, anaweza kuwa na alama ya nyota ya Ng’ombe {Tauras} au Mapacha {Gemini}. Hapa sitazungumzia nyota moja moja, bali nitazungumzia mwezi ambao amezaliwa mtu. Kwa hiyo nitazungumzia waliozaliwa mwezi wa Mei ambapo wewe Koero ni mmoja wapo.

Watu waliozaliwa mwezi wa Mei ni wagumu, hawaambiliki wanapotaka kufanya jambo, wanapopania. Tunaweza kusema ni watu ving’ang’anizi. Lakini kwa bahati mbaya sana, kama wamempenda mtu, hakuna watu wanoporomoka kirahisi kama wao. Yaani kama wamempenda mtu wanashikwa kirahisi kuliko mtu mwingine yeyote.

Ni watu ambao wanaweza kuvumilia shida na suluba za maisha katika kiwango cha ajabu. Ni watu ambao wanamudu kuhimili misukosuko kimwili na kiakili, yaani hawachanganyikiwi kirahisikwenye misukosuko, hasa kama nia yao ya kung’ang’ania bado ipo.

Ni watu wenye uwezo mkubwa wa kumbukumbu. Kama ni uwezo wa kukariri masomo, basi ndiyo wenyewe. Lakini kwa bahati mbaya, wanapenda sana kujumuika na kujimwaga. Kwa hiyo wengi huwa hawafaidi matokeo ya vipaji vyao na wakati mwingine hata hivyo vipaji havionekani kwa sababu vinafungwa na kupenda kwao starehe.

Ni watu pia wanaofaa kwenye kazi kama zile za uhudumu katika ndege au hata mighahawani. Wana sifa ya kujua ladha ya chakula na wanamudu kutengeneza chakula kizuri sana nyumbani hata kama vifaa na fedha ni haba sana.

Ni watu ambao pia wana uwezo wa kuongoza kwenye mashirika au maeneo ya shughuli. Watu waliozaliwa Mei, inawezekana kwa nje wakaonekana kuwa na uwezo sana kuliko walionao kweli.

Hii ni kwa sababu wanajipenda sana, iwe kuvaa au hata kuwa na vitu vingine vya thamani vya nje. Mtu aliyezaliwa Mei anaweza kuwa na gari kubwa, lakini akiba ya shilingi elfu moja mfukoni hata nyumbani hana. Anaweza kuwa anavaa suti kila siku wakati hata godoro la kulalia hana.

Ni watu ambao wakipenda mtu wanakuwa kama vichaa, kwani watampa kila kitu. Kama nilivyosema, wanashikwa kabisa na kuwa kama mazuzu. Lakini wakimchukia mtu watapambana naye hadi waone kinaeleweka. Uzuri wao ni kwamba, wanapenda kukabiliana na mtu ana kwa ana, hawapendi mambo ya chini chini au njama. Wanapenda maisha ya wazi tu, hata kama ni ugomvi au uadui.

Watu waliozaliwa mwezi Mei iwe wanaume au wanawake hawatakiwi kuoa au kuolewa mapema. Hawatakiwi kufanya hivyo kwa sababu mara nyingi, kama sio zote ndoa zao za kwanza huwa wanakuwa wamekosea kuchagua. Labda ni kwa sababu wakishapenda wankuwa ni vipofu halisi. Ni watu ambao wanatakiwa wakitaka kutafakari na kuamua jambo wake wenyewe na kutafakari kimya. Hii ni kwa sababu wakiwa katika watu wengi, wantokea kuwaamini watu hao wengi na kuchukulia mawazo ya hao wengi kama yao. Ni watu ambao huchanganywa na kudanganywa kirahisi. Ni watu ambao wanapoingia kwenye hisia au upendo, hawana tena uwezo wa kufikiri vizuri.

Ni watu wenye wivu sana na mara nyingi wivu wao wa kimapenzi huwafanya kuleta vurugu au kusababisha machafuko ya wazi ya kiuhusiano. Lakini siku zote, baada ya vurugu hizo huhisi kushitakiwa na dhamira. Hujutia tabia zao za wivu lakini hawana uwezo wa kuzidhibiti kama wanavyoamini wao.

Kwenye uhusiano ukiacha wivu, ni waaminifu na wanyeyekevu kwa wapenzi wao. Wanafaa sana kuwa maafisa serikalini. Wauguzi na hata kufanya kazi za bustanini. Ni watu wazuti katika mashairi, muziki na sanaa kwa ujumla.

Kiafya ni watu wanaougua kirahisi maradhi yenye kuathiri koo, pua na mapafu pia. Kwa hiyo wantakiwa kuwa makini sana na mazingira ambayo yanaweza kudhuru koo, pua au mapafu yao. Vitu kama sigara, haviwafai watu waliozaliwa Mei

Sunday, October 18, 2009

KISA CHA SAIDI WA MBEKENYELA......!



Nakumbuka alikuwa na kawaida ya kuja pale ofisini kwangu, maeneo ya mjini na kunisaidia shughuli za usafi na kumlipa ujira kidogo. Kama nilikuwa nataka kununua kitu nilikuwa namtuma. Ni kijana mchapa kazi kweli na mcheshi kupindukia.

Akiwa ni mzaliwa wa Lindi katika kijiji cha Mbekenyela, kijana huyu ambaye ningependa kumwita Saidi *{Sio jina lake halisi}hakubahatika kumuona mama yake. Anasimulia kuwa mama yake aliolewa akiwa na umri mdogo sana miaka 15 na mzee mmoja aliemzidi kwa miaka 50, aliolewa katika zile ndoa maarufu za Korosho. Ndoa ambazo hufanyika sana mara baada ya msimu wa korosho.

