Wednesday, December 29, 2010

ULIKUWA NI MJADALA MZITO ULIOZUA MASWALI MAZITO MWAKA 2010 HAPA VUKANI!

March 24, 2010

DADA SUBI, KUANDIKA MADHILA YA WANAWAKE, LABDA UWE NA MOYO KAMA WA MWENDAWAZIMU.


Hawa ndio waathirika wakubwa

Bubu hupata kusema, mambo yanapomzidi,

Na kiwete husimama, akakimbia baidi,

Ogopa moto wa chuma, sione kiko baridi,

Kama waume si wema, wake wangalikuwaje?


Hata kuku huchachama, unapomtia kedi,

Na jorowe takuuma, iwapo hapana budi,

Nyundo ni nyundo kwa chuma, japo kisiwe baridi,

Kama waume si wema, wake wangalikuwaje?


Dada Subi nimeanza na shairi hilo lililoandikwa na Sheikh Amri Abedi katika kukuandikia waraka huu mahsusi kwako. Nimekuwa nikiandika kila jambo linalogusa maisha ya jamii iliyonizunguka yakiwemo yale ya kufurahisha, ya kuhuzunisha na ujinga kidogo.


Yote hiyo ni katika kujaribu kumgusa kila mtu kuanzia mwenye upeo mkubwa na yule mwenye upeo mdogo sana. Kuna wakati niliwahi kuuliza hapa kibarazani kwangu kuwa, “hivi naeleweka?” Lilikuwa ni swali ambalo wengi hawakunielewa nilikuwa namanisha nini, ingawa wako baadhi waliojaribu kuainisha mtazamo wao juu ya kile ninachowaza.


Hivi karibuni niliweka taswira inayoonesha majukumu yanayowakabili wanawake. Ingawa ni majukumu yetu, lakini nilikuwa najaribu kuonesha jinsi utekelezaji wake ulivyo mgumu kulingana na mazingira yaliyopo, licha ya kwamba tuko kwenye ulimwengu wa sayansi na teknolijia. Nakumbuka nilipata upinzani mkubwa sana kutoka kwa wanaume wengi sana wakiwepo hata wale ambao sikuwatarajia.


Wakati nilitarajia mjadala ambao ungeibua namna bora ya kumuondolea mwanamke huyu madhila anayopambana nayo, lakini ikawa ni kinyume chake. Inashangaza kidogo kuona kwamba mijadala inayohusu haki za binadamu inashindwa kukubali kuwa swala la madhila yanayowakabili wanawake ni kitu ambacho kinahitaji kupewa mtazamo wa kipekee kutokana na kushushwa na kunyimwa haki zao.



Ukatili dhidi ya wanawake na wasichana ni miongoni mwa ukandamizwaji wa haki za binadamu ulio mkubwa na unaofanyika sana duniani hivi sasa. Ukandamizwaji wa mwanamke, kwa mazoea au kwa sababu ya utandawazi, kwa kukosa elimu kutokana na kubaguliwa kijinsia au kwa sababu ya wazazi kufanya uchaguzi nani asome katika familia, kutokana na uhaba wa rasilimali, wanawake wengi wamejikuta hawana elimu ya kutosha ya darasani.


Kwa kukosa elimu ya darasani wanawake wanashindwa kujua haki zao za msingi na kuepuka mila potofu ambazo zinawakandamiza, lakini pia wanakosa ajira na kipato ambacho kingewawezesha kujikimu na kumudu kuendesha maisha yao. Ikumbukwe kwamba wanawake wanafanya saba ya kumi ya watu wote masikini duniani.


Pia ni vyema ikafahamika kwamba kati ya kila wakimbizi kumi hapa duniani, wanane ni wanawake na watoto na kati ya hao, wawili tu ni wanaume. Lakini pia ikumbukwe kwamba migogoro yote ya kisiasa inayosababisha uwepo wa wakimbizi hapa duniani chanzo chake kikuu ni wanaume.


Wakati Fulani umoja wa Mataifa ulitoa taarifa juu ya haki za binadamu bofya hapa kuisoma.


Katika taarifa hiyo umoja huo ulikiri wazi kuwa kusafirishwa kwa lazima kwa wanawake na watoto kote duniani na kuuzwa na kufanyishwa kazi kwa lazima ukiwemo ukahaba, Inaaminika kuwa aina mpya ya UTUMWA hapa duniani na umekuwa ni jambo la kawaida kabisa.


Takwimu mbalimbali za mashirika ya haki za binadamu likiwemo shirika la Human Right Watch zinaonyesha kwamba zaidi ya watoto milioni moja, karibu wote wakiwa ni watoto wa kike wanalazimishwa kuingia kwenye ukahaba, wakiwemo wale wa nchi masikini zaidi kama Tanzania. Hulazimishwa kuingia kwenye ukahaba kwa ulaghai wa kupatiwa kazi mijini, ndani ya nchi husika (Hili nimewahi kulizungumza katika makala zangu za nyuma).


