Saturday, January 2, 2010

HAIKUWA BAHATI, BALI MKOSI

Nikafunguliwa biashara kubwa

Tunaishi katika maisha yenye vishawishi na matamanio makubwa, kuna wakati mtu anaweza kujikuta akiwa mtegoni asijue hata kujinasua. Ama kweli dunia hii ni hadaa na ulimwengu ni shujaa, wakati unapoamini kuwa umepata bahati unaweza kushangazwa na matokeo ambayo kamwe hukuyatarajia, kuna msemo mmoja unasema kuwa kama mlango mmoja ukifungwa mwingine umefunguliwa. Kuna haja ya kuwa makini kwani kuna uwezekano huo uliofunguliwa ukawa ndio nuksi kuliko uliofungwa.
Naamini kinachohitajika zaidi ni subira kuliko kukimbilia mlango mwingine ulio wazi, kuna uwezekano kuna nyoka humo.

Hivi karibuni nilimtembelea rafiki yangu mmoja, ambaye familia yao ni family friend na familia yetu, nilipofika pale alinitambulisha kwa shangazie ambaye aliwatembelea na kutokana na uchangamfu wangu tulizoeana kwa muda mfupi, tuliongea mengi na katika maongezi yetu alinisimulia mkasa wake aliokumbana nao.
Ungana nami katika simulizi hii ya kusisimua.

Alikuja pale kazini kama mteja, lakini hilo jicho, mwenzangu mpaka niliogopa, maana jicho lake liliniganda mpaka nikaona aibu, hata hivyo alipomaliza shughuli zake aliondoka na kuahidi kurudi eti kunipa lifti nikirudi nyumbani kwangu, mwezangu nikamwambia kuwa mpenzi wangu atanifuata, hakuonekana kujali maneno yangu aliondoka na kusisitiza kurudi.

Ilipofika jioni alirudi lakini nilimkwepa na kuondoka zangu nikimwacha ndani akiongea na Bosi wangu kwani alikuwa namizigo yake na makontena Bandarini ambayo yalikuwa yanashughulikiwa na kampuni yetu kutolewa bandarini.

Siku iliyofuata alifika pale ofisini na kuniahidi kunitoa lunch katika Hoteli ya Kitalii ya Nyota Tano pale Kempinski, nilikataa ofa yake na alionekana kushangaa. Akaniambia kuwa tangu kukua kwake hajawahi kukakataliwa kitu na mwanamke, mimi nitakuwa wa kwanza kumfanyia hivyo, sikumjali sana nilimpuuza.

Baadae Bosi wangu alianza kumsifia yule mzee kuwa ni tajiri ambaye anafanya biashara katika nchi za afrika na mashariki na kati aki-supply bidhaa mbalimbali katika nchi hizo. Bosi wangu aliendelea kusema kuwa toka ameanza kufanya kazi na yeye kampuni imeingiza faida kubwa sana na kuna matarajio mazuri mwakani.

Ilipofika mchana alikuja kijana mmoja akauliza kama anataka kumuona Gift (*sio jina lake halisi) nikamwambia kuwa ni mimi, akatoa bahasha na kunikabidhi, nilipomuuliza kama imetoka wapi akanijibu kwa kifupi tu kuwa imetoka kwa mzee, kisha akaondoka zake.


Niliifungua kwa kiherehere ili kujua ina kitu gani, ndani ya bahasha ile nilkutana na cheni ya dhahabu ya Gram 10 na shilingi laki mbili, na ujumbe unaosema, “Samahani sana Gift, nilikuahidi kukutoa lunchi leo, lakini niko na kikao wizarani, nimeshindwa kutekeleza ahadi yangu, lakini hapajaharibika kitu, hiyo cheni , nilikununulia ili nikupe kama zawadi wakati wa Lunch yetu, lakini kutokana na dharura hiyo, basi pokea zawadi yangu hiyo kama ishara ya upendo nilionao kwako na hizo fedha ndio nilikuwa nimeandaa kwa ajili ya hiyo lunchi yetu, unaweza kuzitumia kwa kununua kitu chochote ukipendacho.

Nilishusha pumzi nikabaki nimeduwaa, kisha nikafyonya kwa dharau, na kuitupia ile bahasha kwenye droo ya mezani kwangu.

Jioni boy friend wangu akanifuata tukaondoka kuelekea kituoni kupanda daldala kurudi nyumbani.Kiukweli Boy friend wangu alikuwa hana kazi bali alikuwaakibangaiza kwenye ofisi ya jamaa yake fulani baada ya kumaliza masomo yake ya International Technology. Akiwa amesoma ngazi ya Diploma.