Anasema kuwa kule kwao Lindi, kila baada ya msimu wa korosho wazee wengi ambao wana mashamba makubwa ya Korosho hukimbilia kuoa vibinti vidogo kwa kuwa wanazo fedha za mauzo ya Korosho, kuna wakati watoto wa kike hulazimika kuachishwa shule ili kuozeshwa kwa vibabu hivyo visivyoisha tamaa, na mara nyingi ndoa hizo huwa hazidumu kwani fedha zikiisha na ndoa huingia katika misukosuko na hatimaye kuvunjika kutokana na vizee hivyo kushindwa kumudu gharama za malezi ya wake wawili au hata watatu.

Hali hiyo imesababisha familia nyingi mkoani humo kuwa na vijukuu baada ya mama zao kuachika na kurudishwa nyumbani, hivyo kufanya hali ya maisha katika familia nyingi kuwa ngumu.

Mama yake Saidi alifariki wakati akijifungua, hivyo saidi hakumjua mama yake na hivyo kulelewa na bibi yake. Alipokuwa darasa la tatu babu yake alifariki, na maisha pale nyumbani yakawa magumu kweli. Saidi aliamua kwenda kwa baba yake aliyekuwa akiishi kijiji cha jirani, kule alikutana na mateso ya ajabu kutoka kwa mama zake wakambo na hivyo kulazimika kurudi kwa bibi yake mzaa mama.

Hata hivyo alijitahidi kuendelea na masomo, huku akifanya vibarua vya hapa na pale ili kumsaidia bibi yake ambaye alishakuwa mzee kujikimu. Alilazimika kuacha shule na kukimbilia mjini Lindi ili kujitafutia kipato. Alipofika mjini alikuwa akiishi stendi huku akifanya vibarua vya kubeba mizigo ya abiria na shughuli nyingine za kuosha magari ili mradi mkono uende kinywani.

Siku moja alipata wazo aje Jijini Dar, hiyo ni baada ya kusikia sifa nyingi kuhusiana na jiji hili, kwa kuwa alikuwa na vijisenti vyake alivyojiwekea alikata tiketi na kuja mjini. Alipofika awali alifikia pale ubungo stendi na kama ilivyokuwa Lindi alijishughulisha na shughuli zile zile za kubeba mizigo ya abiria na kuosha magari, baadae alihamishia shughuli zake maeneo ya Posta. Kati kati ya mji, na hapo ndipo nilipotokea kufahamiana naye.

Ni kijana mwenye heshima na muaminifu, siku moja kama kawaida yangu nilianza kumdadisi kwani kutokana na umri wake niliona alistahili kuwepo shuleni, na ndipo aliponisimulia historia ya maisha yake. Ukweli ni kwamba nilishikwa na huzuni sana na wakati ananisimulia kuna wakati nilijikuta nikitokwa na machozi kutokana na kuguswa na maisha magumu aliyoapitia.
Nikisema nisimulie historia yake yote, nitakuchosha wewe msomaji lakini kwa kifupi ni kwamba, Saidi alipitia maisha magumu sana, na yanayosikitisha na kuhuzunisha. Baada ya kusikiliza simulizi yake juu ya maisha yake, nilikata shauri nimsaidie. Nakumbuka kipindi cha nyuma kuna wakati nilikwenda kwa mama yangu mdogo anayeishi maeneo ya Kigogo, pale jirani na anapoishi nilimkuta kijana mmoja anafunga vifuko vya karatasi kwa kutumia unga wa ngano. Alikuwa akitengeneza vifuko vya saizi tofauti tofauti kulingana na matumizi na kisha kuviuza katika maduka ya dawa na wakati mwingine maduka ya kawaida na hata kwa wale wauza CD za muziki kwa ajili ya kufungia bidhaa zao.

Kutokana na udadisi wangu kama kawaida niliweza kuongea na yule kijana mtengeneza mifuko, na ikatokea tukazoeana sana, na hapo ndipo nikajifunza kutengeneza hiyo mifuko, ingawa sikujua kama najifunza ili iweje.

Baada ya kuongea na saidi nilipata wazo la kumfundisha ile kazi yakutengeneza mifuko ya karatasi, na baada ya kumweleza alifurahi sana. Kazi yenyewe haikuhitaji mtaji mkubwa, hivyo nilimpa kazi ya kupita katika maduka ya stationary na kuokota makaratasi na kisha aniletee. Na mimi nilipita pia kwenye maduka ya aina hiyo ambayo yalikuwa jirani na ofisi yangu na kuwaomba wawe wananihifadhia makaratasi wasiyoyatumia kwa kuwa nilikuwa na shida nayo, kwa kweli walinipa ushirikiano, kwani mpaka jioni nilikuwana lundo la makaratasi, naye Saidi kwa upande wake aliweza kukusanya makaratasi mengi sana, hatua ya kwanza ikawa imekamilika.

Tulipanga siku inayofuata ndio darasa letu lianze. Na siku iliyofuata nilinunua unga wangu wa ngano katika duka moja la jirani kule nyumbani kiasi cha kilo moja hivi, niliona hiyo ingetosha kuanzia, na nilipofika ofisini nilimkuta saidi ameshafika na kuanza shughuli zake za usafi kama kawaida, ila siku hiyo alikuwa ni mchangamfu sana. Baada ya kumaliza shughuli za usafi nilikaa naye na kuanza kumfundisha hatua kwa hatua mpaka akamudu kutengeneza mfuko, nilimuacha akiendelea kutengeneza mifuko yake na mimi nikawa naendelea na bishara zangu pale ofisini lakini nilikuwa naikagua kazi yake mara kwa mara na kuitoa makosa madogo madogo, na hatimaye alimudu.