Kwa sehemu kubwa, watoto hao hutoka kwenye familia ambazo mtu akichunguza atagundua kwamba ni masikini na umasikini wao umetokana na mfumo mbaya wa uchumi duniani. Hapa nchini idadi kubwa ya wasichana hutolewa vijijini na kupelekwa mijini hususana Dar es salaam, Mbeya, Arusha, Mwanza na miji mingine ambapo huahidiwa kazi za ndani na shule lakini hakuna litimizwalo na wengine huishia kunyanyaswa na kulazimishwa mapenzi na mmoja ama baadhi ya wanafamilia na haya husababisha kukimbia nyumba bila kujua waendako na wengine kujiingiza katika maisha hatari ya ukahaba, rejea makala ya kaka Mubelwa kwa kubofya hapa


Lakini kuzungumzia swala la madhila wayapatayo wanawake inabidi uwe na moyo kama wa mwendawazimu hivi, kwani unaweza kushuhudia dhihaka na kejeli kutoka kwa wanaume utadhani hawakutoka katika matumbo ya wanawake. Inabidi tufike mahali tuuone ukweli kuwa pamoja na mgawanyiko wa majukumu kati ya wanawake na wanaume, lakini tukubaliane kuwa hatuko kwenye uwanja unaofanana kimazingira.


Kama ukilinganisha mazingira ya wanaume katika utekelezaji majukumu yao ya kila siku, na mazingira ya wanawake katika utekelezaji wa majukumu yao ya kila siku utagundua kwamba kwa asilimia kubwa wanawake wanatekeleza majukumu yao katika mazingira magumu sana ukilinganisha na wanaume kutokana na mfumo dume uliojikita hapa duniani kwa karne nyingi tu huko nyuma.


Kwa waraka huu dada Subi ni kutaka kuweka ufafanuzi wa kile nilichokuwa najaribu kukifikisha kwa wasomaji wa kibaraza hiki ili kufungua mjadala ambao ungefika mahali tukapata suluhisho, lakini nilishangazwa na jinsi baadhi ya wasomaji walipojaribu kupotosha mada na kunishambulia dhahiri. Sijutii kwa kile nilichokifanya yaani kuweka ile mada lakini naamini ujumbe ulifika, mahali pake.


Mimi sio mwanaharakati wa kutetea haki za wanawake kama baadhi ya wasomaji walivyonituhumu, lakini kama mwanamke mtarajiwa nilikuwa nayaangalia madhila wayapatayo wanawake kwa jicho la tatu, lakini kwa kuwa nimeonekana kuwa mhafidhina, sina budi kubadili aina ya uandishi wangu na kujikita kwenye kitu kingine ambacho hakitaleta kusigishana na baadhi ya wasomaji wangu.



Ni mimi mdogo wako


Koero Mkundi






Reactions:



18 Maoni:



wavuti-nukta77 said...


Dada Mdogo Koero,

- uhuru wa kuandika haujaondoshwa.
- hujakiuka sheria wala kanuni.
- hujamzuia yeyote kusema ama kuandika kwa uhuru wake na kwa mujibu wa sheria.
- ukiandika kuhusu wanawake kwa kuwa ndiyo imekugusa na mwingine akataka kuandika kuhusu wanaume kwa kuwa ndiyo imemgusa, ni uchaguzi na uamuzi huru.

Sasa basi,
Makala uliyoandika kipindi kilichopita niliisoma na niliuelewa mtizamo wako na nilisoma baadhi ya maoni ya wachangiaji kwa wakati ule, nao walichukulia kwa mtizamo wako japo ni kweli kuwa wapo waliotoka katika mada kuu na kushambulia mwandishi, nani asiyejua kuwa binadamu ndivyo tulivyo? hasa pale unapokuwa unataka kutoa dukuduku kwa kisa kingine na kufananisha kisa cha sasa na kile kilichopita, ni rahisi sana kubwatuka yote yaliyoujaza moyo wako. Ila hiyo uichukulie kama changamoto kwani hakuna vita rahisi, hasa vita ya kudai haki yako. Unapozungumzia kuhusu wanawake si lazima matatizo yao yawe yamesababishwa na wanaume ingawaje ni vigumu kwa wengine kuliona hilo, vile vile unapozungumzia matatizo ya wanawake hutaacha kugusa wanaume kwa upande mwingine kutokana na jamii ilivyowalea na kuwakuza. Ndiyo maana jamii na jamii hutofautiana, hasa zile jamii ambazo kufanya kazi na kulea familia ni jukumu la wote kwa kuwa si rahisi kumpata 'yaya' wa kuwatunza watoto.
Usichoke kuandika, na mara zote uwe tayari kupokea mitizamo tafauti, inayolenga mada, na inayokulenga wewe binafsi kisha kama ulivyosema, 'ujumbe umefika' nami naongezea, 'that which will not kill you, will make you strong'.
Iko kazi pevu katika kuwaelimisha wanawake juu ya 'misingi na haki ya binadamu' humo ndani kumejaa kila aina ya mazagazaga ya imani, mila, desturi, taratibu, nk nk, tukivuka kigingi hicho tutakuwa tumepiga hatua moja nzuri sana.

PS: Si wewe peke yako unayedhaniwa kuwa kwa kuzungumzia habari za 'wanawake' basi ni 'feminist' ni wengi, mimi pia ni mmojawapo wa kuambiwa hivyo, inagwaje sijawahi kuisoma wala kutaka kuifahamu dhamira ya feminism. Ikiwa kinachoniudhi kimefanyika dhidi ya mwanamke, mwanaume, mnyama nk na inaonekana ni feminism, basi na iwe hivyo, ila kuandika ikiwa kipo cha kuandika ama kusema ikiwa kipo cha kusemea tutaendelea (hata tusipoandika ama kusema sisi, wapo watakaofanya hivyo).

Over and Out!


March 24, 2010 8:24 AM



Fadhy Mtanga said...


Da Koero, mimi sioni tatizo lako. Labda kama mtu ataniambia ukweli ni tatizo. Kama ukweli ni tatizo, basi wewe na da Subi mna matatizo na mnapaswa kuogopwa kama nini sijui!