Nilikuwa na mchanganyiko wa mawazo na kutokana na mawazo hayo nilijikuta nikiwa mbali sana kiasi cha kutosikia yale aliyokuwa akiyasema Boy friend wangu, kuna wakati ilibidi anishtue kwa kuniuliza kama nimemuelewa alichokisema nilimjibu tu ndio lakini kiukweli sikumuelewa kabisa kuwa alikuwa anaongea nini.

Tulipofika Sinza ambapo ndipo ninapoishi tulishuka na kuelekea kwangu lakini karibu na nyumbani tulipisha na gari moja aina ya RAV 4, ilikuwa ikiendeshwa na kijana ninayemfahamu, alinipigia honi na kunipungia mkono, nami nilimpungia mkono. Mpenzi wangu alionekana kutofurahia kile kitendo kwani tulipofika tu nyumbani maswali yakaaza. Yule ni nani? mmejuana lini? ana uhusiano gani na wewe, mbona simfahamu? yalikuwa ni maswali mengi mfululizo ambayo sikuweza kuyajibu yote.


Tatizo la mpenzi wangu ni wivu, yaani bwana yule ana wivu utadhani dume la njiwa. Kama masihara ulizuka mzozo wa maneno kati yangu na mpenzi wangu kiasi cha kufikia kunipiga, na kisha akaondoka zake. Niliwaza sana, kwa kweli sikuwa na uhusiano na yule kijana na nilimfahamu kupitia kwa shoga yangu anayemiliki saluni ambapo ndipo ninapotengenezea nywele na yule kijana ni boy friend wake.

Nililia sana na sikuweza hata kula usiku ule nikalala na njaa. Kesho yake nikiwa ofisini yule mzee alifika tena lakini safari hii hakukaa hata kidogo, alionekana kuwa bize sana,
Ilipofika mchana Boyfriend wangu alinipigia simu lakini sikupokea, alitumia simu ya mtu mwingine kunipigia, lakini nilipopokea na kusikia sauti yake nilikata ile simu alinitumia ujumbe wa simu akiniomba radhi lakini sikumjibu, nilichukizwa sana na kitendo chake cha kunipiga siku ile.

Ilipofika jioni yule mzee akaja kunipitia pale ofisini akiwa na gari lake aina ya GX, niliamua kuondoka naye kwani alinibembeleza sana anipeleke kwangu, wakati tunaondoka nilimuona boy friend wangu akija kunifuata, nilitaka kumuomba yule mzee anishushe lakini nilisita. Yule mzee ambaye ki umri alionekana kuwa sawa na baba yangu alinifikisha nyumbani kwangu, lakini hakushuka kwenye gari, alinipa bahasha nyingine akaniambia ni zawadi yangu, nilipoingia ndani na kuifungua nilikuta dola mia mia kumi, nilishikwa butwaa.......Huyu mzee anataka nini kwangu, hivi anadhani mimi ni wa kutembea na vizee, niliwaza.

Nilishtuliwa na mtu akibisha mlangoni kwangu, nilikwenda kufungua mlango, alikuwa ni mpenzi wangu, nilishtuka sana, aliingia ndani huku akiwa amefura kwa hasira, “niliwaona sana na leo utanieleza” lilikuwa ndio neno lake la kwanza alipoingia ndani, alipitiliza hadi chumbani kwangu na zile dola zilikuwa bado ziko kitandani, nilimfuata kwa nyuma, alipoziona tu akazichukua zote.

Sasa nenda kamwambie nimezichukua na akome kutembea na wachumba za watu. aliniambia huku akizitia zile dola mfukoni, Nilijikuta nikipandwa na hasira, "Safari hii sikubali" nilijisemea moyoni, nilimrukia na kuanguka nae kitandani niliingiza mkono wangu kwenye mfuko wake alipoweka zile dola na kuzichoimoa, na yeye aliukunja mkono wangu kiasi cha kutaka kuuvunja, niliziachia zile dola zikatawanyika kitandani na pale chini, tulipigana hasa na kuvunja vitu mle ndani kosa jirani yetu mmoja kuingilia kati, tungevunja vitu vyote mle ndani.

Nilitoka na kwenda Polisi kuripoti lile tukio na nilipewa PF 3 na RB, sasa mchumba wangu alikuwa akitafutwa na Poilisi, Baada ya kusikia kuwa anatafutwa alitoweka.

