Saturday, May 1, 2010

TAFAKARI YA LEO: JE, SISI TUNAOMBA?

Hata Yesu pia aliomba!

Tafakari ya leo, ningependa kuzungumzia kuhusu maombi na nguvu ya maombi.
Hebu tusome katika Mathayo 7: 7-10

"Ombeni nanyi mtapewa; tafuteni nanyi mtaona; bisheni nanyi mtafunguliwa; kwa maana kila aombaye hupokea; naye atafutaye huona; naye abishaye hufunguliwa.
Au kuna mtu yupi kwenu, ambaye, mwanawe akimwomba mkate atampa jiwe? Au akiomba samaki atampa nyoka?"

Kuna watu ambao hawajui kuomba na hawajawahi kuomba kabisa katika maisha yao. Unaweza kushangaa kuwa miongoni mwa watu hao wapo pia wakristo.

Kuomba maana yake ni nini?

Kuomba ni kumsogelea mungu na kumweleza shida zako, pale tunapopambana na majaribu au dhiki na shida ni wajibu wetu kumsogelea mungu na kumweleza shida zetu.

Yesu anaposema 'Ombeni nanyi mtapewa;' alimaanisha kwamba huwezi kupata kile unachokitaka bila kuomba. Kwa mfano unaweza kuwa na shida ya pesa je unadhani yupo mtu mahali fulani ataota tu kuwa una shida ya pesa na kukuletea bila kuomba? Haiwezekani ni lazima uombe na ndipo utakapo pewa. Inawezekana ukamuomba mtu moja kwa moja na akakupa pesa au kupitia maombi yako kwa mungu akatokea mtu akajua shida yako na kukuletea pesa kwa namna ya kushangaza kidogo. Hii ina maana kwamba haiwezakani ukapata kile unachohitaji bila kuomba.

Na aliposema ‘tafuteni nanyi mtaona;’ Je alikuwa na maana gani?
Labda nikuulize wewe unayesoma hapa, hivi inawezekana ukaona kitu unachokitafuta bila kukitafuta kitu hicho? Hiyo haiwezekani , kwanza ni lazima ujue unatafuta nini , halafu pia ujue kitu hicho kinapatikana wapi na ndipo uelekeze macho yako huko katika kukitafuta kitu hicho.

Yesu anaendelea kusema ‘bisheni nanyi mtafunguliwa;’ akimaanisha kwamba kuomba ni mpaka uende kwa muhusika nakubisha hodi na ndipo utakapofunguliwa. Kwani kubisha maana yake ni kuusogelea mlango na kubisha hodi na ndipo ufunguliwe mlango.
Huwezi kubisha hodi ukiwa mbali inabidi uukaribie mlango na ndipo ubishe. Je ni mlango gani huo? Ni kumsogelea mungu kwa sala na maombi, huku tukirutubisha sala zetu kwa matendo mema, na ndipo sala zetu na maombi zaitakapokuwa na nguvu

Na ndio maana akazidi kusherehesha kwa kuwaambia wanafunzi wake,

‘kwa maana kila aombaye hupokea; naye atafutaye huona; naye abishaye hufunguliwa.
Au kuna mtu yupi kwenu, ambaye, mwanawe akimwomba mkate atampa jiwe? Au akiomba samaki atampa nyoka?’

Ni kwamba, sisi huwa tunapokea kile tunachoomba. Hata siku moja Mungu hawezi kukupa kile ambacho hukuomba. Na ndio maana kuna msemo mmoja usemao ‘utavuna kile ulichopanda’

Katika Mathayo 6: 26, Yesu alisema:
Waangalieni ndege wa angani, ya kwamba hawapandi, wala hawavuni, wala hawakusanyi ghalani; na baba yenu wa mbinguni huwalisha hao. Ninyi je! Si bora kupita hao?

Hapa Yesu anakumbusha kwamba, ikiwa Ndege wa angani hawavuni na wala hawakusanyi lakini Mungu ameweza kuwalisha seuze sisi wanadamu ambao ni bora kuliko hao ndege.

Sisi tumejaaliwa vipawa vyote. Tumepewa akili ya kutuwezesha kufikiri na kupambanua, tumepewa uwezo wa kubuni na kuumba vitu mbalimbali, mfano ndege, magari, majengo marefu. Karibu kila kitu kilichopo katika uso huu wa dunia ni matokeo ya kufikiri kwa wanaadamu.

Lakini hata hao ndege warukao nao sio kwamba wanapewa kila kitu watakacho, bali inategemeana na mazingira waliyopo, haiwezekani ndege walioko katika maeneo ya panapolimwa mpunga akatamani kula mtama wataupata wapi, hiyo itawalazimu waruke maili nyingi kutafuta mahali palipooteshwa mtama ili kukidhi kiu yao.