Mpaka kufikia jioni alikuwa ametengeneza mifuko inayofikia mia sita ya saizi tofauti tofauti na huwezi kuamini ndugu msomaji, wateja alianza kuwapatia pale pale. Na huo ndio ukawa ndio mwanzo wa Saidi kuinuka.

Nililazimika kuibinafsisha ofisi yangu kwa kumuachia rafiki yangu aiendeshe na mimi kuhamia Arusha kwa muda katika kutekeleza majukumu ya kifamilia. Hivi karibuni nilitembelea ofisi yangu, nilipofika pale nilipata ujumbe kuwa Saidi ananitafuta sana na aliacha namba yake ili nikipita pale nimpigie, kwa kuwa sikuwa na simu rafiki yangu alimpigia na kumjulisha kuwa niko pale, Saidi aliniomba nimsubiri kwani alikuwa maeneo ya Kariakoo, niliamua kumsubiri kwa shauku ili kujua sababu ya kunitafuta.

Hata hivyo yule rafiki yang alinijulisha kwamba Saidi mambo yake sio mabaya kwani amenenepa na ana pesa sana simu hizi, kwanza simuamini nikajua ananitania. Haikupita muda Saidi alifika mahali pale, awali sikumjua kabisa mpaka alikiniita kwa jina langu huku akicheka kama kawaida yake. Alinieleza mengi kuhusu maisha yake, baada ya kuwa nimemuanzishia ile biashara. Aliniambia kuwa, ile biashara ilimnyookea na mpaka kufikia wakati ule alikuwa amemudu kufungua duka lake la kuuza CD maeneo ya Tandika na duka lingine la vitenge, khanga na vitambaa vya magauni hapo hapo Tandika pia ameoa na ana mtoto mmoja na amefanikiwa kununua shamba la eka mbili maneno ya Mkuranga, nilimdadisi kama ameanza ujenzi, akanijibu kuwa hajaanza bado lakini yuko kwenye harakati za kuanza, nilimuahidi kumnunulia mifuko kumi ya cement ili aweze kuanza hata msingi, alifurahi sana.

Akisimulia namna alivyomudu, anasema kuwa, kutokana na biashara hiyo ya mifuko kumpatia faida kubwa, rafiki yake mmoja alimshauri aweke fedha zake Saccos, ili akuze mtaji, alianza kuweka kila siku shilingi elfu kumi, na baada ya mwaka mmoja alikuwa amejikusanyia kiasi cha shilingi 3,650,000 kiasi ambacho hakuwahi kuota kuwa nacho.

Mpaka kufikia hapo alikuwa na uwezo wa kukopa shilingi milioni tisa na ushee, lakini hakuwa na dhamana kulingana na mkopo wa kiasi hicho, hivyo alianza na shilingi milioni moja ambapo alianza kwa kufungua biashara ya kuuza kanza na CD kule Tandika na baadae aliweza kuanzisha biashara nyingine ya kuuza vitenge na khanga hapo hapo Tandika. Hata hivyo Saidi anasema kwamba hajaacha biashara ya kuuza mifuko, anaendelea nayo kwani ndio iliyomuwezesha kufikia hapo alipo.

Nilizungumza na Saidi mambo mengi na kusema kweli alionekana kuwa na matarajio makubwa sana, hata mimi alinishangaza sana.

Mafanikio ya Saidi siwezi kujivunia kama sitamtaja yule kijana wa Kigogo ambaye ndiye aliyenifundisha kazi hiyo. Lakini kuna jambo moja najiuliza, hivi kuna watoto wangapi walioko mitaani leo wanaoshi katika mazingira magumu? Bila shaka ni wengi sana, Hivi si tunalo shirika letu la SIDO? Nazungumzia shirika la viwanda vidogovidogo. Hivi hawa wameshindwa kabisa kubuni miradi itakayowawezeka hawa vijana wa mitaani kujiajiri na kumudu maisha ya kujitegemea na hata kuchangia pato la Taifa badala ya kuiacha nguvu kazi hii ikipotea bure.
Tukumbuke kwamba hawa ndio kesho wana Graduate na kuwa vibaka na hata majambazi ambao huishia kupora na kudhulumu roho za watu. Watashindwaje kufanya hivyo ili hali tumewatelekeza watoto hawa. Jamii imewatelekeza, na hata serikali yao imewatelekeza, kwa nini tunakosa ubunifu.

Naomba tutafakari………….

Tuesday, October 13, 2009

HEBU TUTAFAKARI JUU YA KAULI HII!


Bado niko Dar, na huenda wiki ijayo nikarejea Arusha kuendelea na shughuli za kilimo.

Wakati tunaelekea kuadhimisha miaka kumi ya kifo cha muasisi wa Taifa hili Mwalimu Julius Kambarage Nyerere hapo kesho, leo nimeona niweke kipande hiki cha mazungumzo yake juu ya kuuvunja Muungano wakati alipokuwa akiongea na Klabu ya Waandishi wa habari Tanzania.

Zanzibar wanaweza wakajitenga hivi, kwa ujinga, kwa ulevi, lakini kwa ujinga, hasa wa viongozi wao. Wanaweza wakjitenga hivi na Watanganyika wakbaki wameduwaa tu. Lo! Wazanzibari hawa wamefanyaje? Wanatuacha wenzetu hawa: wanatuacha jamani! Wanakwenda zao wenzetu!” Wakawaacha Watanganyika wameduwaa hivi. Watanganyika walioachwa wameduwaa kwa kitendo cha wazanzibari kuwakimbia, watbaki wamoja, hawataparaganyika. Narudia, Wazanzibari wanaweza wakatoka wakajitenga wenyewe tu: “Wengine wan bendera sisi hatuna; wengine wan wimbo wa Taifa sisi hatuna. Kwa nini? “Basi halafu, watajitenga watawaacha Watanganyika wameduwaa. “Hivi kweli wenzetu wametuacha!”. Wakiwaacha Watanganyika katika hali hiyo. Watanganyika wanaowashangaa wazanzibari katika kuwaacha, Watanganyika hawa watakuwa Salama

