Wednesday, May 5, 2010

JE, UTABIRI WA BALDWIN ZACHARIA JUU YA RAIS KIKWETE UMETIMIA?

Mheshimiwa Rais Jakaya Mrisho Kikwete

Mnamo Novemba 9, 2005, katika Gazeti la Jitambue, ambalo halichapishwi kwa sasa kutokana na mhariri wake ndugu Munga Tehenan kuupoteza mwili, kulikuwa na makala moja iliyokuwa ikitabiri utawala wa Rais Kikwete utakavyokuwa iwapo angeshinda.

Utabiri huo ulifanywa na Mtabiri na mwandishi wa makala za kiutambuzi wa gazeti hilo ndugu Baldwin Zacharia. Pamoja na kutabiri juu ya ushindi wa Rais Kikwete jambo ambalo wadadavuaji mbalimbali wa nyota na wachambuzi mbalimbali wa kisiasa hapa nchini walitabiri, lakini mtabiri huyu alikwenda mbali zaidi na kueleza utawala wa Raisi utakavyokuwa kutokana na nyota yake.

Leo hii akiwa ndio anaelekea kutimiza miaka mitano akiwa Ikulu, nimeona nirejee utabiri huo ili kuangalia kama utabiri wake umetimia au la.

Naomba uungane nami katika kuusoma utabiri huu kama ulivyoandikwa na Mtabiri huyu Baldwin Zacharia.

**************************
KIKWETE ATAKUWA RAIS WA MAAJABU NCHINI

Na Baldwin Zacharia.
Gazeti la Jitambue la Jumatano 9, Novemba 2005

Mimi ninaamini katika nyota na huwa ninachambua nyota. Nimeamua, kwa kutumia utaalamu wangu kuchambua nyota ya mgombea wa wa nafasi ya urais wa Jamhuri ya Muungano, Jakaya Mrisho Kikwete.

Ni kwa nini yeye?

Ni kwa sababu, anatajwa katika tafiti zilizofanywa hapa nchini na jumla ya maoni ya wengi kwamba, ana nafasi kubwa ya kuwa Rais wa awamu ya nne wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.

Kikwete amekuwa katika utumishi wa wa chama chake kwa miaka 30 na katika utumishi wa serikali katika nafasi mbalimbali za uwaziri kwa miaka 17.

Baada ya kumaliza masomo yake ya Chuo Kikuu cha Dar es salaam, mwaka 1975 na kupata shahada ya uchumi, akiwa na umri wa miaka 25, Kikwete alijiunga katika utumishi wa chama cha TANU (Tanganyika African National Union). TANU ndiyo iliyoongoza mapambano ya kudai uhuru nchini na Februari 5, mwaka 1977, ilijiungana na chama kilichoasisi mapinduzi ya Zanzibar, ASP (Afro-Shirazi Party) na kuzaliwa Chama cha Mapinduzi yaani CCM.

Jakaya Mrisho Kikwete alizaliwa Oktoba 7, mwaka 1950 katika kijiji cha Msoga, Wilaya ya Bagamoyo mkoani Pwani. Ni motto wa sita wa mzee Khalfani Mrisho Kikwete.

Huenda Kikwete haamini katika nyota, lakini akisoma uchambuzi huu atalazimika kuanza kujiuliza kuhusu nguvu za nyota, kwani atajiona akiwa anazungumziwa yeye, hata kwa mambo ambayo hajawahi kumwambia mtu anayo au anayafikiri.

Kwa kuzaliwa Oktoba 7, kama wengine wote waliozaliwa kati ya Septemba 23na Oktoba 22, Kikwete anaangukia kwenye alama za jua (Sun Sign) ya Mizani (Libra). Hii ni alama ya saba katika mpangilio wa mwenendo wa sayari.

Kwa wale wanaojua kuhusu nyota watakubaliana nami kwamba, alama hii inahusika na uhusiano, ushirikiano, mawazo, maoni, siasa, diplomasia, muziki, amani, uwezo wa kujidhibiti na tabia nzuri.

Nyingine ni pamoja na kuwa na mvuto kwa kutazamwa, uwezo wa kuboresha hali, utanashati, mawazo yenye mantiki ya kupima na mawazo kuhusu unafuu kwa jamii inayomzunguka mwenye nyota hii.

Hata kama wewe sio mtaalamu wa uchambuzi wa nyota, unaweza kusoma kwenye vitabu mbalimbali, ili uweze kuona sifa za mtu wa nyota ya Mizani. Kwenye nyota, Mizani ndiyo inayoonekana kwamba, ni bora zaidi, kwani imetulia na iko mahali ambapo inatengeneza urari au usawazisho wa mambo mengi, ndio maana imeitwa Mizani.

