Tuesday, February 22, 2011

HEBU SOMENI HII YA MMASAI KUTOKA KWA BIBI KOERO

Hapo zamani kidogo kulikuwa na jamaa mmoja alikuwa ni mwizi maarufu wa mifugo maeneo ya huko upareni. Basi alfajiri moja katika harakati zake za wizi akaamua aende kuiba kwenye maboma ya wamasai.

Wakati yuko kwenye harakazi za kuiba, mmasai mwenye ng’ombe akaamka na kuanza kumkimbiza akiwa na shoka mkononi, jamaa yule alikimbia kwa nguvu zake zote lakini kila akigeuka anaona shuka nyekundu ya mmasai ikipepea nyuma yake

Jamaa akajua hawezi kupona mbele ya mmasai yule akaamua kupanda mti mreefu ili kujiokoa. Yule mmasai alipofika katika mti ule aliopanda mwizi wake, akaamua kuukata ule mti ili aweze kumpata mwizi wake kiurahisi. Mwizi alipoona Yule mmasai akiukata ule mti kwa kasi ya ajabu, akajua kuwa siku zake zimetimia kama wahenda wasemavyo siku za mwizi ni arobaini, akajua arobaini yake imefika, ndipo alipomwambia Mungu. “Mungu………nimekuwa nikikuomba mambo mengi na umekuwa ukinisaidia, lakini hili la leo hutaliweza, na kwa kweli sitakulaumu maana huyu Mmasai amepania kweli na sina pa kukimbilia, naamini siku zangu za kuwepo hapa duniani leo zimetimia .”

Alipokwisha kusema hivyo, mara wakapita Wamasai wengine na walipomuona Yule mmasai mwenzao akikata mti ili kumpata mwizi wake, wakamwambia, “Wewe unahangaika na huyo mtu aliye juu ya mti, wakati hana kosa lolote, kuna wezi wamevamia kwenye Boma lako na wameondoka na ng’ombe wote walioko zizini.” Yule mmasai aliposikia hivyo aliacha shoka likining’inia pale kwenye mti na kutimua mbio kurudi nyumbani kwake ili kunusuru ngombe wake wasiibiwe.

Huku nyuma Yule mwizi alisaajabu muujiza ule wa kunusurika kwake, akamwambia Mungu, “Ee Mungu, hakika hakuna lisilowezekana mbele zako, nakushukuru kwa kuninusuru na kifo na kuanzia leo nitakuomba kwa ajili ya mambo mema, ambayo yataniepusha na dhambi, na kuniweka huru”

Na kuanzia siku ile Yule mwizi akawa ni muumuni mzuri baada ya kuacha wizi na kuwa raia mwema.

Kwa mujibu wa Bibi Koero, simulizi hii inaufundisha kuwa kamwe tusimpangie Mungu kwani yeye ndiye muamuzi wa yote.

6 comments:

Rachel Siwa said...

Ni kweli kabisa Mungu si wa mambo madogo tuu!Ubarikiwe bibi Koero kwa mafundisho haya!

Yasinta Ngonyani said...

Mungu ni muweza kweli kabisa...Bibi Koero Ahsante sana kwa hadith/fundisho hili!!!

emu-three said...

Visa kama hivi ni vizuri sana, hasa kwa watoto wetu...NI HEKAYA ZENYE MAFUNZO!

PASSION4FASHION.TZ said...

Koero naomba uanze kutunga vitabu vya hadithi kama hizi kwa ajili ya mafundisho kwa watoto,unakipaji cha utunzi kitumie.

Leo nimefurahi sana kupata simulizi kutoka kwa bibi Koero nilizimmiss sana,ubarikiwe wewe na bibi.

Simon Kitururu said...

Stori hii nzuri kweli kama mtu unaamini MUNGU!

Goodman Manyanya Phiri said...

Pia tunafundishwa hapo kwamba Mungu hasaidii watakatifu wake peke yao: hata wafanyawovu nguvu zao wanaruhusiwa na Yeye, sio naShetani asiyekuwa na nguvu yoyote ila tu ile nguvu ya undanganyifu tu!