Monday, June 20, 2011

NIMEULIZWA TENA HILI SWALI: KWA NINI NILIAMUA KUITA BLOG YANGU VUKANI?

Vukani


Blog hii itakuwa ikiibua mijadala mbalimbali yenye kufurahisha, kuhuzunisha, kuelimisha na ujinga kidogo. Pamoja na yote naamini pia italeta changamoto na migongano ya mawazo, ndio maana nikasema VUKANI.




KWA NINI NILIAMUA KUIITA BLOG YANGU, VUKANI?


Neno VUKANI nimelitohowa kutoka katika lugha ya mama yangu ya kipare.
Neno hili lina maana ya AMKENI, nadhani kaka Mkodo Kitururu atakuwa anafahamu vizuri kwa kuwa ni lugha yake.

Nakumbuka wakati fulani nilikwenda likizo kijijini huko upareni kuwasalimia bibi na babu yangu wanaomzaa mama yangu, basi kila siku asubuhi bibi alikuwa na kawaida ya kutuamsha ili tusali pamoja na alikuwa akitumia neno Vukani. Nilipouliza maana yake nikaambiwa ni Amkeni au kwa msisitizo wa kiingereza WAKE UP. Basi kuanzia siku hiyo nikatokea kulipenda sana hili neno, sijui ni kwa nini lakini lilikuwa linanihamasisha sana kuamka kifikra badala ya kuamka asubuhi tu.

Wakati nilipokuwa nafungua Blog yangu nilikuwa tayari nimeshachagua jina hili, na cha kushangaza nilipoliingiza kwenye mtandao nikagundua kwamba neno hili linatumiwa na makabila mawili ya Ki Zulu na Ki-Xhosa ya nchini Afrika ya Kusini, likiwa na maana moja, yaani Amkeni.

Si hivyo tu bali pia lipo gazeti moja maarufu nchini humo, linaloitwa Vukani.

Kwa maelezo zaidi bofya hapa.

Amkeni nionavyo mimi sio kuamka kutoka usingizini tu bali ni kuamka kifikra na kuhoji kila tulichofundishwa au kuambiwa kama kina ukweli kiasi gani? Si hivyo tu bali pia ni kuamka na kuachana na ile tabia ya kufikiri kwa mazoea na kutenda kwa mazoea. Kila jambo unalolifanya ujue sababu ya kufanya hivyo, sio eti kwa sababu, mama, baba, bibi, babu, mjomba, shangazi, na jamii iliwahi kufanya hivyo.

Nakumbuka wakati fulani nilihudhuria semina ya mambo ya uongozi, basi yule mwezeshaji kutoka nchini Marekani alitutolea mfano mmoja wakati alipokuwa akitufundisha namna ya kuepuka kufanya mambo kwa mazoea.

Kisa chenyewe ni hiki:

Kulikuwa na mama mmoja alikuwa na tabia, kila akitaka kuoka samaki ni lazima amkate mkia kabla ya kumuweka kwenye kikaango, ndipo amuoke. Hata kama samaki mwenyewe ni mdogo.


Siku moja binti yake aliyekuwa na umri wa miaka 10 akamuuliza mama yake sababu ya kukata mkia wa samaki kabla ya kumuoka, mama yake akamjibu kuwa mama yake alikuwa na kawaida ya kufanya hivyo. Alipomuuliza kama aliwahi kumuuliza mama yake sababu ya kufanya hivyo, mama yake akajibu kwamba hakuwahi kuuliza.

Basi wakati fulani bibi yake alipokwenda kuwatembelea, kama bahati mama yake alikuwa akiandaa samaki ili amuoke kama ilivyo kawaida akamkata mkia, binti akaona huo ndio wakati muafaka wa kuujua ukweli maana bibi yupo. Ndipo akamuuliza sababu ya mama yake kukata mkia wa samaki kabla ya kumuoka.

Si mnaona watoto wa wenzetu walivyo wadadisi?

Bibi akamwambia akamuulize mama yake sababu ya kufanya hivyo, yule binti akamjibu bibi yake kwamba, mama yake alimwambia kuwa yeye yaani bibi, ndiye aliyemfundisha kukata mkia wa samakai kabla ya kumuoka. Yule bibi akafikiria kidogo, kisha akamjibu, kwamba alikuwa akikata mkia wa samaki kwa sababu kikaango chake kilikuwa ni kidogo, hivyo ili samaki aweze kuenea kwenye kikaango alikuwa analazimika kukata mkia.