Watanganyika wakiwakataa wazanzibari kwa tendo la dhambi ile ile ya “sisi Watanganyika”, “waoWazanzibari, wakautukuza “usisi Tanganyika” na, kwa ajili hiyo wakwafukuza wazanzibari , hawatabaki salama. Hapatakuwa na Tanganyika. Wakishakujitenga tu Watanganyika hawatabaki salama. Hapatakuwa na Tanganyika. Wakishajitenga tu, Wazanzibari wako kando hivi, mmewafukuza mnajidai wakubwa ninyi: “ hawa nani hawa, wao wan rais sisi hatuna raisi kwa nini? Watimuee” Mnawatimua. Mkampata Yelstin wenu hapa akawatimua. Hambaki. Kwani mtasemaje? Mtakuwa mmeshasema sababu ya kuwafanya ya “wale ni wao” na “ninyi ni ninyi” “wao” vipi wazanzibari; halafu mbaki ninyi?’.

Maana kama leo wapo kabila la wazanzibari, mmewabagua mtaanza vijumba vya wapemba, vipo vijumba vya wapemba humu. Basi watakimbia Wapemba. Baadhi yao wamo waliokimbia wakati ule wa zamani, Vijumba vya kwanza, mtasema ‘Wapemba, Wapemba’ mtamaliza za Wapemba halafu mtajikuta mliokuwa mnajiita ‘sisi Watanganyika’ mtakapoanza kuchoma nyumba za Wapemba. Mnazichoma moto zile, mnakuta eh! Sisi wote sio wamoja. Mbona za Wapemba tulizichoma moto, za Wachaga hatuchomi kwa nini? Maana Wachaga si wazawa bwana!Hapa kuna wazawa, sasamnachoma za Wapemba tu za Wachaga mnaacha..! Mtakuta hakuna watu wanitwa Watanganyika. Mtakuta mnajidanganya tu. Mnadhani kuan watu wanitwa Watanganyika. Hakuna! Kuna Wagogo, Wanyamwezi, Wasukuma,Wazanaki, Wakuria, Wamwera, eh! Wengi sanasiwezi kuwataja wote. Mtakuna hakuna hiki kitu kizima hivi kinaitwa ‘sisi Watanganyika’

Na madhali mmwfanya dhambi ya kusema ‘wao Wazanzibari’ si wenzetu, dhambi ile itawatafuna ninyi. Na mimi nasema, Mwenyezi Mungu anisamehe, mnastahili iwatafune. Hamwezi kutenda dhambi kubwa namna hiyo bila adhabuna adhabu zingine zimo mle mle ndani ya kitendo: hasisubiri. Kwa hiyo la kwanza nimesema tunao ufa wa muungano. Ufa wa kwanza kabisa’

Nimekiweka kipande hiki makusudi kutokana na hali jinsi ilivyokuwa tete kule Zanzibar, Serikali yetu kwa bahati mbaya imejitia hamnazo na inaonekana kupuuzia mgogoro ulioko pale kisiwani lakini kama kuna watabiri naomba watujuze, maana mie naona kabisa tunapoelekea si kuzuri hata kidogo, na litakalotokea pale kisiwani amini nawaambia huku Bara hatutakuwa salama hata kidogo, Tumeona wenzetu wameshaanza kulipuana kwa mabomu, tusijidanganye, vita hiyo itahamia huku, kwani moto mkubwa huanza na cheche ndogo sana.

Mimi naona kabisa kuna dalili za wazi za Rais Kikwete kufunika komba ili mwanaharamu apite, yaani amalize kipindi chake cha uongozi akajipumzishe zake huko Msoga, ili hilo balaa limuangukie mwingine. Hivi viongozi wetu walijisikiaje Rais wa Marekani Barack Obama alipotunukiwa Tunzo ya amani ya Nobel, si ni kutokana na juhudi za kuleta amani, kwanini sisi tunashindwa jambo hili? Tukumbuke kuwa kama ikitokea vita wenzetu hawa wanauwezo wa kukimbilia katika nchi zenye usalama na familia zao na kutuachia sisi balaa huku nyuma, kama tulivyoona huko Somalia, Sudan na kwingineko, wale wanaopiganisha vita katika nchi hizo familia zao ziko salama kabisa katika nchi za ugenini, zikiishi maisha ya kifahari na wengine wakiwa humu humu nchini. Wanaokufa kule ni masikini na familia zao ambao hawana masilahi kabisa na vita hivyo.

Naona sasa wakati umefika kwa wananchi wa kada mbalimbali, wasomi na viongozi wa dini kukutana kwa pamoja na kuiambia serikali, sasa imetosha, tunahitaji amani ya kudumu kisiwani pale, na kama wameshindwa basi waondoke waje viongozi makini na wenye uwezo wa kumaliza mgogoro ule.

Akilihutubia Bunge mara baada ya kupata ushindi wa kishindo, Raisi Kikwete alitoa ahadi kem kem ikiwemo hii ya kumaliza mgogoro wa kisiasa kule Zanzibar. Leo miaka mitano imepita hatuoni juhudi zozote makini za kumaliza mgogoro ule, zimebaki porojo tu,…. Hivi kwa nini lakini!!!!!????

Thursday, October 8, 2009

TUMESHINDWA KUANDIKA HISTORIA YETU WENYEWE?


Hivi karibuni niliomba msaada hapa katika kibarazani, nikiomba kuelekezwa mahali vinapopatikana vitabu mbalimbali vilivyokuwa vikitumika mashuleni miaka ya 1980.

