Saturday, October 31, 2009

LEO TUCHEMSHE BONGO KIDOGO.

Ndugu wasomaji wa blog hii takatifu, leo nataka nijaribu bongo za watu kama zinafanya kazi sawa sawa maana week end hii nimekosa hata cha kuandika kutokana na kuzidiwa na majukumu ya kifamilia.

Nimetenga zawadi za kuwatumia washindi watakaoshinda katika kujibu mafumbo haya yote. Zawadi ya kwanza itakuwa ni Picha yangu kubwa ya ukutani kwa wale walioko ughaibuni au mikoani, au kupata chakula cha usiku mimi na mshindi wa kwanza katika Hoteli maarufu jijini Dar kwa wale walioko hapa Dar. Zawadi ya pili ni kutumiwa zawadi ya kitabu cha The Secret kilichoko online na zawadi ya tatu ni kutumiwa picha ya familia ya mzee mkundi.

Haya tuanze kufumbua mafumbo yafuatayo:


Fumbo la Kwanza:

Mama Yasinta ana watoto watano, wa kwanza anaitwa Nana, wa pili anaitwa Nene, wa tatu anaitwa Nini, wa nne anaitwa Nono, Je wa tano ataitwa nani?

Fumbo la Pili:

Kuna mtu mmoja bubu alikwenda kununua miwani dukani, alipofika alimuonesha muuzaji ishara kama vile anavaa miwani yule muuzaji akamuelewa na kumpatia miwani akaondoka zake, mara akaja kipofu, Je unadhani ataonesha ishara gani ili apatiwe miwani?

Fumbo la Tatu:

Ninazo namba kumi zifuatazo: 1,3,5,7,9,11,13,15,17.19
Kama ukizijumlisha zote yaani 1+3+5+7+9+11+13+15+17+19 unapata 100.
Unachotakiwa kufanya ni kutafuta namba 5 miongoni mwa namba hizo ulizopewa hapo juu na ukizijumlisha unapata 50 yaani nusu ya 100.

Masharti:
Haitakiwa kurudia namba, kwa kuijumlisha mara mbili au kujumlisha namba pungufu ya namba tano zinazotakiwa. kwa mfano: 13+17+15+5 unapata 50. Sio sahihi kwa kuwa idadi ya namba zilizojumlishwa hazifiki 5.

Haya nasubiri majibu yenu…….

Friday, October 30, 2009

HUU NDIO WEMA!

Jirani kala nini?



Huu ndio wema! Unapotenda wema usitegemee fadhila. Unapokuwa na marafiki, ndugu, na jamaa wa karibu, watendee wema bila kudhamiria kupata fadhila kutoka kwao. Ninapoongelea wema na kutoa ninamkumbuka mama Theresa wa Calcutta ambaye kwa umri na maisha yake angelikuwa Bilionea lakini kwa kujitolea kwake alikufa masikini, lakini akiwa ni tajiri wa nafsi. Nina maana alikufa akiwa na ridhiko, kwani kazi aliyotaka kuifanya aliifanya tena kwa kufaulu. Je wewe hufurahii kuwa kama yeye?

Kumbuka amri kuu isemayo “mpende jirani yako kama unavyojipenda” Je unapokula na kusaza huwa unajiuliza kuwa jirani kala nini?

Tafakari………

Wednesday, October 21, 2009

JAMANI HUU NI UTABIRI, UNAJIMU AU DHIHAKA?

Jamani mimi sio mpenzi au mshabiki wa mambo ya Nyota, kwangu mimi nachukulia kama huo ni ushirikina. Jana kuna mdau kanitumia huu utabiri au sijui niite unajimu, akinituhumu kuwa, kwa kuwa nimezaliwa mwezi wa Mei basi ninazo tabia hizi. Ukweli ni kwamba sina uhakika na hicho alichoandika, na siamini kabisa kama ninazo tabia hizo, ila waswahili wanasema Nyani haoni kundule. Kwa hiyo naomba wadau munisaidie kama unajimu huu unanihusu………….maana naona hii ni kaaaaaaaazi kweli kweli.