Tutaishi hivi hadi lini? Kama tunayakubali mabadiliko mengine katika maisha, kama maendeleo ya teknolojia na sayansi, kwa nini hatuyakubali mabadiliko kijamii? Wanawake wataendelea kuwekwa second class hadi lini? Lazima usemwe ukweli. Na ukweli mzuri ni ule unaosemwa na mwathirika wa moja kwa moja wa kadhia fulani. Mambo ya wanawake lazima yasemwe na wanawake wenyewe. Kwani wao ndio waathirika wa moja kwa moja na manyanyaso na kutengwa.

Pana tatizo la wanaoitafsiri dhana ya feminism. Feminism maana yake ni tapo la kupigania ukombozi, haki na usawa wa wanawake. Kiufupi tunasema ni nadharia ya usawa wa wanawake. Ni mtu wa ajabu atakayeona hilo ni tatizo. Kama kuna hitilafu ya mbinu labda zinazotumika katika feminism, hilo ndilo linapaswa kusemwa.

Kuna watu na akili zetu timamu, tunapokusudia kumnyanyasa mwanamke, tunafungua hata Biblia, tunasimamia Mwanzo 3:16 "Akamwambia mwanamke, Hakika nitakuzidishia uchungu wako, na kuzaa kwako; kwa utungu utazaa watoto; na tamaa yako itakuwa kwa mumeo, naye atakutawala."

Nimesoma kifungu hicho kwa sababu nikiwa mdogo nilipata kusikia mahubiri mahali kuhusiana na kifungu hicho.

Nimesema mengi. Nifupishe kwa kusema, ni wajibu wenu na haki yenu wanawake kupigania haki zenu.

Siwezi kuwa adui kwa kusema ukweli.


March 24, 2010 8:49 AM



Yasinta Ngonyani said...


Koero kwanza ahsante sana kwa mada hii nzuri na ambayo imerudiwa mara kwa mara na ambayo mada inarukia upande mwingine.

Saw:- Nimekuwa mara nyingi nikijiuliza hivi kwa nini mwanaume unajifanya kuweza kila kitu lakini lijapo suala la jamii linamshinda tuanze na shughuli za nytumbani utakuta mume anamwambia mke nimekuoa na kukulipia mahari kwa hiyo utazaa watoto, utawalea, utapika, utaleta maji, kuni na shughuli zote za nyumbani. Yaani anamfanya ni mtumwa kabisha Je huu kweli ni upendo wa mke na mume? Na hii inaendelea kizazi hadi kizazi Hivi hayupo au haiwezekana kuwe na MWENYEKITI WA DUNIA WA WANAWAKE. Maana hili swali sio nyumbani Afrika tu wanawake kupata mateso.
Hakika nawaambieni tukijaribu kuwaacha wanaume nyumbani yaani kubadili kazi itakuwa kasheshe. Kwa sababu mwanaume bila mwanamke bado hajakamilika lakini hata hivi anamfanya mwanamke ni mtumwa.Kweli hii ni haki je ule usawa upo wapi?

Tukija kwenye swala la elimu nimeshuhudia mwenyewe na pia kusoma katika vitabu mbalimbali kuwa kuna jamii nyingi wanaamini kuwa hakuna faida kumshomesha mmtoto wa kike, ni kupoteza pesa bure tu. Ndio lakini wanasahau kuwa ni watoto wakiume ndio wawapao mimba watoto wa kike na mwisho kuacha masomo. Kama alivyosema D Subi hii yote inatokana na bado tupo kwenye zile imani za zamani, pia mila na desturi.Kwa hiyo hii ndio inatufanya tuamini kuwa wanawake hawawezi kitu hakuna haja ya kumsomesha kwani akishaolewa basi anakuwa ukoo mwingine. Basi kama wendawazimu na tutakuwa tu kwani ni lazima hili swala la haki za wanawake lipiganiwe na muda wenyewe ndio sasa.Upendo Daima!!


March 24, 2010 2:38 PM



Anonymous said...


Ningependa sana kusikia wanawake mnaongelea nini cha kufanya sasa kuweza kujenga uhusiano na hisia mpya ambayo itampa mwanamke haki sawa na mwanaume bila kuathiri jinsia ya mtu.
Pia, kama wanawake wataacha kupoteza muda mwingi kuzungumzia historia, badala ya kupanga mikakati ya kuondokana na tatizo hili, basi itakuwa ni kupoteza muda bure.
Ukitanguliza chuki kwa kutafuta haki, hata yule ambaye anashutumiwa kwa kukalia haki hataweza kukaa na wewe kusikiliza mlolongo wa pointi za maana ulizo nazo.
Koero, mada zako unazileta vizuri sana, lakini unaingia kwa gia ya hasira na chuki kwa wanaume kiasi kwamba unaonekana kama ....... kwa wanaume, matokeo yake unaishia kusemewa hovyo tu.
Mimi nafikiri mabadiliko yamesha anza kujitokeza, usitegemee kwa usiku mmoja utageuza dhana hii iliyopo.Mambo ni polepole
Bado mimi binafsi sijakuona kama kweli wewe ni mtetezi au mtu wa kukashifu jinsia fulani ndani ya ukweli unaoutoa.


March 24, 2010 4:29 PM



Mzee wa Changamoto said...


"The Way You See The Problem Is The Problem"

Ameeeen


March 24, 2010 11:38 PM



Masangu Matondo Nzuzullima said...


I second the motion..."The Way you see the problem is the problem"

Safari bado ni ndefu!


