Thursday, May 7, 2009

SUBIRA, UVUMILIVU NA UBUNIFU VIKALIPA: SEHEMU YA PILI

Hatimaye subira, uvumilivu na ubunifu vikalipa

Ndugu wasomaji wa bolg hii, kutokana na maombi ya wasomaji wengi nimelazimika kumalizia kisa hiki ambacho niliahidi kukimalizia wiki ijayo. Ukweli ni kwamba hiki kisa ni cha kweli na nilikipata kutoka kwa kaka wa rafiki yangu niliyewahi kusoma nae.
Sikutaja jina la mhusika na pia majina ya maeneo nimebadili ili kuficha utambulisho wa mhusika ili kuepuka usumbufu.
nakumbuka siku moja wakati tunapiga stori akanisimulia kwa kifupi juu ya maisha yake na jinsi alivyoweza kupambana na maisha mpaka akaweza kutimiza ndoto zake.
Nilivutiwa na stori yake nikamuomba niiweke hapa kibarazani ili wasomaji wa blog hii nao waweze kujifunza. Alikubali na kunipa stori yote juu ya maisha yake ingawa pia nimeifupisha ili nisiwachoshe, lakini naamini itakuwa imeeleweka.
Katika maisha sisi kama wanaadamu kila mtu anazo ndoto zake na kila mtu anatamani kufanikisha kile anachoamini kuwa kwake ni mafanikio, kwa hiyo misukosuko ya maisha isitukatishe tamaa kwani mlango mmoja ukifungwa mwingine pembeni yako uko wazi ni kiasi cha wewe kupepesa macho kuchunguza.
Haya ungana nami katika kumalizia kisa hiki chenye kufundisha.
Ingawa nilikuwa na kipato kidogo lakini nilikuwa na ndoto za kutaka watoto wangu wapate elimu bora tofauti na mimi baba yao. Nilikuwa ninaamini tu kuwa nitaweza na sikuwa na wasiwasi na hilo. Mara nyingi nilikuwa nikiwaambia wanangu kuwa lazima wasome mpaka chuo kikuu, lakini mke wangu alikuwa akiguna kila nikisema hivyo, alikuwa akinidharau wazi wazi na wakati mwingine alikuwa akinisema kwa mafunbo akidhani kuwa simuelewi.

Kusema ukweli kama ni kipaji mke wangu alikuwa nacho, alikuwa ni hodari wa kusema kwa mafumbo, kubeza na kushushua mpaka mtu akajisikia vibaya.
Unaweza ukasema jambo mbele ya mgeni akakushushua hivi hivi bila kujali kama kuna mgeni. Baada ya kutafakari sana niliamua nikubali yaishe, nimpe talaka halafu tugawane kile alichoita mali. Ulikuwa ni uamuzi mgumu lakini nilikuwa sina jinsi, niliona kuwa ile itakuwa ni njia sahihi ya kuepuka kero na kupoteza muda na pesa pasipo sababu.

Siku iliyofuata, asubuhi na mapema nilikwenda ukweni na talaka yangu ambayo niliiandika usiku ule ule.

Nilipofika na kumueleza baba mkwe juu ya uamuzi wangu wa kuridhia kutoa talaka, baba mkwe alistuka, kwani hakutegemea uamuzi wangu ule.
Baada ya majadiliano tulikubaliana kiwanja kiuzwe na hela itakayopatikana pamoja na ile hela ya mafao ya kupunguzwa kazi tugawane sawa kwa sawa na hata vitu vya ndani pia vigawanywe kila mtu akaanze maisha kivyake. Iliniuma sana lakini sikuwa na jinsi.

Ndani ya wiki moja tuliuza kiwanja na tukagawane fedha pamoja na vitu vya ndani, nikawa nimeutuwa mzigo.
Nikaanza maisha mapya nikiwa peke yangu.
Niliamua kusafiri na kwenda nyumbani kuwaona wazazi na kupumzisha akili.

Nilirudi Dare s salaam baada ya wiki moja, hiyo ni baada ya kukaa na wazazi wangu kwa muda wa wiki moja nikipata ushauri kutoka kwa wazazi wangu namna nitakavyoweza kupambana na maisha baada ya kutengana na mke wangu.