TABIA ZA WATU WALIOZALIWA MWEZI MEI…….HATA WEWE KOERO UMO

Mtu yeyote ambaye amezaliwa mwezi wa Mei mwaka wowote, anaweza kuwa na alama ya nyota ya Ng’ombe {Tauras} au Mapacha {Gemini}. Hapa sitazungumzia nyota moja moja, bali nitazungumzia mwezi ambao amezaliwa mtu. Kwa hiyo nitazungumzia waliozaliwa mwezi wa Mei ambapo wewe Koero ni mmoja wapo.

Watu waliozaliwa mwezi wa Mei ni wagumu, hawaambiliki wanapotaka kufanya jambo, wanapopania. Tunaweza kusema ni watu ving’ang’anizi. Lakini kwa bahati mbaya sana, kama wamempenda mtu, hakuna watu wanoporomoka kirahisi kama wao. Yaani kama wamempenda mtu wanashikwa kirahisi kuliko mtu mwingine yeyote.

Ni watu ambao wanaweza kuvumilia shida na suluba za maisha katika kiwango cha ajabu. Ni watu ambao wanamudu kuhimili misukosuko kimwili na kiakili, yaani hawachanganyikiwi kirahisikwenye misukosuko, hasa kama nia yao ya kung’ang’ania bado ipo.

Ni watu wenye uwezo mkubwa wa kumbukumbu. Kama ni uwezo wa kukariri masomo, basi ndiyo wenyewe. Lakini kwa bahati mbaya, wanapenda sana kujumuika na kujimwaga. Kwa hiyo wengi huwa hawafaidi matokeo ya vipaji vyao na wakati mwingine hata hivyo vipaji havionekani kwa sababu vinafungwa na kupenda kwao starehe.

Ni watu pia wanaofaa kwenye kazi kama zile za uhudumu katika ndege au hata mighahawani. Wana sifa ya kujua ladha ya chakula na wanamudu kutengeneza chakula kizuri sana nyumbani hata kama vifaa na fedha ni haba sana.

Ni watu ambao pia wana uwezo wa kuongoza kwenye mashirika au maeneo ya shughuli. Watu waliozaliwa Mei, inawezekana kwa nje wakaonekana kuwa na uwezo sana kuliko walionao kweli.

Hii ni kwa sababu wanajipenda sana, iwe kuvaa au hata kuwa na vitu vingine vya thamani vya nje. Mtu aliyezaliwa Mei anaweza kuwa na gari kubwa, lakini akiba ya shilingi elfu moja mfukoni hata nyumbani hana. Anaweza kuwa anavaa suti kila siku wakati hata godoro la kulalia hana.

Ni watu ambao wakipenda mtu wanakuwa kama vichaa, kwani watampa kila kitu. Kama nilivyosema, wanashikwa kabisa na kuwa kama mazuzu. Lakini wakimchukia mtu watapambana naye hadi waone kinaeleweka. Uzuri wao ni kwamba, wanapenda kukabiliana na mtu ana kwa ana, hawapendi mambo ya chini chini au njama. Wanapenda maisha ya wazi tu, hata kama ni ugomvi au uadui.

Watu waliozaliwa mwezi Mei iwe wanaume au wanawake hawatakiwi kuoa au kuolewa mapema. Hawatakiwi kufanya hivyo kwa sababu mara nyingi, kama sio zote ndoa zao za kwanza huwa wanakuwa wamekosea kuchagua. Labda ni kwa sababu wakishapenda wankuwa ni vipofu halisi. Ni watu ambao wanatakiwa wakitaka kutafakari na kuamua jambo wake wenyewe na kutafakari kimya. Hii ni kwa sababu wakiwa katika watu wengi, wantokea kuwaamini watu hao wengi na kuchukulia mawazo ya hao wengi kama yao. Ni watu ambao huchanganywa na kudanganywa kirahisi. Ni watu ambao wanapoingia kwenye hisia au upendo, hawana tena uwezo wa kufikiri vizuri.

