Friday, September 30, 2011

MABALAA HUMUANDAMA MTOTO WA KIKE TANGU AKIWA TUMBONI………!






Tatizo hili hufahamika kama Female Infanticide, yaani mauaji ya kukusudia yanayofanywa kwa mtoto wa kike. Achilia mbali kile kitendo cha mtoto kuuawa muda mfupi tu baada ya kuzaliwa, utelekezwaji wa mtoto wa kike mara tu anapozaliwa na kutoa mimba baada ya ugunduzi kwamba, ni mtoto wa kike, zote ni njia za kumuondoa mtoto wa kike duniani. Tatizo hili liko katika jamii zote zinazomchukulia mtoto wa kike kama balaa na yule wa kiume kama Baraka kwa familia.


Kwa hapa nchini mtoto wa kike huuawa kwa njia isiyo ya moja kwa moja. Watoto wa kike hudharauliwa na kuachwa linapokuja swala la elimu katika familia. Ukichunguza hata wewe utabaini kwamba, katika familia nyingi, ambapo watoto wa kiume wamepata elimu bora, watoto wa kike katika familia hizo wamepuuzwa na hata kutopewa kabisa elimu.


Watoto wa kike, haswa wale wanaozaliwa nje ya ndoa wametelekezwa kirahisi, wamekataliwa na baba zao kirahisi, ukilinganisha na watoto wa kiume. Idadi ya watoto wa kike wanaokufa kutokana na kutelekezwa na kukataliwa na baba zao ni kubwa kuliko ya watoto wa kiume. Hata zile kesi nyingi za watoto kukataliwa na baba zao zinahusisha watoto wa kike zaidi.


Ni jambo la kushangaza kwamba ndoa ambayo ina watoto wa kike watupu hutazamwa kwa bezo na dharau ukilinganisha na ile yenye watoto wa kiume watupu. Hata wale wanawake wanaozaa watoto wa kike watupu hujihisi vibaya na kuamini kwamba walistahili kuzaa watoto wa kiume pia.


Kwa maeneo ua vijijini na katika familia masikini, watoto wa kike hutazamwa kama, ‘biashara ya kesho’ ambapo watauzwa kwa njia ya mahari. Kwa hiyo thamani yao ni kuolewa, ni ile ya kibidhaa na sio kibinadamu. Na ndio maana mtoto wa kike anaposhindwa kuolewa huanza kuonekana kama mzigo usio na thamani, na hata kuzongwa hutokea.


Ili kujinasua na tatizo hili, msichana huenda kwa mwanaume yeyote kama kwa kujilazimisha. Kila mtu anajua kuhusu wazazi hapa nchini, ambao wamekuwa wakiwalazimisha binti zao kurudi kwenye ndoa za mateso kwa hofu ya kurejesha mahari. Kinachotokea ni binti hao kuuawa na waume zao. Ni wazi hii ni njia ya makusudi ya kuwapunguza wanawake, bila kujali mtu ataieleza vipi……………….


Chanzo........Jamii Forum


Monday, September 5, 2011

MCHUMBA ANGU YUKO FINLAND!

Naelekea Uzeeni sasa!




Ni miaka 16 sasa tangu nifahamiane naye, alikuwa ndio kwanza amemaliza kozi yake ya uhasibu na kuajiria katika ubalozi wa mmojawapo ya nchi za Ulaya hapa nchini.


Alipoanza kujitegemea, alipata nyumba iliyoko jirani na nyumbani kwetu, na huo ukawa ndio mwanzo wa kufahamiana naye. Alikuwa akijiheshimu sana na hakupenda kujichanganya na watu. Alitumia muda wake mwingi nyumbani kwake na kama akiamua kutoka mara nyingi alipenda kuwatembelea ndugu zake a marafiki zake waishio maeneo ya mbali.


Nilibahatika kufahamiana naye wakati fulani ilipotokea shida ya maji, na kwa kuwa, nyumbani kwetu kulikuwa na kisima, alikuja kuomba msaada wa maji na huo ukawa ndio mwanzo wa kufahamiana.


