Friday, August 7, 2009

TANZANIA NA SIASA ZA KINYUMENYUME

Wasomaji wapendwa wa blog hii ya VUKANI, naona nimekuwa mtu wa kudesa siku hizi.
Hii nayo nilikutana nayo katika mtandao wa Jamii Forum, kama kawaida yangu nimeona si vibaya wasomaji wa blog hii nao wakitoa mtazamo wao..................


Badala ya kijenga barabara ili ziweze kupitika, Wananunua magari makubwa (heavy duty vehicles) ili kuwawezesha kupita katika barabara hizo mbovu. Bila kuangalia kuwa kuhudumia magari hayo ni inagharimu kiasi kikubwa sana cha pesa ya wapiga kula. Mfano chukulia gari aina ya Toyota Land Cruiser 4000cc or above, kiasi cha mafuta ambacho gari hili linatumia chukulia mfano kutoka Dar es Salaam mpaka Arusha (One way), kwa safari hiyohiyo mtu atakaye tumia Toyota RAV4 atakwenda na kurudi (round Trip) kwa kiasi kile kile cha mafuta na pengine kubakia na kiasi kidogo cha kuzungukia kilomita kadhaa akishafika. ukiachilia mbali na huduma nyingine kama services za kila mwezi /mwaka za magari haya ambazo nazo zinakwenda kwa karibia uwiano ule ule na gari kama RAV4.

Badala ya kusimamia vizuri vyanzo mbali mbali vya mapato na kuhakikisha kuwa zinatumika ipasavyo na katika uwiano unaeleweka, mfano kuboresha huduma za afya, elimu na mishahara na kuhakikisha kunakuwa na uwiano unaokubalika. Hii itasaidia kuboresha maisha ya raia na utawala wa kuheshimu sheria na kwa kiasi kikubwa itasaidia kupunguza uhalifu.

Badala yake njia ya kupunguza uhalifu hasa ujambazi, serikali inaona ni kutoa mafunzo na kuajili askari zaidi. Hata uwiano ukiwa askari 1 kwa raia 1 hii kitu haitafanikiwa kupigana dhidi ya uhalifu kama hali ya maisha ya wananchi itandelea kuwa kama ilivyo kwani hata hao askari ni sehemu ya jamii hii pia na machungu ya maisha na wao yanawapata na uozo unaendela wa viongozi na wao wanaona pia. Sana sana itakuwa ni kufunza majambazi zaidi kwani katika matukio ya ujambazi yanatotokea hivi sasa wahusika wakuu ni askari, ukichukua matukio 5 ya uhalifu/ujambazi wa kutumia silaha matukio 3 kati ya hayo askari (ama askari wastaafu) wamehusika moja kwa moja na matukio.

Badala ya kurekebisha maisha ya vijijini na kupeleka huduma muhumu ili kupunguza tatizo la vijana wazururaji mijini na wengine kuishia kwenye umachinga badala yake wanaajili mgambo kwa ajili yakukabiliana na wachuuzi hao wa bidhaa ndogondogo na Mama lishe.

Badala ya kupima viwanja vingi na kuuza kwa bei ya kawaida kwa raia wote na hatimae watu waweze kununua viwanja hivyo na wajenge kutokana na mipango miji badala yake wanapima vichache na kuviuza kwa bei ya kulinganisha na ile wanayouza watu binafsi. Wanasahau kuwa wao ndio wanatakakiwa wasimamie na kutetea haki ya kila mmoja ya makazi bora yaliyokatika mpangilio badala ya watu wachache tu kusimamia soko hili na kutuwekea bei za ajabu ambazo hauwezi kuziangalia hata mara mbili. Matokea yake kila siku watu wanavamia misitu na kuendelea kujipimia bila mpangilio.

Badala ya manispaa kutumia kodi vizuri za wananchi na kubuni namna gani wanaweza kuweka mazingira safi hasa yale ya ufukweni badala yake wanapiga marufuku watu wasitumie maeneo hayo kwa kisingizio kuwa wanayachafua, kuzuia kuogolea ufukweni (beach), ama kuwa maeneo hayo kwa ajili kupunga upepo.

Badala ya kusikiliza malalamiko ya wanafunzi hasa wale wa vyuo vya elimu ya juu na kuyafanyia kazi wanapuuzia na wanafunzi wakigoma kudai maslahi hayo, wanaishia kuitiwa polisi na kufukuzwa vyuoni na kisha kupewa masharti ya ajabu ajabu kama kuandika barua ya kujieleza na kuorodhesha majina ya waanzilishi wa mgomo wanasahau madai ya mgomo huo ambao ndio mzizi.

