Monday, March 8, 2010

NDIO TUKIAMUA TUNAWEZA

TUPO ndani ya siku kumi na sita za harakati, ili kuhamasisha watu katika nafasi zao kuchukua hatua kupinga kwa nguvu zote ukatili wa aina yoyote dhidi ya wanawake. Ni kweli kwamba katika zama hizi tulizo nazo kama jamii hatuwezi kuendelea kuvumilia ukatili dhidi ya wanawake.

Kampeni hiyo mahsusi ina kaulimbiu kwamba kama jamii tunaweza kuzuia ukatili wa kijinsia. Hakuna ubishi juu ya dhamira hii ni kwamba kama jamii tukiamua kukomesha ukatili dhidi ya wanawake ni kitu kinachowezekana kabisa.


Lakini msisitizo hapa ni lazima uwekwe kwenye nafsi na nafasi ya kila mtu alipo, harakati hii ni kama wokovu, haitoshi tu kutofanya ukatili wa kijinsia wewe mwenywe, unatakiwa kuwa balozi wa mabadiliko, kwa maana kwamba ili jamii yetu ifikie kiwango cha kutokuwa na uvumilivu na ukatili wowote wa kijinsia, ni lazima kutovumilia huko kuanze na nafsi ya mwanajamii wetu mmoja mmoja.
]
Haki za wanawake ni haki za binadamu, hili ndilo jambo la msingi na dira ya kutuongoza katika harakati hizi, hatuwezi kujiita taifa lenye amani na utulivu wakati wapo raia miongoni mwetu wanaoyaona maisha yao ya kila siku ni kama jehanamu.


Kwamba katikati ya kisiwa cha amani na utulivu wapo watu ambao kila uchao, maisha yao yamejaa hofu na wasiwasi, maumivu na uchungu ni sehemu ya maisha yao. Hatuwezi kujiita ni watu tunaofurahia maisha wakati jirani yetu kipigo ndio utaratibu wake wa maisha.
Na haya yanatokea si kwa sababu wao wametaka au wamejiweka katika mazingira hayo magumu, wanawake wengi wanatendewa ukatili huu eti kwa sababu tu waliumbwa kwa jinsia ya kike.


Wapo baadhi ya wanaume - sihofu kuwaita washenzi (hawana ustaraabu) - ambao kwao mwanamke ni kiumbe duni kwa kila hali, eti tu kwa kuwa ni mwanamke. Huu ni ujuha wa hali ya juu sana ambapo mwanajamii wa jamii iliyostaarabika hasitahili hata kuwaza tu wendawazimu huo.

Wapo wanaume na bahati mbaya sana, wengine ni vijana wanajua kuoa maana yake ni kuweka mjakazi ndani ya nyumba yako, kwamba wao wanakuwa ndiyo alfa na omega ndani ya nyumba. Lile wanalolitaka wao ndio linalokuwa bila kujali kwamba mke ni mwenza aliye sawa (a different but equal partner) katika kuamua na kupanga hatima ya maisha yao.
Tofauti za kijinsia hazikuumbwa ili zimfanye mwingine mnyonge kwa mwenzake, tofauti hizo zipo na ziliweka makusudi ili kuyafanya maisha ya dunia hii yawezekane, ilimpendeza Muumba wa Ulimwengu huu kwamba aweke tofauti hizo ili ziwasaidie wanadamu kukamilishana na siyo kunyanyasana.


Lakini kwa bahati mbaya wapo ndugu zetu wengine ambao hudhani kwamba ili kudhihirisha uanaume wao ni lazima kumyanyasa mwanamke, huo ni uzuzu wa kiwango kilichopea, mwanamume halisi ni yule anayejiamini na ambaye anajua kumjali mwenza wake na kumtendea kama yeye anavyopenda atendewe ndiyo msingi wa mwanamume halisi.

Ni bahati mbaya kwamba hali ya unyanyasaji wa kijinsia hapa nchini kwetu inatisha, ndiyo sababu ipo haja ya kutumia kikamilifu siku hizi za harakati, ili kuhakikisha kuweza kunaanzia katika kujishawishi kila mtu aanze kuwekeza katika kubadili tabia na mtazamo, atambue kwamba tunapozungumzia haki za wanawake, tunazungumzia haki za mama zetu, dada zetu na mabinti zetu wenyewe. Ni mwendawazimu tu anayeweza kukubali kuona mama yake, dada yake au binti yake ananyanyaswa eti tu kwa sababu ni mwanamke.

Hatuna cha kujivunia sana linapokuja suala la haki za kijinsia katika taifa letu. Katika utafiti uliofanywa mwaka 2004/5 na Idara ya Takwimu nchini, umeonesha kwamba wanawake watatu katika ya watatno hupigwa na waume zao kwa sababu za kujibishana, kuondoka bila kuaga au kukataa kufanya tendo la ndoa.

