Tuesday, February 17, 2009

HIVI WAMETUZAA ILI TUWE WAO?

Tukiwezeshwa kukuza vipaji vyetu tunaweza.

Wazazi wanatakiwa kujua kwamba, mtoto ni binadamu aliye kamili kabisa. Ni binadamu ambaye anatakiwa kuwa na haiba yake na ubainisho wake kama yeye. Mzazi anapofikiria na kuamini kwamba, mtoto nilazima awe mfano wake anakosea. Kama mzazi ni dakitari kama mzazi anapenda sana mziki, kama mzazi anachukia sana mpira basi anataka mtoto naye awe hivyo, huo sio ukomavu.

Mimi naamini kwamba bila mzazi kujua kanuni au misingi kadhaa inaweza kuwa vigumu kwake kumlea mtoto bila kumwingizia athari mbaya ambazo yeye mzazi aliwekewa na wazazi wake. Hebu fikiri, ni wazazi wangapi ambao wanamlea mtoto kana kwamba mtoto huyo siyo binadamu kamili? Ni wengi sana wanaomlea mtoto huyo awe kama wao au kama wao wanavyotaka.

Kumbuka kila mzazi anapewa dhamana ya kumfanya mtoto kukuwa na kufikia kiwango cha juu kabisa cha ufahamu na binadamu mwenye faida kwa wengine. Ni dhamana ya kuhakikisha kwamba mtoto anapokuwa mkubwa anafanya kila kilicho chini ya uwezo wake.

Mzazi kwa hali hiyo, anapaswa kukagua na kuelewa upendeleo wa mtoto vipaji na hofu zake. Kwa kujua hivyo anakuwa kwenye nafasi ya kumudu kukuza vipaji vyake, lakini pia kumuhakikishia kuhusu usalama na uwezo wake.

Mtoto anatarajia kupendwa na wazazi wake muda wote bila mashariti. Kumpenda mtoto wakati tu anapofanya kile atakacho mzazi na kutompenda anapokosea kwa vipimo vya mzazi huo ni udhaifu mbaya kabisa. Kupenda kwa mashariti huharibu badala ya kutengeneza tabia ya mtoto.

Mtoto anahitaji kuwekewa mipaka ya yale anayoweza kusema kufanya na kujihusisha nayo. Lakini mipaka hii ni lazima iwe ni yenye kuaminika. Mipaka yenye kutegemea mazingira au hali ya mzazi na hivyo kuwa inabadilika sana kumharibu mtoto. Leo mzazi anasema hiki hakifai kesho anasema kinafaa. Leo anasema, watoto hawaruhusiwi kufanya hiki kesho anabadilika na kusema wanaruhusiwa.

Kuna wazazi ambao hawajawahi kuwasifu watoto wao hata mara moja hata wanapofanya mambo mazuri na makubwa sana.wanachosubiri wao ni watoto hao kukosea tu. Inashauriwa wazazi waone mazuri zaidi kuliko kuona mabaya zaidi ya mtoto. Bila kukosea hakuna kukua na mzazi anayemwonesha mwanae kuwa kukosea ni dhambi anajaribu tu kumuharibu mtoto huyo.

Mzazi anatakiwa kumsaidia mtoto kujenga ndoto kubwa za baadaye na sio kumvunja nguvu katika ujenzi wa ndoto hizo. Mtoto anaposema kwamba anataka kuwa raisi wa nchi, mzazi amwambie kwamba inawezekana na kumfundisha angalau kwa kiwango chake cha ufahamu kwamba anaweza kuwa.

Mzazi ana wajibu wa kumfanya mtoto wake kujenga tabia ambazo zitamsaidia ukubwani. Kama mwanaye hataki kuwa wa visasi akikosewa na wenzake mzazi asioneshe kwamba hao wenzake wanastahili adhabu bali zaidi msamaha. Kusisitiza msamaha kwanza kabla ya adhabu humsaidia mtoto kujua umuhimu wa kuvumilia wengine.