Badala ya kufidia wananchi wanaoathirika kutokana na afya zao na maeneo yao kuharibiwa vibaya hasa yale yaliyo katika migodi na wengine kupoteza kazi zao ama kutolipwa mishahara yao kwa muda mrefu, badala yake wanafikiria namna ya kuwalipa fidia watu wachache mabilioni ya shilingi (wawekezaji feki wa migodi hiyo. Mfano KIWIRA).
Kuna mambo mengi sana hawa jamaa wanafanya kinyume na hali halisi.. mnaweza kutoa michango yenu na kuendeleza hiyo list ya REVERSE GOVERNANCE ya serikali yetu...

2 comments:

Masangu Matondo Nzuzullima (MMN) said...

Makala nzuri sana dada Koero na hilo la kudesa lisikupe shida. Nani asiyedesa? Ndiyo mfumo wetu wa elimu ati! (una bahati ulikimbia mlimali kungali mapema vinginevyo ungedesa sana!)

Kuhusu ujambazi pengine Tanzania inabidi ijifunze kutoka Marekani. Marekani sasa ina tatizo kubwa la uhalifu na wamejenga magereza mpaka wamechoka. Imefikia hatua sasa baadhi ya majimbo kama California yana bajeti kubwa ya magereza kuliko bajeti ya elimu. Utashangaa zaidi ukiangalia mchakato wa hawa wafungwa. Zaidi ya nusu ya wafungwa wote walioko magerezani hapa Marekani ni weusi pamoja na kwamba weusi ni karibia asilimia 13 tu ya jumla ya watu wa taifa hili. Kwa nini watu weusi ndiyo wanarundikana magerezani? Ni kutokana na siasa za kibaguzi ambazo zinamnyima mtu mweusi nafasi sawa katika huduma muhimu za kijamii kama elimu, afya na ajira. Matokeo yake Wamarekani weusi ndiyo wanaongoza kwa umasikini. Leo hii mtoto mweusi ana uwezekano mkubwa wa kutomaliza high school mara sita zaidi kuliko mtoto wa kizungu, tineja mweusi ana uwezekano wa kupata mimba zaidi ya mara nane kuliko mwenzake mzungu, kuvuta bangi na madawa ya kulevya, kujiunga na magenge ya uhalifu n.k. Hata wazungu wengine sasa wameanza kusema ukweli kwamba japo siasa zao za kibaguzi za muda mrefu zimefanikiwa sana katika kumsikinisha mtu mweusi, imefikia hatua sasa hata wenyewe hawana furaha kwani kama sehemu kubwa ya pesa inabidi zikahudumie wafungwa, kwa namna moja au nyingine na wao pia wanaathirika kwani huduma zingine zinaathirika pia. Ndiyo maana walipitisha haya mambo ya upendeleo (affirmative action) kwa watu weusi na wengine ambao sio wazungu kuweza kuwarahisishia kidogo uwezekano wao wa kujiunga na vyuo vikuu, kupandishwa vyeo n.k. Lakini hii was too little and too late, na majimbo mengine ama hayakukubaliana na siasa hiyo ya upendeleo ama yameshaifuta tayari. Hitimisho: Nafasi sawa katika huduma za kijamii na hasa ELIMU ndiyo njia pekee ya kupunguza uhalifu. Unapokuwa na watu wachache matajiri sana na wengi ni masikini kabisa hohehahe kiasi kwamba hata hawawezi kula milo miwili kwa siku achilia mbali uhakika wa kupata huo mlo mmoja kama ilivyo Tanzania kwa sasa, hata kama ungewafanya watu wote kuwa mapolisi haingesaidia na pengine wataanza kuibiana wao kwa wao. Kama mambo hayatarekebishwa, hata hao hao wenye mashangingi muda si mrefu hawataona tena raha ya kuyaendesha na hayo mahekalu waliyojijengea, hata waweke ulinzi wa aina gani hayatawapa amani. Mtu mwenye njaa (wakati wewe unakula na kutupa jalalani), mtu ambaye hajui mtoto wake kama atasoma sekondari (wakati wewe watoto wako wanasoma Ulaya)tena kwa kutumia pesa zile zile zilizopaswa kumsomesha mtoto wa huyu masikini, hatatishwa na ulinzi na mageti. Mambo ni lazima yabadilike vinginevyo tunakoelekea si kuzuri.

Mzee wa Changamoto said...

Sasa nilitaka kutoa maoni ya makala, na nimesoma maoni ya Kakangu Prof Matondo nikajikuta nataka kutoa maoni kuhusu maoni yake kwani yameguza kuhusu makala. Na sasa niko tayari kutoa maoni najikuta ntaishia "kudesa" maoni ya Profesa na sanasana ntamchosha msomaji kwa kurudiarudia maneno.
Ila serikali yetu ndio hiyo wapendwa. Ambayo inahitaji KUBADILISHWA kwa namna yoyote ile ili kuiweka sawa.
Ni hayo Dadangu. Nisije "desa" mdeso wako.
Much Luv