Thursday, September 23, 2010

JE NI SAHIHI KIJANA KUTAFUTIWA MWENZA NA WAZAZI ANAPOFIKIA UMRI WA KUOA AU KUOLEWA?

Mwenzenu jana nilikuwa na mjadala hapa nyumbani, na mada kuu ilikuwa ni juu ya namna nzuri ya kupata mwenza.

Dada yangu mkubwa ndiye aliyeanzisha huo mjadala kwa kumuuliza mama kama ni vyema mtu kutafutiwa mke au mume wa kuoa au kuolewa, au kila mtu anawajibika kujitafutia mwenyewe mwenza wake na kuanza maisha?

Mama alikuwa na haya ya kusema. Alisema kuwa kimsingi hapo zamani wazazi walikuwa wakiwatafutia watoto wao wenza wa kuoa au kuoelwa na lengo kuu lilikuwa ni kutaka mtoto wao aangukie katika mikono salama na mojawapo ya vigezo vikuu vilivyokuwa vikiangaliwa ilikuwa ni historia ya ukoo husika, kwa mfano, je ukoo huo unaanguka kifafa? Je ni ukoo wa wachapa kazi kwa maana ya kujituma kwa kufanya kzi kwa bidii ( Ikumbukwe kuwa zamani kazi kuu ilikuwa ni kilimo). Je Sio ukoo wenye mkono mrefu, yaani sio wezi ( Sijui kwa nyakati hizi kuna haja pia ya kuwajumuisha na mafisadi yaani kama ukoo una hulka ya ufisadi)

Jambo lingine lilikuwa ni kuangalia kama ukoo unashambauliwa na magonjwa sugu, kama vile anemia (Upungufu wa damu wa mara kwa mara) Kansa, kisukari na maradhi mengine yaliyokuwa yakitafsiriwa kuwa yanaweza kuushambulia ukoo.

Sina hakika kama vigezo hivyo bado vinazingatiwa kwani kule vijijini bado utaratibu a kutafutiana wenza upo lakini sio kwa kiwangom kama cha zamani kwa sababu ya mabadiliko yaliyoikumba jamii, kwani kila mtu sasa na lwake.

Kulizuka hoja mbalimbali ambazo kama nikiziweka hapa nitawachosha, na lengo langu ni kutaka kuwashirikisha wasomaji wa kibaraza hiki kisichoisha visa na mikasa kutafakari kwa p

Monday, September 20, 2010

WAKATI IDADI YA WASALANDIAJI NA WAMEZEA MATE TONGE IKIONGEZEKA, MASHARTI NAYO YAONGAZEKA PIA.

Kazi ipo.....


Ni jambo ambalo sikulitarajia kuwa kumbe pamoja na kunangwa kuwa sioleki na sitakuwa na ndoa imara lakini soko langu liko juu kiasi hiki!

Kusema kweli nimekuwa na wakati mgumu hasa maana kuna wengine ambao wao wamepitia mlango wa nyuma na kuleta CV zao ili kutaka bahati iwadondokee, lakini hata hivyo hilo sio tatizo, bali wasiwasi wangu ni kuwa mzee Mkundi kaongeza masharti kadhaa ambayo nahisi kuna ambao watadondokea pua.

Masharti yenyewe ni haya yafuatayo:

*Mtarajiwa hatakiwi kuwa na umri wa ubarubaru yaani umri wake uwe umefikia kati ya miaka 40 hadi 45, kwani vijana wa umri wa ubarubaru wanakuwa wasumbufu kwa sababu bado ujana unawazuzua.
*Mtarajiwa anatakiwa awe ni mkristo wa dhehebu la sabato (Hili sharti nadhani litakuwa gumu maana mweh! kwa nyakati hizi dini zina vijimambo vyake)
*Mtarajiwa hatakiwi awe mlevi wa kilevi chochote na asiwe anavuta sigara.
*Mtarajiwa anatakiw awe ni mtu wa nguvu kazi asiwe anachagua kazi.
*mtarajiwa anatakiwa awe mtanashati, mpole kiasi, awe na tabia njema na mwenye upendo wa dhati .