Kwa tabia za watu wa nyota hii, kama Kikwete atachaguliwa kuwa Raiswa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, watu watarajie kitu gani?

Watarajie kuona mtu mtendaji zaidi kuliko mtu wa nadharia. Ingawa atachukua muda mrefu kutafakari jambo (ndivyo watu wa nyota yake walivyo), lakini kutenda ni lazima, pale anapoona jambo linaweza kufanyika bila kuumiza watu.

Kwa nini nataja kuumiza watu katika suala hili? Utaona mbele kwenye uchambuzi wangu, namna watu wa nyota ya Kikwete wanavyohusiana na wengine kwenye maisha.

Kama atakuwa Rais wananchi wategemee kuona mtu mbaye kabla hajatoa uamuzi, atakaa kwa muda kutafakari. Watu wa nyota ya Mizani huwa hawaamui kwa jazba au haraka.

Kama Kikwete hana furaha na yuko katika ugiligili (Frustration) ataonesha tabia zifuatazo.ambazo sio nzuri sana. Ndivyo watu wa nyota yake walivyo: Atakuwa ni mwenye hasira za haraka na anayependa makuu yasiyo na kitu. Atakuwa ni mwoga na asiye na uwezo wa kufanya uamuzi hata pale ambapo kila kitu kiko wazi.

Lakini pia atakuwa ni mtu anayetumia wengine kwa faida yake. Hivyo hutokea kuwa mtu anayependa kuwadhibiti au kuwaendesha wengine kwa njia yenye kukera sana.

Hata hivyo kila anayemfahamu Kikwete, anajua kwamba hayuko kwenye ugiligili na ana furaha karibu muda wote. Kwa hiyo ni Mizani ambaye anatarajiwa kuonesha upande mzuri wa nyota hiyo, siyo huo mbaya.

Kwa upande mzuri, Mizani ni watu wanaojua sana kushirikiana na wengine, wanakubalika kwa wengi, kwani wanaingilika kirahisi, ni watu ambao wanaweza sana kuzungumza na kufanikisha muafaka kati ya watu wanaogombana, wanapenda sana haki au uhalali katika kutenda, hupenda kuongoza kwa faida ya wale wanaowaongoza zaidi, kuliko kwa faida yao. Kama nilivyosema, hufikiri vizuri sana kabla ya kutenda na ni watu wa vitendo badala ya maneno.

Kwa kumtazama Kikwete na kutazama kila alikopita tangu akiwa shule ya msingi ya Lugoba, sekondari Kibaha, sekondari Tanga, na Chuo Kikuu cha Dar es salaam, na baadae makazini, nimegundua kwamba, ameathiriwa n asana na nyota yake, tena athari za upande mzuri.

Kwa hali hiyo, Kikwete anatarajiwa kuwa Rais aliyetulia sana na anayemudu kuficha hofu zake na kubabaika kirahisi. Ana uwezo wa kudhibiti hali ambayo kwa mwingine angebabaika sana. Lakini watu wa Mizani wana hofu ya kuwa peke yaona ndio maana mara nyingi wanakuwa na kundi la marafiki au ‘kampani’ kama tunavyoita. Je, Kikwete hayuko hivyo?

Ukweli ni kwamba, Kikwete anaweza kuwa Rais wa ajabu ambaye nchi hii haijawahi kumshuhudia kwa sababu ana athari za wazi ambazo ni chanya za nyota yake. Kwani kwa nyota yake anatarajiwa pia kuwa rais mwenye upendo sana na mwenye kusikiliza kwa makini mawazo ya wengine.

Lakini anaweza kukasirika kupindukia na kupinga sana pale atakapotakiwa kufuata amri. Mizani ni wajanja kupindukia, tofauti na wanavyoonekana au namna wanavyozungumza. Ni watu wanaopenda sana kuzungumza na wengine, labda wakitafuta mawazo au kujivua na upweke. Lakini kwa bahati mbaya, wanaweza kuamini watu wasio wakweli bila wenyewe kujua na watu hawa wakawathiri.

Kwa athari za sayari ya Zuhura (Venus) ambayo ndiyo yenye kuongoza nguvu ya kinyota ya Mizani, mtu aliyeathiriwa na nyota yake kama Kikwete anakuwa ni mpenda amani sana na hana mazungumzo ya kumwaga damu au kukomesha. Lakini anapokerwa hadi kufikia ukomo, hufanya mambo ambayo wengi wanaweza wasiyasahau kirahisi.