Kuna kanuni nyingi ambazo mzazi anatakiwa kuzifuata katika kujaribu kuwa mzazi bora zaidi ambaye halei mtoto kwa kufuata athari ambazo alipewa na mzazi wake bali kwa kuzingatia hali halisi ya saikolojia ya binadamu. Hizo nilizokutajia ni baadhi tu.

3 comments:

Christian Bwaya said...

Koero,

Ni kweli kwamba wazazi wanahusiaka sana kumfinyanga mtoto kuwa vyovyote wapendavyo. Wao wana mchango wa kijenetiki (nature) na mchango wa kimalezi (narture)

Alivyo mtoto ni picha ya alivyo mzazi wake.

Mwanafalsafa Illich anasema mzazi anaweza kumtengeneza mwanae kuwa chochote anachokihitaji kutoka kwake. Iwe kazi yoyote. Iwe tabia yoyote. Iwe haiba yoyote.

Hayo yanawezekana kama ataelewa kuwa vitu vilivyomo ndani ya mwanae (potentials) vinaweza kudhihirika ikiwa ataichukulia kazi ya malezi kama jukumu la kiuwekezaji.

Kwa maneno mengine, mzazi asipolichukulia jukumu la ulezi kwa uzito unaotakikana, mtoto huyo huyo ambaye angeweza kuwa mtu wa maana katika jamii, anaweza kufanyika bingwa wa majambazi kwa sababu tu ya uzembe wa huyo anayejiita mzazi (mzaaji).

Aidha, mafanikio ya mzazi si kujaribu kumfanya mtoto afanane na yeye. Mafanikio ya malezi ni kwanza kugundua kile hasa mtoto alichonacho kwa asili (ambayo bila shaka ameichangia yeye) na namna ya kukipalilia (nurturing) kiwe halisi kwa matakwa ya asili ya mwanae.

Tukiliangalia hilo kwa makini, tutaona kuwa wazazi wengine hata kama hawapendi, wamekwama.

Na ajabu iliyo kuu ni kwamba wazazi wenyewe wamekuwa mabingwa wa kulaumu watoto walioharikia mikononi mwao pasipokujua kuwa walivyo wanao ni picha (reflection) ya aina ya uwekezaji wao.

Sasa wazazi wanaweza kulea kwa mafanikio, hapo ndiko unakoweza kuwa mjadala mpana.

Je, malezi wakati unafanya kazi masaa kumi na mbili na kumwacha mwanao na hausi geli usimfahamu vya kutosha yanafaa? Malezi ya kumtelekeza mwanao katika kituo cha kulelea watoto wadogo ni malezi sahihi?

kamala Lutatinisibwa Lutabasibwa said...

kama nimewahi kuisoma ndani ya gazeti la jitambue vilee? inaonekana ulianza kuandika muda?

kazi nzuri, Munga tehenan angekuwa hai?

Simon Kitururu said...

Ukiongea na Serina na Venus katika jinsi ambavyo ni mabingwa wa tenesi watakuambia ni Baba aliyekuwa na ndoto na kabla ya kuwazaa alianza kujifunza ukocha ili watoto wake wacheze tenesi. Na mpaka sasa ni masupa staa watu wazima na hawalaumu kwanini tokea hawajazaliwa wazazi walipanga watoto wao wacheze tenis.



Tukumbuke tu kuwa binadamu ni tofauti. kuna wapendao kufuata viongozi na kuna waongozao hata kama hatutaki. Na si ukweli ni kutokana na waongozwao walitishwa wakiwa watoto ndio maana hawataki kuongoza.

Nakubaliana na yote yaliyosemwa lakini si rahisi namna hiyo.

Ila ningependa wazazi wajaribu kujua watoto wao kama wao ingawa naamini kuna watoto wanazaliwa majiniasi na wazazi hawawezi kuelewa nini kinaendelea.