Wanawake 46 katika ya 100 wanakubali kwamba mwanaume ana haki ya kumpiga mke iwapo atajibishana naye, 47 kati ya 100 wanakubali kwamba mume ana haki ya kumpiga mkewe iwapo atazembea kuangalia watoto. 29 wanakubali ni sawa kupigwa na wanaume zao iwapo watakuwa wamekataa kufanya tendo la ndoa.

Utafiti uliofanywa na Shirika la Afya la Umoja wa Mataifa (WHO) kuhusu hali ya ukatili wa wanawake katika mikoa ya Mbeya na Dar es Salaam, takwimu zinaonesha kuwa asilimia 48 ya wanawake waliowahi kuwa na mahusiano wamewahi kufanyiwa ukatili, asilimia 60 ya wanawake waliofanyiwa ukatili hawakutoa taarifa katika mamlaka zinazohusika.

Wakati asilimia 56 walisema wanaona ukatili kama sehemu yao ya maisha na asilimia 30 hawakumweleza mtu yeyote juu ya ukatili wanaotendewa. Takwimu hizi si kitu kizuri hata kidogo. Kinaonesha ni kwa kiasi gani tafsiri yetu ya Tanzania kuwa kisiwa cha amani haina mantiki wala maana.

Kwa sababu huwezi ukawa na amani wakati ambapo sehemu ya jamii yako hufanyiwa ukatili, hunyanyaswa na kuteswa ni sehemu yao ya maisha. Ipo haja ya kubadilika na kuamua kwa dhati kila mmoja kwa nafsi yake kuapa kutofanya ukatili na kutovumilia ukatili pale unapoona unafanyika.

Shirika la kutetea haki za wanawake la jijini Mwanza la Kivulini, pamoja na wadau wengine katika kampeni ya ‘Tunaweza’, limedhamiria kuwa na waleta mabadiliko milioni moja na laki sita, mpaka kampeni hiyo itakapokamilika.

Kwa msingi kwamba mtu mmoja mmoja anaweza kubadili tabia na mienendo ya watu wengine, kwa kuwapata hao, hawa ndio watakaokuwa nuru ya kuwaangazia wengine hawa watakuwa chumvi ya jamii iliyobaki katika kufanikisha mabadiliko hayo, ni muhimu ukiwa sehemu ya nuru na chumvi hiyo.

Lakini kama jamii iko haja ya kutafari upya mienendo yetu juu ya haki za binadamu, jamii yetu kwa kweli imefika mahali pasipotakiwa. Tumeanza kuwa jamii sugu inayovumilia kila aina ya ubaya miongoni mwetu eti kwa vile tu hautuhusu moja kwa moja.

Lakini tukumbuke kitu kimoja kwamba kila kinachotokea kwenye jamii yetu, taathira yake hatuwezi kuikwepa isipokuja leo itakuja kesho. Na hapo ndipo ule umuhimu wa kupigana na ukatili dhidi ya wanawake na kutovumilia kila aina ya ukatili unaotuhusu wanajamii wote kwa pamoja.

Haya ni mapambano ya wanajamii wote bila kujali rika au jinsia, haki za wanawake ni haki za familia, ni haki za jamii yetu ni haki ya taifa letu, bila kujali sisi ni wa jinsi gani.
Na kwa vile kila mmoja wetu ana nia ya kulifanya taifa letu kuwa sehemu salama na inayostahili kukaliwa na watu wastaarabu na wake kwa amani bila aina yote ya hofu, kutishia amani na utulivu wetu, ni lazima basi amani na utulivu huu uanzie nyumbani.


Kampeni hii inatualika Watanzania tuweze kupinga ukatili dhidi ya wanawake, Baba wa Taifa aliwahi kutuasa katika hekima zake kwamba inawezekana ikiwa tutatimiza wajibu wetu. Katika hili wala hatutahitaji kuhofu inawezekana kabisa kutokomeza aina zote za unyanyasaji wa kijinsia katika jamii yetu, ilimradi tu kila mtu ataamua kutimiza wajibu wake. Ndiyo tunaweza tukiamua kutimiza wajibu wetu.

Mungu ibariki Tanzania.

Makala hii imeandikwa na mwandishi Deus Bugaywa, na ilitoka katika Gazeti la TANZANIA DAIMA, wakati leo tunasherehekea siku ya wanawake leo nimeona sio vibaya kuirejea.

Hii sijaandika mimi jamani, wanaume msije nitoboa macho,..........LOL

3 comments:

Mija Shija Sayi said...

..na ndiyo tumeshaamua.

Asante kwa makala Koero.

kamala Lutatinisibwa Lutabasibwa said...

inachanganya.

wanawak ndio wanaozaa wanaume na kuwalea, sasa mnamlaumu nani? si mtulee mnavyotaka? ehe

msiletena tunda la mauti

chib said...

@ Kamala... !! #... :-)