Naam, urafiki wetu ulimea na kukua, kiasi kwamba tulikuwa tukitembeleana mara kwa mara, alitokea kufahamiana na wazazi wangu pia na walimkubali sana, kutokana na jinsi alivyokuwa akijiheshimu.


Jambo moja lililonishangaza, ni kwamba sikuwahi kumsikia akizungumzia juu ya mahusiano yake, nilishikwa na udadisi na siku moja nikamuuliza kma anaye mchumba. Alinijulisha kuwa mchumba ake yuko Finland kwa masomo, nilimdadisi zaidi kama yuko huko kwa muda gani, akanijibu kuwa ni miaka miwili sasa. Alinijulisha kuwa mchumba ake huyo anasoma kule na itamchukua miaka 3 hadi kumaliza masomo yake na ndipo atarejea nchini na kuungana naye.


Ukweli ni kwamba rafiki yangu huyu alikuwa akifuatwa na wanaume wengi tu tena wa kutosha wakitaka kuwa na uhusiano naye, nadhani ni kwa sababu alikuwa ni mrembo sana, lakini alikuwa akiwakataa kwa maelezo kwamba, anaye mchumba tayari ambaye yuko nje ya nchi kwa masomo.


Nilimuheshimu sana kwa msimamo wake. Mwaka uliofuata binti yule alihama katika numba ile na kuhamia maeneo ya Sinza. Nilipoteana naye kwa takriban miaka 16. Ni hivi karibuni nimebahatika kukutana naye, alionekana dhahiri kuwa umri umekwenda.


Alinikaribisha nyumbani kwake maeneo ya Kimara, alinijulisha kuwa amebahatika kujenga nyumba yake mwenyewe. Wiki iliyofuata nilimtembelea nyumbani kwake. Alikuwa amejenga nyumba nzuri na alikuwa ameizungushia ukuta na kuweka geti. Alinikaribisha sebuleni kwake. Alinitambulisha kwa mdogo wake wa kike aliyekuwa akiishi naye ambaye alikuwa akisoma Chuo Kikuu Dodoma, na pia kwa msichana wake wa kazi.


Nilishikwa na udadisi wa kutaka kujua alipo mume wake, na labda kama ana mtoto. Alicheka sana na kisha akanishika mkono na kunipeleka chumbani kwake. Alikuwa na chumba kikubwa chenye nafasi ya kutosha na pia kulikuwa na meza kubwa ambayo ilikuwa imepambwa vizuri na vifaa vya ofisini pamoja na lap top, kwa ajili ya kazi zake.


Aliniacha kwa muda ili niridhishe macho yangu, kisha akaanzisha mazungumzo.


Mwenzangu, alianza simulizi yake, …….. unadhani kipindi kile wakati nakwambia kuwa ninaye mchumba na yuko masomoni Finland ilikuwa ni kweli, la hasha, haikuwa kweli, bali nilikuwa nadanganya tu kwa sababu sikutaka kusumbuliwa na wanaume. Si unajua wanaume wa siku hizi wanapenda kuwachezea wanawake!, sasa mimi kwa kuliepuka hilo nikaona nitumie mbinu hiyo ili kuepuka usumbufu. Nilibaki mdomo wazi….


Basi bi dada………… aliendelea…….. nilipohama pale Mikocheni, na kuhamia Sinza, niliendelea na msimamo mwangu, sikuwapa wanaume nafasi, nilikuwa na malengo yangu na nilitaka nihakikishe yanatimia.


Ni malengo gani hayo…… nilimdadisi……


Kwanza, nilitaka nijenge nyumba yangu mwenyewe, na pia ninunue gari na kuanzisha biashara zangu na sasa nimetimiza malengo yangu, sasa tatizo linakuja.


Tatizo gani tena………..nilimuuliza.


Sitongozwi na wanaume……… na wananiogopa!..............haki ya Mungu Koero, yaani nina wakati mgumu kweli.