March 25, 2010 2:55 AM



Markus Mpangala said...


KOEROOOOOOOOOOOOOOOOOOOOOOOO! andika kwa uhuru, andika kwa

mtazamo wako sidhani kama kuna haja ya kuangalia nani anasema nini. Hujui watu tunatofautiana? nakumbuka ulinishtua shutuma hizo, lakini niliandika inawezekana kila mtu anaona aonavyo, hivyo wewe andika unachoamini.

Ingawaje mimi huwa napingana na mambo kadhaa ikiwemo la kulazimisha vita dhidi ya wanaume au kumtazama mwanaume kama tatizom lakini naheshimu sana mchango wako na wengine, nawasikiliza sana kama nilivyosema kwa

Dk Benadetha Kilian kwamba siyo haki kudai usawa wa uwiano wa maamuzi kati ya wanaume na wanawake kwamba lazima tuunde mfumo wa kulenga jinsia, nsema katiba inasema wazi wote ni sawa na hakuna mwanaume aliyepewa haki zaidi.

si kweli kwamba wanawake wananyima haki, usawa hauombwi jamani, utafuteni, sidhani kama wanaume walipewa haki au usawa, na nani aliwapa?

kwa ypte haya lakini nakubali tunahitajika kuzingatia katibu na siyo kusema tuwape upendeleo wanawake na swali linakuja nai alimpa mwanaume?

KWAHIYO, KWA MAONI YANGU KOERO unastahili kuandika kwa haki na kwa ujnzi wa hoja, mwangalie Rais Arroyo hakufika pale kwa kupendelewa bali ana sifa.

kama wanawake kupata fursa au kukandamizwa mimi nalia na hawa wanaharakati wanaotumila 'mihela' kufanya makongamano huku wahitaji wanaumia.

inakera, lakini nani alipewa dhamana zaidi wakati katiba inatamka wote sawa/

ANDIKA, NDIYO UANDISHI WA RAIA HUU, WATU TUNATUKANWA SANA KATIKA MAKALA ZETU, MIMI NI MPINZANI WA MASUALA KADHAA YA MAREKANI

nimeshaitwa gaidi mara kadhaa na nimeongea sana na wakurugenzi wa ubalozi wa marekani mwaka 2008 nikiandikia Rai, nilisema nitaacha kuipinga endapo itaacha ufidhuli.

ninatukanwa hadi kesho na hata na rafiki zangu, lakini nasema mimi siyo RUNNING DOGS vile vijibwa vinavyobweka lakini having'ati na havina msimamo wa masuala wnayotetea.
kwahivyo SIMAMA andika bila WEWE WANAWAKE

WATASAIDIWAJE?????????????????????????????? ANDIKA ANDIKA ANDIKA tena uwe unaandika ukiwa na HASIRA KALI ndiyo hoja inapanda vema kichwani.


March 25, 2010 8:12 AM



John Mwaipopo said...


Leo sichangii.


March 25, 2010 12:31 PM



Anonymous said...


Mwaipopo una busara. Kama mambo menyewe ndio haya. Haina haja bro! Even me, sitacomment again on this childish blog. Koero is an emotional wreck and I swear she will never have a stable marriage huyu. Frustrated and emotionally unstable women like these are dangerous even if they have kids.

Blogs zingine ni miyeyusho tu. Kwa nini ufungue blogu if you can handle the heat? Unataka kila mtu akubali tu mawazo yako finyu? Jesus was criticized sembuse weye uliyekimbia shule? Please? Kama ligwaride limekuwa too much, funga blogu ukauze....bullshit!


March 26, 2010 3:19 AM



Anonymous said...


Mdau wa March 26,2010 3:19, Taratibu ndugu yangu wewe ni mtu mzima na watu tunakueshimu. Kuna haja gani ya wewe kutumia lugha chavu za mitaaani kwenye blog hii?
"Kaero is an emotional wreck" sasa umeishageuka psychologist, wakati unashindwa kujitibu mwenyewe.

Blog za watanzania zimejaa, haukulazimishwa kuingia humu au kucomment chochote, Please grew up!!!

Bloggers, msiwanyamanzie watu kama hawa pindi wanapoingia kwenye viwanja vyenu, kwani njemba kama hizi lengo lao ni kulimit the freedom of speech.

HAHAHAAAAAAAA! HE CAN'T STAND WOMEN IN PANTS.


March 26, 2010 2:50 PM



Anonymous said...


Mdau wa March 26,2010 3:19, Taratibu ndugu yangu wewe ni mtu mzima na watu tunakueshimu. Kuna haja gani ya wewe kutumia lugha chavu za mitaaani kwenye blog hii?
"Kaero is an emotional wreck" sasa umeishageuka psychologist, wakati unashindwa kujitibu mwenyewe.
**************
YOU DON'T HAVE TO BE A PYSCHOLOGIST TO IDENTIFY SOMEONE WHO IS SICK AND NEEDS EMOTIONAL HELP
*************************
Blog za watanzania zimejaa, haukulazimishwa kuingia humu au kucomment chochote, Please grew up!!!
************************
I AM FREE TO VISIT ANY BLOG AND LEAVE MY COMMENTS. PLEASE GREW UP - NO COMMENT HERE. HUNIJUI!!!
*************************
Bloggers, msiwanyamanzie watu kama hawa pindi wanapoingia kwenye viwanja vyenu, kwani njemba kama hizi lengo lao ni kulimit the freedom of speech.
***********************
IT IS PEOPLE LIKE YOU WHO WANT TO LIMIT THE FREEDOM OF SPEECH. SIMPLE, KAMA HAMTAKI KUWA CRITICIZED, THEN DISABLE YOUR COMMENTS PAGE. YOU ARE STILL KIDS WHO CANNOT BE CHALLENGED. MKIGUSWA KIDOGO TU MNAPIGA MAKELELE. THIS BLOG HAS A LOT OF PROBLEMS AND YOU KNOW IT!!!
**************************
HAHAHAAAAAAAA! HE CAN'T STAND WOMEN IN PANTS.
*************************
NAKANYAGA WANAWAKE KWA UZURI NA I AM NOT SCARED OF NO ONE, EVEN YOUR MOM. UKIMLETA MI NABWENGA TU...

