Wednesday, May 25, 2011

NI MIAKA 26 SASA TANGU AZALIWE, LAKINI MIKASA, VISA NA VIJIMAMBO, VIMEENDELEA KUMTIA NGUVU.




Ilikuwa ni siku ya Jumamosi ya Sabato ya May 25, 1985, majira ya saa nne usiku ndipo binti huyu alipozaliwa. Alizaliwa akiwa na afya njema na uzito wa kuridhisha, ambapo siku iliyofuata mama wa binti huyu aliruhusiwa kutoka na kurejea nyumbani na kichanga chake.


Kalikuwa ni katoto kazuri ka kike ambako kalileta faraja katika familia ile ambayo tayari ilikuwa na watoto watatu wa kike na wawili wa kiume na hivyo kakawa kameongeza idadi ya watoto wa kike na kuwa wanne na kufanya idadi ya watoto katika familia hiyo kuwa na watoto sita.


Naambiwa kuwa binti huyu alikuwa na kipaji cha ajabu, hadi kiliwatisha wazazi wake, zile hatua za makuzi ya mtoto alizipitia lakini akiwa amewahi zaidi, kwa maana ya kuwahi kukaa, kusimama, kutembea na hata kuongea.


Akiwa na umri wa miaka miwili, tayari alikuwa amemudu kuwasha luninga na kubadilisha channel atakavyo, na si hivyo tu, alikuwa ni mdadisi na alikuwa ni mtoto anayependa kujifunza kila jambo.


Binti yule aliendelea kukua kwa umri na kimo huku akiwa na afya njema. Ni pale alipofikisha umri wa miaka mitano ndipo jambo lisilo la kawaida lilipomtokea binti huyu na kubadilisha kabisa historia ya maisha yake.


Inasimuliwa kuwa ilikuwa ni majira ya usiku ndipo binti huyu alipopatwa na homa kali sana, ambayo iliambatana na kile kinachoitwa degedege.


Kuumwa ghafla kwa binti yule kuliistua familia ile, na katika jitihada za kutaka kuokoa maisha yake alikimbizwa hospitali ya binafsi iliyopo jirani na pale kwao.


Alipofikishwa Hospitalini mama wa binti huyu alishauriwa na Daktari amkande na maji ya baridi ili kushusha joto la mwili ambalo lilikuwa limepanda kiwango cha kutisha. Daktari yule alitoa ushauri kuwa itakuwa ni jambo la hatari kuanza matibabu huku mgonjwa akiwa na joto kali kiasi kile.


Kwa kuwa Daktari alikuwa amemaliza zamu yake aliondoka nakuacha maagizo kwa Daktari na Muuguzi waliokuwa zamu akiwaelekeza hatua za kuchukua kulingana na maelekezo aliyoyaandika kwenye cheti.


Baada ya joto la mwili kupungua mama alimwita yule Muuguzi wa zamu na kumjulisha kuwa joto la mwil limepungua. Yule Muuguzi akiwa bado ana hali ya kuonesha kuwa katoka usingizini alisoma cheti na kisha akaenda kuchukua dawa.


Alirejea akiwa na vichupa vya dawa na sindano, na kumchoma sindano binti yule. Ile sindano ilisababisha binti kupoteza fahamu. Kuona hivyo alikimbia kumwita Daktari wa zamu.


Daktari wa zamu alipofika alimpima binti yule na kutoa maelekezo achomwe sindano nyingine haraka na kisha atundikiwe Drip. Maelekezo ya daktari yalifanyiwa kazi lakini binti yule hakuzinduka, ilibidi zifanyike Juhudi za kumhamishia Hospitali ya Rufaa ya Muhimbili ambapo alipelekwa moja kwa moja chumba maalum kwa wagonjwa mahututi (ICU). Alikaa kule kwa siku tano, na alipopata nafuu, akarudishwa kwenye wodi ya watoto na kuendelea na matibabu.



Binti aliendelea kupata nafuu, lakini kulikuja kugundulika kuwa amepatwa na tatizo lingine, nalo ni la kupoteza uwezo wa kusikia. Juhudi za Madaktari wa masikio kumtibu binti huyo zilishindikana, lakini mwishowe wakasema kuwa lile ni tatizo la muda tu, na limetokana na sindano ya kwinini aliyochomwa katika zahanati aliyotibiwa awali, hivyo ikiisha nguvu atarudisha uwezo wake wa kusikia.


