Sunday, April 18, 2010

ULE MRADI WETU SASA UMEIVA………..

Dada Yasinta

Makao makuu ya NGO yetu

Kwako dada yangu mpendwa Yasinta Ngonyani, natumaini wewe na watoto wako pamoja na huyo shemeji yangu anayejifanya kutojibu salaam zangu muwazima wote. Unajua dada simlaumu sana huyo mumeo, maana najua alitishwa wakati anakuchumbia kuwa sisi Watanzania tuna shida sana, kwamba tukiona ndugu yetu kaolewa basi shida zetu zote zitaishia kwake. Naomba umtoe mashaka kwamba ukoo wa Ngonyani hatuka hivyo, yaani hatuko kama ule ukoo wa mzee Makalioni, yule anayependa kusingizia misiba kila uchao ili kujipatia ridhiki.

Mwambie kuwa ukoo wa Ngonyani ni Jiniazi na una watu makini sana na wenye akili za ziada, kwani haoni hao wanae wawili uliomtotolea baada ya kukumimbisha kuwa wana akili sana kama mama zao wadogo na wajomba zao.

Samahani dada ngoja niachane na hayo, unajua leo nimeamua kukuandikia waraka huu asubuhi huku nikinywa chai na mkate wa bofulo nilionunu hapo jirani kwa mpemba kwa sababu waraka huu ni muhimu sana, kwani unahusiana na lile dili nililokudokeza wakati ule ambalo limeanza kutema, kama yale machimbo ya Tanzanite kule Mererani.

Dada mimi sio mbinafsi na ndio maana nikaona nikushirikishe ili wote mimi na wewe na ukoo wote wa Ngonyani tuwe matajiri kama Bill Gate wa Sudani, yule anayetoa tunzo ya Raisi bora wa Afrika. Eti huyu jamaa amegundua kuwa maraisi wa Afrika kwetu wana njaa sana na ndio maana wanakuwa mafisadi na ili kuwatoa wasiwasi akaanzisha tunzo yenye mapesa mengi ili kuwaondolea tamaa ya wizi.

Naamini hata huyo mzungu wako ataamini kuwa ukoo wa ngonyani sio mchezo na una watu makini na mahiri katika kuzitafuta ngawira.

Dada huku nyumbani nimeanzisha mradi wa kuhamasisha ukimwi. Na nimeona nikushirikishe ili wote tuwe matajiri, lakini usidhani nakushirikisha bure, lazima utoe kamchango kako kama kianzio yaani utoe mtaji, kwani usione vinaelea vimeundwa. Sasa ili uwe na wewe ni mmiliki wa NGo yangu…….hapana yetu inabidi utumbukize kama Krona Milioni mia moja ili tuweze kuwavuta wafadhili kuwa NGo yetu sio ya kuganga njaa, dada naamini hizo pesa unazo kwani huyo mzungu wako hawezi kukosa pesa kidogo hivyo, maana hicho kiasi cha pesa ni kama vile anatoa hela ya kununulia Tooth Picks. Naomba hizo pesa uzitumbukize kwenye akaunti ya NGo yetu ambayo ni XXL 000055557788JK/KoeroNGo/Yasinta/Camilla/Eric.com hiyo ndiyo akaunti namba yetu.

Kama nilivyokwambia kuwa nimeanzisha huu mradi wa Ukimwi ambao nimeamua kuuita Intaneshino NGo for fool people of Ruhuwiko die because of ngono zembe. Na kama unavyoona hilo jina linatisha na kuvutia sana.

Dada huku ili uweze kuishi kwa amani na usalama ni lazima uwe mbunifu, ili uweze kuendesha gari linaloitwa Rav 4 au Toyota Haria ni lazima uwe na akili ya ziada ya kuwaona wengine ni wajinga na wewe ndiwe Generali Brigedia mwenye akili nyingi kuwazidi.

Mradi wetu wa ukimwi unaendeshwa kwa njia ambayo ni lazima tutapata fedha za wafadhili kwani tuna watu wanaoweza kubuni na wengine wanaoweza kutusaidia kuthibitishia dunia kwamba Tanzania inayo watu wanaoteketea kwa ukimwi hata kabla bwana hajarudi katika ule ujio uliotabiriwa kwenye kitabu kitakatifu cha biblia.

Kwanza tunajitahidi kuwasiliana na wafadhili na kuwaeleza kwamba huku nchini katika kila watu kumi unaokutana nao, basi kumi na moja wana virusi na kumi na mbili kati yao tayari wanaumwa mahututi. Na ili upate fedha za wafadhili haraka ni lazima takwimu zako ziwe zimechanganyikiwa kidogo kwani takwimu zikiwa sahihi wafadhili lazima wataingia mashaka au watakweri .