Na hata sisi kila tunapoomba tunaangalia mazingira tuliyo nayo. Kwa mfano unaomba kupata pesa, sawa lakini je unakipawa cha thamani gani cha kubadlishana na pesa.
Mungu hatoi pesa bali anatoa njia mbadala ya kupata pesa.

Tunapojiwekea malengo makubwa, ni lazima tujue pia tutafikaje huko, kwa kuwa safari ya kuelekea huko pia yaweza kuwa ndefu. Kuna mwanafalsafa mmoja aliwahi kusema, “Ukitaka kuung’oa mlima mrefu, basi anza kwa kuondoa mawe madogo madogo”

Lakini pia ikumbukwe kwamba haihitaji kuomba kwa sauti au kutamka kwa vinywa vyetu ili jambo liwe, hata kufikiri kwetu pia ni namna mojawapo ya kuomba,

Katika Mathayo: 6: 7-8, Yesu anawaambia wanafunzi wake:
“Nanyi mkiwa katika kusali, msipayuke-payuke, kama watu wa mataifa; maana wao hudhani ya kuwa watasikiwa kwa sababu ya maneno yao kuwa mengi. Basi msifanane na hao; maana baba yenu anajua mnayohitaji kabla ninyi hamjamwomba.”

Hii ina maana gani?
Ina maana kwamba Mungu anafahamu lile lililo katika mioyo yetu, kama tunafikiri katika maanguko basi tutaishia kuanguka na hatutofanikiwa kamwe, lakini kama tunafikiri katika kumudu hakika tutamudu, kwa kuwa sisi wenyewe ndio mainjinia wa kile tulicho nacho leo.

Kamala anazungumzia sana juu ya tahajudi, (Meditation) hii ni njia mojawapo ya namna ya kuratibui kile kinachoingia ndani yetu, kwa kufanya tahajudi tunakuwa na uwezo wa kuwa karibu na mungu nakumweleza shida zetu.

Niliwahi kuzungumzia juu ya imani huko nyuma, lakini pia ni lazima ifahamike kuwa imani bila kuomba ni kazi bure.
Yatupasa kuomba kwanza na ndipo imani inafuata.

Tukutane Jumamosi ijayo………………

5 comments:

o'Wambura Ng'wanambiti! said...

Tatizo si kuomba Da Koero!

Kinachogomba hasahasa ni NINI tuombacho na muda gani tuombe!

Unawezajikuta unaomba mume (tena unaweka vigezo- awe mdhuri, awe na kitambi, awe na kagari na awe na nyumba) wakati Mungu anajua kabisa huyo umtakaye awe wako hana uwezo wa kukuzalisha mtoto wa kike....lol

Jinsi ya kumtafuta huyo MUNGU pia ni ishu kwani waweza kujikuta unamtafuta nje yako wakati yuko ndaniyako katulia NDANI yako!

Kaaazi kwelikweli!

kamala Lutatinisibwa Lutabasibwa said...

eti tuome wakati wa shidaa????

Mungu gani huyo wa kutafutia shida tu?? we need to be in HIM and HIMU in us sio wakati wa shida

ukiongelea kupayuka wa naanisha nini tu-meditate au??

Yasinta Ngonyani said...

nanukuu "Katika Mathayo: 6: 7-8, Yesu anawaambia wanafunzi wake:
“Nanyi mkiwa katika kusali, msipayuke-payuke, kama watu wa mataifa; maana wao hudhani ya kuwa watasikiwa kwa sababu ya maneno yao kuwa mengi. Basi msifanane na hao; maana baba yenu anajua mnayohitaji kabla ninyi hamjamwomba.”

Hii ina maana gani?
Ina maana kwamba Mungu anafahamu lile lililo katika mioyo yetu, kama tunafikiri katika maanguko basi tutaishia kuanguka na hatutofanikiwa kamwe, lakini kama tunafikiri katika kumudu hakika tutamudu, kwa kuwa sisi wenyewe ndio mainjinia wa kile tulicho nacho leo."mwisho wa kunukuu. Tafakari ya leo ni kweli inabidi kutafakari maana kuomba sio kuomba tu ni lazima uwe na imani na kile uombacho. Upendo Daima!! Amina

chib said...

Mimi nina imani tofauti, siamini kuomba... bali naamini kujituma na kuwa muaminifu kwako binafsi na kwa wengine ndio chachu ya mafanikio.

o'Wambura Ng'wanambiti! said...

@Chib: na hiyo ndo sala kubwa kuliko zote ;-)