KOERO, CLOSE THE BLOGU IF YOU CAN'T HANDLE THE HEAT..........


March 26, 2010 6:49 PM



Mzee wa Changamoto said...


Hii ndio raha ya kuwa na ma-Anony.
Japo wana utambulishi, hawataki watambulike hata wanapoamini kuwa wanaelimisha na kukosoa.

Hii yanikumbusha aliyoandika Prof Mbele hapa http://hapakwetu.blogspot.com/2009/06/viumbe-anonymous-katika-blogu.html


March 27, 2010 1:26 AM



Godwin Habib Meghji said...


Kutofautiana kimitazamo kwa binadamu ni kitu cha kawaida kabisa. NAJUA HILI LINATOKANA NA MAMBO MENGI, KAMA UWEZO WA KUFIKIRI, MAZINGIRA TULIYOKULIA NA TUNAYOISHI SASA, ITIKADI ZETU ZA KISIASA NA MENGINE MENGI.

Mimi binafsi huwa sishangai nikiona watu wanatofautiana kwenye mijadala mingi

ILA TOFAUTI HIZI ZINAPOVUKA MIPAKA NA KUFIKIA KUMSHAMBULIA MTU BINAFSI BADALA YA HOJA, HUWA SI ELEWI KABISA

Bado sipati mantiki ya annon hapo juu badala ya kutetea hoja yake, anakwenda moja kwa moja kumshambulia mtoa hoja

Kinachonishangaza zaidi ni mtu huyo kujiona ana upeo mkubwa wa kufikiri


March 27, 2010 4:01 AM



Anonymous said...


DUH! Kweli stress mbaya, huyu jamaa anapata uhuru akiwa amejificha kwenye screen ya computer. Inaonekana una matatizo mbele ya kadamnasi, au ukweli unakuuma sana.
Pole sana na yaliyokusibu ndugu yangu. Hauna haja ya kutukana ili ueleweke. Actually unavyotukana ndio unavyodhihirisha udhaifu wako.

ETI I AM NOT SCARED OF NO ONE,EVEN YOUR MOM!!! HA HA HA HA HA HA HA.
Umesahau kunywa dawa zako za stress nini?


March 27, 2010 5:54 AM



Ramson said...


Naona sasa mjadala huu umeingiliwa na mpaka wendawazimu, hivi hakuna lugha nzuri inayoweza kutumika katika kujenga hoja mpaka watu mtukanane matusi ya nguoni?

Hivi alichokosea binti huyu ni kitu gani hasa mpaka astahili kudhalilishwa?

haiyumkini kuna watu wamepata mahali pa kumalizia hasira zao baada ya kutendwa na wenzi wao...

Mnakosa hata busara ya kujadili jambo kwa mantiki?

Sikatai kuwa kila mtu anao uhuru wa kutoa maoni yake, lakini inapofikia mahali watu kuacha kujenga hoja juu ya mjadala husika na kukimbilia matusi na kashfa, inaoneasha udhaifu mkubwa kwa muhusika, haijalishi una elimu kiasi gani kukosa adabu ni kukosa adabu tu.....hebu msikigeuze kibaraza cha VUKANI kuwa pango la wavuta bangi, hapa ni mahali ambapo kunakutanisha migongano ya mawazo na mijadala yenye kufikirisha.

Acheni hizo.....Ebo!!


March 27, 2010 8:37 AM



kamala Lutatinisibwa Lutabasibwa said...


""the way you dont see the problem is not the proble""

swali, hivi kinyume cha neno problem ni kipi??

nimeupenda mchango wa mwaipopo

THANK YOU gOD FOR CREATING ME A MAN. amen

jamani wanawake, kila mwezi lazima mfe kidogo, kwenye ligwaride mko chini (mnakandamizwa)

ila mimi bila mwanamke, sidhanikama ntakuwa nimekamilika. mnateseka ehe??

ila inabidi tuongelee pia matatizo ya wanaume --- nilazima yapo.

labda, wanaharakati waandamane vitabu vya dini hasa biblia ibadilishwe, inawakandamiza vibaya wamama

harafu,wanawake ni wazuri na muhimu sana ndo maana nikawowa mmjoa wao, hupenda kuwaangalia wakitembea na kuwasikiliza wakiongea kwa kubana pua

ila, anony mmoja kaongea kwa lugha iliiyoko uchi, lakini swali muhimu, Koero una Mume/mchumba, rafiki nk?? kama huna kwa nini? kama huna Mume au huonjwi ligwaride, ni vigumu kumtetea mwanamke kwenye ishu za familia, ni lazima ujue siri ya kumzuia mwanamke kuiacha ndoa inayoonekana ni ngumu. kuna siri kubwa hapo

ila pia, wanawake ndo wabaya kwani wanazaa na kulea wanaume wababya.

lakini kwa "the way you see the pro......."

mapambano haya ya jminsia yamelta ajira na kuwajengea umaarufu baadhi ya watu na hasa wanawake kwa hiyo unyanyasaji endelee, bila hilo Koero sijui angeandika nini. so siyo prob.