Habari ile haikuwafurahisha wazazi wa binti, lakini wafanye nini, na limeshatokea. Walisubiri kwa taktiban mwaka mzima, lakini hapakuonekana dalili yoyote ya kupona wala kupata nafuu. Ni dhahiri sasa walizidi kupata wasiwasi, kwani binti yao kipenzi alikuwa hana uwezo wa kusikia na ule uchangamfu, udadisi, na utundu aliokuwa nao, ulitoweka. Hali hiyo iliwanyima usingizi.


Hawakukata tamaa, wakageukia kwenye maombi, lakini maombi yao hayakujibiwa haraka kama ambavyo watu wengi wangependa. Wakakata shauri kwenda nchini Afrika ya Kusini, kwa matibabu zaidi. Walipofika kule, Daktari aliyewapokea, alimfanyia binti vipimo na kwa kushirikiana na Madaktari wenzie walitoa pendekezo wamfanyie binti upasuaji, ili kurekebisha ile hali.


Lakini siku iliyofuata, ambapo ilikuwa afanyiwe vipimo zaidi kabla ya upasuaji, yule Daktari alibadilisha uamuzi na badala yake akatoa pendekezo binti anunuliwe vifaa vya kumuwezesha kusikia, (Hiring aid) halafu baada ya mwaka mmoja warudi kwa ajili ya vipimo zaidi.


Kwa kifupi walisema kuwa ni mapema mno kukimbilia upasuaji kwa kuwa waliamini kwamba kuna uwezekano mkubwa binti akapata uwezo wa kusikia baada ya dawa aliyochomwa kuisha nguvu.


Walirudi nchini, na kuendelea na maisha, na baada ya mwaka mmoja hali haikuonekana kutengemaa, waliporudi Afrika Kusini maelezo yalikuwa ni yaleyale. Waliambiwa warudi Tanzania na kama kutakuwa na tatizo basi waende Muhimbili, kwani tatizo la binti linaweza kutatuliwa hapo. Juhudi mbalimbali za kitabibu zimefanyika lakini bado hazijazaa matunda.


Hali hiyo imemfanya Binti huyo kuwa mbali na mawasiliano ya simu hususan za mkononi akitumia zaidi Ujumbe wa badala ya kuongea, kutokana na tatizo hilo. Mawasiliano mengine anayopendelea anapotaka kuwasiliana na ndugu jamaa, wanablog, wasomaji wa blog na marafiki ni kwa kutumia barua pepe, kwani hiyo imemjengea marafiki wengi na amekuwa akiwasiliana nao kiurahisi zaidi.


Leo hii ni miaka 26 kamili tangu alipozaliwa binti huyu, na ni miaka 21, tangu alipopatwa na tatizo hilo ambalo ki-ukweli bado linaaminika kuwa lilisababishwa na muuguzi ambaye alimchoma sindano ya kwinini, badala ya kumtundikia Drip, kama alivyoandikiwa na Daktari aliyempokea binti huyo.


Bado anawaza ni wangapi baada ya mkasa wake wamepata matatizo kama haya? Ni wangapi wamesababishiwa maumivu, ulemavu na hata kifo kwa maamuzi finyu ya kutofuata maelezo ya Madaktari?


Anawaza ni wauguzi ama Madaktari wangapi ambao wametenda makosa kama haya na kuonywa ama kuwajibishwa kwa namna yoyote ile ili matatizo wanayosababisha kwa jamii yasiwe kitu kinachotokea kila mara?


Anawaza ni wangapi ambao tofauti na yeye hawawezi kuendelea na masomo kwa kuwa hawawezi kupata HEARING AID kulingana na gharama zake? Na hivyo kushindwa kuonyesha vipaji vyao halisi kwa matumizi ya nchi na dunia?


ANAWAZA namna ambavyo mimi nawe tunaweza kuwa suluhisho la matatizo haya ambayo YANAUMIZA SANA. ..........