Ni watu wenye wivu sana na mara nyingi wivu wao wa kimapenzi huwafanya kuleta vurugu au kusababisha machafuko ya wazi ya kiuhusiano. Lakini siku zote, baada ya vurugu hizo huhisi kushitakiwa na dhamira. Hujutia tabia zao za wivu lakini hawana uwezo wa kuzidhibiti kama wanavyoamini wao.

Kwenye uhusiano ukiacha wivu, ni waaminifu na wanyeyekevu kwa wapenzi wao. Wanafaa sana kuwa maafisa serikalini. Wauguzi na hata kufanya kazi za bustanini. Ni watu wazuti katika mashairi, muziki na sanaa kwa ujumla.

Kiafya ni watu wanaougua kirahisi maradhi yenye kuathiri koo, pua na mapafu pia. Kwa hiyo wantakiwa kuwa makini sana na mazingira ambayo yanaweza kudhuru koo, pua au mapafu yao. Vitu kama sigara, haviwafai watu waliozaliwa Mei

Sunday, October 18, 2009

KISA CHA SAIDI WA MBEKENYELA......!



Nakumbuka alikuwa na kawaida ya kuja pale ofisini kwangu, maeneo ya mjini na kunisaidia shughuli za usafi na kumlipa ujira kidogo. Kama nilikuwa nataka kununua kitu nilikuwa namtuma. Ni kijana mchapa kazi kweli na mcheshi kupindukia.

Akiwa ni mzaliwa wa Lindi katika kijiji cha Mbekenyela, kijana huyu ambaye ningependa kumwita Saidi *{Sio jina lake halisi}hakubahatika kumuona mama yake. Anasimulia kuwa mama yake aliolewa akiwa na umri mdogo sana miaka 15 na mzee mmoja aliemzidi kwa miaka 50, aliolewa katika zile ndoa maarufu za Korosho. Ndoa ambazo hufanyika sana mara baada ya msimu wa korosho.

Anasema kuwa kule kwao Lindi, kila baada ya msimu wa korosho wazee wengi ambao wana mashamba makubwa ya Korosho hukimbilia kuoa vibinti vidogo kwa kuwa wanazo fedha za mauzo ya Korosho, kuna wakati watoto wa kike hulazimika kuachishwa shule ili kuozeshwa kwa vibabu hivyo visivyoisha tamaa, na mara nyingi ndoa hizo huwa hazidumu kwani fedha zikiisha na ndoa huingia katika misukosuko na hatimaye kuvunjika kutokana na vizee hivyo kushindwa kumudu gharama za malezi ya wake wawili au hata watatu.

Hali hiyo imesababisha familia nyingi mkoani humo kuwa na vijukuu baada ya mama zao kuachika na kurudishwa nyumbani, hivyo kufanya hali ya maisha katika familia nyingi kuwa ngumu.

Mama yake Saidi alifariki wakati akijifungua, hivyo saidi hakumjua mama yake na hivyo kulelewa na bibi yake. Alipokuwa darasa la tatu babu yake alifariki, na maisha pale nyumbani yakawa magumu kweli. Saidi aliamua kwenda kwa baba yake aliyekuwa akiishi kijiji cha jirani, kule alikutana na mateso ya ajabu kutoka kwa mama zake wakambo na hivyo kulazimika kurudi kwa bibi yake mzaa mama.

Hata hivyo alijitahidi kuendelea na masomo, huku akifanya vibarua vya hapa na pale ili kumsaidia bibi yake ambaye alishakuwa mzee kujikimu. Alilazimika kuacha shule na kukimbilia mjini Lindi ili kujitafutia kipato. Alipofika mjini alikuwa akiishi stendi huku akifanya vibarua vya kubeba mizigo ya abiria na shughuli nyingine za kuosha magari ili mradi mkono uende kinywani.