Nilipofika tu nilitafuta kiwanja maeneo ya kule kule Segerea na nilibahatika kupata eneo la eka moja na haraka haraka nilisimamisha kibanda changu chenye chumba na sebule.
Niliamua kujikita zaidi kwenye kazi ya kupiga picha na niliamua kununua kamera mpya ya kisasa, kama masihara nilianza kuzururra mitaani maeneo ya Tabata kutwa nikipiga picha kwenye mabaa na mitaani na ghafla nikawa maarufu.

Nilianza kupata tenda za kupiga picha kwenye sherehe mbali mbali, misibani na kwenye matukio mbali mbali mitaani, na kijipatia fedha za kutosha.
Baadae nilipata wazo la kununua video kamera, hiyo ni baada ya kuwa naulizwa sana na wateja wangu.
Ili niweze kuitumia vizuri nikajiunga na chuo kimoja pale mjini ili kusomea mambo ya Video Production pamoja na Masomo International Technology ili niweze kufanya kazi zangu kwa ufanisi.

Ilinichukuwa miaka miwili kupata cheti changu cha diploma.

Nilikuwa napata kazi mbali mbali mpaka za mikoani na mpaka kufikia mwaka 2005 nilikuwa nimejenga nyumba yangu ya kubwa na kufungua studio yangu pale pale nyumbani ambapo nilikuwa nikifanya shughuli zangu mwenyewe.

Mke wangu tuliyeachana alikuwa akiendelea kujirusha na wanaume kwenye kumbi za starehe, niliamua kuwachukuwa wanangu na kuwapeleka nchini Uganda wakasomee huko.
Mwaka 2006 aliyekuwa mke wangu alifariki kwa kile wazazi wake walichoita TB, lakini dalili zote zilikuwa ni za kuugua ukimwi.
Sikusikitika sana kwani hayo yalikuwa ndio majaaliwa yake, alikuwa amevuna kile alichopanda.

Mnamo mwaka 2007 nilifunga ndoa na mchumba wangu baada ya kuwa wachumba kwa takribani miaka miwili.
Mchumba wangu huyu ambaye ni mwenyeji wa Mkoani Kilimanjaro, Mchaga ni mtumishi katika kampuni moja binafsi.

Ni mwanamke makini ambaye anajiheshimu na kuwathamini watoto wangu na amekuwa ni mshauri wangu katika mambo mengi na hata wazo la kuwapeleka watoto wangu Uganda kwa ajili ya kusoma ni yeye aliyelitoa.

Mpaka sasa tumejaaliwa kupata mtoto mmoja wa kiume ambaye ana umri wa mwaka mmoja.
Ili kuimarisha kazi yangu hii nimenunua mitambo yangu ya kusafishia picha na vyombo vya kupigishia muziki Katika sherehe mbalimbali.

Kutokana na kazi yangu kuwa nzuri na yenye ufanisi nimekuwa nikipata kazi mbalimbali za mikoani.

Nimeweza kujenga nyumba zangu nyingine mbili, moja ikiwa Tabata Kimanga na nyingine ikiwa maeneo ya Kimara na zote nimezipangisha.

Matarajio yangu ni kumpeleka mke wangu nje akajifunze mambo ya upambaji ili tufungue kampuni kubwa itakayojishughulisha na upambaji katika sherehe mbalimbali.

Maisha ninayoishi sasa ni ndoto nilizokuwa nazo miaka 15 iliyopita kwani baada ya subira, pamoja na misukosuko mingi hatimaye nimeweza.
Subira, Uvumilivu na ubunifu vikalipa, hata wewe ukiamua unaweza.

2 comments:

Yasinta Ngonyani said...

Ama kweli mvumilivu hula mbivu. Nampa hongera zote kwa uvumilivu wake. na pia bila kukata tamaa kweli ukiamua utaveza tu. Hakuna lisiwezekana duniani hapa. Asante Koero kwa kiasa hiki nimejifunza kitu

Mzee wa Changamoto said...

Hiki ni kioo. Na kazi yake ni kukupa taswira ya wewe kama wewe na pengine mwingine alivyo. Lakini hakikupi taswira a nmwingine ukijiangalia wewe. Maana yake ni kuwa katika nyakatai na maono tofauti, kioo kitakupa aswira halisi. Na kila taswira itatoka kama isimamavyo mbele ya kioo. Mwenye kukitazama na ajione.
Asante saaana Dadangu