Siku iliyofuata nilikwenda kazini,lakini kutokana na hali yangu iliidi niombe ruhusa ili kujiuguza majeraha ya kupigwa na mchumba wangu.

Nilipewa ruhusa ya kupumzika ya siku tatu na Bosi wangu, lakini sikwenda nyumbani kwangu bali nilikwenda kwao na mpenzi wangu Mwenge ili tuyamalize nilipofika nilimkuta shangazi yake anayeishi naye, akaniambia kuwa menzi wangu ameenda Moshi. Lakini hakumwambia shangazi yake kuwa tuligombana.

Nilimsimulia shangazie tukio zima, shangazi yake alishangazwa na habai ile na alijaribu kumpigia simu lakini simu yake ilizimwa. Niliondoka na kurejea nyumbani.
Ilipofika jioni nilisikia mlango wangu ukigongwa na nilipofungua nilikutana uso kwa uso na yule mzee, nilimkaribisha huku nikiw nimetahayari kwani sikutegeme ujio wake, nilimkaribisha ndani.
Alistushwa na hali yangu kwani macho yangu yalikuwa yamevimba na uso wangu pia, alinidadisi, nilimdanganya kama nilikutana na vibaka usiku nilotoka kwenda kununuas chipsi, alitaka kunipeleka katika Hospitali ya rafiki yake lakini nikataa kwa maelezo kuwa natibiwa na kampuni.
Hakukaa sana aliondoka, siku inayofuata alikuja asubuhi kunijulia hali na aliniahidi kunifuata mchana ili tukale lunch pamoja, nilimkubalia.

Nikweli alikuja na tulitoka pamoja hadi katika Hoteli moja iliyoko katikati ya mji, tulikula na kuongea mambop mengi sana, yule mzee a litaka kujua kama nina matarajio gani juu ya maisha yangu ya baadae nilimweleza kuwa nia yangu ni kujiendeleza zaidi kieleimu kwani elimu yangu ya kidato cha sita na diploma ya usekretari sijaridhika navyo aliniuliza kama nataka kusomea nini, nilimjibu kuwa nataka kusomea sayansi ya jamii ngazi ya shahada, aliniuliza kama ningependa kusomea nje ya nchi au hapa hapa nchini.

Nilishangazwa sana na swali lile, nilimjibu kuwa kwa kuwa sina uwezo kifedha nitasomea hapa hapa nchini, alinimabia kwa upole, “ Sikiliza Gift, kwa kuwa mimi nipo, kila kitu kinawezekana, usiwe na wasiwasi nitakusmesham tafuta shule mahali popote nitakusomesha” nilishangazwa na ukarimu wa yule mzee, na aliongea akionekana amedhamiria hasa.

Tulipotoka pale aliniambia kuwa anataka kuni-surprise, sikumuelewa kabisa, alinimbia nisubiri kidogo, tulikuwa tumesimama pale nje ya ile Hoteli na mara ikaja Toyota Rav 4 ya kijivu, na kusimama mbele yetu ilikuwa ni mpya kabisa, na yule dereva akashuka na kumkabidhi yule mzee funguo za lile gari. Yule mzee ambaye alijitambulisha kwangu kuwa anaitwa Alex, aliniuliza kama naweza kuendesha gari, nilimjibu kuwa sijui, alimuita yule dereva aliyekuja na lile gari amabye alionekana ni dereva wake na kumuamuru anipeleke kwangu na kisha anipeleke chuo chochote kizuri nikajifunze udereva.

Aliniambia kuwa lile ni gari langu ameninunulia ili kuniondolea usumbufu wa kugombea daladala.
Nilibaki nimeduwaa sikujua hata niseme nini.

Kwa kifupi nilianza uhusiano na yule mzee na alinishauri niache kazi kisha akanitafutia nyumba kubwa nzuri maeneo ta Mikocheni.
ITAENDELEA..........................

5 comments:

Mija Shija Sayi said...

Mbona kazi, mmmh mi'nnasibiri kwa hamu muendelezo.

Stay blessed.

Yasinta Ngonyani said...

Ni kweli ni simulizi ya kusisimua, Duh duniani hapo kazi ipo nami nasubiri muwndelezo maana weee acha tu.

Godwin Habib Meghji said...

Nasubiria..... Ndio yale yale ya magari mekundu.

MARKUS MPANGALA said...

NJE YA MDA: NAMTAFUTA DADA ASIMWE, nduguye Koero, nina TIFU naye labda!

Mzee wa Changamoto said...

Lol Markus