Siku moja alipata wazo aje Jijini Dar, hiyo ni baada ya kusikia sifa nyingi kuhusiana na jiji hili, kwa kuwa alikuwa na vijisenti vyake alivyojiwekea alikata tiketi na kuja mjini. Alipofika awali alifikia pale ubungo stendi na kama ilivyokuwa Lindi alijishughulisha na shughuli zile zile za kubeba mizigo ya abiria na kuosha magari, baadae alihamishia shughuli zake maeneo ya Posta. Kati kati ya mji, na hapo ndipo nilipotokea kufahamiana naye.

Ni kijana mwenye heshima na muaminifu, siku moja kama kawaida yangu nilianza kumdadisi kwani kutokana na umri wake niliona alistahili kuwepo shuleni, na ndipo aliponisimulia historia ya maisha yake. Ukweli ni kwamba nilishikwa na huzuni sana na wakati ananisimulia kuna wakati nilijikuta nikitokwa na machozi kutokana na kuguswa na maisha magumu aliyoapitia.
Nikisema nisimulie historia yake yote, nitakuchosha wewe msomaji lakini kwa kifupi ni kwamba, Saidi alipitia maisha magumu sana, na yanayosikitisha na kuhuzunisha. Baada ya kusikiliza simulizi yake juu ya maisha yake, nilikata shauri nimsaidie. Nakumbuka kipindi cha nyuma kuna wakati nilikwenda kwa mama yangu mdogo anayeishi maeneo ya Kigogo, pale jirani na anapoishi nilimkuta kijana mmoja anafunga vifuko vya karatasi kwa kutumia unga wa ngano. Alikuwa akitengeneza vifuko vya saizi tofauti tofauti kulingana na matumizi na kisha kuviuza katika maduka ya dawa na wakati mwingine maduka ya kawaida na hata kwa wale wauza CD za muziki kwa ajili ya kufungia bidhaa zao.

Kutokana na udadisi wangu kama kawaida niliweza kuongea na yule kijana mtengeneza mifuko, na ikatokea tukazoeana sana, na hapo ndipo nikajifunza kutengeneza hiyo mifuko, ingawa sikujua kama najifunza ili iweje.

Baada ya kuongea na saidi nilipata wazo la kumfundisha ile kazi yakutengeneza mifuko ya karatasi, na baada ya kumweleza alifurahi sana. Kazi yenyewe haikuhitaji mtaji mkubwa, hivyo nilimpa kazi ya kupita katika maduka ya stationary na kuokota makaratasi na kisha aniletee. Na mimi nilipita pia kwenye maduka ya aina hiyo ambayo yalikuwa jirani na ofisi yangu na kuwaomba wawe wananihifadhia makaratasi wasiyoyatumia kwa kuwa nilikuwa na shida nayo, kwa kweli walinipa ushirikiano, kwani mpaka jioni nilikuwana lundo la makaratasi, naye Saidi kwa upande wake aliweza kukusanya makaratasi mengi sana, hatua ya kwanza ikawa imekamilika.

Tulipanga siku inayofuata ndio darasa letu lianze. Na siku iliyofuata nilinunua unga wangu wa ngano katika duka moja la jirani kule nyumbani kiasi cha kilo moja hivi, niliona hiyo ingetosha kuanzia, na nilipofika ofisini nilimkuta saidi ameshafika na kuanza shughuli zake za usafi kama kawaida, ila siku hiyo alikuwa ni mchangamfu sana. Baada ya kumaliza shughuli za usafi nilikaa naye na kuanza kumfundisha hatua kwa hatua mpaka akamudu kutengeneza mfuko, nilimuacha akiendelea kutengeneza mifuko yake na mimi nikawa naendelea na bishara zangu pale ofisini lakini nilikuwa naikagua kazi yake mara kwa mara na kuitoa makosa madogo madogo, na hatimaye alimudu.

Mpaka kufikia jioni alikuwa ametengeneza mifuko inayofikia mia sita ya saizi tofauti tofauti na huwezi kuamini ndugu msomaji, wateja alianza kuwapatia pale pale. Na huo ndio ukawa ndio mwanzo wa Saidi kuinuka.