Sisi tuna mtaalamu wetu mmoja aitwae Chacha o’Wambura Ng’anambiti ambaye ni mwenyeji wa kule Kyabakari Barracks Musoma, Mara. Huyu kijana tumemuingiza katika mradi wetu kwa kuwa anajua kubuni na kutunga kiasi kwamba anaweza kukushawishi kwamba jina lako sio Yasinta bali unaitwa Jasimini na ukakubali.

Hata hivyo yuko kijana mwingine aitwae Kamala Lutatinisibwa, ambaye amelikimbia jiji la Dar Es Salaam na kwenda kuishi kule Karagwe kutokana na ukata, huyu ndio yuko kwenye mchakato wa usaili akiwania nafasi ya Meneja mahusiano katika NGo yetu. Unajua hii nafasi ya meneja mahusiano inahitaji watu makini na mahiri walio na utaalamu wa utambuzi. Kama atafauli katika usaili atatusaidia sana katika kupiga tiralila za propaganda kwa wafadhili pale watakapotaka kuthibitisha takwimu zetu.

Kwa upande wa huyu kijana Chacha o’Wambura Ng’wanambiti kazi yake ni kuandaa taarifa za kuombea pesa kwa mujibu wa matukio yaliyo katika jamii kwa wakati huo.

Kwa mfano hili tatizo la mafisadi lililoikumba nchi yetu, huyu mwenzetu amewaandikia wafadhili akiwambia kuwa Mafisadi na ukimwi ni ndugu kabisa kwani ukimwi unasambaa sana katika kipindi hiki ambacho mafisadi wameshika hatamu za nchi, kwa sababu mafisadi hao wamekwiba fedha za Richimondi ambazo zingesaidia mradi wa umeme vijijini na kwa kuwa mradi huo umekwama na kusababisha vijiji vyetu kama vile kule Ruhuwiko, Kashasha, Kyabakari, na kwingineko kukosa umeme, watu wanatumia fursa hiyo kuendelea kufanya ule mchezo mtamu gizani yaani ule mchezo ulikataliwa na mungu katika amri ya sita katika zile amri zake kumi.

Ameendelea kuwaeleza kuwa kwa kuwa huko vijijini bado wananchi wako gizani kutokana na kukosa umeme wanaume hawavalishi vilambio vyao vifanyio na inakuwa ni vigumu wanawake kug’amua janja yao kwa kuwa kuna giza totoro na hivyo kuambikizwa ukimwi kirahisi.

Kijana huyo ameendelea kuandika kwamba katika utafiti wetu tumegundua kuwa wakati mwingine hata wale wauza vifanyio huwauzia wateja vifuko vya ashikirimu wakidai ni vifanyio orijino kumbe ni feki, na hivyo vinashindwa kuhimili vishindo na kupasuka kiurahisi.

Kutokana na Write up hiyo Wafadhili wametujibu kwamba utafiti wetu ni wa kiwango cha juu na wameahidi kutupatia kiasi kikubwa cha pesa ili kudhibiti hali hii ya vijana kuendelea kuambukizana ukimwi ambapo unachagizwa na kupenda sana ngono.

Dada namuona Chidakwa, huyu binti wa mzee Makalioni anakuja kwa kasi sijui baba yake kabuni msiba mwingine ili tumpe michango ya rambirambi, hebu ngoja nifiche huu waraka maana akiuona atakwenda kumwambia baba yake ili na yeye aanzishe NGo yake na kujipatia fedha…….unajua dada ukiwa na aidia zilizokwenda shule inabidi ufanye siri maana kuna wezi wa aidia ile mbaya, unaweza kushangaa wenzako wamekupiku……hebu ngoja nimsikilize…..nitakumalizia hii habari wakati mwingine…LOL

3 comments:

o'Wambura Ng'wanambiti! said...

Ha ha ha haaa! You made my day :-)

Message sent.

Yasinta Ngonyani said...

Koero! ahsante kwa kunikumbusha kwa kweli inabidi tuanze na ni sasa. Ahsante sana. Nimeipenda hii makala kwa kweli. Upendo Daima.

Jacob Malihoja said...

Koero good work! But the mind needs to be firm and not a joke! I do not like jokes when bad things are heating up in the country. It should be Real! hataka kama sio hivyo hivyo lakini kitu fulani kifanyike!