Friday, April 12, 2013

KUMBE WAMAKONDE WANAOGOPA KUFA...!



Inaelezwa kwamba Maziko Wamakonde huwa na maombi tofauti na yale yanayofuatwa na madhehebu mengine. Badala ya Sheikh au Kasisi kusoma dua, Wamakonde wana desturi ya kuieleza maiti maombi na maonyo ili marehemu huyo asije patwa na madhara wala asiandamwe na mikasa katika safari yake huko aendako, na pia ndugu wanaobaki nyuma wasikabiliwe na mabalaa na mikosi ya aina yoyote. Wenyewe wanaamini kwamba mabalaa huongozana, yaani likitokea moja hufuata la pili, la tatu na kadhalika. Kwa mujibu wa simulizi zao, kuna madai kwamba pale mambo hayo ya mila yanapopuuzwa vifo mfululizo hutokea katika familia husika.

Mkuu wa mazishi Huieleza maiti wakati wa maziko:

“Ndugu umeacha jembe, mshale, shoka, nyumba na kazi kwa hiyari yako mwenyewe, hakuna aliyekulazimisha kufunga safari hii, ile wewe mwenyewe umeazimia. Umetuacha sisi huku nyuma kwa hiyari yako mwenyewe, Hivi, ufikapo kwenye ukomo wa safari yako, ukaeleze yanayokuhusu wewe binafsi. Wakikuuliza  ‘Wako wanadamu wengine waliobaki?’ ukawajibu, ‘hapana.’ Ujitahidi kuwathibitishia kwamba ni wewe tu peke yako, hakuna mtu mwingine aliyebaki.”

Kwa maneno hayo, inadhihirisha wazi kabisa kwamba waliobai nyuma wanaogopa kufa. Ingawa wanajua kuwa kufa kupo, ila kama kunaweza kukwepeka basi ombi lao lisikilizwe! 

Hata hivyo inadaiwa kwamba mila hii bado inafuatwa na Wamakonde wa Msumbiji, tofauti na Wamakonde wa Tanzania ambao mila kwa kiasi kikubwa zimeathiriwa  muingiliano wa makabila na dini hizi za mapokeo

GAZETI LA VUKANI ....!!!!!


Aisee, hata sikujua kwamba kuna gazeti linaitwa VUKANI

Thursday, April 11, 2013

HILI NENO, "MWANAUME NI KICHWA CHA NYUMBA," HUWAPA KIBRI SANA HAWA VIUMBE




Kuna jambo moja ambalo hufundishwa na viongozi wa dini mbalimbali, ambalo pia waumini hulihubiri vizuri kila mahali wapatapo nafasi ya kufanya hivyo. Nalo si jingine ni lile la ‘mwanaume ni kichwa cha nyumba,’ ikiwa na maana kuwa mwanaume ndiye mkuu wa nyumba au familia. Suala hili linazungumzwa kama kwamba, mwanaume kuwa mkuu wa familia ni jambo la kimaumbile, lakini pia huzungumzwa kama vile, ukuu huo ni tiketi ya mwanaume kuikandamiza familia au mke. 

Nijuavyo mimi, wanaume wengi kuwa wakuu wa nyumba au familia ni suala la mazoea zaidi kuliko maumbile. Kwa miaka milioni kadhaa, mwanaume amejikuta akiwa ndiye mkuu wa familia. Kutokana na mazoea haya, jambo hili limekuwa kama vile ni la kimaumbile, yaani haliwezi kubadilika au kubadilishwa.

Lakini mbona kuna wanawake ambao ndiyo wakuu wa familia na familia hizo zinakwenda vizuri tu. Lakini vilevile kuna wanawake ambao hawana waume na wanaongoza vyema familia zao. Kwa bahati mbaya kwenye jambo hili, ni kwamba, kumekuwa na msisitizo kuwataka wanawake wawaheshimu waume na siyo wanandoa kuheshimiana. ‘mwanaume ni kichwa cha nyumba, ndiye msemaji wa mwisho. Inabidi aheshimiwe.’ Kuna watu ambao bila aibu huzungumza lugha hii.

Ni kweli wanaume wanahitaji au wanapaswa kuheshimiwa. Lakini siyo wanaume peke yao, bali binadamu wote wanapaswa kuheshimiwa bila kujali wanafanya nini au wakoje. Kwa hiyo siyo kwa sababu ni wasemaji wa mwisho, basi wao ndiyo wanaopaswa kuheshimiwa. Kwa kuamini hivyo wanaume wengi wamekuwa wakitumia nafasi hiyo kuwakandamiza wake zao na hata watoto. ‘Mimi ndiyo msemaji humu ndani, nimesema sitaki, basi.’ Mara nyingi matumizi ya mabavu kwa namna hiyo hutumika.

Kuna haja kwa wanaume kujua kwamba, kuwa kwao viongozi wa familia hakuwapi ubora wa ziada. Wanawake nao wanapaswa kujua kwamba, kutokuwa kwao wasemaji wa mwisho wa familia, hakupunguzi hata chembe ya thamani ya ubinadamu wao, kwani binadamu na wanandoa wanapaswa kuheshimiana.