Nililazimika kuibinafsisha ofisi yangu kwa kumuachia rafiki yangu aiendeshe na mimi kuhamia Arusha kwa muda katika kutekeleza majukumu ya kifamilia. Hivi karibuni nilitembelea ofisi yangu, nilipofika pale nilipata ujumbe kuwa Saidi ananitafuta sana na aliacha namba yake ili nikipita pale nimpigie, kwa kuwa sikuwa na simu rafiki yangu alimpigia na kumjulisha kuwa niko pale, Saidi aliniomba nimsubiri kwani alikuwa maeneo ya Kariakoo, niliamua kumsubiri kwa shauku ili kujua sababu ya kunitafuta.

Hata hivyo yule rafiki yang alinijulisha kwamba Saidi mambo yake sio mabaya kwani amenenepa na ana pesa sana simu hizi, kwanza simuamini nikajua ananitania. Haikupita muda Saidi alifika mahali pale, awali sikumjua kabisa mpaka alikiniita kwa jina langu huku akicheka kama kawaida yake. Alinieleza mengi kuhusu maisha yake, baada ya kuwa nimemuanzishia ile biashara. Aliniambia kuwa, ile biashara ilimnyookea na mpaka kufikia wakati ule alikuwa amemudu kufungua duka lake la kuuza CD maeneo ya Tandika na duka lingine la vitenge, khanga na vitambaa vya magauni hapo hapo Tandika pia ameoa na ana mtoto mmoja na amefanikiwa kununua shamba la eka mbili maneno ya Mkuranga, nilimdadisi kama ameanza ujenzi, akanijibu kuwa hajaanza bado lakini yuko kwenye harakati za kuanza, nilimuahidi kumnunulia mifuko kumi ya cement ili aweze kuanza hata msingi, alifurahi sana.

Akisimulia namna alivyomudu, anasema kuwa, kutokana na biashara hiyo ya mifuko kumpatia faida kubwa, rafiki yake mmoja alimshauri aweke fedha zake Saccos, ili akuze mtaji, alianza kuweka kila siku shilingi elfu kumi, na baada ya mwaka mmoja alikuwa amejikusanyia kiasi cha shilingi 3,650,000 kiasi ambacho hakuwahi kuota kuwa nacho.

Mpaka kufikia hapo alikuwa na uwezo wa kukopa shilingi milioni tisa na ushee, lakini hakuwa na dhamana kulingana na mkopo wa kiasi hicho, hivyo alianza na shilingi milioni moja ambapo alianza kwa kufungua biashara ya kuuza kanza na CD kule Tandika na baadae aliweza kuanzisha biashara nyingine ya kuuza vitenge na khanga hapo hapo Tandika. Hata hivyo Saidi anasema kwamba hajaacha biashara ya kuuza mifuko, anaendelea nayo kwani ndio iliyomuwezesha kufikia hapo alipo.

Nilizungumza na Saidi mambo mengi na kusema kweli alionekana kuwa na matarajio makubwa sana, hata mimi alinishangaza sana.

Mafanikio ya Saidi siwezi kujivunia kama sitamtaja yule kijana wa Kigogo ambaye ndiye aliyenifundisha kazi hiyo. Lakini kuna jambo moja najiuliza, hivi kuna watoto wangapi walioko mitaani leo wanaoshi katika mazingira magumu? Bila shaka ni wengi sana, Hivi si tunalo shirika letu la SIDO? Nazungumzia shirika la viwanda vidogovidogo. Hivi hawa wameshindwa kabisa kubuni miradi itakayowawezeka hawa vijana wa mitaani kujiajiri na kumudu maisha ya kujitegemea na hata kuchangia pato la Taifa badala ya kuiacha nguvu kazi hii ikipotea bure.
Tukumbuke kwamba hawa ndio kesho wana Graduate na kuwa vibaka na hata majambazi ambao huishia kupora na kudhulumu roho za watu. Watashindwaje kufanya hivyo ili hali tumewatelekeza watoto hawa. Jamii imewatelekeza, na hata serikali yao imewatelekeza, kwa nini tunakosa ubunifu.