Hata hivyo hali hiyo haikumkatisha tamaa kwani alimudu kusoma katika shule mbalimbali za kawaida huku akitumia vifaa maalum vya kusikia, ambapo alimudu kufika hadi kidato cha sita. Binti huyu hakutaka kuendela na elimu ya juu, na badala yake aliamua kujiingiza katika biashara akiwa ni mjasiriamali mchanga lakini mwenye matarajio makubwa.


Si hivyo tu, bali pia amekuwa ni mwelimishaji katika tasnia ya Blog akiwa anamiliki Blog yake ambayo imekuwa ikiibua mijadala mbalimbali yenye kufurahisha, kuhuzunisha, kuelimisha na ujinga kidogo, lakini pia pamoja na yote anaamini kuwa blog hiyo imeleta changamoto na migongano ya mawazo, jambo lililowa “amsha” wengi na ndio maana akaiita VUKANI.


Hata hivyo hawezi kujivunia hapo aliopofikia katika tasnia ya Blog bila kuwataja wanablog wote wenye kumiliki blog za kiswahili, wasomaji wa blog, wazazi wake, marafiki na wale ambao kwa njia moja ama nyingine walifanikisha uwepo wa blog hiyo ya VUKANI. Hata hivyo HASITI kuwataja Kaka Markus Mpangala, kaka Mubelwa Bandio, na Dada Yasinta Ngonyani, hawa amekuwa akiwasumbua sana pale anapohitaji ushauri kabla ya kuweka bandiko katika kibaraza chake.


Asingependa kuwasahau Mzee wa Mataranyirato Chacha o'Wambura, Ngw'anambiti, Kamala Lutatinisibwa, Fadhy Mtanga, Christian Bwaya, Simon Mkodo Kitururu, Godwin Meghji, Evarist Chahali, Dada Subi, Faith Sabrina Hilary, Shaban Kaluse, Mwanamke wa Shoka Mija Sayi, Mariam Yazawa, Emuthree, Ramadhan Msangi, Salehe Msanda, Ma-Annonymacy............. na wengineo wengi, ambao kwa kweli wamekuwa mstari wa mbele katika kuifanya blog hiyo ya VUKANI kufikia hapo ilipo


WAKATABAHU


NI MIMI KOERO JAPHETI MKUNDI

Monday, May 16, 2011

HARUSI YA WAPEMBA.

Mbwembwe za nini? Kimya kimya tu Mwali akaondoka!



Siku ya Ijumaa ya wiki iliyopita, wakati niko nyumbani majira ya mchana akaja jirani yetu mmoja Mpemba akitaka kumuona baba. Kwa bahati mbaya baba alikuwa hajarudi kutoka katika shughuli zake za kuganga njaa, hivyo akamuachia mama ujumbe kuwa alikuja kutujuza kwamba mdogo wake anaolewa siku hiyo ya Ijumaa majira ya usiku baada ya swala ya Waislamu ya Insha. Alituomba tujumuike nao itakapofika hiyo saa mbili usiku ili kufanikisha shughuli hiyo ya ndoa.


Mie nilishangaa kidogo kwa kuwa tangu asubuhi pale kwa majirani zetu ambao nyumba yao iko mkabala na ya kwetu, kulikuwa kuko swari kabisa na hapakuonesha dalili yoyote kuwa kuna pilika pilika za kufungwa ndoa au Harusi. Kwa kawaida nafahamu kuwa nyumba yenye maandalizi ya Kufungwa ndoa huwa inakuwa bize na pilikapilika za hapa na pale hasa kwa zile shughuli zinazofanyikia nyumbani, kwa kawaida huwa ni lazima kunakuwa na shughuli mbalimbali zitakazowafanya hata majirani wajue kuwa kuna jambo hapo kwa wenzetu, lakini mweh! Kulikuwa kuko shwari tu kutwa nzima.