Kutokana na ushirikiano mzuri wa wasomaji wa kibaraza hiki na wanablog wenzangu, nilielekezwa maeneo kadhaa ambapo niliambiwa nikajaribu huko, kwamba huenda nikavipata vitabu hivyo.

Ukweli ni kwamba sijavipata vitabu hivyo, lakini katika juhudi zangu za kutafuta vitabu hivyo nilipita katika taasisi ya kiswahili pale chuo kikuu mlimani {TUKI} na katika jengo la Quality Plaza lililoko Nyerere Road, pale kuna duka moja, nadhani linaitwa Mkuki na Nyota kama sikosei.
Nilikutana na vitabu vingi sana katika maeneo hayo, kwa mfano katika duka la vitabu lililopo pale Quality Plaza, nilikutana na vitabu vya elfu lela ulela, visa vya Sindbad baharia, na vingine vingi tu, hivyo hivyo pale Mlimani nilikutana na kazi nyingi za tafiti zinazozungumzia historia za makabila yetu, mila desturi na historia ya nchi yetu, bara la Afrika kwa ujumla na kadhalika na kadhalika.

Nilivutiwa na vitabu kadhaa ambavyo nilivinunua, lakini kilichonishangaza sana ni kukuta vitabu vingi vinavyoelezeza historia ya nchi yetu, makabila yetu na hata mila na desturi zetu vimetungwa na Wazungu.

Yaani nilishangaa sana kuona kwamba wazungu ndio wanaotufahamu zaidi kuliko sisi wenyewe. Pamoja na kuwa na wasomi wengi tena wa kutosha, lakini bado tumeshindwa kuandika historia ya nchi yetu, makabila yetu na mila na desturi zetu mpaka wazungu waje watuandikie?

Ina maana maisha ya mkazi wa pale Rufiji au Kipatimo kule Kilwa anayajua mzungiu kuliko Mtanzania mwenyewe? Au maisha ya mkazi wa kule Katerero Bukoba, Ruhuwiko Songea, Manyoni Singida, Mlima Kilimanjaro kule Moshi, Kyela kule Mbeya, au Kibaigwa kule Dodoma, wasomi wetu wameshindwa kufanya tafiti za makabila na mila na desturi za wakazi wa huko mpaka wazungu waje watusaidie kuandika?

Inashangaza kuona kuwa waliondika historia ya nchi yetu ni wazungu wengi sana ukilinganisha na sisi wenyewe.
Hata hivyo nilijaribu kumuuliza yule muuzaji wa vitabu na jibu lake lilikuwa ni rahisi sana, eti alidai kuwa wazungu wanazo fedha za kuendeshea tafiti mbalimbali ukilinganisha na sisi wenyewe. Ujinga gani huu..

Sina uhakika sana kama kilichoandikwa katika vitabu vyao kuwa ni sahihi kwani, habari zinazopendwa na hawa wenzetu ni zile zilizopotoshwa na kutiwa chumvi nyingi ili zivutie, hakuna habari inayohusu Bara la Afrika itakayoandikwa kwa usahihi kama ilivyo bila kutiwa chumvi. Lakini cha kushangaza huko mashuleni na vyuoni tunaambiwa tuvisome vitabu hivyo ili kuja kuvifanyia mitihani.
Hivi wasomi wetu wako wapi? Wanafanya nini? Na tafiti zao juu ya nchi yetu, makabila, mila na desturi zetu ziko wapi?

Friday, October 2, 2009

JE VITABU HIVI VINAPATIKANA WAPI?

Wasomaji wapendwa na wanablog wenzangu, baba yangu Mzee Mkundi anaomba msaada wa kutaka kujua vinapopatikana vitabu vya DARUBINI, yaani vile vitabu vilivyokuwa vimeandikwa UJINGA WA MUAFRIKA, anakumbuka baadhi ya hadithi zinazopatikana humo kama vile:

KAUTIPE NA UTUMBO WA KUKU

UREMBO WA NDONYA

KAWAMBWA NA KAPU LA KARANGA

CHAI YA DC

Pia anatafuta vitabu vya KISWAHILI vya darasa la nne, la tano na la sita, vya miaka ya 1980 anakumbuka hadithi zinazopatikana humo kama vile:

BROWN ASHIKA TAMA,

KAPULYA MDADISI

KIBANGA AMPIGA MKOLONI

MWEKA NADHIRI NA SHETANI

NUNDA MLA WATU

CHILUNDA APAMBANA NA CHUI

Mwenya kujua vinapopatikana vitabu hivi anijuze, baba anataka kuweka maktaba yake vizuri kwa ajili ya wajukuu zake………

Sunday, September 27, 2009

VUA NGUO NIKUPE UTAMU!!!!!!!!

Jamani hii sio falsafa ya kaka yangu Simon Mkodo wa Kitururu, kwa hiyo naomba msistushwe na kichwa cha habari hapo juu. Jana nikiwa nimejipumzisha nyumbani baada ya kutoka kanisani, niliamua kufungulia redio ili kusikiliza habari mbali mbali.

Nilipofunga redio nilikutana na kipindi cha watoto kilichokuwa kikirushwa hewani na Redio One, wakati huo ilikuwa ni wakati wa vitendawili, nilijikuta nikivutiwa na kile kipindi kwani kilinikumbusha enzi zile nikiwa mwanafunzi, nilitulia kwenye kiti na kusikiliza kipindi kile.