Naomba tutafakari………….

Tuesday, October 13, 2009

HEBU TUTAFAKARI JUU YA KAULI HII!


Bado niko Dar, na huenda wiki ijayo nikarejea Arusha kuendelea na shughuli za kilimo.

Wakati tunaelekea kuadhimisha miaka kumi ya kifo cha muasisi wa Taifa hili Mwalimu Julius Kambarage Nyerere hapo kesho, leo nimeona niweke kipande hiki cha mazungumzo yake juu ya kuuvunja Muungano wakati alipokuwa akiongea na Klabu ya Waandishi wa habari Tanzania.

Zanzibar wanaweza wakajitenga hivi, kwa ujinga, kwa ulevi, lakini kwa ujinga, hasa wa viongozi wao. Wanaweza wakjitenga hivi na Watanganyika wakbaki wameduwaa tu. Lo! Wazanzibari hawa wamefanyaje? Wanatuacha wenzetu hawa: wanatuacha jamani! Wanakwenda zao wenzetu!” Wakawaacha Watanganyika wameduwaa hivi. Watanganyika walioachwa wameduwaa kwa kitendo cha wazanzibari kuwakimbia, watbaki wamoja, hawataparaganyika. Narudia, Wazanzibari wanaweza wakatoka wakajitenga wenyewe tu: “Wengine wan bendera sisi hatuna; wengine wan wimbo wa Taifa sisi hatuna. Kwa nini? “Basi halafu, watajitenga watawaacha Watanganyika wameduwaa. “Hivi kweli wenzetu wametuacha!”. Wakiwaacha Watanganyika katika hali hiyo. Watanganyika wanaowashangaa wazanzibari katika kuwaacha, Watanganyika hawa watakuwa Salama

Watanganyika wakiwakataa wazanzibari kwa tendo la dhambi ile ile ya “sisi Watanganyika”, “waoWazanzibari, wakautukuza “usisi Tanganyika” na, kwa ajili hiyo wakwafukuza wazanzibari , hawatabaki salama. Hapatakuwa na Tanganyika. Wakishakujitenga tu Watanganyika hawatabaki salama. Hapatakuwa na Tanganyika. Wakishajitenga tu, Wazanzibari wako kando hivi, mmewafukuza mnajidai wakubwa ninyi: “ hawa nani hawa, wao wan rais sisi hatuna raisi kwa nini? Watimuee” Mnawatimua. Mkampata Yelstin wenu hapa akawatimua. Hambaki. Kwani mtasemaje? Mtakuwa mmeshasema sababu ya kuwafanya ya “wale ni wao” na “ninyi ni ninyi” “wao” vipi wazanzibari; halafu mbaki ninyi?’.

Maana kama leo wapo kabila la wazanzibari, mmewabagua mtaanza vijumba vya wapemba, vipo vijumba vya wapemba humu. Basi watakimbia Wapemba. Baadhi yao wamo waliokimbia wakati ule wa zamani, Vijumba vya kwanza, mtasema ‘Wapemba, Wapemba’ mtamaliza za Wapemba halafu mtajikuta mliokuwa mnajiita ‘sisi Watanganyika’ mtakapoanza kuchoma nyumba za Wapemba. Mnazichoma moto zile, mnakuta eh! Sisi wote sio wamoja. Mbona za Wapemba tulizichoma moto, za Wachaga hatuchomi kwa nini? Maana Wachaga si wazawa bwana!Hapa kuna wazawa, sasamnachoma za Wapemba tu za Wachaga mnaacha..! Mtakuta hakuna watu wanitwa Watanganyika. Mtakuta mnajidanganya tu. Mnadhani kuan watu wanitwa Watanganyika. Hakuna! Kuna Wagogo, Wanyamwezi, Wasukuma,Wazanaki, Wakuria, Wamwera, eh! Wengi sanasiwezi kuwataja wote. Mtakuna hakuna hiki kitu kizima hivi kinaitwa ‘sisi Watanganyika’