Yule binti akamwambia bibi yake, “Mbona sisi kikaango chetu ni kikubwa na isitoshe tunavyo vikaango vingi tu vya saizi tofauti tofauti, je kuna ulazima gani mama aendelee kukata mkia wa samaki kabla ya kumuoka?

Bibi akamjibu kwamba hakuna ulazima wowote.
Basi kuanzia siku hiyo yule mama akawa hakati tena mkia wa samaki.

Si mnaona jinsi mtoto huyu alivyokataa kulishwa kitu bila ya kijua sababu?
Naamini kwamba wote mtakubaliana na mimi kwamba sisi tumelelewa hivi, tunaambiwa tukate mikia ya samaki kabla ya kuwaoka na tunafuata, na wala hatuulizi sababu.

Kwa hiyo ninaposema VUKANI ninamaanisha AMKENI, ili muweze kuhoji baadhi ya mambo tunayofundishwa au kuambiwa ambayo hayana mantiki.


10 comments:

emu-three said...

Mimi kidogo nawaza hili neno kuwa ndivyo lilivyo au ni mazoea ya matamshi, kwani kama sikosei Wapare wanasema `VUKENI'...Labda ni kapare cha kusini, kwani Wapare wa Kusini na kasikazini wanatofautiana kidogo katika matamshi ya baadhi ya maneno!
Kweli jina hilo limekaa vyema maana unatuamsha kia-akili, au sio TUPO PAMOJA DAIMA....ndugu yangu!

emu-three said...

Oooh, wakati naandika hili nikawasiliana na jamaa yangu akaniambia ni kweli neno hilo linatokana na neno `VUKA'...maana `amka' ...
Mfano ukisalimiana kipare wakati mwingine wanasema `Wavukaze' maana yake `umeamukaje'...kwahiyo upo sawa!

Goodman Manyanya Phiri said...

Basi, Mpare na Mtonga (yaani kabila wanapotokea Wangoni kama Waswaziland, Wazulu, Wandebele na Waxhosa wote wa Afrika Kusini au majirani) hawatakua mbali.


Mimi binafsi sikua na matatizo ya kuelewa "Vukani" katika Blog yako, kwani kwa vilugha vya ki kwetu kama nilivyotaja hapo juu ndivyo mambo yanavyokwenda! Wapo hata watoto wenye jina la "Vukani", wewe Dada Koero!


ZULU/SWAZI/NDEBELE/XHOSA: "Vukanani, Bantwana!"= "Amkeni [nyie] Watoto!"


"Vukani, Maafrika! Izwe lenu litatwa okwesibili ngabeLungu!"="Amkeni, Waafrika! Nchi yenu inachukuliwa mara-ya-pili na-Wazungu!"

kamala Lutatinisibwa Lutabasibwa said...

imuka au imukamu

Godwin Habib Meghji said...

Na-avache Mchekuu

Yasinta Ngonyani said...

yimukayi!!

Celana Hernia said...

I visited several web pages however the audio quality
for audio songs existing at this website is truly fabulous.

Vimax Asli Canada said...

I like it this blog information, thanks for sharing

Obat Kuat Asli said...

I like it this blog information, thanks for sharing

poker said...

PROMO DELIMA
poker online | Agen Domino | Agen Poker|Kumpulan Poker | bandar poker | Judi Poker | bandar qiu | Judi online terpercaya

Bonus yang kami sediakan :
* TO (Turn over) sebesar 0.3% yang akan di kami bagikan setiap hari senin
* Bonus referal sebesar 10%

Ayo segera daftarkan diri anda dan bergabunglah bersama kami !!
Delimapoker.com Situs Agen Poker Online Terpercaya di Indonesia akan melayani Anda dengan profesional, memproses depo/wd dgn cepat.
Come join and be a winer with us !!

Untuk info selanjutnya silakan chat ke :
Livechat_____: delimapoker
BBM__________: 7B960959
Facebook_____: Facebook
Phone number_: +85595678845
pendaftaran___http://www.delimapoker.com/?ref=19860605