Mara mwanafunzi mmoja aliyetakiwa kutoa kitendawili chake akasema ‘Kitendawili’
Wenzake wakajibu ‘tega’, na ndipo akasema ‘Vua nguo nikupe utamu’
Yule mwendesha kipindi ambaye alikuwa ni miongoni mwa wale wanafunzi alimkata yule mwanafunzi kalma, na kumuonya yule mwanafunzi, kwa maneno yake mwenyewe alisema, ‘Jamani hivyo vitendawili haviruhusiwi, kwa nini huwaulizi wenzio, muwe mnawaelimisha wenzenu’

Akamchagua mwanfunzi mwingine na kipindi kikawa kinaendelea. Hata hivyo mimi bado nilibaki na swali, Je yule mwanafunzi alimaanisha nini katika kitendawili chake?
Kwa nini hakupewa nafasi ya japo kutoa jibu akiwa Off Air na kisha muongoza kipindi akatoa ufafanuzi? Je watoto walioko majumbani ambao walikuwa wakisikiliza kile kipindi watakuwa na picha gani juu ya kile kitendawili?

Unajua siku hizi kiswahili kimegeuzwa sana kiasi kwamba kila neno siku hizi limegeuka kuwa matusi.

Kwa kawaida watoto ni wadadisi sana na hicho kitendawili huenda watoto wengine waliokuwa kwenye kipindi na wale waliokuwa wakisikiliza majumbani mwao wamewauliza wazazi wao, na kwa bahati mbaya sana mwenye jibu la kitendawili kile alinyimwa haki ya kutoa jibu, Je wazazi watajibu nini?

Mpaka leo bado natafuta jibu la kitendawili kile, mwenye nalo anisaidie……

Saturday, September 19, 2009

HUYU NDIYE KAMALA LUTATINISIBWA

Kamala Lutatinisibwa,
Picha kwa hisani ya Blog ya Kijiwe cha Nyegerage.

Ni kijana wa kutoka kabila la Kihaya, na mzaliwa wa kule Bukoba mkoani Kagera. Alizaliwa miaka 28 iliyopita, tarehe 30 July.

Maisha yake ya udogoni hayakuwa mazuri sana kwani hakuwahi kufurahia upendo wa mama kwani inasemekana baba na mama walitengana mwaka mmoja tu baada ya yeye kuzaliwa akiwa ni mtoto wa mwisho hivyo akalelewa na bibi yake akishirikiana na shangazi zake kadhaa na binamu zake.

Binamu na baadhi ya ndugu alioishi nao kwa upendo na anaowakumbuka ni Jennifer Lukambuzi, Jovian na Elivida Binomutonzi, na dada yake Julieth na kaka yake Japhet ambao walikua pamoja wakicheza na kufurahia maisha ya utotoni. Alibatizwa tarehe 12/12/1982, rasmi bila ridhaa yake na kuwa mkirsto mfuasi wa ulutheri na kupewa jina la James.

Anakiri mwenyewe kuwa mpaka leo hajaweza kuelewa falsafa ya dhehebu hilo wala malengo yake na hivyo alibadili jina na kujiita Kamala Lutatinisibwa, na kubadili falsafa yake kutoka ile ya kimapokeo na kuhamia katika falsafa ya Spiritual yaani kujitambua.

Mwishoni mwa miaka ya 1980 kijana huyu akaanza shule ya awali maarufu kama vidudu au chekechea iliyokuwa ikimilikiwa na kanisa.

Anakiri kwamba hakuwa na mapenzi na shule hiyo ya awali kwani kuna wakati alikuwa akiishia njiani badala ya kwenda shuleni hivyo kuchapwa bakora kwa utoro. Alipokuwa darasa la tatu, alisomeshwa kipaimara na kuanza kula mkate kanisani ambao hujulikana kama kushiriki meza takatifu, ingawa hakuwahi kupenda kula mikate hiyo.

Kuna wakati alipenda mambo ya dini na kutaka kusomea uchungaji lakini baadaye alibadilisha uamuzi wake huo na kuamua kuishi kwa misingi ya falsaya ya Spiritual baada ya kuvutiwa na falsafa ya Budha na Osho.

Mnamo August 1, 1998 akiwa kidato cha pili kijana huyu alimpoteza baba yake mpendwa Omwami Ta Jasson Lutabwasibwa Kamala.

Baada ya kumaliza masomo yake ya Sekondari mnamo mwaka 2004 alihamia rasmi jijini Dar es salaam na kujiunga na vyuo mbalimbali ili kujifunza taaluma tofauti tofauti ambapo mpaka sasa ameweza kuwa mtaalamu wa Kompyuta, ingawa mwenyewe anakiri kuwa haipendi taaluma hiyo bali anapenda uandishi wa habari taaluma ambayo anaiendeleza kupitia kibaraza chake cha kublog akifundisha maarifa ya Utambuzi na stori za hapa na pale ili mradi maisha yanaendelea.

Ni mchangiaji mzuri katika blog za wengine ila msomaji asipokuwa makini anaweza kumuona kama mpotoshaj. Ni mkweli na hafichi kile anachokiamini bila kujali kama utakasirika au utafurahi.

Mara nyingi watu wasioelewa wanaweza kudhani labda ninapolumbana nae ninakuwa niko katika kiwango cha juu cha hasira, la hasha, ni katika kupendezesha mada husika na kuleta changamoto kuhusiana na mada hiyo.

Naomba nikiri kuwa Kamala ni mmoja kati ya wanablog ninaoheshimu sana misimamo yao, pamoja na kuonekana kuwa huwa natofautiana nae, lakini naomba nikiri kuwa sio kwamba nafanya hivyo kwa kuwa simpendi au sipendi misimamo yake. Ukweli ni kwamba napenda na ninaheshimu sana misimamo yake na maoni yake binafsi yawe ni mabaya au ni mazuri.

Hata hivyo naomba nikiri kuwa yapo mengi nimejifunza kutoka kwake na pia naamini kuwa

wasomaji wa blog hizi watakubaliana na mimi kuwa Kamala anao mchango mkubwa sana juu ya uwepo wa blog zetu kutokana na kutia hamasa kila achangiapo mada.