Na madhali mmwfanya dhambi ya kusema ‘wao Wazanzibari’ si wenzetu, dhambi ile itawatafuna ninyi. Na mimi nasema, Mwenyezi Mungu anisamehe, mnastahili iwatafune. Hamwezi kutenda dhambi kubwa namna hiyo bila adhabuna adhabu zingine zimo mle mle ndani ya kitendo: hasisubiri. Kwa hiyo la kwanza nimesema tunao ufa wa muungano. Ufa wa kwanza kabisa’

Nimekiweka kipande hiki makusudi kutokana na hali jinsi ilivyokuwa tete kule Zanzibar, Serikali yetu kwa bahati mbaya imejitia hamnazo na inaonekana kupuuzia mgogoro ulioko pale kisiwani lakini kama kuna watabiri naomba watujuze, maana mie naona kabisa tunapoelekea si kuzuri hata kidogo, na litakalotokea pale kisiwani amini nawaambia huku Bara hatutakuwa salama hata kidogo, Tumeona wenzetu wameshaanza kulipuana kwa mabomu, tusijidanganye, vita hiyo itahamia huku, kwani moto mkubwa huanza na cheche ndogo sana.

Mimi naona kabisa kuna dalili za wazi za Rais Kikwete kufunika komba ili mwanaharamu apite, yaani amalize kipindi chake cha uongozi akajipumzishe zake huko Msoga, ili hilo balaa limuangukie mwingine. Hivi viongozi wetu walijisikiaje Rais wa Marekani Barack Obama alipotunukiwa Tunzo ya amani ya Nobel, si ni kutokana na juhudi za kuleta amani, kwanini sisi tunashindwa jambo hili? Tukumbuke kuwa kama ikitokea vita wenzetu hawa wanauwezo wa kukimbilia katika nchi zenye usalama na familia zao na kutuachia sisi balaa huku nyuma, kama tulivyoona huko Somalia, Sudan na kwingineko, wale wanaopiganisha vita katika nchi hizo familia zao ziko salama kabisa katika nchi za ugenini, zikiishi maisha ya kifahari na wengine wakiwa humu humu nchini. Wanaokufa kule ni masikini na familia zao ambao hawana masilahi kabisa na vita hivyo.

Naona sasa wakati umefika kwa wananchi wa kada mbalimbali, wasomi na viongozi wa dini kukutana kwa pamoja na kuiambia serikali, sasa imetosha, tunahitaji amani ya kudumu kisiwani pale, na kama wameshindwa basi waondoke waje viongozi makini na wenye uwezo wa kumaliza mgogoro ule.

Akilihutubia Bunge mara baada ya kupata ushindi wa kishindo, Raisi Kikwete alitoa ahadi kem kem ikiwemo hii ya kumaliza mgogoro wa kisiasa kule Zanzibar. Leo miaka mitano imepita hatuoni juhudi zozote makini za kumaliza mgogoro ule, zimebaki porojo tu,…. Hivi kwa nini lakini!!!!!????

Thursday, October 8, 2009

TUMESHINDWA KUANDIKA HISTORIA YETU WENYEWE?


Hivi karibuni niliomba msaada hapa katika kibarazani, nikiomba kuelekezwa mahali vinapopatikana vitabu mbalimbali vilivyokuwa vikitumika mashuleni miaka ya 1980.

Kutokana na ushirikiano mzuri wa wasomaji wa kibaraza hiki na wanablog wenzangu, nilielekezwa maeneo kadhaa ambapo niliambiwa nikajaribu huko, kwamba huenda nikavipata vitabu hivyo.