Sifa nyingine za ziada zitapewa kipaumbele…..LOL

Haya mwenye sifa hizo aweke CV zake hadharani, hata wale wenye kupitia nyuma ya pazia karibuni kwenye kinyang’anyiro.

Friday, September 17, 2010

KOERO UTAOLEWA NA NANI? BADO NI KITENDAWILI, LAKINI LABDA MARKUS AU MTANGA…………….LOL

Najua wengi watashangaa maana wanajua mie sioleki, lakini naamini mmeona wenyewe jinsi wanaume hao wawili wanavyojifaragua, kwa mie binti kimwana.

Nakumbuka kuna mdau mmoja aliwahi kudai tena humu humu kwenye kibaraza cha Vukani kuwa mie sifai kuolewa na sitakuwa na ndoa imara kwa sababu eti nina kiherehere na kiroho papo cha kudai haki za wanawake.

Lakini Waswahili walishawahi kusema kuwa kama ni kibaya waachie wenzio……… sasa je kiko wapi?

Najua wahafidhina watatia fitina (hata hivyo nimeshawazoea) lakini wakae wakijua kuwa bahati imenidondokea….LOL

Ila kuna jambo moja, niliwahi kumuuliza bibi Koero kuhusiana na swala la wapiga emcheku kugongana kwa binti mmoja, Je inakuwaje? Jibu lilikuwa ni rahisi sana……. Ni kwamba watakaribishwa mmoja baada ya mwingine kupata mlo na baba mkwe na yule atakayekuwa anakata matonge makubwa ya ugali aka nguna na kula ugali mwingi unaofikia kilo moja kasorobo ndiye atakayepewa jiko,kwani hiyo ni ishara kuwa huyo atakuwa ni mkulima hodari na binti yao hatakufa na njaa.

Hivyo nawaomba wamezea mate na wasalandiaji waanze kuchukua mazoezi ya kumega matonge makubwa…. La sivyo hakuna ndoa….LOL

Na kwa maandalizi, wiki ijayo mwanamwali nawekwa ndani kusubiri hatima ya ndoa yangu……..je ni nani atapata bahati ya kujivinjari na kimwana……. Usikose kusoma hapa.

Wednesday, September 8, 2010

JELA MIAKA MITATU, KISA DADA WA KIJANA KANIKATAA!