Ni kweli majira ya saa mbili hivi tukaona majamvi yanatandikwa kibarazani, na sie kama majirani, yaani mie, mama na baba tukaenda kuungana nao. Mie na mama tuliingia moja kwa moja sebuleni ambapo tulikuta pametandikwa majamvi na akina mama kadhaa wakiwemo baadhi ya majirani zetu walikuwa wamekaa na baba alifikia pale kibarazani ambapo aliungana na wazee wengine ambao walikuwa wamekaa pale nje. Kwa kawaida waislamu wanawake hawachangamani na na wanaume kwenye shuguli zao, na ni lazima mjitande ushungi. Waswahili wanasema ukienda kwa waroma basi vaa kama waroma, nasi yaani mie na mama tulijitanda ushungi.


Baada ya muda kidogo, tukasikia watu wakisalimiana huko nje, na mie ili nisipitwe, maana napenda sana kupekua mambo, nikajisogeza karibu na mlango, ili nione yatakayojiri hapo nje. Nilipata sehemu nzuri ambapo niliweza kuwaona watu waliokaa pale nje vizuri tu. Karibu watu wote pale nje walivaa kanzu, akiwemo baba yangu. Mzee mkundi naye anayo kanzu yake ambayo huivaa akipata mialiko ya aina hii.


Basi mara kikaletwa chetezo na ubani ukawekwa, wakanyanyuka wazee kadhaa na wakiongozana na kaka wa binti na kuingia ndani ambapo walielekea katika chumba ambacho alikuwa amewekwa huyo Bi harusi ambaye kiukweli sikumfahamu. Baadae niliambiwa kuwa alikuwa akiishi na dada yake huko Kinondoni na baada ya kupata mchumba ikabidi shughuli za posa na ndoa zihamishiwe kwa kaka yao mkbwa ambaye ni huyo jirani yetu, na ndio maana, wahudhuriaji wengi sikupata kuwafahamu.


Baada ya kitambo kidogo, wakatoka, na kurejea sebuleni. Nilisikia bwana harusi akiulizwa kama mara tatu hivi kuwa amekubali kumuoa huyo Binti ambaye alitajwa kwa jina la Salha kwa mahari ya elfu sabini na tano? Ambapo alishatoa elfu hamsini na kuna deni la elfu ishirini na tano. Bwana harusi mara zote alikubali.


Lakini jambo lililonifrahisha zaidi ni kile kiwango cha mahari, sikujua kama kuna watu bado wanatoza kiwango kidogo cha mahari kiasi kile. Sikusita kuonesha mshangao wangu, na mama mmoja aliyekuwa amekaa jirani namie akaniambia kuwa hata hivyo yule (Yaani bwana harusi) kagongwa, yaani katozwa kiasi kikubwa cha mahari, eti kwa kawaida waislamu hususan Wapembahutoza kiwango kidogo sana cha mahari hata kufikia elfu ishirini na tano!, ndio elfu ishirini na tano!


Nilimuangalia mama, nikamkonyeza kwa mbali, naye akatabasamu akijua ninamaanisha kitu gani, kwani wao kwa dada zangu watatu walioolewa, walilamba zaidi ya laki tano kwa kila mmoja! Na hapa nazungumzia tukio la miaka zaidi ya mitano iliyopita!


Sijui kati ya Fadhy, Markus au Kitururu, atakayebahatika kunichumbia atagongwa ngapi, maana kwa jinsi ugumu wa maisha ulivyopanda, sijui kama watamudu dau la Mzee Mkundi…………LOL


Haya baada ya kusomwa dua kadhaa na shughuli ikawa imeisha, na tukatangaziwa kuwa tusubiri Sadaka kabla hatujaondoka.


Mnajua ilikuwa ni nini? Mh! Tuliletewa chai iliyoungwa vizuri na viungo toka Pemba, na vijiandazi vidogo, baada ya hapo, shughuli ikawa imeisha, na jamaa mmoja akaenda barabarani na kudaka Hiace moja ya Kipawa akaikodi na kuja nayo pale, Bwana na Bi harusi walikaa mbele na wapambe walikaa nyuma kisha wakondoka kimya kimya hapakuwa na vigelegele wala nini. Nilipouliza kwa nini hapakuwa na shamrashamra, nilijibiwa kuwa ni kharamu. Mweh! Mwenzenu nilishangaa kweli, maana kusema kweli ile ilikuwa ni mara yangu a kwanza kuhudhuria shughuli ya ndoa ya kimya kimya.