March 27, 2010 12:16 PM



Masangu Matondo Nzuzullima said...


Kuna msemo usemao kwamba "Don't argue with a fool, people may not notice the difference"

Mara nyingi njia bora na muafaka ya "kujibizana" na hawa ma-anony "wakorofi" ni kuwapuuza na kukaa kimya. Ukianza kutukanana nao hutashinda hata kama uwe na kamusi nzima ya matusi kichwani. Japo kukaa kimya wakati unatukanwa kunahitaji ushupavu, hii ndiyo njia bora kabisa ambayo nimejifunza tangu nifungue blogu.

Kuna mtu mmoja wa mambo ya utambuzi hapa Marekani ameandika kwa kirefu sana kuhusu jambo hili; na jinsi ya kutafuta furaha wakati unaposongwa. Ni elimu inayosaidia sana katika maisha yetu yaliyojaa wivu, kuoneana na kudharauliana bila sababu yo yote.


March 28, 2010 6:23 AM



Chacha o'Wambura a.k.a Ng'wanambiti! said...


Anayejidanganya kuwa Koero hatakuwa na STABLE marriage skurubu za kichwa haziko sawa.

Koero, kaza buti kwani huna haja ya kufunga kijiwe chetu kwa kuwa si lazima ukubaliane na mawazo ya kila mtu ama woote wanaopita hapa wakubaliane nawe.

Nikiwa mmojawapo wa watu watokao katika jamii zinazomkandamiza mwanamke naunga mkono hoja unazozitoa kwani nadhani mfumo dume hauna nafasi katika zama hizi za utandawazi wizi!


Tuko pamoja dada!


Friday, December 24, 2010

MBOMBO JILIPO!

Mkurugenzi wa Takukuru Dr. Edward Hosea

Hili ni neno la Kinyakyusa, kabila ambalo linapatikana kule mkoani Mbeya, likiwa na maana ya ‘Kazi ipo’ ni neno ambalo nilijifunza kupitia kwa rafiki yangu ambaye tulikuwa tulisoma wote wakati fulani hapa jijini Dar.

Niliwahi kumuuliza maana ya neno hilo ambalo alikuwa akilipenda sana kulitamka hasa pale anaposhikwa na butwaa linapotokea jambo la kushangaza na ndipo aliponieleza maana ya neno hilo kuwa ni ‘Kazi ipo’

Nililipenda sana neno hili na nimekuwa nikilitumia sana pale ninaposhangazwa na kitu au jambo lolote. Wiki hii nimejikuta nikitamka neno hilo baada ya kusoma taarifa katika magazeti ya hapa nchini ambayo yalinukuu taarifa uiliyoandikwa katika gazeti la The Gardian la nchini Uingereza ambalo nalo lilinukuiu taarifa zilizovujishwa na tovuti ya Wikileaks.

Taarifa yenyewe ni ile ya mahojiano ya Mkuu wa TAKUKURU, Dr. Hosea, na Jasusi lililobobea la Kimarekani Bwana Purnell Delly ambayo yalifanyika jijini Dar es Salaam mnamo Julai 14 mwaka 2007.

Katika mahojiano hayo yaliyovujishwa na Wikileaks Dk. Hoseah alinukuliwa akidai kuwa Rais Jakaya Kikwete, ndiye chanzo cha baadhi ya vigogo waliotajwa kushindwa kuchukuliwa hatua katika sakata la rushwa.

Lakini katika hali ya taharuki Dr. Hosea akakurupuka na kukanusha kuwa amenukuliwa vibaya. Kitendo cha kukurupuka na kukanusha juu ya taarifa hiyo hakikumsaidia Dr. Hosea na badala yake kimezusha maswali mengine magumu zaidi.


Kunazuka maswali magumu zaidi kwa sababu kile kilichunukuliwa katika mahojiano hayo ya Dr. Hosea na Bwana Purnell, ndicho ambacho Watanzania wanachokiamini. Watanzania wanaamini kuwa kuna ajizi kubwa katika kuwashughulikia wahusika wa ufisadi. Na haiyumkini hilo ndilo lililopunguza idadi ya Kura za Uraisi kwa Muhueshimiwa.

Ama kweli mbombo Jilipo, maana kama taarifa hii ingevuja kabla ya uchaguzi mkuu, sijui matokeo yangekuwaje. Hata hivyo sitashangaa kama yatazuka mengine zaidi ya haya kwani kwa jinsi ninavyoona, nadhani bado kitambo kidogo kila kitu kitakuwa peupe...........

Wednesday, December 22, 2010

JINSI WATU WATOFAUTIANAVYO KATIKA KUSIKIA TUSI!

Katika kuelekea kuumaliza mwaka 2010, nimevutiwa na makala hii ya kaka Simon Mkodo Kitururu ambayo aliiweka pale kibarazani kwake mwanzoni mwa mwaka huu ilikuwa ni Januari 31, 2010.

Nimeona sio vibaya kujikumbusha jinsi watu watofautianavyo katika kusikia tusi..........!

Kunauwezekano kabisa UKIFIKIRIA,....

... utagundua UBUNIFU wa jinsi ya kustukia ni nini hasa ni TUSI haupo katika JAMII .:-(

Swali:

· Huwa unafikiria ni nini hasa siri ya misingi ya fikira zako za UTAMBUZI WAKO WA ni nini hasa ni TUSI?