Kinajimu Zuhura ni sayari ya thamani, nafsi, umiliki, uzuri, na upendo. Kwa maana hiyo, Kikwete akiwa Rais wa nchi, atasababisha thamani ya nchi kupanda kupitia kwake, umiliki kuwa mkubwa zaidi, utanashati yaani kutakata kwa watu na uhusiano mzuri na amani kuongezeka.

Kuhusu mwonekano, kwa kawaida hakuna mwonekano wa mtu kufuata nyota yake. Lakini watu wa nyota ya Mizani, hutokea kuwa na kishimo cha shavu au kidevuni. Wana ung’avu wa sura na kuonekana kuwa wazuri au wa katikati, yaani wasio wazuri au wabaya. Ni watu wanaopenda sana kujikagua asubuhi kabla hawajatoka kwenye shughuli zao. Kubadili nguo kutwa mara mbili siyo ajabu kwao, mradi hali inawataka wafanye hivyo.

Lakini kwa kawaida watu nyota hii, hata wanapokuwa wamekasirika, nyuso zao hazioneshi kutisha. Mara nyingi sana wanakuwa na tabasamu pana au lenye kuvutia, ambalo si la kinafika. Sijapata nafasi ya kumkagua Kikwete kwenye mambo haya, lakini waliowahi kuwa naye karibu wanaweza kusema.

Akiwa nyumbani ambako hupapenda sana baada ya kazi, mtu wa nyota ya mizani hupenda kusikiliza muziki na kusoma. Ni mtu anayependa sana kubishana na familia yake kuhusu chochote kwa makusudi tu, ili kuchangamsha familia. Sijui kuhusu kikwete anapokuwa nyumbani, lakini hivi ndivyo anavyotakiwa kuwa.

Ni mtu mabaye pia anapokuwa nyumbani hupenda wageni na kuwakarimu ambapo pia huwa na mazungumzo mazuri, yenye kuvutia. Anapenda vile vile kuona watoto wake wakipata uhuru wa kufanya mambo yao. Hata hivyo kwa kutaka kwake kutoikera familia huweza kujikuta akiimiliki kama mali yake.

Kazini ni mtu ambaye, huchukua muda kuyaweka mambo sawa, kwani hataki kubahatisha, ni mwaminifu na ambaye anachangia zaidi mawazo kwenye mambo anayohusishwa kuliko wengine. Ni mwenye uwezo wa kujenga mtandao mzuri wa uhusiano na wengine kiofisi au na ofisi nyingine.

Mtu wa nyota ya Mizani hushauri majibu au suluhu ambazo wengine wanaweza kuziona za kushangaza awali, lakini ndizo sahihi mara nyingi. Anakauwa hatua moja mbele katika kuona suluhu. Katika kuamua huwa anaangalia hali halisi, sio visasi au sifa, ingawa anajisikia vizuri watu wakimhusudu.

Kwa kawaida mtu wa nyota ya mizani hatagemei kuishi kwa majungu au umbeya. Anapenda sana kila kitu kiende wazi na kufanyika bila lengo la kuumiza mwingine. Huyu ndiye atakayekuwa Raisi wa awamu ya nne hapa nchini, endapo Kikwete ndiye atakayepita.

Ni mtu anayeweza au kupenda kuwa kati kama msuluhishi. Kama nilivyosema, hupenda amani na anajua kusuluhisha. Hana kawaida ya kuwa mkatili au mjeuri, ingawa ana misimamo inayoweza kumfanya akaonekana kuwa hivyo.

Mizani ni watu ambao hupenda sana kujihusisha na masuala ya kisheria, siasa na mambo ya kimataifa. Bila shaka msomaji unaweza kudhani naandika haya kwa sababu Kikwete ni waziri wa mambo ya nje na ni mwanasiasa, hapana. Jaribu kutafuta vyanzo vingine ujifunze kuhusu upendeleo kitaaluma wa watu wa nyota ya Mizani.

Pengine sifa moja ya watu wa nyota ya Mizani, ambayo ni vema sana kuitaja ni ile ya kupenda kuwatumikia watu. Watu wa nyota hii hupenda kuona kila wanachofanya kinagusa watu na kuwafaidisha, ndipo wanaporidhika ndani mwao.

Mizani hawajali sana kuhusu fedha, yaani hawatoi jasho kiasi hicho. Wakiwa nayo wanaona ni sawa, lakini wakiona hawana haiwafanyi wakose amani. Lakini wanajua ubahili pia kwa namna fulani, kwani hupenda sana kuweka kwa ajili ya baadae.

Lakini huchukia sana kubishana kunakohusisha kelele badala ya mantiki. Huchukia pia ugoigoi hasa unaofanyika hadharani au unaowahusu watu wengi (jamii). Hii ikiwa na maana kwamba wanapenda kuona watu wakiwajibika.