Niliamua kurudi shamba na kuwa mkulima


Kwa kifupi sana ni hivi. Mwaka 1975 nikiwa mwalimu kijana bado, nilifanya jambo ambalo kwa wakati ule wala halikunisumbua ingawa lilikuwa baya sana.
Bila shaka, wale wanaokumbuka mfumo wa elimu wa wakati ule wanajua kuhusu wanafunzi waliokuwa wanaitwa maripita ambao walikuwa ni wale wanaoanguka mtihani wa darasa la saba shule fulani na kwenda kudurusu darasa hilo kwenye shule nyingine.
Serikali ilikuwa inakataa kabisa wanafunzi kukariri tena darasa la saba au la nyuma yake baada ya kuanguka mtihani. Nikiwa shuleni kule Mbeya mwanafunzi mmoja ambaye baba yake alikuwa na urafiki na mkuu wa shule niliyokuwa nafundisha alikuja kudurusu darasa.Siku alipokuwa anakuja kuripoti, nilikuwepo mimi ofisini kama mwalimu mkuu msaidizi.
Kijana huyo aliletwa na dada yake ambaye alikuwa anafanya kazi hospitali ya mkoa. Nilimpokea kijana yule nikijua kwamba anarudia shule.Baadaya kumpokea na kujua dada yake anapofanyia kazi, niliona nami ningepata. Kama mkuu wa shule alipata fedha kupitia Yule kijana kudurusu darasa, nilijua na mimi ningepata rushwa ya mwili.
Nilimwandikisha kijana huku nikisema kwamba, kudurusu darasa ni mbayasana. Yule dada wa kijana alisema ni kweli, lakini ni suala la kusaidiana.Nilitania kwakusema, “nasi tukija kuomba msaada hospitalini itabidi tusaidiwe.” Yule dada alisema hakuna tabu. Basi kijana alianza masomo darasa la saba nami nilianza kumfuatilia dada yake kule hospitali ya mkoa. Nilifuatilia kwa miezi miwili bila mafanikio zaidi ya ahadi tu.
Nilijua kwamba, Yule muuguzi, dada wa yule kijana alikuwa anataka tu kuvuta muda ili mdogo wake amalize masomo ili anitolee nje. Ilibidi nimwambie kwamba, kama asiponikubalia ombi langu, mdogo wake ni lazima angeanguka mtihani kwani ningekwenda kuchongea mkoani kuhusu kudurusu kwake.Yule dada aliniambia, kama hilo ndilo lengo langu, ni vizuri nikalifanya.
Kuanzia hapo sikufuatilia tena na nilipania kumchongea Yule mdogo wake, jambo ambalo sikujua kwamba, lingemdhuru na bosi wangu, yaani mwalimu mkuu. Ni kweli nilikwenda mkoani na kutoa taarifa kisiri kwa wanaohusika.Ukweli ni kwamba kijana Yule ambaye alikuwa na uwezo sana darasani alishindwa baada ya jina lake kukatwa na mkuu wa shule kushushwa cheo.
Nilifurahi sana baada ya matokeo hayo. Nilikwenda kule Hospitalini kumjulisha Yule dada mtu kwamba mimi ndiye niliyemwangusha mdogo wake.
Yule dada alilia nikiwa hapohapo, huku moyo wangu ukiwa umeridhika. Jioni ya siku ile ile, Yule kijana alikuja nyumbani kwangu hapo shuleni na kuniuliza ni kwa nini nimemfanyia roho mbaya . Nilimwambia amuulize dada yake na kumsisitiza kwamba sio mimi bali ni sheria zanchi.Yule kijana aliondoka huku akisema, Mungu ndiye anayejua kulipa au kutoa hukumu kwa haki.
Nilicheka na kumwambia aende akafie mbali. “Dada yako ni ndege mjanja amenasa kwenye tundu bovu” Nilimpigia kelele. Aligeuka na kunitazama kwa muda, halafu aliondoka. Nadhani angekuwa na nguvu angeweza kunipiga ngumi nyingi sana, lakini hakuwana ubavu.Miaka ilipita na nikawa nimesahau kabisa jambo lile. Ilikuwa ni miaka 25 baadae, mwaka 2000 ni kwamba mwaka 1995 niliacha kazi ya ualimu na kurudi kwetu Iringa. Nilianzisha biashara na kuwa mfanyabiashara.
Mwaka huo 2000 nilipata matatizo ambayo yalinifikisha mahakamani.Kesi iliendelea kwa mwezi mmoja, kabla ya kutolewa hukumu. Haikuwa kesi kubwa, wala ambayo ingenitisha kwa kweli, Haya hukumu yake kwa mujibu wa wanasheria ambao niliwauliza, hakimu alikuwa anaruhusiwa kutoa faini au kifungo cha nje. Sijui walinidanganya kunipa moyo au vipi.
Lakini siku ya hukumu hakimu alinihukumu kwenda jela miaka Mitatu adhabu ya juu kabisa ya kosa langu. Nilibabaika sana na wala sikuamini kama nimehukumiwa kwenda jela. Wakati nikipelekwa kufungiwa selo Yule hakimu aliyenihukumu alinijia na kuniambia.“Siyo mimi, bali sheria za nchi. Nadhani safari hii dada yangu sio ndege mjanja tena.” Ilinichukua muda, lakini polepole akili ilizibuka wakati nikiwa jela mwezi wa pili, ambapo nilikumbuka lile tukio la mwaka 1975. Sijui nilihisi nini, lakini niliumia sana.
Sipendi kukumbuka nilivyoishi kwa huzuni kule jela, nikijutia ufedhuli ule nilioufanya kwa kijana yule wakati ule.Baada ya kumaliza kifungo changu, bado nikiwa na harufu ya jela nilikwenda nyumbani kwa hakimu yule na kubisha hodi. Alifungua mlango na kunikaribisha ndani kwake bila kinyongo. Nilimsalimia na kumwambia moja kwa moja. “Naomba radhi kwa yale niliyokufanyia wakati ule….”Yule hakimu alinikata kalma na kusema, “hukufanya lolote baya, ilikuwa ni sheria kweli. Kama ambavyo nami nimetimiza sheria za nchi.
Wala huna haja ya kuomba radhi, labda tu kwa sababu, wewe ulikuwa unalipa kisasi baada ya dada yangu kukukataa, wakati mimi sikutimiza wajibu wangu kwa kinyongo.”Niliinuka na kutoka nje, nikielekea kwangu. Maisha yalikuwa ndiyo kwanza yanaanza na uzee umeingia . Kisa kujisahau.
Hii simulizi nimependa sana. Ukitaka kujua nilipoipata basi waweza kubofya hapa

