Friday, April 1, 2011

BIBI KOERO NA KIKOMBE CHA BABU AMBILIKILE

Misitu kama hii ni hazina kubwa kwa dawa za miti shamba



Hivi karibuni nilimtembelea bibi Koero kule kijijini, nilipitia huko wakati nikitokea Arusha kurudi Dar. Nilimkuta yu buheri wa Afya, na kama kawaida yake alinipokea kwa bashasha kubwa pamoja na tabasamu pana usoni pake.


Mara zote anajua mjukuu wake nina hamu ya simulizi zake zinazonipa tanuri la fikra, kwa kweli Bibi yangu huyu ananipenda sana.Daima napenda sana udadisi,napenda kuchokonoa, kudadavuliwa na kudadavua niwapo na bibi Koero, kama vile alivyo Yasinta na mie siko nyuma katika Ukapulya.


Yaani ni zaidi ya falsafa na wazo ndani ya neno ya kaka Kitururu pamoja na chakula kitamu kiliwacho.


Basi katika hali ya utani nikamuuliza kuwa kwa nini na yeye asiende Loliondo kwa Babu Ambilikile Mwasapile kupata Kikombe? Nilimuuliza hivyo baada ya kuniambia kuwa juma lililopita alikuwa anasumbuliwa na maumivu ya mgongo na kichwa.


Bibi Koero aliniangalia, kisha akacheka kwa dharau. Nikajua kuna jambo lenye wazo na chakula kitamu kusimulia. Alicheka kisha akasema kwa dharau, ‘umri huu niende kwa Babu Loliondo kufanya nini?, umri huu nilio nao (Bibi Koero anatimiza miaka 92 mwaka huu) siwezi kujisumbua kiasi hicho, nimeshakula chumvi nyingi na hivyo nasubiri kupumzika’.


Alinishika mkono na kuniambia nimfuate, kwani wakati huo alikuwa kwenye kijishamba chake akipalilia Tangawizi zake. Tukajongea kwenye kivuli cha mti ulioko jirani tukakaa chini. Akaanza riwaya zake zenye maono; sikiliza mjukuu wangu, alisema bibi Koero, kisha akaendelea………..Kuibuka kwa huyo Babu Ambilikile sio jambo la kustaajabisha, ni mambo ya kawaida kabisa, na inawezekana wakaibuka wengine na wengine (wakati tunazungumza ilikuwa bado hazijasikika habari za kuibuka kwa kijana mwingine huko Mbeya, Morogoro na Mama wa Tabora ambao wote wamedai kuoteshwa dawa na Mungu).


Aliendelea, Kabla ya ujio wa tiba za Hospitali, Watu walikuwa wakiugua na kutibiwa kwa miti shamba, na sio kwamba kulikuwa hakuna maradhi kama wakati huu, yalikuwepo, tena maradhi mengine yalikuwa ni ya kutisha, Je watu hao walikuwa wakitibiwa na nani kama sio Mungu? Labda kitu ambacho watu wa kizazi chenu msichokifahamu, ni kutokujua utendaji kazi wa Mungu.


Zamani kulikuwa na imani ya kuamini Mizimu Matambiko au Mizungu na kadhalika na kupitia imani hizo mambo mengi yalifanyika. Ujio wa hizi dini za Mapokeo, ambazo hata hivyo mimi ni mmojawapo ya watu tuliojikuta tukibadilika kutoka katika imani zetu tulizorithi kutoka kwa mababu zetu na kuingia katika imani hizo za dini za mapokeo, tulijikuta tukiziacha na kuzibatiza jina la imani za Kishenzi kwa kuwa tu tulilazimishwa kuzikana. Sasa basi kwa upande wa utendaji kazi wa Mungu, kwa kweli hilo ni jambo ambalo bado linazusha maswali kila uchao. Mungu yupo na anayo namna yake ya kuwasiliana na wanaadamu, kama alivyofanya tangu huko zamani.


Wanaadamu walipitia nyakati tofauti na kila nyakati zilikuwa na kitabu chake, yaani historia yake. Msomaji keti kitako…,..ngoja nikusimulie mkasa huu uliompata baba yetu.Wakati nilipokuwa binti mdogo kigori. Baba yetu aliumwa sana, kiasi cha kulala kitandani kwa mwaka mzima, kama ingekuwa ameugua kipindi hiki labda mngesema kuwa ni huo ugonjwa wenu wa Ukimwi. Tulifika mahali tukakata tamaa, tulimpeleka kwa waganga mbalimbali wa asili wenye sifa za kutibu maradhi yaliyoshindikana lakini hawakuweza kumtibu, tulibaki kumuomba Mungu.


Ilifikia mahali ikabidi sasa tubadilishe sala zetu, kwamba badala ya kumuombea apone, tukamuomba Mungu ampumzishe kwa sababu alikuwa ameteseka sana kwa maradhi hayo.



Ilitokea siku moja Mjomba wake na baba aliyekuwa akiishi Kijiji kingine alikuja nyumbani alfajiri na mapema, na sisi tulijua kuwa amekuja kumuona mgonjwa, lakini alipofika tu, aliomba jembe na panga, kisha akamchukua kaka yetu mkubwa na kwenda naye kwenye Msitu wa Shengena.


Sikiliza hili, msomaji, msitu wa Shengena ni miongoni mwa Misitu yenye maajabu makubwa hapa nchini, msitu huo uko jirani na kijiji alichozaliwa mama yetu yaani hapo Mamba Miamba wilayani Same mkoani Kilimanjaro. Simulizi juu ya maajabu ya Msitu huo yanahitaji makala inayojitegemea. Nitawasimulia nikipata muda.


