Friday, April 16, 2010

UNAPOSUBIRI KUSIFIWA!


Unapofanya jambo lolote, fanya tu kama nafsi yako inakubali na inafurahia jambo hilo.
Usifanye jambo kwa kutegemea kusifiwa. Kumbuka usiposifiwa itakuuma sana, lakini ukisifiwa bila kutegemea sifa hiyo, utajisikia furaha sana.

Bila shaka utakubaliana na mimi kuwa Binadamu ni kiumbe anayependa kusifiwa, lakini ikitokea ukawa na kiu kubwa ya kupenda kusifiwa , basi inabidi ujiulize, ni wapi pana kasoro kwenye fikra zako.

Haiyumkini katika malezi yako hukuwahi kusifiwa kamwe na maisha yako yalitawaliwa na kulaumiwa kwingi na kukosolewa, hivyo ukajikuta ukihitaji kukamilishwa.

Haya burudika na shairi hili la Malenga wa Mvita.

UWATAPO HAKI YAKO


Namba nawe mlimwengu, pulikiza matamko
Nikweleze neno langu, uzinduwe bongo lako
Nayo nda M'ngu si yangu, na ayani haya yako
Uwatapo haki yako, utaingiya motoni


Simama uitete, usivikhofu vituko
Aliyo nayo mwendee, akupe kilicho chako
Akipinga mlemee, mwandame kulla endako
Uwatapo haki yako, utaingiya motoni


Amkani mulolala,na wenye sikio koko
Isiwe mato kulola,natutizame twendako
Tuwate na kuduwala,usingizi si mashiko
Uwatapo haki yako,utaingiya motoni


Teteya kwa kula hali, usiche misukosuko
Siche wingi wala mali,sabilisha roho yako
Unyonge usikubali, ukaonewa kwa chako
Uwatapo haki yako, utaingiya motoni



Siche kifaru na ndovu, wangazidi nguvu zako
Wapempe kwa uwekevu, unusuru haki yako
Siandame wapumbavu,kilicho chako ni chako
Uwatapo haki yako, utaingiya motoni


Cha mtu hakifitiki,kikafungiwa kiliko
Huzuka kikawa hiki,kazana utwae chako
Uwatapo yako haki,fahamu ni dhara kwako
Leo na kwa Mola wako,utaingiya motoni



Fumbuwa unyang'arize, uone duniya yako
Bure sijiangamize,kuangalia wendako
Utatupa upoteze,wende ambapo si pako
Uwatapo haki yako,utaingiya motoni


Kadhalika nako pia,huko ambako sikwako
Huwezi kujitetea,wala huwi na mashiko
Basi iwaze duniya,kwani ya kale hayako
Uwatapo haki yako ,utaingiya motoni


Kadi tamati shairi,sitii la ongezeko
Mwanati iwa tayari, utete haki yako
Unyonge usiukiri,Jifunge ufe kwa chako
Uwatapo haki yako, utaingiya motoni

Shairi hili limetungwa na Ahmad Nassir wa Malenga wa Mvita

2 comments:

o'Wambura Ng'wanambiti! said...

Hata ukipenda kusifiwa kama sifa hazikustahili ni kazi bure tu!

Utakuwa unajipa faraja na kulimbikiza makosa ilhali ulikuwa na nafasi ya kujitathmini ili ufanye marekebisho lakini waaapiii!

Ninashuhudia watu wakiambiwa wewe ni baba mzuri wakiondoka wanatetwa nyuma ya pazia kuwa familia imemshinda!

Kuna viongozi wanasifiwa kwa uongozi mzuri na kusikiliza wanyonge huku nyuma wakielezwa kuwa kijiji, wilaya, mkoa na hata nchi imewashinda kutawala

:-(

Markus Mpangala. said...

ipo kazi hapa mkuu!
TOMORROW NEVER DIES baby!