Nimejifunzazjambo kwa kweli.

Saturday, May 7, 2011

JAMAA AKASAHAU KIFANYIO NDANI YA GARI!


Waliamua kumalizia hapa


Jana niliamua kutoka na kuwatembela rafiki zangu ambao nilipoteana nao kwa muda mrefu sasa. Ilikuwa ni furaha iliyoje kukutana na rafiki zangu hawa ambao baadhi nilisoma nao na wengine nilijuana nao kwenye mishe mishe za kutafuta Ngawira. Baada ya kupigiana simu na kutumiana ujumbe wa simu zetu za kiganjani, tukakubaliana tukutane kwenye mghahawa mmoja ulioko maeneo ya Masaki maarufu kwa kutengeneza Pastries unaojulikana kwa jina la Epidor.




Nilifika pale majira ya saa kumi za jioni na kuwakuta wenzangu wanne wameshafika, na walikuwa wakiendelea kupashana habari za hapa na pale. Nilijumuika nao, na tukaanza kukumbashana stori zetu za zamani hususana vituko tulivyokuwa tukifanya wakati tulipokuwa shule na vituko vya Waalimu wetu. Si mnajua wanafunzi wa zamani wanapokutana hukumbushana ujinga wao wa zamani?


Wakati tukiendelea na stori zetu akaja Shoga yangu Zulfa na kijana mmoja aliyemtambulisha kuwa ni Binamu yake anayejulikana kwa jina la Kishindo, Alikuwa ni kijana mtanashati lakini mwenye maneno mengi. Kwa muda mfupi alikuwa ameshachukua nafasi ya kuwa mzungumzaji mkuu akanifunika hata mie, ambaye najulikana kama kiranja wa kupiga soga. Alikuwa ni mtu wa masihara na mwepesi kudakia jambo na kuligeuza Comedy, naamini mnawajua watu wenye tabia za Comedy au Chale Chaplin ambao ukikaa nao ni lazima ucheke. Basi ngoja nifupishe maelezo, kwa kifupi ni kwamba wakati tunapiga tiralila zetu, akatupa stori mbili tatu hivi ambazo zilituvunja mbavu wote tuliokuwa pale, lakini kubwa zaidi zilituacha na maswali. Moja ya stori ambayo ningependa kuwashirikisha ni hii ya KIFANYIO. Tega sikio…………



Kuna jamaa mmoja alikuwa na rafiki yake anayeishi maeneo ya Ukonga naomba nimtambulishe kwa jina Ulimbo , sasa siku moja wakapanga na rafikiye anayeishi maeneo ya Tabata, (naomba huyu tumuite Kizito) wakutane kwenye Baa moja maneo ya Mwenge wajumuike pamoja na kupata moja moto moja baridi. Kizito alifika pale na usafiri wake na akamkuta Bwana Ulimbo ameshafika zamani . Wakati wanendelea kupata kilaji a.k.a ugimbi, Bwana Kizito akapata mgeni, hakuwa mwingine bali mfanyakazi mwenzie ambaye alifika mahali pale kama nasibu tu (Coincidence), Bwana Kizito akamtambulisha yule Binti kwa Bwana Ulimbo ambaye hakuwa ameoa, na kisha wakajumuika pamoja na kuendelea kupata vinywaji.



Muda wote wakati wanakunywa, Ulimbo alionekana kuvutiwa na yule Binti, hivyo muda wote alikuwa bize akimdadisi kutaka kumjua zaidi. Walizoeana ghafla na hatimaye walibadilishana namba za simu. Ilipofila usiku, yule Binti aliomba kuondoka, lakini Ulimbo akaomba kumsindikiza, walipofika nje ya Baa, yule Binti akamuaga Ulimbo kuwa anawahi kupanda Daladala kwani ilikuwa ni usiku majira ya saa nne hivi.