· UKIFIKIRIA unafikiri binadamu wenye busara na akili UWAJUAO HUWA wanapatia tusi la kulikasirikia?

Kuna uwezekano kabisa UKIFIKIRIA,....

..... utagundua labda tafsiri ya tusi katika mawazo ya wengi ni potofu ndio maana hawastukii TUSI HASA ila wanasikia WALILOFUNZWA KUTAFSIRI TU kuwa ndio tusi katika jamii NA JAMII ,....


..... ambalo laweza kuwa kwa mfikiriaji wala SIO TUSI na ni jinsi tu ya lipakuliwavyo na kuwekwa mbele za mtu kumfanyako mtu kuacha kufikiria na kukasirika kisa kaambiwa ana meno kama uchi wa kuku na haki yanani kapandisha mori kuwa alicho ambiwa ni TUSI.

Swali:

· Ukifikiria kama BINADAMU AKIFIKIRIA unafikiri wengi wadhaniayo ni MATUSI yata faulu mtihani wa kuitwa ni MATUSI duniani ?

Na labda kimfano ,...

.. tusi la kweli ,....

.....KISIASA- ni lile la kubwa zima kufanywa mjinga kwa kuahidiwa AHADI ZA uongo na MWANASIASA KILA WAKATI WA UCHAGUZI MPYA ili umpigie kura KITU AMBACHO kirahisi kikiwekwa katika sentensi chaweza kuwa: ``Haya majinga kweli yani nikitunga TU stori kila wakati wa uchaguzi na kuahidi nisiyoweza hayaachi kunipigia KURA.Yaone vile kama vile haya stukii vile KUWA nalia ofisini na wala siwazi TATUZI la matatizo yao!´´

Na matusi KAMA hayo hutukanwa watu KIJAMII, KIDINI, KIUCHUMI au hata KIUTU tu WAO hata bila kustukiwa kwa kuwa kwa kiswahili watu wamefikia MPAKA kufikiria TUSI KUBWA ni mpaka tu jina la sehemu za siri za mtu.

Swali:

· Si ushastukia moja ya tusi maarufu kwa kiswahili ni kutajiwa JINA LA SEHEMU ZA SIRI ZAKO halafu mbele ya jina la NYETI ZAKO ikaongezewa neno ``YAKO´´?

· Hujastukia watu wengi hukasirishwa na wayatambuayo kama MATUSI ambayo hayana kabisa UBUNIFU?

· Unauhakika ulishawahi kutukanwa au ni tafsiri yako tu ndio itafsiriyo na kulijenga tusi?

· Unauhakika hatuhitaji kuwa na somo mashuleni ya jinsi ya kustukia tusi halisi ni nini ili tuache kukasirikia tafsiri za tusi ambazo zina fanya watu wakosee kustukia tusi halisi ni lipi?


Kwa bahati mbaya,...

... NA WASIWASI kuna uwezekano mkubwa,...

...wengi wadhaniao wamewahi KUTUKANWA na kufanikiwa kulikasirikia TUSI,...


...walichofanya ni kukasirikia TAFSIRI tu zao ZA KILE walichojifunza kukitambua kama TUSI,....

....na wote twajua tafsiri ni mwanaharamu ndio maana hata sentensi ``BAISKELI WEE!´´- ikilengwa kwa mtu mwenye udhaifu na baiskeli anaweza akakurukia kichwa, kabla ya kukukaba kabali halafu akakukata ngwala huku yuko bize akikukutajia jina la kikojoleo cha mwanamke halafu akaongezea neno ``WE´´mbele yake kwa kuwa anaamini kwa kufanya hivyo ana KUTUSI .:-(


Swali:

· Si unakumbuka kusikia au kutambua tusi ni kitendo cha kujifunza KUTAFSIRI TU ndio maana IRAKI kumrushia Rais George Bush KIATU ni tusi wakati kwa Mmarekani kumrushia mtu kiatu MAANA YAKE ni KUMRUSHIA MTU KIATU?

· Unauhakika jina la sehemu zako Nyeti chini kidogo ya kitovu ni MATUSI au ni kitendo tu cha kuzitumia hizo sehemu kabla ya kuhalalishiwa na Kanisa au Msikiti au VIBABU FULANI ndio matusi?



NI WAZO tu hili BINGWA na usikonde!:-(

Thursday, December 2, 2010

NAHISI MIKONO YANGU IMELOA DAMU!

Najutia nafsi yangu

Ni kweli mikono yangu imeloa damu. Nahisi damu ya dhuluma, tena dhuluma ya uhai wa kiumbe ambacho kilihitaji kuishi. Aaah! Moyo unaniuma sana lakini walisema Wahenga kuwa maji yakimwagika katu hayazoleki na pia majuto ni mjukuu.

Sisi ni binadamu, kuna matukio ambayo hututokea na kamwe hatuwezi kuyasahau kutokana na kuguswa na matukio hayo hasa unapogundua kwamba wewe ndiwe chanzo cha hayo yote.

Je wewe unayesoma hapa hujawahi kumwaga damu? Je mikono yako haijaloa damu? Kama jawabu lako ni hapana basi utakuwa unajidanganya, kwani ukweli ni kwamba umeshwahi kumwaga damu, labda tu ujitie hamnazo ila ukweli umeshawahi kumwaga damu.

Ni tukio ambalo siwezi kulisahau. Daima naliwaza,katu halitoki. Nakumbuka ilikuwa mwaka 1995, tukio lilijiri.