Naomba niishie hapa nisije nikatia chumvi sana na mchuzi ukachachuka.

Huyu ndiye Kamala Lutatinisibwa Omwami Ta Jasson Lutabwasibwa.

Bofya hapa kumsoma zaidi

Friday, September 18, 2009

SALAAM ZA MAKABILA YETU

Kijijini kwetu

Wasomaji wapendwa wa blog hii isiyoisha vituko, Kwa sasa niko jijini Dar es salaam nimerejea kimya kimya na leo nilikuwa najaribu kufanya utafiti wa lugha za makabila yetu hapa nchini. Kwa mujibu wa tafiti inasemekana kuna makabila zaidi ya 120 hapa nchini.Niliamua kuangalia zaidi salaam, hususan za asubuhi, Kutokana na utafiti wangu nimepitia makabila kadhaa na kukutana na maneno yanayotumiaka katika salaam za asubuhi ambayo yanafanana kidogo, hebu tuone maneno hayo ni yapi:


KINGONI: Uyimwiki = Habari za asubuhi

KIZIGUA: Kugona vihi = Habari za asubuhi

KINYAKYUSA: Ughonile = Habari za asubuhi

KIYAO: kwimukaga = Habari za asubuhi

KIPARE: Murevuka = Habari za asubuhi

KIUNGUJA: wambaje = Habari za asubuhi

KISAMBAA: Onga makeo = Habari za asubuhi

KIANGAZA: Mwalamtse = Habari za asubuhi

KINYAMWEZI: Mwangaluka = Habari za asubuhi

KICHAGA: Shimbonyi = Habari za asubuhi

KIMERU: Konumbware = Habari za asubuhi

KIMASAI: Sopai = Habari za asubuhi

KISUKUMA: Mwadila = Habari za asubuhi

KIHEHE: Kamwene = Habari za asubuhi

KIBENA: Kamwene = Habari za asubuhi

KIKINGA: Ulamwihe = Habari za asubuhi

KINYIRAMBA: Ulalaliani = Habari za asubuhi

KIHAYA: Wabonaki = Habari za asubuhi


Kwa leo naishia hapa mwenye nyongeza anaweza kuongeza ili tujifunze pamoja.
Tukutane wakati ujao

Monday, August 31, 2009

SERA YETU YA ELIMU HAPA NCHINI MBONA IMEPOGOKA HIVI!

Ni hivi karibuni niliandika juu ya habari ya vibaka wa pale Tandale kwa Mtogole na Manzese niliyoipa kichwa cha habari kisemacho “DAR ES SALAAM: TANDALE KWA MTOGOLE NA JARAMBA LA SASAMBUA SASAMBUA” . Niko Arusha kwa sasa na niko huku kutokana na shughuli za kifamilia.

Kwa hapa Arusha eneo ambalo unaweza kulifananisha na Tandale kwa Mtogole au Manzese ni Unga Limited, Ngarenaro, Kimandolu, na Sanawari eneo la Mbwa Chini.
Nimetolea mfano maeneo hayo kwa kuwa ndio maeneo ninayoyafahamu vizuri, lakini naamini mikoa yetu yote hapa nchini inayo maeneo fulani fulani ambayo ni korofi kwa uhalifu.

Lengo langu leo sio kuongelea uhalifu na hao vibaka, bali nataka kuzungumzia sera yetu ya elimu hapa nchini. Nilipokuwa Dar es salaam, kila nikipita katika vituo vya daladala nakuta kundi la vijana wanaopiga debe maarufu kama mateja, na hao hao ndio vibaka wanaopora watu hapo vituoni.

Katika utafiti niliofanya nimegundua kuwa kila mwaka idadi ya wapiga debe katika vituo vya daladala inazidi kuongezeka, hii ina maana gani, ni kwamba kila mwaka wanafunzi wanapomaliza darasa la saba lipo kundi kubwa la wanafunzi walioshindwa kuendelea na masomo ya sekondari hivyo huishia mitaani.

Je nini majaaliwa ya wanafunzi hawa? Je ni kwa nini nguvu kazi hii inaachwa ikipotea bure, hivi kupiga makelele ya kuita abiria na kujipatia shilingi mia au mia mbili ndio uzalishaji? Je kijana huyu anachangiaje pato la Taifa?

Ukweli ni kwamba sera yetu ya elimu hapa nchini imepogoka mno na haimuandai kijana kujiajiri ili kujiletea maendeleo na kuongeza pato la Taifa, na hili niliwahi kulijadili katika mada niliyoipa kichwa cha habari kisemacho “
HIVI MSOMI HASA NI NANI?

Nakumbuka wachangiaji wengi waliojitokeza kila mmoja alisema lakwake na mjadala ule uliisha bila kupata muafaka. Sina haja ya kurudia kile nilichokisema, bali leo ninayo maoni tofauti kidogo katika kulizungumzia hili.

Kuna siku nilikuwa naongea na mzee Mkundi, ambaye ni baba yangu, huyu mzee mie hupenda kumuita M-Conservative, kutokana na misimamo yake.
Siku hiyo nilimuuliza juu ya tofauti iliyopo kati ya mfumo wa elimu tulionao sasa na ule uliokuwa ukitumiwa na wakoloni, kabla ya kupata uhuru.

Baba alishangazwa na swali langu hilo, lakini hata hivyo alinijibu. Kwa mtazamo wake alisema kwamba pamoja na kwamba sera ya elimu ya mkoloni haikuwa na nia ya kutaka Muafrika ajitawale, lakini yalikuwepo maeneo ambayo sera hiyo ilifanikiwa sana.
Kwa mfano, wale wanafunzi ambao walikuwa hawana uwezo darasani lakini walionesha kuwa na vipaji, hao waliandaliwa kulingana na vipaji vyao huku wale wenye uwezo darasani waliendelea na masomo ya elimu ya juu.