Ulimbo alimuuliza kama anaishi wapi, yule Binti alimjulisha kuwa anaishi Mwananyamala, Kizito alimuomba amsubiri pale nje, akamuage Bwana Kizito ili aje amsindikize. Ulimbo alikwenda kumuomba Kizito Gari lake kwa kuwa yeye hakuwa na usafiri ili amsindikize kimwana maeneo ya Mwananyala. Kizito alimpa gari lakinialimtahadharisha kuwa aendeshe kwa makini ili kuepuka ajali. Ulimbo alimhakikishia Kizito kuwa atarudi salama. Alichukua gari na kuondoka na yule binti kuelekea Mwananymala, walipofika njiani Ulimbo alisimamisha gari kwenye duka la dawa na kumuomba binti amsubiri ili akanunue dawa, kwani mdogo wake anasumbuliwa na Malaria na kuna dawa aliandikiwa angependa kumnunulia.



Baada ya muda alirejea ndani ya gari, na kuondoka, walipofika maeneo ya Mwananyamala, Ulimbo alisimamisha gari tena na kudai kuwa anajisikia kwenda haja ndogo, yule binti alimshauri waendelee na safari kwani nyumbani kwake anapoishi sio mbali hivyo wakifika atajisaidia hapo kwake kuliko kujisaidia njiani. Ulimbo alikaidi ushauri wa yule binti akidai kuwa amebanwa. Alishuka na kuzunguka nyuma ya gari aliporudi akazima gari na hadithi ikageuka, ilikuwa ni kama Swala ndani ya himaya ya Chui, Ulimbo hakukubali kumrejesha binti yule bila kumuonja, na kweli baada ya kutumia maneno matamu kama asali hatimaye binti akajikuta akikubali kumpa ulimbo utamu lakini kwa masharti ya kutumia Kifanyio a.k.a Condoms.



Kumbe Ulimbo aliposimama kwenye duka la Dawa hakuwa akitaka kununua dawa bali alitaka kununua Condoms kwa kuwa alishayapima maji na kuyaona kuwa hayakuwa na kina kirefu hivyo isingemuwia vigumu kuvuka hata bila mtumbwi (Yaani isingemgharimu kutafuta Guest House ya chapchap).


Sharti la kutumia Kifanyio lililotumiwa na Binti halikuwa kikwazo, Ulimbo alishakuwa nazo zamaani, (Wanaume waasherati huwa wana akili za ziada) Zoezi likafanyika mle mle ndani ya gari kisha akampeleka Binti nyumbani na kumshusha na kuagana kwa Mabusu kemkem. Alirudi pale Baa na kumkuta Kizito akiwa na ameungana na jamaa wengine wawili, hivyo wakaendelea kupata vinywaji hadi usiku wa saa sita hivi. Kwa kuwa Kizito ni mtu na familia yake akawaaga wenzie na kuondoka zake kurudi nyumbani.




Asubuhi mkewe Kizito alimuamsha mumewe na kumuomba funguo za gari ili waende Kanisani, kwani Kizito alidai kuchoka hivyo alimuomba mkewe aende na watoto, yeye wamwache apumzike.Mkewealipofika kwenye Gari aliamua kulifanyia usafi kwa kutoa Kapeti za gari na kuzikung’uta na kisha kuzirejesha ndani ya gari, alianza na kapeti za mbele na alipotoa kapeti za nyuma……….. Lahaullah……….. akakutana na Kifanyio kilichotumika kikiwa bado kina ubichi………….


Mwanamke yule alikurupuka na kwenda ndani kumuita Mumewe na kumtoa nje….walipofika kwenye Gari alifungua mlango wa gari wa nyuma na kumuonesha mumewe kile Kifanyio kilichotumika…… Mumewe alishikwa na Butwaa na kujikuta akitamka…………….. "Aaaaaaakh Ulimbo umeiponza masikini"…………… Msimuliaji hakufanya hitimisho, alituachia tafakuri kuwa, Je mume atawezaje kumuelewesha mkewe mpaka amuelewe?

Wednesday, May 4, 2011

JIONI HII PALE POSTA JIJINI DAR




Shiranga la foleni Jijini Dar linatisha, maana leo imenilazimu nijitulize ndani ya mjengo huo jirani na kupata kinywaji barrrrdi ili kuvuta muda foleni iishe, lakini hiyo bei ya vinywaji ni balaa tupu kwa siye tuliyozoea soda za mia tano, roho inauma kweli..............wanapaita Holiday Inn.