Sifa zilizotajwa hapa kuwahusu watu wa nyota Mizani nyingi ni zile chanya. Nimeamua kuzitaja hizo kwa sababu baada ya kumsoma Kikwete kwenye maeneo mengi kimaisha nimebaini kwamba ameathiriwa vizuri (Positive) na nyota yake. Hii ina maana athari nzuri za nyota hii anazo.

Watu maarufu duniani waliokuwa au wenye nyota hii ya Mizani ni pamoja na Mahatma Gandhi (Kiongozi wa kidini na kijamii wa India) Bob Geldof (Mwanamuziki na mchangaishaji kusaidia wengine) Oscar Wilde (Mtunzi wa vitabu) na wengine wengi.

Shukrani za pekee zimwendee kaka Shabani Kaluse wa kibaraza cha Utambuzi na Kujitambua kwa kufanikisha kupatikana kwa kumbukumbu hii.

5 comments:

Unknown said...

Karibu ktk libeneka la KATUNI...
www.artsfede.blogspot.com

o'Wambura Ng'wanambiti! said...

Labda utatimia ama usitimie!

Yetu macho na masikio...lol

Mzee wa Changamoto said...

Duh!!Kuna
Hiyo "range" ya birthdates yaangukia kwa mwanangu Pau. Sijui itakuwaje.
Kuhusu Kikwete, nadhani angekuwa peke yake tungeweza kuangalia zaidi utabiri huu, ila kazingirwa na "watu" ambao wananifanya niwe na wasiwasi kama nikionacho ni utendaji wa Kikwete ama la.
Ila tutafika tuuu

MARKUS MPANGALA said...

Utabiri mzuri. na wakati mwingine kuna swali dogo tu. JK ATAWEZA BILA LOWASSA? ukifikiria hilo halafu rudi kwa kauli ya NABII JULIUS KAMBARAGE NYERERE mwaka 1995 katika joto la uchaguzi kuwania kuteuliwa CCM alisema hivi wakati huo 'MKIWAPA UONGOZI HAWA VIJANA WATAWASUMBUA SANA HUKO MBELE' wakati ule alisema kwa kuwalenga waliokokuwepo katika kundi la JK katika kuwania urais, ndipo akawaonya kuwa kundi la VIJANA wale ambao sasa ndiyo wazee litatupatia shida... nadhani ndiyo hayo. Inakuwaje Rais asiijue katiba? hadai aseme TUCTA msiponichagua wengine watanichagu? Hee inamaana CCM wameshamteua? Je hajui hilo ni kosa kwa mujibu wa tume ya uchaguzi? Au mwandishi wa hotuba zake ni kalumekenge? Ipo kazi hapa haki ya nani hivi

Anonymous said...

Utabiri wake umetimia haswa pale aliposema atafanya maamuzi ambayo watu wengine wataona kuwa hayako sahihi. Na ni kweli hasa huu uamuzi wa kuzuia mgomo wa TUCTA uko sahihi kabisa ingawa kwa sasa sisi hatuoni kama uko sahihi kwa sababu tunataka kima cha chini kiongezeke. Ukiongeza kima cha chini na wote wanaofuatia huko juu lazima wasogee hawawezi kubaki static. Na suali la kujiuliza je hizo pesa tunazo? Je huu mgumu hautayumbisha zaidi uchumi ambao umeshayumba kutokana na msuko suko wa kuyumba kwa uchumi wa dunia? Je tukigoma watakaoathirika zaidi na mgomo ni nani? Ni walio nazo au sie kima cha chini. Mara nyingi athari za migomo zinawaumiza watu wa chini zaidi wenye kutumia huduma za serikali za kijamii na nyinginezo.

Leo hii kwa mfano mishahara UK imepanda kwa asilimia 1.7 wakati gharama za maisha zimepanda 3.4% na inflation inazidi kupanda kila uchao. Kama rais wa nchi ilibidi achukue uamuzi ule tutake tusitake. Tunahaki ya kudai nyongeza pale ambapo tunaona kabisa uchumi unakua, tija imeongezeka, pato la taifa kutokana na makusanyo ya kodi na mauzo ya bidhaa nje limeongezeka. Lakini kinyume cha hapo ni kujidanganya na kumuona Rais mbaya kwa sababu tu ya utashi wa kisiasa.

Najua wengi watanishambulia kutokana na utashi wa kisiasa, mie mawazo yangu yanatokana na kutazama hali halisi na jinsi sisi wenyewe watanzania tunavyofanya kazi na si ushabiki wa kisiasa. Mwenye data atwambie tija imeongezeka shirika fulani lakini mishahara midogo.