Mh! Niliguna…… wewe unadhani tatizo ni nini? Nilimuuliza,


Sijui sababu, lakini, naona kama vile hakuna anayevutiwa na mimi, najitahidi kuongea na wanaume lakini tunaishia kupiga stori tu, na wengine wananitongoza lakini ni waume za watu. Mwenzio naogopa kweli, mpaka nimejenga wasiwasi kuwa labda nimelogwa.


Mh……….Nilishusha pumzi……….Vumilia dada Jane, utampata atakayekufaa, muombe sana Mungu, atakupa mume aliye mwema, nilimpa moyo.


Mh, Koero, umri huu? Unajua mwakani natimiza miaka 39, mwenzio nazeheka hivyo, atanioa nani…. Nimekuwa nikibadilisha makanisa kama nini, katika kuombewa na kote huko naona maombi yangu hayajibiwi.


Marafiki zangu karibu wote wameolewa na wanaishi na waume zao, mimi tu, sijui nina mkosi gani…. Nilimuona Dhahiri machozi yakimlengalenga….


Nilimpa moyo na kumshauri asikate tamaa. Nilimwambia arudi kwenye kanisa lake la awali na ajiunge na kwaya ikiwezekana ashiriki kwenye kamati mbalimbali za kanisa na zitakazomfanya akutane na watu mbalimbali. Nilimwonya awe makini sana na wanaume walaghai kwani wapo wengine wanawezakutumia mwanya huo kummimbisha na kumtelekeza.


Alikubaliana na mimi na tukamaliza mazungumzo yetu kisha nikaondoka kurejea nyumbani…….. mweh dunia hii……. Habari ya dada Jane si kwamba tu ilinishangaza, bali pia ilinisikitisha. Yaani zaidi ya miaka 16 aliishi kwa kusema uongo ili kuwakwepa wanaume! Alichokuwa akikiogopa kwa wanaume ni kitu gani hasa?


Nilibaki nikijiuliza maswali chungu mzima na sikupata majibu. Ndio maana mie nasema wazi, jamaniee sijaolewa na wala sina mchumba Mbeya, Lundu Nyasa, Marekani wala Ulaya, niko Single, ready to mingle….leteni maombi na sifa zenu mtajibiwa…………LOL


Friday, September 2, 2011

WANAUME BWANA, HIVI MKIONA UCHI WA MWANAMKE MNAPATA NINI?

Wanaume wengine hata wakiona hivi huchanganyikiwa!



Kuna wakati huko Berlin, nchini Ujerumani, kulikuwa na unesho ambapo wanawake walikuwa wakionesha maungo yao kwa malipo. Wanawake hao walikuwa wakionesha maungo hayo kwa wanaume ambao wanaamini kwamba, kuona sehemu uchi wa mwanamke ndicho kilichowaleta hapa duniani.


Hebu sikia ujinga huo zaidi. Waandaaji wa onesho hilo ambalo lilihusisha wanawake wapatao 100 wa umri wa miaka 19 hadi 65 walilazimika kuwaita Polisi ili kudhibiti midume iliyokuwa ikifanya fujo wakati wa kukata tiketi kila mmoja akitaka awe wa kwanza kuingia kwenye onesho hilo.


Kila mmoja alikuwa akitaka awahi yeye kuona sehemu za siri ambazo bila shaka mkewe na watu wengine wa jinsia ya kike wanaomzunguka wanazo!


Mwandaaji wa onesho hilo, Vanessa Beecroft, ambaye ndiye mgunduzi wa njia hii ya kujipatia fedha kirahisi kutoka kwa wanaume hao wasio na haya, hufanya maonesho haya kwa jina la VB55 kwa nyakati na miji tofauti Ulaya.


Msije mkashangaa siku akija na huku Afrika kujichotea mamilioni ya dola, au akajitokeza mjanja mwingine huku Afrika na kuanzisha hayo maonesho, naamini wanaume watauana wallahi.