Bibi Koero aliendelea kusimulia, walirudi baada ya saa kama tatu hivi wakiwa na mizizi na majani ya mti tusioujua. Mjomba alitueleza kuwa siku mbili zilizopita alioteshwa na kuoneshwa dawa itakayomtibu baba, awali alipuuza, lakini kwa mara nyingine siku iliyofuata alioteshwa tena na kuoneshwa dawa hiyo.


Kwa mujibu wa maelezo ya mjomba alidai kuwa akiwa usingizini, aliona kivuli cha mtu pembeni ya kitanda, alikuwa ni mtu mwanaume na alikuwa akimuamsha kwa kumwita kwa jina lake lakini kwa kunong’ona, aliamka na yule mtu akamuonesha ishara kuwa amfuate, alinyanyuka na kumfuata, mjomba alidai kuwa hawakupitia mlangoni, bali kulitokea uwazi kwenye ukuta wakapita na ule uwazi ukajifunga na walipokuwa nje mavazi ya yule mtu yalikuwa yanang’aa kama theluji na hivyo kutoa mwanga.


Kwa kuwa kulikuwa na giza totoro, ule mwanga ulimwezesha kuona njia na waliendelea kutembea kuelekea mahali asipopajua.


Walitembea mwendo mrefu hadi wakafika msituni, na ndipo akaambiwa achimbe mizizi ya mti fulani baada ya kuchimba ile mizizi walienda kwenye mti mwingine na kukata majani ya ule mti kisha wakarudi nyumbani.


Walipofika walipitia pale pale ukutani na walipoingia ndani yule mtu aligeuka kuwa kivuli na kisha akamwambia kwa kunong’ona kuwa ile ni dawa ya kumtibu mjomba wake ambaye ni baba yetu.


Alimwelekeza namna ya kuitayarisha ile dawa kabla ya kumpa mgonjwa kisha akatoweka.Mjomba alistuka usingizini na kumsimulia mkewe, juu ya ndoto ile, shangazi alimshauri aende kwa mtaalamu ili kupatiwa tafsiri ya ile ndoto, lakini alipuuza, siku iliyofuata alioteshwa tena, na ndipo akakata shauri kuitafuta hiyo dawa ambayo kwa kweli ndiyo iliyomtibu Baba.


Baada ya baba kupona hakupata kuumwa tena zaidi ya maradhi madogo madogo hadi alipofarikia akiwa na miaka tisini na ushee.


Muda wote wakati Bibi Koero akinipa simulizi hiyo ya kuvutia nilikuwa nimemtumbulia macho nikiwa nimeshika tama.


Hivyo basi mjukuu wangu, aliendelea Bibi Koero, Mungu amekuwa akiwasiliana na wanaadamu hadi hivi leo, lakini wengi waliokuwa wakioteshwa hapo zamani walikuwa wakifanya siri, na hata hivyo hapakuwepo na wingi wa vyombo vya habari na mawasiliano kati ya eneo moja hadi jingine yalikuwa ni magumu na ndio sababu habari hizo hazikupata kuvuma kama hivi sasa.


Labda jambo lingine na lile la wananchi kukata tamaa na gharama za matibabu katika Hospitali zetu kuwa juu, hiyo nayo ni changamoto nyingine ambayo inaikabili sekta hiyo ya afya sio kwa hapa nchini tu bali dunia nzima kwa ujumla.


Kwa kifupi alinieleza kuwa Mungu yupo na ataendelea kuwasiliana na wanaadamu kwa namna tofauti kulingana na jinsi anavyoona. Lakini hata hivyo, alisema kuwa sio kwamba wote watakaotumia dawa hiyo watapona, haiwezekani, wapo watakaopona na wapo ambao hawatapona kwani kuponya kwa dawa za namna hiyo kunatokana na imani watakayokuwa nayo watumiaji.


Kwa ujumla tuliongea mengi na bibi Koero ikiwemo kutahadharisha juu ya kuibuka kwa Matapeli watakaosingizia nao kuotesha dawa na Mungu kwa ajili ya kujipatia fedha kwa hila na kujijengea umaarufu, kwani katika msafara wa Mamba hata Kenge nao pia wapo.


Hata hivyo msichoke kupitia kibaza hiki maana nikipata muda nitamalizia mazungumzo yetu na Bibi Koero sehemu ya pili ikiwa ni mwendelezo wa kile tulichojadili. Mmmh! Kumbe kikombe cha babu hakikuanza leo!

4 comments:

Yasinta Ngonyani said...

Ni siku nyingi kidogo nimekuwa nimecheka....eti Kapulya kama Yasinta:-) Kwa kweli IMANI NI KITU CHA AJABU SANA!!

emu-three said...

Twasubiri kwa hamu muendelezo wake, kweli bibi zetu, wazee wetu ni hazina, na wanajue mengi...lakini ..mmmh, sidhani taifa letu linawajali sana hawa wazee...ni kila mtu na mzee wake, haya mmwaona miujiza yao, huyo na wengine wengi wapo na wananjua mengi...leo tunao kesho hawapo nani atajua siri iliyopo moyoni mwao!

o'Wambura Ng'wanambiti! said...

wewe umeshakwenda Loliondo? @Koero

Anonymous said...

Naona sasa imekua mchezo kila mmoja na kikombe hii balaa tena jamani yani watu haswa wabongo wamekua wajinga kupindukia wakisikia kikombe kwa fulani wameshajaa kama utitiri.