Wednesday, September 1, 2010

YATOKANAYO NA WASIFU WA DK. BEN CARSON

Dk. Ben CarsonDk
Nimependezwa sana na maoni ya wasomaji wa kibaraza hiki kuhusiana na mada niliyoiweka wiki iliyopita ya wasifu wa Dk. Carson.

Naomba nikiri kuwa maoni ya kaka yangu Mubelwa Bandio yalinifanya nijiulize maswali kadhaa ambayo ningependa kuwashirikisha wasomaji ili tutafakari kwa pamoja:

Maswali yenyewe ni haya yafuatayo:

*mama yake aliolewa akiwa na umri wa miaka 13 na mchungaji mzee kwa kukimbia shida za pale nyumbani kwao, ambapo pia aliachika na kuachiwa kuwalea watoto wawili pake yake.

*mama huyu aliishia darasa la tatu, ambapo sio kiwango kizuri cha elimu cha kujivunia, lakini kwa shida sana alilazimika kufanya kazi zaidi ya tatu ili ahakikshe anawatengenezea wanae hao future.

*Carson alikuwa mbumbumbu darasani, lakini kutokana namsimamo wa mama yake wa kuwalazimisha kusoma libarary, alipata mwamko na kusoma kwa bidii hadi kufikia kuwa daktari bingwa wa upasuaji.

Haya ni mafanikio makubwa kwa mama huyu (Mwanamke huyu) ambaye hakupata elimu kubwa. Je kuna wazazi wangapi ambao wana elimu ya kutosha tu lakini malezi kwa watoto wao yamewashinda?

Hata hivyo kuna jambo moja nimeliona kwa upande waserikali ya Wamarekani, nalo ni lile la kutambua mchango unaofanywa na wataalamu mbalimbali nchini humo.

Pamoja na Carson kupata tuzo nyingi, lakini Rais wa Marekani wa wakati huo G W Bush alitambua mchango wake na kumwalika Ikulu na kumpa tuzo ya Uhuru ambayo ni tuzo kubwa kutolewa nchini humo na Rais.

Je ni wataalamu wangapi au niseme ni Watanzania wangapi ambao wanatoa au wametoa mchango mkubwa hapa nchini hata wengine wakapoteza maisha yao au wakawa wameathirika kwa kiasi kikubwa lakini mpaka leo hii hawajawahi kupewa tuzo yoyote na Rais au hata kutambuliwa na Serikali?

Je hakuna haja ya kuliomba bunge lijalo litunge sheria itakayounda jopo la watu ambao kwa kuzingatia vigezo maalum wateue mtu mwenye sifa fulani kulingana na kile alichokifanya katika jamii na kukabidhi jina lake kwa rais ili apewe tuzo kubwa na ya heshima?

Tuzo hiyo isiwe ni tuzo tu ya kawaida bali pia iwe ni tuzo itakayoambatana na fedha za kutosha na kuwe na sherehe maaluma wakati wa kukabidhi tuzo hiyo.

Hilo naamini litawezekana kwani huko mikoani kuna watu wamefanya mambo makubwa lakini kutokana na urasimu yanaishia kwenye makabati ya wakuu wa wilaya au wenyeviti wa vijiji.

Nataka kuwasha moto......