Katika wale ambao walikuwa hawana uwezo darasani ndio waliokuja kuendelezwa katika fani mbalimbali kama vile utalamu wa kilimo, ufundi washi, useremala, makenika, ufundi mitambo, uhunzi na fani nyingine za michezo.
Yote hayo yalifanyika katika program maalum kwa hiyo hakuna mwanafunzi ambaye hakuwa na uwezo darasani ambaye alitelekezwa.

Tulipopata uhuru ndio kila kitu kilipoanza kuvurugwa taratibu, katika mfumo wa elimu.
Labda kulikuwa na nia nzuri ya kutaka kubadili ule mfumo wa elimu wa kikoloni uliokuwa umejikita zaidi katika kuwaandaa makarani wa kusimamia shughuli za wakoloni na kuweka mfumo wa kizalendo, lakini mabadilliko hayo hayakufanywa kwa umakini, kwani ilitakiwa tuache yale mabaya na kuchukua mazuri kama hayo ya kuwaandaa vijana katika nyanja mbali mbali kutokana na vipaji vyao. Lakini hata hivyo mzee Mkundi alibainisha kuwa, inawezekana ni kweli makosa yalifanyika kutokana na upeo finyu tuliokuwa nao wakati huo, lakini hivi mpaka leo bado tumeshindwa kutengeneza sera maridhawa ya kuwaandaa vijana wetu ili kujiajiri?

Hayo ndio majibu ya mzee Mkundi kwa mtazamo wake, hata hivyo niliamua kumshirikisha Profesa Matondo {bonyeza hapa kumsoma} katika mjadala huu, naye alikuwa na haya ya kusema:


Ukweli ni kwamba mfumo wa elimu yetu ni mbovu na kama ulivyosema haumwandai kijana kuweza kufanya lolote mbali na kuajiriwa baada ya shule. Tatizo ni kwamba hatuna ajira za kutosha na vijana wengi wanaishia kutelekezwa. (1) Kuna shule chache sana za sekondari na vijana wengi wanashindwa kukivuka hata kizingiti cha darasa la saba. Sijui hawa ni asilimia ngapi lakini nadhani ni wengi sana pengine karibia asilimia 75. Hakuna anayejua wala kujali hawa wanakwenda wapi baada ya kumaliza darasa la saba. Wengine wanajaribu umachinga, upiga debe na bila shaka kuwa vibaka na ujambazi. Halafu serikali inajaribu kupambana na tatizo hili kwa kuajiri mapolisi zaidi. Tazama maoni yangu niliyoweka katika blogu yako hapa:

(2) Hivi ulishawahi kujiuliza ni kwa nini watu wanaofeli mitihani ndiyo tunawatuma wakawe waalimu na waelimishaji wa taifa letu? Eti ukishindwa kwenda High School (division 3 na division 4) ndiyo unapelekwa ualimu. Unaweza kupata F zote na D mbili tu au tatu tu lakini bado taifa likakupa wajibu mzito wa kuandaa vijana wake. Huu nao ni muujiza. Literally kipofu anamwongoza kipofu mwenzake. Hapo unategemea nini? Kwa wenzetu huku kuanzia mwalimu wa chekechea ni lazima awe na digrii ya kwanza ya chuo kikuu, na awe "certified". Shule za msingi ndiko hasa tunapaswa kuweka misingi na kama mtoto anaanza na waalimu wetu hawa waliopata F zote na D mbili katika masomo yao ya kidato cha nne, unamtegemea mtoto huyo atakuwaje hata katika viwango vya juu vya elimu?

(3) Suala jingine ni lugha. Miaka saba ambayo ni ya muhimu sana kwa mtoto, mtoto anafundishwa kwa lugha nyingine na kimiujizaujiza tu anategemewa kwamba anapokwenda sekondari basi atakuwa amekifahamu Kiingereza sawasawa kiasi cha kukitumia ipasavyo katika masomo yake. Watoto wengi wanakwenda kidato cha kwanza hata hawajui kujitambulisha katika Kiingereza halafu wanategemewa eti waweze kuzifahamu Newton's Laws of Motion na maana zake pamoja na manufaa yake. Hapa ndipo elimu inakosa maana na kuwa zoezi la kukariri tu. Unakariri, unakopi kwenye mtihani, unapata A unasonga mbele ingawa hujui kitu. Na hili linaendelea mpaka pale Mlimani. Unapata digrii yako, unabahatika kuajiriwa, unaboronga na mambo yanaendelea. Japo leo kuna mfumuko mkubwa wa hizi "academy" zinazofundisha kwa Kiingereza tupu, tatizo ni kwamba nyingi zipo mjini wakati walengwa wake wako kijijini; na hata huko mjini ni wangapi wanaweza kumudu gharama zake?

Mzee Mkundi yuko sawa. Wakoloni hawakumtelekeza mtu kwani walihitaji sana watu wenye ujuzi fulani kuweza kuwasaidia katika shughuli zao nyingi. Walihitaji mafundi seremala, waachi, mafundi umeme, mafundi wa magari n.k. kwani wasingeendelea kuagiza watu hawa kutoka kwao Ulaya. Sijui tulishindwa nini kuendeleza sera nzuri kama hii. Siasa ya Kujitegemea mashuleni ilikuwa na lengo kama hili lakini bila vifaa na vitendea kazi, siasa hiyo iliishindwa. Badala yake ikawa wakati wa kujitegemea watoto mnakwenda kufagia na kumwagilia maua maji!Je wadau wengine mnasemaje juu ya hili?

Tujadili kwa pamoja