Ukweli ni kwamba sijavipata vitabu hivyo, lakini katika juhudi zangu za kutafuta vitabu hivyo nilipita katika taasisi ya kiswahili pale chuo kikuu mlimani {TUKI} na katika jengo la Quality Plaza lililoko Nyerere Road, pale kuna duka moja, nadhani linaitwa Mkuki na Nyota kama sikosei.
Nilikutana na vitabu vingi sana katika maeneo hayo, kwa mfano katika duka la vitabu lililopo pale Quality Plaza, nilikutana na vitabu vya elfu lela ulela, visa vya Sindbad baharia, na vingine vingi tu, hivyo hivyo pale Mlimani nilikutana na kazi nyingi za tafiti zinazozungumzia historia za makabila yetu, mila desturi na historia ya nchi yetu, bara la Afrika kwa ujumla na kadhalika na kadhalika.

Nilivutiwa na vitabu kadhaa ambavyo nilivinunua, lakini kilichonishangaza sana ni kukuta vitabu vingi vinavyoelezeza historia ya nchi yetu, makabila yetu na hata mila na desturi zetu vimetungwa na Wazungu.

Yaani nilishangaa sana kuona kwamba wazungu ndio wanaotufahamu zaidi kuliko sisi wenyewe. Pamoja na kuwa na wasomi wengi tena wa kutosha, lakini bado tumeshindwa kuandika historia ya nchi yetu, makabila yetu na mila na desturi zetu mpaka wazungu waje watuandikie?

Ina maana maisha ya mkazi wa pale Rufiji au Kipatimo kule Kilwa anayajua mzungiu kuliko Mtanzania mwenyewe? Au maisha ya mkazi wa kule Katerero Bukoba, Ruhuwiko Songea, Manyoni Singida, Mlima Kilimanjaro kule Moshi, Kyela kule Mbeya, au Kibaigwa kule Dodoma, wasomi wetu wameshindwa kufanya tafiti za makabila na mila na desturi za wakazi wa huko mpaka wazungu waje watusaidie kuandika?

Inashangaza kuona kuwa waliondika historia ya nchi yetu ni wazungu wengi sana ukilinganisha na sisi wenyewe.
Hata hivyo nilijaribu kumuuliza yule muuzaji wa vitabu na jibu lake lilikuwa ni rahisi sana, eti alidai kuwa wazungu wanazo fedha za kuendeshea tafiti mbalimbali ukilinganisha na sisi wenyewe. Ujinga gani huu..

Sina uhakika sana kama kilichoandikwa katika vitabu vyao kuwa ni sahihi kwani, habari zinazopendwa na hawa wenzetu ni zile zilizopotoshwa na kutiwa chumvi nyingi ili zivutie, hakuna habari inayohusu Bara la Afrika itakayoandikwa kwa usahihi kama ilivyo bila kutiwa chumvi. Lakini cha kushangaza huko mashuleni na vyuoni tunaambiwa tuvisome vitabu hivyo ili kuja kuvifanyia mitihani.
Hivi wasomi wetu wako wapi? Wanafanya nini? Na tafiti zao juu ya nchi yetu, makabila, mila na desturi zetu ziko wapi?

Friday, October 2, 2009

JE VITABU HIVI VINAPATIKANA WAPI?

Wasomaji wapendwa na wanablog wenzangu, baba yangu Mzee Mkundi anaomba msaada wa kutaka kujua vinapopatikana vitabu vya DARUBINI, yaani vile vitabu vilivyokuwa vimeandikwa UJINGA WA MUAFRIKA, anakumbuka baadhi ya hadithi zinazopatikana humo kama vile:

KAUTIPE NA UTUMBO WA KUKU

UREMBO WA NDONYA

KAWAMBWA NA KAPU LA KARANGA

CHAI YA DC

Pia anatafuta vitabu vya KISWAHILI vya darasa la nne, la tano na la sita, vya miaka ya 1980 anakumbuka hadithi zinazopatikana humo kama vile:

BROWN ASHIKA TAMA,

KAPULYA MDADISI

KIBANGA AMPIGA MKOLONI

MWEKA NADHIRI NA SHETANI

NUNDA MLA WATU

CHILUNDA APAMBANA NA CHUI

Mwenya kujua vinapopatikana vitabu hivi anijuze, baba anataka kuweka maktaba yake vizuri kwa ajili ya wajukuu zake………