Tukio ambalo lilinitokea kwa bahati mbaya sana, yaani sikulitarajia. Ilikuwa ni majira ya jioni nilikuwa nimekaa sebuleni na mama tukiangalia runinga. Mara mama akaniambia niende jikoni kuandaa chakula cha usiku. Nilipoingia jikoni nikakuta paka ameinamia chunguni, huku anakula mboga, katika hali isiyotarajiwa nilijikuta nanyanyua kiji-mchi cha kutwangia viungo na kumpiga kichwani.

Yule paka alikimbia mithiri ya mbio za nyika, huku akiyumba na kuingia katika bustani ya Maua. Wala sikuhangaika kumfuatilia, niliosha ule mchi na kuendelea na shughuli zangu za mapishi.

Siku iliyofuata, ilikuwa asubuhi nikawa namwagilia maua maji ndipo nilipomkuta yule paka akiwa amekufa pale bustanini.

Nilishtuka sana,woga ulinijaa,fadhaa ikanitawala, nikahisi ni luya ya saba. Nilitazama mara nyingine ili kuthibitisha.

Hakika lilikuwa kweli ingawaje sikutarajia kuwa pigo lile moja tena dhaifu kutoka kwa mwanamke, kama lingemtoa uhai Paka yule!

Niliingiwa na hofu mara nyingine kwani kuna simulizi nyingi kuhusiana na huyu mnyama Paka kuhusishwa na ushirikina. Imani hizi siyo haba, na zingine zimejengeka kuwa Paka anazo roho saba, sasa iweje afe kwa pigo dhaifu kama lile.

Nilihisi mikono yangu kuloa damu kwani kula vile vipande kadhaa vya samaki, sidhani kama alistahili adhabu ya kifo.

Naam, hilo limeshatokea na sina uwezo wa kumrejesha uhai wake Paka yule ambaye daima nilimpenda.

Naomba niweke wazi kuwa miongoni mwetu kuna idadi ya kutosha ya watu ambao wameshawahi kumwaga damu, iwe kwa kukusudia au bahati mbaya kama mimi.

Hivi ni watu wangapi ambao wanaweza kusimama na kudai kuwa hawajawahi kusababisha kifo hata cha mnyama?

Itakuwa ni unafiki kukanusha, lakini hebu nirejee kwenye uhalisia, hebu tuangalie kauli zetu, maamuzi yetu na kazi zetu, Je hakuna uwezekano ikatokea kusababisha vifo, iwe ni kwa wanyama au binadamu?

Nitakupa mfano, Polisi akimhoji mtuhumiwa kwa mateso ili akiri kosa halafu ikatokea mtuhumiwa yule akafariki, je mikono yake haijaloa damu?

Je daktari anapompa mgonjwa dawa isiyo sahihi akapoteza maisha au anapotoa mimba, Je mikono ya daktari huyo haijaloa damuViongozi wanapopitisha sheria au maamuzi kisha yakasababisha vifo vya wananchi, Je mikono yao haijaloa damu?

Dhahiri itakuwa imeloa damu, na kwa taarifa tu ni kwamba kuna sheria na maamuzi mengi yamefanyika hapa nchini na kusababisha vifo kwa wananchi wasio na hatia, hebu tuangalie kwa uchache tu sheria zinazowalinda wawekezaji wa madini.

Wananchi wa maeneo yanakochimbwa madini hayo wameathirika na uchafuzi wa mazingira kutokana na wawekezaji hao.

Lakini serikali imekaa kimya, huku wananchi wakiendelea kupoteza maisha. Katika kutibu malaria kuna dawa nyingi tu zimeidhinishwa na serikali kuwa ndizo zinazostahili kutumiwa katika kutibu malaria na zimesababisha vifo vya watu chungu mzima lakini hakuna anayejali.

Kuna utitiri wa madawa feki kuanzia madawa ya hospitalini na vipodozi ambapo watu wengi wameathirika na kupoteza maisha lakini hatuoni Juhudi zozote kutoka kwenye serikali yetu kudhibiti hali hiyo, je mikono ya viongozi hao ambao tumewapa dhamana ya kutulinda haijalowa damu?

Vipi kuhusu kauli zetu tu? Kuna ukweli kwamba kuna watu wengi wamepoteza maisha kutokana na kauli.

Kama hujui nitakukumbusha kiduchu, somo likolee! Unaweza kukuta mtu anaweza kumwambia mwenzie kuwa ameathirika na virusi vya ukimwi aidha kutokana na kudhoofika au kuugua mara kwa mara, na hiyo ikasababisha mtu huyo kujitoa roho.

Je mikono ya yule mtoa kauli haijaloa damu? Vipi kuhusu wale wanaowanyayasa wenzao kutokana na madaraka au nafasi walizonazo hadi kusababisha wenzao kujitoa roho. Mikono yao haijaloa damu?

Kuna watu wamefuatilia haki zao katika vyombo vya kutoa haki, au kufuatilia mafao yao mpaka wakakata tamaa na kufa kwa sononi au kujitoa roho kutokana na kutitindikiwa na mawazo. Je mikono ya wahusika haijaloa damu?

Kwa kifupi kama ukichunguza utagundua kuwa kuna watu wengi mikono yao imeloa damu, sio kwa kuua Paka tu, bali kwakutoa roho za wanaadamu wenzao kwa aidha makusudi au bahati mbaya na hivyo mikono yao kuloa damu.


Tunahitaji kubadilika na kutenda wema, na sio kwa wenzetu tu, bali hata kwa wanyama, kwani nao ni viumbe na wanaostahili kuishi.

Je bado unakanusha kuwa hujamwaga damu?